JF sio mahali pa udaku...ni vilelelezo tuuu.....
Uliyoyasema je, yanaukweli gani? Soma habari ifuatayo
Monday, 13 December 2010 20:45 0diggsdigg
Daniel Mjema,Moshi
www.mwananchi.co.tz
KUNDI la watu wanaoaminika kuwa ni majambazi ambao idadi yao haijajulikana, wamevamia katika Kijiji cha Kiraracha. Moshi Vijijini, mkoani Kilimanjaro na kumwagia petroli nyumba mbili ikiwamo ya mwenyekiti wa kijiji na kuua familia yake.
Habari za uhakika kutoka katika kijiji hicho, zilisema unyama huo umefanywa ili kupinga mpango wa Ulinzi Shirikishi, ulioanzishwa katika kijij hicho.
Tukio hilo ambalo limeibua simanzi kubwa katika kijiji hicho, lilitokea saa 4:00 usiku wa juzi ambapo majambazi hao wakiwa na silaha na madumu ya petroli, walivamia nyumba ya Mwenyekiti wa kijiji kupitia tiketi ya TLP, Andrea Lekule na kufanya kitendo hicho.
Mwenyekiti huyo alijeruhiwa vibaya kwa moto na sasa amelazwa katika Hospitali ya Kilema wakati mke wake, Catherine Lekule (45) na mtoto wao mdogo Flora Andrea (6) waliteketea kwa moto na kubakia majivu.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Lucas Ng'hoboko alilithibitishia Mwananchi kuhusu kutokea kwa tukio hilo,
"Ni kweli kwamba kuna watu walikwenda nyumbani kwa mwenyekiti wa kijiji hicho wakiwa na madumu ya petroli na kuchoma moto nyumba yake. Tayari tumewakamata watu wawili ambao mwenyekiti anasema amewatambua," alisema Ng'hoboko.
Kamanda Ng'hoboko alisema ingawa chanzo tukio hilo hakijafahamika,lakini taarifa za awali za uchunguzi wa polisi zinaonyesha kuwa tukio hilo lilifanywa mahsusi ili kulipiza visasi.
Alisema kiongozi huyo akishirikiana na mgambo waliendesha msako wa kutafuta wahalifu katika kijiji hicho na kuwakamata watu watatu wanaohisiwa kuhusika katika matukio mbalimbali ya ujambazi.
"Sasa badala ya kuwapeleka watuhumiwa hawa polisi, wao wakaenda kuwahifadhi nyumbani kwa Mrema (Agustino) kwa siku nzima sasa huwezi kufahamu kama ni kikundi cha watu kilichukizwa na jambo hilo au ni majambazi,"alisema.
Kamanda Ng'hoboko alisema katika ulipuaji huo wa nyumba ya mwenyekiti wa kijiji, nyumba ya kaka yake, Michael Lekule (64) nayo ilishika moto na kuteketea ingawa hakuna aliyejeruhiwa.
Mbunge wa Vunjo na Mwenyekiti wa Taifa wa TLP, Agustino Mrema ambaye anaishi katika kijiji hicho, aliliambia Mwananchi jana kuwa kama polisi hawatapiga kambi katika eneo hilo. hali inaweza kuwa mbaya zaidi.
"Tunaamini ni tukio la kulipiza kisasi kwa sababu jana yake asubuhi baada ya ibada tulifanya kikao na wananchi kukubaliana kuwa kuna haja ya kuanzisha ulinzi wa sungunsungu kwa sababu ujambazi wa silaha umeongezeka,"alisema.
Kikao hicho kilishirikisha Mrema kama Mbunge wa Jimbo hilo, Diwani wa Marangu Magharibi, Paul Meela, viongozi wa dini na wananchi na kukubaliana kuanzisha ulinzi shirikishi.