Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,809
- 15,409
Wiki iliyopita nakumbuka ilikuwa ni siku ya Alhamisi asubuhi na mapema nilikuwa naendesha gari nikitokea nyumbani kwangu Tabata Mawenzi kuelekea kazini kwangu maeneo ya Posta huku nikisikiliza mziki mwororo ambao ulikuwa ukiuburudisha moyo wangu ili kuifanya siku yangu kuwa nzuri kwa siku hiyo.
Nilipokaribia maeneo ya Tabata Bima nilimuona msichana mmoja mrembo hasa akiwa kituoni. Alikuwa ni mjamzito lakini urembo wake ulificha ule ujauzito wake. Alikuwa ni binti mrefu na mwenye rangi ya chokoleti na umbo namba nane.
Nilihisi alikuwa anaenda kazini, na kwa kuwa kulikuwa na dalili ya mvua niliona nimsaidie kumpa lifti. Nilisimamisha gari na kumuuliza kama anaenda Posta nimsaidie kwa sababu ya hali yake ya ujauzito niliona msaada wangu ungekuwa ni muhimu kwake. Yule binti hakukataa aliingia kwenye gari tukaanza safari ya kuelekea mjini.
Tulipofika mjini aliniomba nimshushe pale posta mpya mtaa wa Azikiwe, Sikuweza kufahamu kwamba anafanya kazi wapi kwa sababu hatukuzungumza sana ndani ya gari zaidi ya kusalimiana. Nilipofika kibaruani kwangu niligundua kwamba yule binti alikuwa amesahau pochi yake ndogo ndani ya gari.
Niliamua kufungua pochi ile kwa imani kwamba naweza kupata kitambulisho chake na hivyo kurahisisha mawasiliano. Niliweza kupata kitambulisho chake nikagundua alikuwa anafanya kazi kwenye benki moja maarufu iliyopo mtaa wa Azikiwe.
Nilipiga namba ya hiyo benki na baada ya kumweleza operator aliyepokea simu kuhusu huyo binti aliniunganisha naye. Nilipomweleza kwamba mimi ni yule kijana niliyempa lifti, akadakia haraka haraka na kuniuliza kama niliona pochi yake, nikamjibu kwamba asiwe na wasiwasi kwa sababu ninayo hapo ofisini kwangu. Nilimuuliza ni namna gani naweza kumpelekea hiyo pochi yake. Akanijibu kwamba atanipigia simu karibu na muda wa kutoka kazini.
Ilipofika majira ya saa kumi na mbili jioni alinipigia simu na kuniomba kama naweza kumpitishia pochi yake nyumbani kwake maeneo ya Tabata Bima, alinielekeza nyumba anayoishi na kwa kuwa mimi ni mwenyeji katika maeneo hayo, nilipafahamu mahali anapoishi kwa urahisi na nikamuahidi kwamba nikitoka kazini nitampitishia hiyo pochi yake, lakini wakati tukiendelea kuongea mara nikasikia sauti ya kiume kwenye simu…
"Unataka kufanya nini na mke wangu, ngoja nikuone hiyo jioni ukija hapa nyumbani kwangu nitakupiga risasi nikuulie mbali pumbavu kabisa, unacheza na mke wa mtu… Nakwambia nikuone uje hapa nitakumaliza achana na mke wangu kabisa…….."
Ilibidi nikate simu huku mwili ukinitetemeka na kijasho chembamba kikinitoka nilijikuta nikikata network kwa muda hata sikujua nilitaka kufanya nini kwa wakati ule.
Nilikusanya nguvu na kuendelea na kazi zangu kama kawaida na nilipotoka kazini nilielekea nyumbani moja kwa moja. Nilipofika nyumbani nilioenakana kuwa na lindi la mawazo kiasi kwamba hata mama Ngina alinishtukia. Aliponidadisi nilimwambia kwa kifupi tu kwamba ni mambo ya kazi. Kuna wakati nilitaka nimweleze, lakini nikaona atanigeuzia kibao akidhani kwamba labda nina mahusiano na huyo binti mjamzito. Wakati mwingine hawa wake zetu wanaweza kuzusha balaa mahali usipotarajia. Ilinibidi nipige kimya.
Siku iliyofuata yaani Ijumaa majira ya saa tatu asubuhi nikiwa ofisini, yule mwanamke mjamzito alinipigia simu tena, nilipoipokea aliniomba sana radhi. Aliniambia kwamba yule mwanaume aliyenikaripia jana jioni alikuwa ni mumewe. "Kwa kweli hata mimi nimemchoka kwa sababu ya wivu wake, yaani mume wangu hataki kabisa kuniona nawasiliana na mwanaume wa aina yoyote, hata wafanyakazi wenzangu wa kiume huwa hawanipigii simu nikiwa nyumbani hata kama kuna jambo muhimu la kazini…………. Hata sijui nifanye nini?
Nikamwambia, "samahani dada, sitaweza kukuletea pochi yako nyumbani kwako kama unaweza upitie hapa kazini kwangu uje uichukue".
Aliniambia kwamba hatoweza kuja hapa kazini kwangu kwa sababu mumewe anaweza kumpitia jioni akitoka kazini, aliniomba muda wa chakula cha mchana tukutane kwenye mghahawa wa mmoja uliopo katikati ya jiji. Nilikubali ingawa moyo wangu ulikuwa ni mzito, hata hivyo nilijipa moyo kwa sababu sikuwa na ajenda ya siri na huyo mwanamke na isitoshe lengo lilikuwa ni kumpa pochi yake kisha nirudi zangu ofisini kwangu.
Majira ya saa sita kamili nilikuwa tayari ndani ya mghahawa ule nikinywa juisi nikimsubiri huyo mwanamke mjamzito. Mara simu yangu ikaita nilipoiangalia nikaona ni namba ya yule mwanamke. Nikaipokea. Alinijulisha kwamba tayari yupo pale mghahawani, nilimwambia kwamba niko ndani akaniambia anakuja kisha nikakata simu.
Alipofika pale nilipiokaa nilisimaa kumkaribisha kisha tukasalimiana kwa bashasha na uso wake ulipambwa na tabasamu pana lilisindikizwa na dimples zilizojitokeza dhahiri katika mashavu yake yaliyotuna. Pale ndipo nilipouona uzuri wa yule mwanamke, alikuwa ni mzuri wa sura na umbo na mcheshi kupindukia. Nadhani mumewe ana haki ya kuwa na wivu.
Wakati namkabidhi ile pochi yake, ghafla waliingia jamaa watatu waliojazia miili ya mazoezi na mmoja kati yao akaninyooshea kidole huku akisema….
"Wewe kijana, nilikuonya uachane na mke wangu sasa unafanya nini na mke wangu hapa. Kabla sijajibu nilishtukia nimepigwa ngumi ya uso nikaenda chini kama furushi, vile nanyanyuka jamaa mwingine aliyeshiba akanikaa mtama nikarudi chini kwa kishindo. Kwa kifupi wale jamaa walinigeuza mpira wa kona maana nilipewa kipondo, na wakati huo nilimuona yule mwanamke mjamzito akilia kwa kunionea huruma huku akimsihi mumewe na ile mijamaa iliyojazia iniache kwa sababu sina kosa.
Mara mlinzi wa ule mgahahwa alikuja na kwa kushirikiana na raia wema walinifanikiwa kuniokoa kutoka katika kadhia ile. Kusema kweli tukio lile lilikuwa kama senema pale mghahawani maana watu walijaa wakishuhudia nikipewa za uso kama mwizi. Pamoja na kuokolewa hata hivyo nilipoteza fahamu.
Nilipozinduka nilikuwa nimelazwa katika hospitali moja maarufu iliyoko katikai ya jiji nikiwa na bendeji usoni ilikuwa ni usiku na pembeni yangu alikuwepo mama Ngina, na baadhi ya wafanyakazi wenzangu na wana JF wenzangu, al;ikuwepo Mentor, Jiwe Linaloishi, KakaKiiza, Asprin, Paloma, sister na dada yangu Ennie wakinifariji. Tukio lile lilinirudia mawazoni mwangu nikajikuta nikitokwa na machozi. Mama Ngina na wote waliokuja kuniona walinituliza na kunitaka nijikaze na nisiwaze chochote na nitulize mawazo.
Siku iliyofuata yaani Jumamosi niliruhusiwa na daktari akanijulisha kwamba natakiwa kufika kituo kikuu cha polisi siku ya Jumatatu asubuhi kutoa maelezo yangu kwa sababu wale jamaa watatau walionishambulia wamekamatwa na wako ndani…
Leo Jumatatu nilifika pale Polisi kama nilivyotakiwa na kuandikisha maelezo yangu kwa kina hata hivyo nilishtuka kuambiwa watuhumiwa walionishambulia walishaachiwa tangu siku ile waliyokamatwa, na sikupewa maelezo ya ziada nikaambiwa nitaitwa upelelezi wa shauri langu utakapokamilika.
Niliporudi nyumbani nikajkuta nikiwa na mtihani mwingine wa kujieleza kwa mama Ngina…..
Nimemuomba anipe muda nitulize kichwa lakini sina amani kabisa.
Sijui nitaanzia wapi……..
Last edited by a moderator: