Mitanange mikali Duniani

Damaso

JF-Expert Member
Jul 18, 2018
1,590
2,088
Mpira au Soka ni moja kati ya michezo ya kipekee sana, ni mchezo ambao umejaa makeke mengi sana na nyakati za huzuni na Furaha, kwa wengi mpira umevunja ndoa za watu kwa wale wenzangu ambao ni mashabiki kindakindaki, wale ambao wapo Tanzania ila wanafuatilia mpaka Ligi kuu ya Brazil ambapo Mechi zake nyingi huchezwa kuanzia saa 8 ama saa 9 usiku.



Sasa mwanamke anaona ni bora aende kwao tu kuliko kulala peke yake huku mumewe yuko anaangalia mechi kali kati ya Flamengo dhidi ya Internationale.

Mpira umewaleta karibu watu, mfano tu kupitia matawi mbalimbali ya vilabu vya soka nchini, watu wengi wamejenga urafiki wa kudumu, na wengine wamepata na nduu zao humo humo.

IMG_1703.jpg


Lakini pia mpira umejenga chuki na uhasama mkubwa sana baina ya mashabiki wa timu kadhaa. Chuki ambazo huonekana wazi wakati wa mitanange mbalimbali endapo tu timu hizi zikakutana uwanja. Baadhi ya mashabiki hutoleana maneno makali, wengi hupigana na kuchoma wenzao kwa visu huku vifo pia vikitokea.

Leo Nitakupa mechi kali ambazo kwa hakika kabsa ni mechi ambazo duniani zimekuwa kivutio kikubwa sana, ni mechi ambazo zimevuta hisia za mashabiki kwa ukaribu sana na zingine zimeleta mpaka fujo na ugomvi kwa watu na ugomvi mkubwa.

Karibu kwenye sehemu ya kwanza;

1. Borussia Dortmund dhidi ya Schalke 04
IMG_1681.jpg


Tuanzie huko Ujerumani twende Kaskazini ambapo tunakutana na timu mbili kubwa zenye historia ya kuheshimika sana ndani ya Ujerumani na Ulaya. Nazungumzia klabu za Borussia Dortmund na Schalke 04 ambao hawa ni watani haswa kwani mechi yao ya watani wa jadi ilianza mwaka 1925 huku mashabiki wa timu hizi mbili wakiwa ni maadui haswa, na endapo timu moja ikifungwa basi washindi hutengeneza jezi maalumu kushangilia ushindi wao.


Na wajuzi wameipatia mechi hii jina la The Revierderby, na hii ndio mechi ya kwanza ya watani wa jadi ndani ya Ujerumani.

2. Ugiriki dhidi ya Uturuki


Ugiriki dhidi ya Uturuki ni mechi nyingine kubwa ambayo sio ya kubeza hata kidogo, timu hizi mbili za taifa ni watani wa jadi ambao hata mashabiki wake huishia kuchapana makofi endapo wakikutana uwanjani.
View attachment 2648173

Mwaka 2002 Uturuki alipambana sana mpaka kufikia hatua ya nusu fainali huku Ugiriki akitoka kwa aibu, na mwaka 2008 Ugiriki na Uturuki walipangwa kundi moja kwenye michuano ya EURO huku Uturuki akipata bahati tena ya kuingia hatua ya nusu fainali akimuacha mwenzake Ugiriki mbali sana.

3. Porto dhidi ya Sporting
IMG_1693.jpg


Twende mpaka Ureno ambapo tunakutana na timu mbili zenye historia na heshima kubwa sana kwenye tasnia ya mpira wa miguu, hawa ni Porto pamoja na Sporting Lisbon. Ukipata nafasi ya kushuhudia mchezo baina ya timu hizi mbili kwenye uwanja wa taifa wa Ureno, Estadio Nacional basi utakubaliana nami kuwa ni vita kubwa sana ndani ya dakika 90 za mchezo. Porto wanaotokea Kaskazini mwa Ureno na Sporting Lisbon wanaotokea Kusini mwa Ureno wamecheza michezo mingi baina yao huku Porto akiwa na historia nzuri kuliko Sporting Lisbon, huku wote hawa wawili wakiwa hawajawahi kuteremka daraja tokea wamepanda kwenye ligi ya Ureno Premeira Liga.

View attachment 2648174

Mtanange huu naufananisha kwa ukaribu zaidi ya ule mtanange wa Minho baina ya Vitória de Guimarães dhidi ya SC Braga.

4. Flamengo dhidi ya Vasco de Gama
View attachment 2648178

Tutoke Ureno na twende Amerika Kusini mpaka Ardhi ya Marehemu Pele, maskani kwa kina Ronaldinho Gaucho, Romario, Ronaldo De Lima,Neymar, Dida na kadhalika. Ardhi iliyobarikiwa mafundi na wasanifu bora sana wa kucheza na mpira wa miguu. Huko tunakutana na mechi moja kali sana baina ya Flamengo dhidi ya Vasco De Gama. Wababe hawa wawili wakikutana uwanjani basi nyasi hutoa cheche kabsa, wameibatiza mechi hii kwa jina la "Clasico dos Milhoes" au Mechi ya Matajiri, huku Flamengo pamoja na Vasco De Gama wakiwa na mashabiki wengi sana kutoka Brazili, na nchi jirani mpaka Amerika ya Kusini kwa ujumla, na kwa kawaida watu takribani milioni 50 hufuatilia mechi hii na hii inachukuliwa ndo mechi kubwa sana ndani ya Brazili.

Ukifika kwenye uwanja wa Maracana, pale kwenye Jiji la Rio de Janeiro ni kawaida kuona mashabiki wakiwasha moto majukwaani na fujo ambazo kwa mara kadhaa zimepelekea ugomvi na hata vifo vya mashabiki.

5. Marseille dhidi ya Lyon
Tuondoke Brazili na twende moja kwa moja mpaka Ulaya na tufikie pale Ufaransa ambapo tunakutana na mechi kubwa sana ndani ya Ufaransa, baina ya Olympique Marseille dhidi ya Olympique Lyon.


Mechi haina uadui sana kiasi cha kutoana roho bali ni mashabiki tu wamekuwa wakiwapatia moto sana wachezaji. Wafaransa wameibatiza mechi hii jina la Choc des Olympiques kwa maana ya Mpambano wa Olimpiki.

6. Partizan dhidi ya Red Star
Tutoe Ufaransa na tusogee mpaka Serbia ambapo tunakutana na mechi kubwa sana ndani ya soka la nchi ya Serbia baina ya Partizan dhidi ya Red Star, timu mbili zenye mafanikio makubwa ndani ya Serbia na zenye mashabiki wengi sana. kitu cha pekee ni mashabiki wake ambao hujipanga vyema sana katika namna ya kuwashangalia wachezaji wao kuanzia nje ya uwanja mpaka ndani ya uwanja.

Mashabiki hutumia bendera za timu zao pamoja na nyimbo wakiwa uwanja na kuoneshana nani zaidi kwenye uwezo wa kuwaunga mkono wachezaji wao.

7. Besiktas dhidi ya Fenerbahce
Tutoke Serbia na turejee Uturuki kidogo na kuangalia mechi moja kubwa sana baina ya wababe, Besiktas dhidi ya Fenerbahce, ambapo wana historia ya kukutana zaidi ya miaka 100 huku ikiwa ni moja ya mechi kubwa sana ndani ya Jiji la Istanbul, kwa mara kadhaa timu hizi huchuana kuwa namba moja kwenye misimamo wa ligi kuu ya Uturuku na mara nyingi mechi hizi baina yao ndo huamua ni nani anatakiwa awe juu ya misimamo.

Timu hizi mbili hazina uswahiba hata kidogo, huku mashabiki wake wakichapana ngumi, na kupelekea mpaka majeraha wakati wa kubishana kuhusu uwezo wa timu fulani. Besiktas ilianzishwa na watu waliokuwa wakiishi Uturuki iliyokuwa upande wa Ulaya, wakati Fenerbahce ikianzishwa na watu waliokuwa wakiishi Uturuki upande wa Asia, na hii inatosha kuweka mafuta kwenye makaa ya moto, na kuipatia mechi hii utamu wa ajabu sana.

8. Nacional dhidi ya Penarol
Tuondoke Uturuki na kueleka tena Amerika Kusini mpaka nchi ya Uruguay, maskani ya miamba ya soka la Amerika, Luiz Suarez, Edson Cavani na kadhalika. Basi huko tunakutana na mchezo baina ya Nacional dhidi ya Penarol, timu ambazo zote zinapatikana kwenye jiji la Montevideo, ingawa timu hizi hazina mafanikio makubwa nje ya Amerika Kusini ila zimesaidia sana soka la Amerika Kusini kupita hatua sana, ndani ya Uruguay pamoja na michuano ya Bara la Amerika ya Kusini al maarufu kama Copa Libertadoes. Wajuvi wa mambo wameipatia mechi hii jina la Clasico of Uruguay.

Sasa mechi hii ndo vita halisi kwani sio tu mashabiki bali hata wachezaji wamekuwa wakionesha uvunjifu wa amani na utovu mkubwa wa nidhamu. Tarehe 14 Aprili mwaka 1990 timu hizi mbili zilicheza mchezo wake ambao ulikuwa mgumu kweli na walitoshana nguvu wa magoli sifuri bin sifuri huku wachezaji 22 wakitolewa nje kwa kadi nyekundu, wachezaji wa Nacional 11 walitolewa nje kwa utovu wa nidhamu huku pia wachezaji 11 kutoka timu ya Penarol wakitolewa nje kwa makosa hayo, dakika 85 mchezo huo ulisimama kwa sababu timu zote hazikuwa na wachezaji wa kutosha uwanja, hakuna timu iliyokuwa na wachezaji saba, kwa Kifupi walibakia wachezaji wawili tu.

Mwaka 1991 wakakutana tena na uwanja ambao ulitakiwa wachezaji wacheze soka basi ukabadilika na kuwa ulingo, wachezaji wakabadilishana vitasa kwa kiwango kikubwa sana huku wachezaji 9 na kocha moja wakifungwa jela mwezi mmoja kutokana na kuanzisha ugomvi huo, kutokea mwaka 1800 mpaka sasa timu hizi mbili zimeshakutana zaidi ya mara 520.

9. Chelsea dhidi ya Liverpool
Tuondoke Uruguay na tupae mpaka Uingereza ambapo tunakutana na mechi kali sana baina ya wababe wawili, Chelsea dhidi ya Liverpool, ingawa sio mechi kubwa sana yenye historia ila kukutana kwako kwenye michuano mikubwa kama UEFA pamoja na Kombe la Ligi kumeongeza utamu wa mechi hii.

Namkumbuka John Arne Riise alivyojifunga goli kwenye dakika za majeruhi kwenye nusu fainali ya ligi ya mabingwa ya UEFA ya mwaka 2008 na kuifanya Chelsea kuingia fainali.

Lakini sitosahau mwamba, goli kipa bora sana, Mhispania, Pepe Reina alivyoizuia penalty ya Geremi akiwa pale kwenye uwanja wa Majogoo wa Anfield mwaka 2007. Lakini uadui mkubwa ulichochewa na uhamisho wa mchezaji Fernando Torres ambapo Chelsea walivunja kibubu na kutoa paundi milioni 50 ili wamchukue Torres huku Bwana Mkubwa Torres akidai kuwa Chelsea ndo timu kubwa kuliko Liverpool, basi tegemea kukutana na kitu cha moto sana endapo Chelsea akienda Anfield ama Liverpool akienda darajani pale Stamford Bridge.

10. LA Galaxy dhidi ya San Jose Earthquakes
Tutoke Uingereza na twende mpaka Amerika Kaskazini pale kwa Biden ambapo tunakutana na mechi kubwa baina ya LA Galaxy dhidi ya San Jose Earthquakes. Ukipata nafasi ya kuingia kwenye dimba la Buck Shaw Stadium, pale Santa Clara, California basi utaona utamu wa mpira na ufundi mkubwa wa soka la Marekani.

Ingawa soka bado halijanoga sana ndani ya Ardhi ya Marekani kama ilivyo michezo ya Golf, Tennis ama Mbio za Magari ila mechi baina ya LA Galaxy ikichuana na San Jose Earthquakes sio mechi ya kubeza kabsa kwani huvutia watu wengi kwenda kushuhudia ufundi wa soka.

Mtananage huu ni baina ya Kusini wa Jimbo la California dhidi ya Kaskazini mwa Jimbo la California, na wameibatiza mechi hii kwa jina la California Clasico.

Nakumbuka mpira safi sana uliopigwa na San Jose Earthquakes dhidi ya LA Galaxy tarehe 21 Agosti mwaka 2010 kwenye uwanja wa Buck Shaw Stadium uliopo pale Santa Clara, California na San Jose Earthquakes kutoka kifua mbele kwa ushindi wa goli moja kwa sifuri.

Tuungane kwenye sehemu ya pili!!!
 
1.Birmingham City dhidi ya Aston Villa
IMG_1704.jpg


Tuondoke Marekani na turejee Uingereza ambapo tunakutana na timu mbili za Birmingham City pamoja na Aston Villa, mechi hii imepewa jina la The Second City derby huku ikichochewa sana na hasira za mashabiki wa timu hizi, ni nadra sana kukuta mashabiki wanatii amri kwa kuondoka uwanja bila kutimuliwa na askari polisi.
IMG_1705.jpg


Mechi hii imeanza kuchezwa tokea mwaka 1879 huku mashabiki wa timu hizi mbili kutoka Jiji la Birmingham wakiwa ni wenye fujo na ugomvi kwa kiasi kikubwa sana. mwaka 1963 Birmingham City alishinda kombe lake la kwanza la Ligi mara baada ya kumpiga kisawa sawa Aston Villa kwenye fainali, lakini katika msimu wa mwaka 1980-81 Aston Villa alimpiga nje ndani Birmingham City na kushinda taji lake la kwanza la ligi kuu ya Uingereza tokea mwaka 1910.

Mwaka 2010 tarehe 1 Disemba mashabiki wa Birmingham City walivurugwa kweli mara baada ya kuanza kung’oa viti na kuwatupia mashabiki wa Aston Villa, kitendo ambacho kiliwalazimu askari polisi kuingia kutuliza ghasia hizo, hii ilikuwa ni kwenye hatua ya robo fainali ya kombe la Ligi la Carling pale kwenye uwanja wa St. Andrews, Birmingham Uingereza.

2. America dhidi ya Guadalajara
IMG_1706.jpg


Turejee tena Amerika ya Kusini mpaka kwenye nchi ya Mexico ambapo tunakutana na El Super Clasico ambapo ni mechi baina ya wababe wawili kutoka majiji ya Guadalajara na Mexico City, hawa ni Chivas pamoja na America, mara kadhaa imekuwa ikichukuliwa kama ni mechi kati ya Mexico City dhidi ya sehemu zingine za Mexico, timu hizi mbili ni timu zenye mafanikio makubwa ndani ya Mexico.
IMG_1707.jpg


Mechi hizi zilianza rasmi mwaka 1943 lakini hazikuchukuliwa uzito sana mpaka miaka 20 baadaye, huku utofauti mkubwa ukiwa ni kwamba timu ya Guadalajara hupenda kuchezesha wachezaji wazawa kutoka ndani ya Mexico huku timu ya America wao wakisajili wachezaji kutoka nje ya Mexico.

3. USA dhidi ya England
IMG_1720.jpg


Marekani dhidi ya Uingereza ni mechi nyingine kubwa, mechi yenye uzito wake kutokana na uhasama na uadui mkubwa baina ya timu hizi mbili, hapo ni mkoloni dhidi ya koloni lake, wakati Uingereza akiwa ndo Mkoloni basi Marekani akiwa ndo Koloni la Uingereza basi historia ya ukoloni inatosha kuipatia mechi hii utamu wa kipekee sana. mwaka 1950, timu ya taifa ya Marekani iliishangaza dunia mara baada ya kumpa dozi moja nzito sana Uingereza kwenye Kombe la Dunia, na wakati Marekani wanasheherekea ushindi wao basi Uingereza wakajenga chuki juu ya Marekani moja kwa moja.
IMG_1721.jpg


Bado malipo ya ukoloni hayakuishia hapo kwani mwaka 2010 wakati wa Kombe la Dunia limetuna kwenye ardhi ya Afrika kwa Tata Madiba, basi Marekani akapangwa kundi moja na Simba watatu huku chuma kizito sana cha Clint Dempsey kikitosha kupeleka maumivu kwa Robert Green na Uingereza kwa ujumla ambao hawakuwa na wakati mzuri katika mashindano hayo.

4. Corinthians dhidi ya Sao Paulo
IMG_1723.jpg


Turudi Brazili ambako tunakutana na mtanange mkali baina ya Corinthians dhidi ya Sao Paulo, mchezo ambao umebarikiwa kwa kupewa jina la Classico Majestico huku timu zote mbili zikitokea kwenye Jiji la Sao Paulo.
IMG_1722.jpg


Basi mashabiki zake hujikuta wakichapana ngumi sana kiasi kwamba vifo na majeraha hutokea kwa wingi. Timu hizi mbili zimekuwa zikikutana mara kwa mara kuanzia mwaka 1936 mpaka sasa.

5. West Ham dhidi ya Millwall
IMG_1724.jpg


Ingawa timu hizi zimepata kucheza mchezo wao wa mwanzo kabsa mwaka 1897 ila mpaka sasa wamekutana mara 120 tu, na bado ni mtanange mkubwa katika soka la Uingereza. West Ham na Millwall wapo kwenye madaraja tofauti hivyo kukutana kwao ni nadra sana labda kwenye kombe la Ligi ama michezo ya kirafiki. Ubabe wa mtanange huu ni mkubwa kiasi kwamba umepelekea mpaka kuchezwa filamu ambazo zinaonesha kiwango cha ugomvi unaotokea endapo timu hizi zikakutana uwanjani.
IMG_1725.jpg


Nakumbuka ule mchezo wa Kombe la Ligi baina ya West Ham vs. Millwall kwa mwaka 2009 ambapo mashabiki wa West Ham walivamia uwanja na kufanya fujo huku wengine wakichapana ngumi na mateke nje ya uwanja.

6. Fenerbahce dhidi ya Galatasaray
IMG_1726.jpg


Uturuki bado hakujaisha mizozo kwani kuna mchezi baina ya Fenerbahce dhidi ya Galatasaray, mchezo ambao umepewa jina la Kitalar Arasi Derbi au mchezo wa mabara kati ya timu mbili kubwa ndani ya Jiji la Istanbul Uturuki.
IMG_1727.jpg


Mchezo wa kwanza ulichezwa mwaka 1909 ila uhasama ulianza rasmi mwaka 1934 kwenye mchezo wa kirafiki. Mashabiki walikuwa wakifanya fujo huku wachezaji wakicheza michezo isiyo ya kungwana kabsa, mitama na ubabe wa kutumia nguvu sana, vitendo hivi vilitosha kwa mwamuzi kuachana na mchezo huu. Mwaka 1996 kwenye mchezo wa Kombe la Ligi Galatasaray alimpiga nje ndani Fenerbahce na kocha wa Galatasaray, Bwana Mkubwa Souness alikwenda kuweka bendera ya Galatasaray katikati ya uwanja wa Fenerbahce.

4. Benfica dhidi ya Sporting
IMG_1728.jpg


Kwenye dimba la Jose de Alvalade, Lisbon, Ureno itabakia historia pale ambapo timu ya Benfica ilipofanya maangamizi kwa kuifunga timu ya Sporting Lisbon goli moja kwa sifuri. Wareno wameubatiza mchezo huu jina la Derby de Lisboa ambapo huzikutanisha timu mbili kubwa kutoka Jiji la Lisbon na Timu bora sana katika soka la Ureno kwa Ujumla.

Uhasama ulianza mwaka 1907 pale ambapo wachezaji kadhaa kutoka Benfica walipoondoka kwenye timu hiyo na kuelekea Sporting Lisbon ili kupata sehemu yenye masilahi mazuri ya kazi. Ingawa Benfica inaonekana kama ni timu ya wafanyakazi na Sporting Lisbon inaonekana ni timu ya matajiri. Vita baina ya timu hizi unaweza kuliganisha na harakati za ufundi wa mpira baina ya Boavista vs. FC Porto, au kama Wareno wanavyopenda kusema O Dérbi da Invicta. Ufundi wa mpira ndani ya Ureno unazidi kung’aa kila kukicha ni sawa ana mtanange baina ya Farense dhidi ya Portimonense.

3. Sunderland dhidi ya Newcastle
IMG_1729.jpg


Uingereza kuna mchezo mkali sana baina ya timu mbili, Sunderland dhidi ya Newcastle, ambapo imepewa jina la Tyne-Wear derby, uhasama wa timu hizi mbili ulianza tokea vita ya Uingereza ya wenyewe kwa wenyewe, wao Newcastle waliunga mkono jitihada za upande wa Hanovers, huku Sunderland wakiunga mkono sera na jitihada za Stuarts.
IMG_1730.jpg


Mchezo wao wa kwanza ulikuwa ni mwaka 1888 huku mchezo wa mwaka 1901 ukishindwa kuchezwa kutokana na mashabiki zaidi ya elfu 70 kutaka kuingia kwenye uwanja wenye uwezo wa kuingia mashabiki elfu 30 tu, kila uongozi wa timu moja kati ya hizi umekuwa ukiwafungiwa mashabiki wa timu pinzani kutokuingia uwanjani kwa ajili ya tahadhari za kiusalama.

2. Leeds dhidi ya Manchester United
IMG_1731.jpg


Turejee tena Uingereza ambapo tunakutana na mechi nyingine kubwa kati ya Leeds dhidi ya Manchester United, mechi ambayo imepewa jina la The Roses derby ingawa timu hizi mbili hazijakutana mara nyingi tokea Leeds aliposhuka daraja kwenye miaka ya 1980 pamoja na mwaka 2004, lakini mashabiki bado wanachukulia mechi hii uzito mkubwa sana.


Vurugu pamoja na mapigano baina ya mashabiki ni kawaida sana kutokea wakati timu hizi zikikutana uwanjani, haswa tokea mwaka 1960, kipindi ambacho kikosi cha Manchester United kikinolewa na Matt Busby huku wao Leeds wakifundishwa na Don Revie. Katika nusu fainali ya kombe la Ligi FA mwaka 1965, Jack Charlton (Kaka yake na Sir Bobby) wa kikosi cha Leeds pamoja na Denis Law wa Manchester United walizichapa ngumi uwanja kwenye mchezo ambao ulikuwa mgumu sana kwa pande zote mbili.

1. Lyon dhidi ya Saint-Eteinne


Twende huko Ufaransa ambapo tunakutana na Derby du Rhone ambapo tunakutana na miamba miwili kutoka soka la Ufaransa, Lyon pamoja na Saint-Eteinne. Mashabiki wa timu hizi huongeza joto kwenye mitanange ambayo itakutanisha timu hizi mbili.


Huku ikiwa ni nadra sana kwa mchezaji wa Lyon kwenda Saint Eteinne au Saint Eteinne kwenda Lyon, na historia inaonesha kuwa ni wachezaji 13 tu ndio walioweza kucheza timu hizi mbili ndani ya kipindi cha miaka 60.


BONUS:

1. USA dhidi ya Mexico


Tuondoke Ufaransa na tuelekee Amerika ya Kaskazini ambapo tunakutana na timu mbili za mataifa jirani kabsa, timu ya taifa ya Marekani na timu ya taifa ya Mexico, wababe ambao hutesa timu nyingine za taifa kwenye michuano ya CONCACAF.


Uhamasa wako kwenye mpira ulikomaa sana kipindi cha Kombe la Dunia la mwaka 2002 ambapo Marekani alimcharaza Mexico mabao 2 kwa sifuri, na mashabiki wa Mexico wakaamua kulipiza kisasi kwenye michuano ya Olimpiki kwenye mchezo wa kufuzu uliopigwa huko Guadalajara, ambapo mashabiki hao wa Mexico waliimba neno Osama muda wote. Na mwaka 2004 Landon Donovan wa Marekani aliwalipa mashabiki hao kwa kukojoa kwenye uwanja wa Estadio Jalisco.

2. Arsenal dhidi ya Manchester United


Tutoke Amerika Kaskazini na twende mpaka Uingereza ambapo tunakutana na miamba miwili ambayo hata walimu wake hawakuwahi kuwa marafiki kabsa. Ni mechi ambayo Sir Alex Ferguson na Arsene Wenger waliongeza zaidi utamu wa uhamasa wake.


Nakumbuka ule mchezo wa Daraja la Kwanza tarehe 20 Oktoba mwaka 1990, baina ya Arsenal dhidi ya Manchester United, ambapo timu ya Arsenal ilishinda kwa goli moja, wachezaji walichapana makonde hatari sana kisa tu Nigel Winterburn alipomshambulia Denis Irwin basi wachezaji wa Manchester United wakaona sio vyema kukaa kinyonge nao wakajumuika kuwashambulia wachezaji wa Arsenal.

3. Spain dhidi ya Portugal


Nikurudishe nyuma kidogo mpaka Bondeni kule kwa Mzee Madiba katika kipindi cha Kombe la Dunia la mwaka 2010, kwenye mechi kati ya Uhispania dhidi ya Ureno kwenye hatua ya 16 bora, nyasi za uwanja wa Green Point Stadium pale kwenye Jiji la Cape Town ziliwaka moto kweli kweli, huku mlinda mlango wa Uhispania, gwiji Iker Casillas akionesha ufundi wake wa kuzuia nyavu za Uhispania zisiguswe kabsa na Wareno.


Uhispania akaondoka kwenye uwanja wa Green Point Stadium akichekelea na baraka juu juu mpaka kwenda kuchukua Kombe la Dunia mbele ya Uholanzi, hivyo wakawa wamelipiza kisasi kwani kwenye michuano ya Uero mwaka 2004, Ureno alimchakaza vibaya sana Uhispania.

4. Chelsea dhidi ya Arsenal


Majabari wakubwa ndani ya Soka la Uingereza, wababe wawili ndani ya Jiji la London, ukiachana na Tottenham ila hawa wawili wanabakia kuleta mpira bora sana kwenye viunga vya London, huku Chelsea akionesha ubabe sana kuanzia Mwanzoni mwa miaka ya 2000 mbele ya Arsenal. Lakini aliyeleta mgogoro mkubwa ni Ashley Cole ambaye alinaswa akiwa kwenye mkutano na viongozi wa timu ya Chelsea miezi kadhaa kabla ya kukamilisha uhamisho wake kutoka viunga vya Emirates na kwenda Stamford Bridge.


Nakumbuka vyema sana ile fainali ya kombe la Ligi ya mwaka 2007 baina yao, ambapo tulishuhudia John Terry akipigwa kichwani, huku Emmanuel Adebayor akipewa kadi nyekundu na kutolewa nje, kisha Frank Lampard kutaka kuzichapa na Cesc Fabregas huku mashabiki wa Chelsea wakiwatusi sana pamoja na kuwarushia chupa za maji wachezaji wa Arsenal.

5. Denmark dhidi ya Sweden


Tuondoke Uingereza na tusongee mpaka pale Scandinavia ambapo tunakutana na timu mbili za taifa, ambazo zimekuwa zikikutana kwa miaka takribani 100, hawa ni Denmark na Sweden lakini mechi zao za hivi karibu kuanzia miaka ya 2000 ndio zimeongeza sana uhamasa mkubwa baina ya mashabiki.


Kwenye kufuzu michuano ya Euro mwaka 2008, wawili hawa walipangwa kundi moja, timu ya Taifa ya Sweden walishinda goli tatu kwa sifuri huko Copenhagen, lakini waliporudiana Denmark alipambana sana na kufanya matokeo yawe 3 kwa 3, kabla ya mwamuzi kuwapatia Penalti Sweden, Penalti ambayo ilileta kizaazaa, basi kuna mshabiki mmoja alitoka Jukwaani na kuingia uwanja kwenda kumpiga mwamuzi, ingawa Denmark hakufanikiwa kufuzu kwenda michuano ya Euro ya mwaka 2008, walilipiza kisasi kwa kumzuia Sweden asiende kwenye michuano ya Kombe la Dunia ya mwaka 2010.

Je kwako wewe umeipenda derby ipi dunia mpaka sasa? Derby ambayo upo radhi kulala usiku ili tu upate kuitazama?
 

Attachments

  • IMG_1708.jpg
    IMG_1708.jpg
    42.1 KB · Views: 5
  • IMG_1709.jpg
    IMG_1709.jpg
    106.7 KB · Views: 5
  • IMG_1710.jpg
    IMG_1710.jpg
    45.4 KB · Views: 6
  • IMG_1711.jpg
    IMG_1711.jpg
    67.6 KB · Views: 5
  • IMG_1712.jpg
    IMG_1712.jpg
    57.8 KB · Views: 6
  • IMG_1713.jpg
    IMG_1713.jpg
    40.4 KB · Views: 5
  • IMG_1714.jpg
    IMG_1714.jpg
    108 KB · Views: 5
  • IMG_1715.jpg
    IMG_1715.jpg
    31.6 KB · Views: 5
  • IMG_1716.jpg
    IMG_1716.jpg
    55.3 KB · Views: 4
  • IMG_1717.jpg
    IMG_1717.jpg
    19.4 KB · Views: 5
  • IMG_1718.jpg
    IMG_1718.jpg
    57.3 KB · Views: 5
  • IMG_1719.jpg
    IMG_1719.jpg
    74.4 KB · Views: 4
  • IMG_1732.jpg
    IMG_1732.jpg
    57.3 KB · Views: 4
  • IMG_1733.jpg
    IMG_1733.jpg
    49.3 KB · Views: 5
Derby ni moja tu duniani. Boca juniors vs River plate football. Partizan Belgrade vs Crevna Zvezda basketball. Nyingine ni mbwembwe na uwongo wa mitandaoni.

Hao jamaa sijui wana matatizo gani
 
1, River Plate vs Boca Junior's
2, Orlando Pirates vs Kaizer Chiefs
3, Liverpool vs Manchester United
4, Espanyol vs Fc Barcelona
5, Partizan vs Svena Zvelda
6, Spartak Moscow vs CSKA Moscow
7, As Roma vs Lazio
8, Galatasalay vs Besiktas
9, Al Ahly vs Zamalek
10, Simba vs Young African
 
1, River Plate vs Boca Junior's
2, Orlando Pirates vs Kaizer Chiefs
3, Liverpool vs Manchester United
4, Espanyol vs Fc Barcelona
5, Partizan vs Svena Zvelda
6, Spartak Moscow vs CSKA Moscow
7, As Roma vs Lazio
8, Galatasalay vs Besiktas
9, Al Ahly vs Zamalek
10, Simba vs Young African

Barcelona vs Real Madrid
 
Nilivyosoma tu heading nikategemea kukutana na mechi kati ya Boca Junior na River Plate lakini wapi. Hii ndio namba moja duniani
 
Chelsea vs Liverpool siku hizi game inadharaulika sana.

Banda umiza wanaandika pwagu vs pwaguzi!
 
Back
Top Bottom