Mheshimiwa rais, hatudanganyiki tena!

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,419
21,254
Mheshimiwa rais, hatudanganyiki tena!
ban.kalamu.jpg


Samson Mwigamba

amka2.gif

MHESHIMIWA Rais wa Jamhuri ya wa Wadanyanyika, salaam! Awali ya yote naomba uniwie radhi kwa kutoanza na kile kifupisho cha ‘Dk’ cha kupewa kwa heshima.
Hii ni kwa sababu niliwahi kukichambua huko nyuma na sikuona ‘ustahili’ wake na ndipo nikaweka nadhiri ya kutokukitumia. Nisingependa kuvunja nadhiri hiyo kungali mapema kiasi hiki. Hivyo natumaini utanivumilia.
Mheshimiwa rais, nimepokea ujumbe mfupi wa maandishi katika simu ya mkononi kutoka kwa msomaji wangu. Ujumbe ulikuwa mfupi tu uliokwenda moja kwa moja kwenye lengo.
Kwa kifupi ujumbe (baada ya kuuhariri) ulisema hivi: “Umemsikia JK akijinadi, eti akipewa miaka mitano mingine atajaza vijana kwenye Baraza la Mawaziri! Washtue wadanganyika tuepuke balaa hiyo!”
Mheshimiwa, kwanza nilipata shida kujua kwamba JK ni nani. Lakini baadaye nikajiuliza mbona mara kwa mara vyombo vya habari vikiandika JK huwa vinaandika habari zinazomhusu mheshimiwa? Nikasema labda ni yeye.
Kuna wakati nilipata kumpigia simu msomaji yule, kwa bahati mbaya nikasahau kumuuliza JK ni nani. Lakini, nilimuuliza kapata wapi hizo habari, akaniambia alikuwa akisikiliza dondoo za magazeti asubuhi ya Jumatatu ya wiki hii akasikia habari hiyo.
Kama ni kweli JK ni wewe mheshimiwa, na kama kweli ulisema hayo, naomba nikuambie kwamba safari hii ‘hatudanganyiki’! Na uthabiti wa kauli hii mara moja unajionyesha kwenye kitendo cha kijana yule kusikia tu hiyo habari akanitumia ujumbe mfupi tena akaniambia ujumbe huo aliutuma hata kwa Mwalimu Mkuu wa Watu, yule mwananchi wako mnyonge anayekupenda ambaye kila akiandika hawezi kuanza bila kukuita kwa heshima “rais wangu”.
Mwaka 2005 ulikuja na mbinu, mbinu ya kujitambulisha kama kijana miongoni mwa wagombea 10 waliokuwa wakitafuta fursa mbele ya wadanganyika ya kuingia ‘patakatifu’ pa dunia ya wadanganyika.
Mahali ambapo ukishafika huwezi tena kuulizia bei ya sukari, bei ya nyama, nauli ya mabasi yaendayo mikoani, siku za usafiri wa treni ya reli ya Kati na TAZARA.
Huwezi tena kujua foleni ya barabara za Dar es Salaam wala kushuhudia jinsi Bajaj zilizotengenezwa maalumu kwa ajili ya ndugu zetu walemavu zilivyogeuzwa teksi ndani ya jiji, na kadhalika.
Natambua kwamba miongoni mwenu kulikuwa na vijana zaidi yako ambao wewe ulikuwa hata miaka zaidi ya 10 mkubwa kuliko wao. Lakini, ukatuaminisha wadanganyika kwamba wewe ni kijana.
Kwa kaulimbiu hiyo ambayo wewe na wapambe wako mliitengeneza kwa ustadi vijana wengi hawakuhangaika hata kusoma wasifu wako ikiwa ni pamoja na kuangalia umri wako. Wakajikuta wamekumbwa na kokoro haramu kama yale anayoyapiga vita Magufuli.
Ndani ya kokoro la ‘rais kijana’ hakuna aliyeona uzee wako wala kuishtukia mbinu yako ya kujipatia kura migongoni mwa vijana. Kila aliyekuwa ndani ya kokoro hakuweza kuona nje.
Upeo wao wa kuona uliishia ndani ya kokoro na pale walipojaribu kuangalia upeo uliishia tu kuona ndani ya maji yaliyolizunguka na kulifunika kokoro. Na ilitegemea tu na kijana mwenyewe na macho yake.
Kwa vijana wa vyuo vya elimu ya juu, waliona mikopo ya elimu ya juu ikiboreshwa na rais kijana. Waliona wakimwagiwa mapesa mengi bila masharti magumu hata kama kapata udahili vyuo viwili anapata mikopo miwili. Wakashangilia na ‘kuvaa’ kijani ndani ya kumbi maarufu kama Diamond Jubilee.
Upeo wao uliishia ndani ya kokoro lililotengenezwa na matundu madogo madogo yanayozuia kuchomoka pale utakapoona unakaribia kuvunwa. Baada ya uchaguzi kawaulize vijana wa elimu ya juu leo. Kawaulize watakuambia madaraja ni nini.
Kwa mara ya kwanza chini ya rais kijana wakashangaa wanafunzi wanapewa madaraja ya kukopeshwa kwa asilimia. Kwa mara ya kwanza mitihani isiyo na ulinganifu ya kidato cha sita kikawa ni kigezo cha kupata mkopo.
Kwamba, mwenye uwezo mkubwa darasani kiasi cha kupata daraja la kwanza kwenye mtihani wa kidato cha sita na yule mwenye uwezo wa kifedha wa kuweza kununua mitihani hiyo hiyo na kupata daraja la kwanza ndio watakaokopeshwa.
Kwamba kwa mwanafunzi wa kiume aliyejitahidi kwa uaminifu na kwa uwezo wake wote akapata daraja la pili ama mtoto wa kike aliyefanya hivyo na kupata daraja la tatu, mkopo kwao hakuna.
Kwa wamachinga wa Manzese darajani, wao waliona ajira. Maskini wadanganyika!! Eti mtu ambaye hakusoma wakati hata elimu ya msingi ni shida na kazi yake ni kushinda akipayuka na sauti kukaukia kwa kuita wateja na mwisho wa siku auze nguo moja au asiuze kabisa, yeye akiwa ndani ya kokoro la rais kijana akajipa matumaini kwamba atapewa ajira.
Mgombea mmoja wa chama maarufu cha upinzani alipofika Manzese akawaambia vijana: “Hakuna cha ajira, labda kama huyo rais wenu atawachongea mikokoteni mingi ya kubeba mizigo ndiyo iwe ajira yenu.” Lakini, wapi, ndani ya kokoro hawakusikia kitu. Walimpuuza na kumwona mwendawazimu.
Wasingeweza kumsikiliza wakati walishaona wanavutwa na mvuvi kuelekea kwenye vilindi vya maji marefu ambako wataogelea na kupiga mbizi bila shida. Kumbe hawakujua kwamba kokoro lilikuwa linavutwa kuelekea ufukweni, mahali ambako hakuna maji na hakika watakufa.
Ndicho kilichotokea. Hapakuwa na ajira na hata zile walizokuwa wamejiajiri wakiuza angalau nguo moja ama mbili kwa siku zote zilifagiliwa kwa madai kwamba wanachafua jiji.
Ndiyo! Wapiga kura wenye kuheshimika mwaka 2005 ambao walipata kukaribishwa ndani ya ukumbi mkubwa wa Diamond Jubilee tena kwa heshima na kubebembelezwa, ghafla 2006 wanageuka uchafu unaochafua jiji. Wakaanza kufukuzana na mgambo wa jiji utadhani paka na panya!
Ndani ya kokoro pia kulikuwa na vijana wengi wenye elimu mbalimbali kuanzia kidato cha nne, kidato cha sita, cheti, stashahada na hata shahada, waliohitimu elimu zao na kukaa nyumbani huku wakisaga soli za viatu kila siku kwenda huku na kule kusaka nafasi ya kazi.
Hawa waliposikia ngonjera za rais kijana na nafasi zake za ajira milioni moja, nao wakakurupuka na kuingia ndani ya kokoro. Wakaingia wakiwa na matumaini makubwa. Walitarajia kuajiriwa viwandani, kwenye migodi, kwenye mashirika ya umma, kwenye taasisi za serikali kama Benki Kuu na kwenye serikali yenyewe!
Yarabi! Walijikuta wako nchi kavu. Vilindi vya maji wanaviona kwa mbali sana. Wakiwa nje ya maji wakihema hema na kuvuta pumzi yao ya mwisho wanaona kundi kubwa la ‘samaki’ linaloitwa ‘wanamtandao’ likipiga mbizi kwa furaha ndani ya bahari.
Walikuwa wakiogelea kwenye utajiri wa ‘maji’ tele usio kifani. Ni mkusanyiko wa ‘maji’ mengi ndani ya ‘bahari’ yanayoingia kutokana na ‘mito’ mingi. Waliona mto EPA ukitiririsha maji mengi kwa mbali huku wao wakiwa hawana hata pumzi ya kujivuta kuusogelea mto huo.
Kwa upande mwingine waliona mto Deep Green Finance na ndipo walipogeuka huku na kule waliona mito mingine mingi kama IPTL, Meremeta pamoja na mito mipya ya Richmond, vitambulisho vya taifa na kadhalika. Vyote hivi vilikuwa ni kwa ajili ya wateule wachache 144 elfu wa kutoka makabila 12 ya mtandao.
Vijana, nisikilizeni vizuri. Hatujapata rais kijana wala hatujapata rais anayewajali vijana. Tumekuwa tunapata marais wanaowabeba vijana wakati wa kampeni na kuchota kura zao kisha kuwatupa mitaani wakalelewe kama watoto wa mitaani.
Rais kijana ambaye anawajali vijana angeonekana hata katika chama chake. Ni chama kimoja tu ambacho nimekiona kikiwaweka vijana mbele na kuwapatia madaraka makubwa ndani ya chama na ndani ya taasisi nyeti kama Bunge.
Hicho ndicho chama ambacho hata kama kingesimamisha mzee kugombea urais bado ningekuwa na imani kwamba kitawapa kipaumbele vijana. Ni chama ambacho hata wewe msomaji unakijua.
Natoa wito kwa vijana wote kwamba sasa si wakati wa kudanganyika tena. Tusikubali tena kudanganyika. Kama kweli mkuu katoa kauli hiyo, ni dhahiri keshasoma upepo. Keshaona jinsi vijana tulivyoamka na jinsi tulivyodhamiria kukata mzizi wa fitina mwakani.
Kaangalia uchaguzi wa serikali za mitaa na jinsi ambavyo vijana mliamka ikawalazimu watawala kutumia gharama nyingi sana kufanya hujuma ili washinde kwa lazima. Niliwahi kuwasimulia kisa cha uchaguzi wa Mtaa wa Kijenge ndani ya Manispaa ya Arusha. Uchaguzi ambao vijana waliamua.
Wakajiandikisha kwa wingi na kusimamisha mgombea uenyekiti kijana kupitia ‘chama cha vijana’. Kijana yule akashindana na mwenyekiti mzee aliyekuwapo. Siku ya uchaguzi wakataka kucheza rafu ikashindikana baada ya kura kulingana mara tatu.
Wakataka kumtangaza mgombea wao kwamba kashinda kwa kura moja, vijana wakasimama kidete mpaka Mkurugenzi wa Manispaa akaufuta uchaguzi ule na kutangaza marudio baada ya wiki moja.
Jumapili iliyofuata nikajongea maeneo yale wakati wa jioni wakiwa wanahesabu kura. Askari walijaa na mbwa wa polisi. Lakini yalipokuja kutangazwa matokeo, kijana yule alikuwa ameshinda kwa zaidi ya kura 70.
Ndipo nilipoona vijana wakishangilia na kuinua bendera ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) juu, nikajua kumbe kijana yule ni kutoka chama hicho.
Kwa mara ya kwanza nikashuhudia vijana wa CHADEMA, wakimzuia dereva wa gari la polisi asiwashe gari. Wakalisukuma gari la polisi lililokuwa linaondoka kwa amani baada ya matokeo kutangazwa.
Nilishangaa zaidi niliposhuhudia kwa macho yangu vijana wanasukuma gari na kushangilia wakiwa wameinua bendera za CHADEMA juu huku wakionyesha alama ya vidole viwili, ghafla askari polisi ndani ya gari la polisi nao wakawa wanainua vidole viwili juu kuishangilia.
Naam! Kumbe hata askari wamechoka! Walimu wamechoka, wanajeshi nao wamechoka, maana napokea ujumbe mfupi kutoka kwa wanajeshi wengi mno. Wanafunzi wamechoka, watumishi wa umma wamechoka, madaktari na wauguzi nao wamechoka, wanataaluma nao wamechoka. Kwa nini tusiungane sasa? Tumwambie mkuu ‘hatudanganyiki tena!” Hatuhitaji baraza la mawaziri vijana wa kuendeleza ufisadi. Tutaingia madarakani na kutengeneza baraza letu la mawaziri vijana wa kukimbiza taifa kuelekea kwenye maendeleo.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom