Mfahamju balozi Job Lusinde na kisa cha kusisimua wakati wa vuguvugu la mwaka 1994

MeinKempf

JF-Expert Member
Jun 11, 2013
11,094
7,218
Balozi mzee Job Lusinde ni waziri pekee wa baraza la kwanza la mawaziri la Mwalimu Julius Nyerere mara baada ya kupata uhuru kwa sasa baada ya Sir George Kahama kufariki dunia.

Wakati Jeshi linaasi mwaka 1964 Balozi Mzee Job Lusinde ulikuwa waziri unayesimamia usalama wa taifa. Ulikuwa wapi wakati jeshi linaasi?



Jeshi lilipoasi nilikuwa nyumbani kwangu nimelala kwa sababu tukio lilifanyika usiku, bahati mbaya ofisi yangu nadhani hawakujua vizuri ingawaje pengine kulikuwa na viashiria ambavyo sisi havikutufikia vizuri. Kwa hiyo, nilikuwa nyumbani lakini mara moja polisi walikuja kunichukua ili niende ofisini kwamba hali sasa imeharibika, askari wameasi. Walikuja kunichukua wakiwa wametakiwa kufanya hivyo na mkuu wa polisi, nilichukuliwa na gari ya polisi kwenda Ikulu pale tukakuta mlango umekwishatekwa na jeshi, wakahoji, unakwenda wapo hakuna ruksa ya kuingia, nikaona hapa tusipoteze muda, nikasema sawa.

Kisha nikapata mawasiliano na Emir Mzena (Mkuu wa Usalama wa Taifa) ambaye akanieleza kwamba walipopata habari tu walikwenda kumwondoa Mwalimu Nyerere na Kawawa, akasema wamewaweka mahali salama nami sikutaka kuuliza wapi kwa sababu wasingeniambia kwa kuwa wakati ule hamuaminiani kabisa. Baada ya kutoka Ikulu (langoni) nilikwenda ofisini (wizarani) nilikuwa na risasi zangu na bunduki yangu binafsi aina ya rifle nilitoka nayo (nyumbani) kwa sababu nilijua katika suala al uasi hakuna usalama, nia yangu ilikuwa kutoka pale kwenda Ikulu ili kama kuna mapigano nilikuwa nishiriki. Nilikuwa na risasi zangu 12 ningeshiriki na nilipanga kuhakikisha ‘wanalala’ watu 12 (kila risasi itumike vizuri), lakini kama nilivyosema nilipofika Ikulu Mwalimu alikuwa amekwishaondolewa. Sasa tukatoka kwenda ofisini nikapanda juu (ghorofani) nikashindwa kutumia simu kwa kuwa zilikuwa zimekatwa mawasiliano.



Akili yangu ikaja ngoja nitoke maana mawaziri wengi wanakaa karibu karibu, niende nikawaambie msitoke ndani. Ile natoka tu, napambana na wanajeshi waliokuwa wameasi wananitafuta, kumbuka wakati ule polisi waliponifuata nyumbani wanajeshi nao walikwenda kumchukua Osacr Kambona na kwenda naye kambini jeshini, kambi ya Kolito, kule wakaanza kumweleza madai yao, sasa mimi natoka ofisini … nakutana na gari la jeshi nadhani walikuwa wameniona, nikaambiwa haya wewe nani? Sikujitambulisha. Kulikuwa pia na DCI wetu ambaye naye alikataa kujitambulisha vizuri akasema tu yeye ni mtumishi wa ndani wa Ikulu kwa hiyo akawa anapita pale wanajeshi wakawa wanajua ni mtumishi wa ndani tu, kwa hiyo baadaye nikawaambia mimi ni Waziri wa Mambo ya Ndani, Job Lusinde, oooh! wewe ndiye tunakutafuta ingia, wakaniambia mikono juu nikakataa, kuna polisi alikuwa analinda mlangoni (wizarani) akaniambia inua … inua, silaha yangu niliiacha kwenye gari, nikainua mikono lakini polisi (wa wizarani) waliona kwamba awali nilipoteremka kutoka kwenye gari niliacha bunduki humo ndani ya gari.

Sasa wameniweka kati askari huku na huku (pale Twiga hoteli ukija mashariki unaingia kwenye bookshop fulani ukija kama unakwenda bahari ilikuwa wizara ya maji sasa ule mtaa ukawa ndio wa kuingia, upande wa barabara ya sokoine ( ya katikati) wakaizuia, kwa hiyo barabara ikawa hii ya wizara ya elimu mpaka Sokoine, mahali pa kutokea ni pamoja) nikapelekwa hapo nikawakuta wengine alikuwapo mwanahabari wa Ikulu, alikuwa mzungu, mara naona balozi wa Uingereza na Marekani wapo pale, wengine siwakumbuki, tukawekwa pale.

Nikaona hapa ni tatizo, bunduki nimeacha kwenye gari, mimi nina risasi 12, sasa wakini-‘sach’ itakuwaje sina mahali pa kuzitupa, kwa hiyo sasa pale ikawa nafikiri katika hali kama ile, wakati nimekaa tumechuchumaa akaja askari mmoja, akatamka wewe nani sogea huku, fanya upesi, kaa hapo, chuchumaa, basi yule askari akaniita mjomba … mjomba. Nikamtazama ni kweli mjomba wangu, akaniuliza una bastola nikasema sina … nina risasi tu bunduki nimeacha kwingine, basi chukua hizo risasi tumbukiza pale anasema kwa kunifokea fokea, kisha akaanza kuniuliza kwa njia ya kunipeleleza, Mwalimu yuko wapi? Yuko salama? Nikasema sijui, kwa sababu nilitaka kwenda Ikulu mlinikataza, kwa hiyo mimi sijui. Akasema sisi (wanajeshi) bado tunampenda Mwalimu, yule askari alikuwa na cheo cha sajenti na ndio hao walikuwa wanachukua komandi (watoa amri) maana hata wakubwa zao waliwatia ndani, akasema mkimdhuru Mwalimu tutawaua, hatutaki kuchukua serikali, waasi wenyewe walisema mkimuua Mwalimu tutawaua, tunachotaka sisi ni africanation (jeshi lifanye la Waafrika tu wazungu waliokuwa jeshini waondolewe),akahoji mbona polisi mmewatoa (wazungu)?

Nikasema ndio hili tu mjomba? Basi tukakaa pale mpaka saa 12 alfajiri akasema wamepata simu, askari wote warudi kambini tumekwishamaliza, basi, wamemaliza kitu gani mimi sikujua. Sasa baada ya kuachiwa pale ile asubuhi nilichofanya mimi ni kurudi Ikulu, kwanza nilirudi ofisini wakaniambia bunduki ipo lakini nikaiacha, nilipofika pale Ikulu sikukuta wale askari (kwenye lango kuu). Nikaingia nikamwona mama Maria, nikamuuliza uko salama akanijibu yumo salama, nikaenda kwa mama Kawawa, Sofia, akaniambia kuna matatizo, nikajaribu simu nikabaini moja inafanya kazi, nikasema hapa hapa ndipo sasa ofisini kwangu nabaki hapa hapa, nikawapigia kwanza mawaziri wabakie ndani ya nyumba wasiondoke, wasihatarishe maisha yao, nimekaa pale nikaanza kupata imani nikaanza kuwapigia wakuu, Mzena na wengine nikawauliza mko wapi? Wakasema vijana ‘tumewamwaga’ mjini tumejipanga lakini wengi wanafanya kazi kutokea Dar Club, sasa Mzena anamjua Kambona, bahati nzuri akaja DCI akajua niko kwa Kawawa akaniletea taarifa kwamba kule wanachosema (madai ya waasi) ni hiki hiki na wako na Kambona, watakuja Ikulu.



Baadaye ni kweli walikuja wakasema wanachotaka, walipofika hawakumkuta Mwalimu, nikasema elezeni Mwalimu hayupo lakini mnachotaka nitamweleza, mnataka nini africanisation? Tutafanya hivyo, kesho tutawaondoa wazungu kwa ndege, wakataja na suala la nyongeza ya mishahara tukakubali, tukawauliza mnataka nani awe kamanda wa jeshi ili tumwondoe mzungu wakamtaja Elisha Kavana, alikuwa luteni, tukakubaliana. Kavana akatafutwa akapandishwa cheo akawa brigedia huyu alikuwa mwanafunzi wetu mimi na Kambona Shule ya Alliance, sasa kwake ikawa vigumu huku mwanajeshi huku anaasi, ana muasi mwalimu wake, akakataa wakataka kufyatua kwa risasi, akakubali, tukamwambia tupe orodha ya makamanda wako .. wale waasi wakawa wamekwishatayarisha, tukauliza nani atakuwa doctor in charge wa jeshi wakamtaja mtu ambaye tulikuwa tumesoma naye basi sasa nikasema kuna linguine? Wakajibu hakuna. Asubuhi tumekubaliana (askari wazungu) waondoke lakini tukawaomba wasidhuru familia zao, tukakubaliana kila kitu. Ilipofika saa 12 Elisha Kavana akatoa amri askari wote warudi kambini.

Lakini awali, wakati Kambona anakuja Ikulu mimi ndipo nilikamatwa nikiwa njiani sijarudi tena Ikulu (ndipo tulipopata habari huyu mtumishi anayefanya kazi Ikulu akawa anawasiliana, anakwenda kule anawasiliana na kina Mzena anarudi ananipa mimi habari, ndipo ikawa njia ya mawasiliano yetu na hata mengine wametuambia baadaye hata yule askari aliyekuwa anatulinda alisema tumekwishakubaliana mjomba) sasa tulipokuwa pale ndipo ikawa operesheni yangu kujua wenzangu wako wapi, wakaniambia tupo hapa … fujo nyingi askari wanapiga watu, baadaye kama saa nne au saa tano asubuhi askari waliondoka kambini na kuingia mjini kwa malengo ya kuweka doria lakini walipofika mjini wakakuta bia za bure na mambo megine sasa badala ya kulinda wao ndio wakaanza kuleta fujo, uporaji ukatokea na askari polisi wengi wengine nao wakajiunga katika uporaji.

Tukawa, tunafanyaje sasa? Wakati natoka Ikulu Elangwa Shaidi anatoa amri FFU waliobakia (kambini) wakae kivita wakiona askari yeyote mjini piga risasi ua, lakini ukitafakari kama wangefanya hivyo wale askari wakauawa na wengine wakarudi kambini na kujipanga upya ni lazima iwe vita, nikaamuru mimi waziri amri hiyo ifutwe, askari wote waweke silaha ghalani na wakae bila silaha kwa sababu ingekuwa vita ya wenyewe kwa wenyewe, na hata wananchi wangeingia maana walikuwa na uzalendo, hata hawa askari wengine walikuwa wanakamatwa na wananchi, nikawaambia hamna silaha wala uwezo wa kupigana na hawa wanajeshi.



Baadaye tukajitahidi tukadhibiti hali, nilikwishamwambia Kambona niko wapi naye akaniambia, sasa tunakwenda TBC kutangaza tukitoka hapo tunakwenda Airport akatuma askari kuja kunifuata pale kwa Kawawa, tukaenda wote TBC, wakati huo tumekwishampata Munanka, alikuwa ametusaidia sana kipindi kile wakurya walikuwa wengi sana jeshini hivyo alishiriki kuwatuliza, tukaenda hadi TBC kwenda kutangaza, nilikuwa mimi, Kambona na Bokhe Munanka, tukafika pale wakaanza wao kueleza kwamba matakwa yao yamekubaliwa kwa sababu wakati huo tunaongea Tabora waliasi pamoja na Nachingwea, Tabora alikuwa Sarakiya, Nachingwea sikumbuki, basi, tukamaliza pale, sasa tulipotoka hapo tukaenda Airport kusimamia wazungu waondoke, walikuwa wanakamatwa huko wanaletwa pale, anakamatwa mzungu anatumbukizwa ndani ya ndege, ilikuwa hali mbaya, lakini aliyekuwa brigedia (mkuu wa jeshi mzungu) alikwishatoroka nadhani alikwenda ubalozi wa Uingereza.

Usiku huo ukawa umepita, kesho yake tunapanga kumrudisha Mwalimu Ikulu. Awali hatukuwa tunajua sisi wengine Mwalimu yuko wapi isipokuwa wakati wa kwenda kumchukua. Mzena ndiye aliyekuwa anajua. Mwalimu na Kawawa walikuwa mahali pamoja, Kigamboni. Sasa kipindi kile ambacho Kambona yuko huko mimi niko hapa hatuna nguvu, hakuna serikali isipokuwa maaskari tu, tunafanyaje? Mimi niko peke yangu nafanya baadhi ya uamuzi na Kambona naye yuko huko anafanya baadhi ya uamuzi, bila mawasiliano.



Mwalimu hakuwa na mawasiliano na komandi, mimi nikampigia balozi wa Marekani nikamwambia hali yetu si nzuri nadhani wenzetu wa Kenya wanaweza kutusaidia akasema nilikuwa naomba waambie Kenya kama wanaweza kutuletea majeshi kutusaidia ilikuwa ni siku ya pili, unajua wazungu tena wakasema ndio, baadaye akasema message imekwishakwenda kwa Kenyatta wataleta majeshi, alipomaliza tu kusema hiyo sentensi tumeweka simu, nikawaza sasa hawa (askari wa Kenya) walikuwa wote na hawa (wa Tanzania) KAR sasa watoke huko waje kwetu wawapige rafiki zao, hawa huko walipo hawatamani haya madai ya wenzao? Nikapiga simu kwa balozi wa Marekani kumwambia hakuna haja ya kuita askari tumepooza mambo. Kasoro tu iliyotokea ni kwamba siku iliyofuata eneo la Magomeni wakati ule kulianza kuzuka vitendo vya uporaji, askari wetu wakati wanakwenda Magomeni mwarabu mmoja pale Magomeni alikuwa ndani ya nyumba yake anamiliki bunduki akaona wale askari wanakuja akaamini wanakwenda kwake na ilikuwa kama kuna vuguvugu la kupinga uarabu kwa hiyo kilichotokea akaanza kuwapiga risasi, akaua askari wanne, haa wale askari wakaja na RPG wakaifumua ile nyumba wakafa wote kasoro mtoto mdogo aliyetoka humo akiwa mweusi tii akilia, alikuwa anawafuata wale askari wakafyatua naye pia. Siku nyingine iliyofuata tukamfuata Mwalimu mimi na Kambona, aliyekuwa anatuongoza ni Mzena, ndiye aliyewapeleka huko.



Mlipofika mlimkuta Mwalimu yuko katika hali gani?

Kwanza tulipokewa na Bwimbo (askari wa Mwalimu Nyerere), akatuamuru mikono juu… ilikuwa saa nane mchana, akatuma vijana wake wakatuangalia tukajitambulisha sisi kina fulani, akaturuhusu. Tukamkuta Mwalimu kwenye kijumba, tukampa pole, alikuwa amechoka wote na Kawawa. Nakumbuka tumetoka kule tulikuwa tumenyamaza, hatukupanda kwenye feri nadhani tulizunguka sikumbuki sawasawa. Tulitumia magari binafsi, tumetoka hapo hadi tumefika Ikulu tukasema Mwalimu apumzike kidogo ingawa tulimpa taarifa za muhtasari baada ya kufika na kuweka mikakati afanye nini, ikiwamo kuhutubia taifa. Kwa hiyo maasi yakapita.



Namna gani askari wa Uingereza walifika kambi ya Jeshi ya Kolito na kuwanyang’anya silaha askari wetu?



Baada ya Mwalimu kurudi na kuhutubia taifa sasa tukakaa kutathmini (cabinet) baada ya mimi na Kambona na Munanka kumpa taarifa ya muhtasari. Baada ya hapo akaitisha cabinet akaeleza hali ilivyo kwamba vijana wamekwishatuadhiri na maaskari wanatembea tu mjini hovyo wanaambiwa watulie hakuna anayetaka, wamekuwa kama walevi wanakuja mjini bila utaratibu kwa hiyo tunafanyaje? Tuiteni nani atusaidie? Hatuna FFU wanaoweza kuwanyang’anya silaha hawa kwa hiyo kwa machungu zaidi ikabidi tukubali kwamba wanaowaweza hawa ni wale waliowafundisha … Waingereza, Waingereza walifurahi sana kuja kufanya kazi hiyo, wakati huo tukawa tumejua nini wafanye. Nadhani Mwalimu alijua, Kambona, mimi na Munanka tulijua. Walikuwa wanatakiwa kuwanyang’anya silaha na kisha tuvunje jeshi kabisa, Waingereza wakasema tunawafahamu hawa kwa hiyo wakajipanga wenyewe huko huko na meli zao (za kivita).

Unaweza kujiuliza kwa nini kulikuwa na meli za kivita kwenye eneo letu la bahari. Kwanza, kulikuwa na masilahi ya aina mbili, la kwanza ni mapinduzi ya Zanzibar na usalama wake, Marekani na Uingereza walileta meli zao, kwa hiyo wiki moja baada ya mapinduzi ndipo hayo maasi yakatokea, sasa wakaona itakuwa hali ya hatari ikabidi wabaki kufanya doria, naamini ndicho walichoamini. Lakini nadhani nao hao tuliowaita hawakuwa mbali sana na wakati tunawaondoa wale askari Waingereza wenzetu walihoji lakini mbona meli ziko hapa? Kwa nini wako hapa, waambieni waondoke askari wetu walikuwa wakitueleza.

Basi wakakubali kufanya kazi hiyo wakasema tutafanya usiku huu, tukaweka ulinzi kwa Mwalimu ili akae mahali salama zaidi, tuliwaondoa Ikulu lakini walikuwa sehemu salama Dar es Salaam. Baada ya hapo, usiku wakaanza kazi wale askari wa Uingereza, wamefanya kazi hiyo kwa mpigo Dar es Salaam, Tabora na Nachingwea, walivamia kambi hizo.

Walichofanya kwanza wakaja na brigedia yule aliyekuwa mkuu wa awali wa majeshi yetu pamoja na kijana wetu akiitwa Nyirenda ndiye aliyekuwa anakaribia cheo cha brigedia, wakaja na kikosi kidogo usiku wakawaambia walinzi pale Kolito, jisalimisheni wakakataa, walipokataa wakalipua bomu askari sita wakafa pale pale, sasa wakati hawa wamekwishawapiga wakaja kushambulia kwa mizinga mingine, hawakuwa walikuwa wakijiuliza mizinga imetoka wapi kwa hiyo wakaanza kukimbia, wakapigwa waliokimbia msituni wananchi waliwakamata. Na wakati huo huo walifanya hivyo Tabora, kule walikuta helikopta za vita zilizokuwa kwenye meli, nyinyine zikaenda Tabora nyingine Nachingwea.



Askari wetu walikuwa dhaifu kwa sababu walikuwa wanalewa. Ndipo ikawa mwisho wa jeshi letu, nchi ikaamua kuunda jeshi lake jipya, Jeshi la Wanachi wa Tanzania, swali lilikuja kwamba tunakuwaje na ulinzi kamili? Waingereza wamekwishakuja walikwua wakifanya doria mjini kama wiki hivi, tulikuwa ni kama tunatawaliwa tena na Waingereza, tukafanya uamuzi wa kuwaomba Wanaijeria waje kutoa mafunzo kwa askari wa miguu, Ethiopia waje kwa ajili ya mafunzo ya anga. Wale wote askari waasi tukawafukuza tukabaki na wachache wenye utii, na wale wengine tuliokuwa tumekwenda kuwafundisha nje ya nchi tukawarudisha.

Tukafanya uamuzi kila mtu anayekwenda kuingia kwenye vyombo vya ulinzi lazima kwanza apate mafunzo ya kijeshi kwanza iwe anakwenda magereza au popote, kuna maofisa wengine tuliwapeleka Israel kwa ajili ya mafunzo na wengine katika kambi zetu, kwa hiyo tukafanya mageuzi makubwa sana kwa upande wa polisi tukajenga chuo chao kule Moshi, Wachina walitusaidia na walipokamilisha kupata mafunzo wengine walikwenda Jeshi la Polisi na Jeshi la Magereza, na ndipo Jeshi la Polisi na Magereza wakawa kama askari wa akiba na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) likaundwa.

Lakini pia tulifanya uhakiki katika Jeshi la Polisi, tukasafisha wale waliojihusisha na uporaji wakati wa maasi. Wanajeshi wakaruhusiwa kuwa wanachama wa TANU na wana- TANU wakaruhusiwa kuwa wanajeshi, vijana wengi wa TANU Youth League tukawachukua kuingia jeshini, tukiamini wanao utii mzuri zaidi, tukaendelea hivyo mpaka tulipofika tena kuachia nafasi za kuingia jeshini ziwe huria kwamba yeyote anaweza kwenda JKT, JWTZ au polisi hapo ndipo tukaingiza wengine wasiofaa, mtoto wa kiongozi au tajiri wote wakaingia, watoto wa wakubwa nao wakaingia wakiona ni wakubwa pia, hawajali, watoto wa marafiki wakaingizwa, unakuta mwanajeshi yuko pale naye analeta ndugu zake kwa hiyo jeshi likaingiza mchanganyiko wa watu wengine wenye shaka ya uadilifu, na unajua baada ya hapo kuna majaribio ya maasi ya kijeshi yalijaribu kufanywa ingawa bila mafanikio.

Credit: Raia Mwema.
 
Ex spy yupo makini sana. Alipofika kwenye kipande cha walirudi kwa njia ipi kutoka Mwalimu walipokuwa mafichoni akasema "tulitoka lakini sikumbuki tulipita wapi"
Ahaaaaaa....
Umeshituka kitu enhee
 
good, bahati mbaya hatusomi kwenye mitaala ya elimu sijui wanaficha nn
Kirikou1,
Naomba na mimi niweke hapa katika jamvi historia ya Balozi Lusinde kama
nilivyoiandika katika kitabu cha Abdul Sykes:
1953
''...mwaka wa 1953 Nyerere alipokwenda Dodoma kuhudhuia mkutano wa Kamati ya Elimu ya Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, Nyerere alifikia kwa Hassan Suleiman mmoja wa viongozi wa TAA na Nyerere akatambulishwa kwa wazalendo wengine waliokuwa wakiondokea katika siasa kama Oscar Kambona, wakati huo akifundisha katika Kikuyu Secondary School, Nsilo Swai na Kanyama Chiume ambao wote hapo baadae walikuja kuwa mawaziri katika Tanganyika huru. Kanyama Chiume naye vilevile alikuja kuwa waziri Nyasaland (Malawi) ilipopata uhuru.

1955
Haruna Taratibu, Omari Suleimani na marafiki zake wachache waliunda kamati ndogo kisha wakaandika barua kwenda makao makuu ya TANU Dar es Salaam kuomba ruhusa ya kufungua tawi la chama. Katibu mwenezi wa TANU, wakati ule Oscar Kambona, aliwaandikia kuwaeleza kuwa Hassan Suleiman tayari alikuwa ameshaisajili TANU na ikiwa uchaguzi wa viongozi haujafanyika basi waonanena na yeye pamoja na Ali Ponda. Omari Suleiman na Haruna Taratibu hawakuridhika na majibu kutoka makao makuu ya TANU kwa hiyo walikwenda kutafuta ushauri kwa Edward Mwangosi, aliyekuwa mwanachama mkongwe wa African Association. Mwangosi aliishauri kamati ile iitishe mkutano Community Centre ili kujadili kufungua tawi la TANU, na Hassan Suleiman na Ali Ponda waalikwe kuhudhuria. Kadhalika Mwangosi aliishauri kamati ile kuwaalika walimu waliokuwa wakifundisha Kikuyu Secondary School, wengi wao wasomi kutoka Makerere kuhudhuria mkutano huo. Mwangosi aliwaambia wajumbe wa kamati ile ndogo kuwa wasomi wa Makerere walikuwa ni muhimu sana kwenye chama kwa kuwa wangetoa uongozi uliokuwa unatakiwa.


Karibu ya watu arobaini pamoja na wale wasomi wa Makerere, miongoni mwao Job Lusinde walihudhuria mkutano ule. Lusinde alikuja kuwa waziri, na Amon Nsekela, alikuja kushika nyadhifa muhimu katika serikali na vilevile kuwa balozi wa Tanzania nchini Uingereza. Hassan Suleiman na Ali Ponda hawakutokea mkutanoni. Wakati wanakusanyika kwa ajili ya mkutano, afisa wa Community Centre aliwaambia kuwa alikuwa amepokea amri kutoka kwa DC kuwa mkutano huo usifanyike. Kufuatia amri ile watu walitawanyika mara moja. Alexander Kanyamara aliyekuwa Mwafrika tajiri mjini Dodoma na rafiki wa John Rupia, wakati ule makamu wa rais wa TANU, aliwataka kuahirisha mkutano huo kwa sababu ya kutokuwepo kwa viongozi wa juu wa TAA, Hassan Suleiman na Ali Ponda. Kutokana na sababu hii na vile vitisho vya DC, mkutano uliahirishwa bila kupanga tarehe ya mkutano mwingine.

Asubuhi iliyofuata Taratibu alikamatwa na polisi na kupelekwa kwenye ofisi ya DC, (hivi sasa ofisi hiyo ni ofisi ya Waziri Mkuu). Taratibu alimkuta Hassan Suleiman pale ofisini akizungumza na DC, Bwana Smith. DC alianza kumsaili Taratibu kwa kumuuliza kama alikuwa akijua kuzungumza Kiingereza. Taratibu alijibu kuwa yeye hakusoma. Akizungumza Kiingereza Hassan Suleiman alimwambia DC kuwa yeye ndiye katibu wa TANU mjini Dodoma. DC, Bwana Smith, alimshutumu Taratibu kwa kuunda chama haramu na kwa kuitisha mkutano usio na idhini ya serikali katika Community Centre jana yake ambao ulielekea kuvuruga amani. Bila woga Taratibu alijibu kwamba yeye alikuwa na mamlaka ya kuitisha mkutano kwa sababu alikuwa mwanachama wa chama cha siasa kilichosajiliwa kihalali. Taratibu aliichomoa kadi yake ya TANU kutoka mfukoni kwake yenye rangi nyeusi na kijani na kumwonyesha DC. Bwana Smith alimuuliza Hassan Suleiman kama ikiwa na yeye pia alikuwa na kadi ya TANU. Hassan Suleiman hakuwa nayo. Hassan Suleiman na DC walizungumza Kiingereza kwa muda baada ya hapo aliwataka wote wawili kuandika maelezo yao. Baada ya kuandika maelezo yake Taratibu aliruhusiwa kurudi nyumbani. Inasadikiwa kuwa wakati ule mwanachama pekee wa TANU mjini Dodoma walikuwa Haruna Taratibu na Alexander Kanyamara ambae yeye alikata kadi yake Dar es Salaam.

Wasomi wa Makerere, ambao Mwangosi aliwaamini sana katika kuunda TANU, walipopata habari kuhusu mkasa wa Taratibu na DC, Bwana Smith, waliogopa. Waliamua kujiweka mbali kabisa na mambo ya siasa na kuendelea na kazi yao ya kufundisha. Haruna Taratibu na Omari Suleiman sasa waliamua kugeuza mbinu, waliitisha mkutano wa siri usiku nyumbani kwa Swedi bin Athumani. Mkutano huu uliamua kuwa Taratibu lazima aende makao makuu ya TANU Dar es Salaam akazungumze na Nyerere ana kwa ana kuhusu matatizo yaliyokuwa yakiikabili TANU Dodoma. Mahdi Mwinchumu aliyekuwa mwanachama wa TANU Dar es Salaam alijitolea kufuatana na Taratibu hadi makao makuu ya chama Dar es Salaam kwa kuwa alikuwa akijuana na viongozi wa TANU. Said Mussa mjumbe mwingine wa ile kamati ya siri alijitolea vilevile kufuatana na Taratibu na Mwinchumu hadi Dar es Salaam. Siku ya kuondoka Job Lusinde alikwenda stesheni ya gari moshi kuagana na ule ujumbe uliokuwa ukielekea Dar es Salaam, makao makuu ya TANU. Lusinde aliuambia ule ujumbe kuwa jamaa wa Makerere wanaunga mkono maamuzi yote yatakayoamuliwa na ile kamati ya siri...''

DrNIjpGaL-qZqZfcqbB44TA8TC5lhvae0QJjej80boqn77v0IX7NpkxdlHyd7X49sSvlpuQpRdNoSmf-w3Av-miVXaxwGF5lq_8CQbfJf95VdKW4E1uJeQz-ull-a_pGeP-fLrkpM04sACikNT3xuXLEpGdhi5j71iFmQPgxVGvEymXr6tDoY2_eB367L9UZ5Dm0I5WLdf9WE_VsdRG6_pjpV9__ihwo83JwOXUwoPV58RyP7K6dirQxdyZtDa8R0F2nDw0_foUa_DOoZJdn_TecwLzfVwJha8Fokeb_ihc2GdKwLlXAGWg3CPXOXqbmXBVAo01Bg3IwQLQZvrGe9eyoqXpCTG_N_Rpr80fcu5y_9gIsVOg7j_JeUTNaj1HXvlwL7VbnCg-wp2U85K_wNtIJ26jPfAOlovkJglLAW68XWVQgFNbfXrvdBoYTBUsqO6LUvPTr57_qkGXghXlebcxgDnqmf0o9DobzIptt19_oSoz7FuIaYCZA_xToMXX68L4ZMS5VGucnhIUBpznokgohXCbOaJACnt4APInT7DILY6eVQDLIAFRmmL4KnrFRa2I-D2MdMStKopv8GR_0RgnNwO06cxQ3-EGWVjY4WIab7npJ8sfiMg=w488-h629-no


Kushoto wa kwanza ni Ali Ponda
 
Back
Top Bottom