Elections 2010 Miongozo ya kidini ya uchaguzi ruksa

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,316
33,125
MIONGOZO iliyotolewa na madhehebu ya dini za Kiislamu na Kikristo nchini kuhusu uchaguzi mkuu, haina matatizo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Philip Marmo amesema.

Pia amesema Rais Jakaya Kikwete, ameamua kukutana na viongozi wa dini kwa kinachoelezwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kuwa ni sehemu ya kutoa elimu ya wapiga kura.

Rais Kikwete amepangiwa kukutana na viongozi wa dini kesho; lakini kabla ya mkutano huo, leo viongozi hao wa dini ambao idadi yao ni zaidi ya 60 watahudhuria semina maalumu yenye lengo la kujadili sheria za uchaguzi.

Serikali imetangaza rasmi kubariki nyaraka mbalimbali zilizotolewa na wanataaluma wa Kanisa Katoliki na Mwongozo uliotolewa na baadhi ya waumini wa Kiislamu, kuwa hazina matatizo kwani zililenga kutoa elimu kwa waumini.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Phillip Marmo, akizungumza jana Dar es Salaam, alisema kabla ya viongozi hao kukutana na Rais kesho, leo watapigwa msasa wa sheria ya rushwa ambayo itatolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah.

Sheria ya Gharama za Uchaguzi ni mada nyingine watakayojifunza viongozi hao na itakayotolewa na Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa.

Taratibu na sheria ya uchaguzi ni mada itakayotolewa na Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Rajab Kiravu. Marmo alisema Serikali imeamua kutoa elimu ya wapiga kura kwa viongozi hao wa dini kutokana na kuwa na ushawishi mkubwa kwa waumini wao, na kuwa na wafuasi wengi ambao wanashiriki kupiga kura.

Viongozi watakaohudhuria semina hiyo ni maaskofu 25 kutoka Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), mashehe 17 kutoka Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), maaskofu 10 kutoka Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) na viongozi wengine 10 kutoka madhehebu ambayo hayako kwenye umoja huo.

Awali Marmo alisema mkutano huo utakuwa wa ndani na waandishi wa habari wataruhusiwa tu wakati wa ufunguzi na ufungaji, lakini baada ya kuulizwa swali kwa nini elimu ya uraia kwa viongozi wa dini uwe mkutano wa ndani alijibu: “Sijasema kama mkutano huo utakuwa wa ndani, yote yatajulikana leo na itategemea na waandaaji wenyewe.”

Aliulizwa sababu ya Serikali kuamua kuwapa semina viongozi wa dini katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu na kama haoni hatua hiyo inaweza kulalamikiwa na wadau wengine wa demokrasia, alisema mkutano huo hauna lengo la kuwashawishi viongozi hao waiunge mkono CCM.

Rais Kikwete anakutana na viongozi wa dini wakati kukiwa na mvutano na kusigana kati ya viongozi hao na Serikali yenyewe katika mambo kadhaa.

Miongoni mwa mambo hayo ni Ilani ya Uchaguzi iliyotolewa na Kanisa Katoliki na Mwongozo uliotolewa na taasisi za dini ya Kiislamu.

Kiongozi mkongwe serikalini, Kingunge Ngombale-Mwiru, alitoa shutuma nzito kwa Kanisa Katoliki kuwa linachukua mamlaka ya chama cha siasa kwa kutunga Ilani ya Uchaguzi, kwani kazi hiyo hufanywa na chama cha siasa.

Kanisa Katoliki lilitoa waraka na kuufafanua kuwa lengo lake ni kufundisha waumini wake na kuwaelimisha namna ya kupata viongozi bora na kwamba viongozi hao watapatikana kutokana na uwezo wao si kwa kutoa rushwa.

"Viongozi wasio na uwezo ndio wanaotumia nguvu kubwa (rushwa) kupata nafasi za kuingia madarakani, ambapo badala ya kulitumikia Taifa, wanafikiria kujilimbikizia mali ili kufidia gharama walizotumia wakati wa uchaguzi, hivyo tuwe makini nao," ilisema sehemu ya Ilani hiyo.

Baada ya Ilani, Waislamu nao walitoa Mwongozo kwa ajili ya kuandaa waumini wake. Kwenye Waraka huo waumini wa dini ya Kiislamu wametakiwa kuchagua viongozi ambao wana maslahi na Waislamu.

Wakati wa uzinduzi wa Mwongozo huo kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam, kiongozi wa kutetea haki za Waislamu Shehe Ponda Issa Ponda, alisema: “Tunataka kuwaandaa Waislamu waingie kama kundi wakati wa kupiga kura kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, tunataka wapige kura yenye maslahi kwao."

Alipoulizwa kama hatua hiyo itakidhi matakwa ya sheria za nchi, na hususan Katiba ya Tanzania, Shehe Ponda bila kusita alisema: "Katika vigezo hivyo kumeainishwa sifa mbalimbali za kiongozi bora mwenye maslahi na Waislamu, lakini kwa kuzingatia sheria za nchi."

Marmo alipoulizwa kama kwenye kikao hicho wataomba madhehebu yaliyotoa nyaraka hizo kuzifuta, alijibu, “zile nyaraka zote hazina matatizo kwani zimetolewa na viongozi werevu na wenye busara na lengo lake lilikuwa ni kutoa elimu ya uraia.”

Eneo lingine ambalo Serikali huenda ikabanwa na viongozi wa dini ya Kiislamu ni suala linalohusu Mahakama ya Kadhi na suala la kujiunga kwenye Jumuiya ya Waislamu (OIC).

Marmo hakutaka kulizungumzia suala la Mahakama ya Kadhi kwa maelezo kuwa linashughulikiwa na Tume ya Kurekebisha Sheria, hivyo haoni sababu ya kulizungumzia.

CCM katika Ilani yake ya mwaka 2005, ilieleza kuwa ingelipatia ufumbuzi suala la kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi Tanzania Bara jambo ambalo halijatekelezwa, hivyo waumini wa dini ya Kiislamu kulidai kwa nguvu.

Suala la OIC nalo limewahi kupata upinzani kutoka kwa kundi la Wakristo licha ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, kutangaza kuwa Serikali haina pingamizi juu ya hilo. Suala hilo pia linadaiwa na waumini wa dini ya Kiislamu.

http://www.habarileo.co.tz/kitaifa/?n=7423
 
Sasa Kingunge Ngombale Mwiru alitumwa na nani kuwashambulia wakatoliki? au alitumwa kutikisa kiberiti kuona kama kimejaa au la?
 
Sasa Kingunge Ngombale Mwiru alitumwa na nani kuwashambulia wakatoliki? au alitumwa kutikisa kiberiti kuona kama kimejaa au la?
Naona wameamua 'kukimvua nguo' hicho kizee!
 
Back
Top Bottom