Missile of the Nation
JF-Expert Member
- May 24, 2018
- 16,863
- 62,390
Ndugu Membe,
Nakusalimia kwa salamu ya uzalendo.
Nichukue nafasi hii kukupa pole kwa misukosuko na mihangaiko ya kila siku ya maisha lakini pamoja na hayo nakupa pongezi tena pongezi za dhati kabisa kwa kusimama kidete kusema ukweli na kuutetea ukweli ukiwa ndani ya chama cha mapinduzi kwa ujasiri mkubwa kabisa. Katika nyakati hizi ambazo watu ndani ya chama cha mapinduzi wamejikunyata kama vifaranga vya kuku kwa uoga kwa bwana mkubwa na wapambe wake, wewe umesimama kidete kutaka utawala bora, kutaka demokrasia nchini, kutaka pasiwepo matendo ya kunyanyasa wananchi kisiasa.
Kutokana na hayo ningependa kuzungumza na wewe yafuatayo:
1: Mahasimu wako wanakuogopa, ndiyo maana wamekuchezea faulo kukutoa mchezoni
Ndugu Membe, walioko nyuma ya faulo uliyochezewa ndani ya CCM wanajua kuwa, kama mkisimama kwa vigezo vya ubora iliwemo uadilifu kwa taifa letu, kwa uzoefu wa uongozi, kwa exposure, kwa mipango mkakati ya kupambana na umasikini, kwa imani ya demokrasia pana katika nchi, kwa kuchukia rushwa, kwa utaalamu wa kuanalyse mambo mtambuka ya kinchi kisiasa, kiuchumi na kijamii na uwezo mkubwa wa diplomasia, hawa watu wanaujua uwezo wako, wanajua kuwa wewe ni tishio katika nafasi zao kwa sababu wanajua kuwa ukichukua fomu basi bwana mkubwa hana chance.
Wewe unajua vizuri tu kuwa bwana mkubwa kukalia kile kiti ni kwa sababu ya ugomvi wako wa kisiasa na mheshimiwa Lowasa, kwa hiyo aliokota dodo chini ya mnazi. Nje ya hapo mwaka 2015 mgombea kwa tiketi ya chama cha mapinduzi alikuwa ama uwe wewe au Lowasa, hilo analijua wazi na ndo maana kambi yake imejawa hofu baada ya wewe kuonyesha msimamo, wakaamua uchezewe figisu mapema kabla hujaingia uwanjani
2: Usikubali kusikiliza kelele za kukutaka ubwage manyanga
Ndugu Membe, baada ya tukio lilitokea la kufanyiwa figisu, wamejitokeza wale wanaojiita 'watoa ushauri', wanasema eti ukae kimya, usiongee, uachane na ndoto za kugombea urais. Mimi ningependa kukwambia kuwa usiwasikilize hao, hao ni watu waoga, fear mongers, hao ni quitters, hao ni appeasers wa madhalimu, hawana utofauti na Neville Chamberlain mwanasiasa wa uingereza kipindi cha vita kuu ya dunia ya pili aliyetaka Uingereza ifanye compromise fulanifulani na kiongozi wa Third Reich ya Ujerumani na kwamba Uingereza isimpinge na wala isimconfront. Laiti Winston Churchill angeusikiliza ushauri huo, huenda kule Birmingham wangekuwa wakiongea kijerumani sasa.
Ninachotaka kusema ni kwamba usisikilize kauli za hawa wanaotaka uiache azma yako adhimu ya kugombea uraisi ili uweze kuwakomboa watanzania waondokane na utawala wa kiimla, sera mbovu za kiuchumi, diplomasia inayofeli, siasa chafu za kununua watu, watu kufunguliwa kesi za uhujumu uchumi kwa sababu za kisiasa, Matumizi mabaya ya madaraka na umasikini wa kutisha.
3. Taifa linakuhitaji sana
Ndugu Membe, kama ulitaka kugombea uraisi kwa ajili yako binafsi basi achana na ndoto hiyo, ila kama kwa dhati ya moyo wako kwa ndani kabisa unadhani kwa dhati kabisa kuwa unataka kugombea uraisi kwa ajili ya wananchi wa Tanzania, kwa ajili ya kutengeneza serikali inayoheshimu Katiba, kwa ajili ya kutengeneza serikali inayoheshimu haki za watu wake kwamba wananchi wana haki za kuchagua viongozi wao bila kulazimishiwa kama tulivyoshuhudia katika uchaguzi feki wa serikali za mitaa uliopita.
Kama unaamini katika umoja na mshikamano wa kitaifa kuwa nchi hii ni yetu sote na kwamba kuwa na mawazo mbadala wa mawazo ya kisiasa siyo dhambi, kama unaguswa na umasikini wa watu wetu na unaamini kabisa katika kuheshimu bunge na mahakama bila kuziingilia basi Taifa linakuhitaji sana. Na kutokana na kwamba wewe tangu ukiwa kijana ulikula viapo vizitovizito vya kuitumikia nchi yetu kwa vipahi na akili zako zote, basi nakuomba sana mheshimiwa Membe uendeleze azma yako ya kugombea Uraisi ili uweze kutumia vipawa vyako vikubwa kuinusuru nchi kutoka katika hii free fall tunayoishuhudia inayoipeleka nchi katika shimo refu lenye kiza kinene
4: Uraisi hutoka kwa Mungu, usiache kuutafuta
Ndugu Membe, Mungu akitaka kukupa uraisi anaweza kukupa ukiwa ndani ya CCM au nje ya CCM.
Kwa hiyo usiache nia yako na azma yako njema kabisa ya kugombea uraisi eti kwa sababu mahasimu wako wamekuchezea faulo, kikubwa ni kuwa unapaswa kuutaka uraisi, unapaswa kuutafuta uraisi na unapaswa kuhakikisha hubwagi manyanga chini. Kama unavyojua, vitu vyenye thamani vinahitaji juhudi na kutokata tamaa, basi nakushauri uendelee kuutafuta uraisi hata nje ya CCM kwa ajili ya kulinusuru Taifa letu. Taifa letu liko njia panda, unaliachaje achaje?. Kama ipo ipo tu.
5. Wamekutosa kwenye Tanga, Piga mbizi kapande Jingine
Mahasimu wako wamekutosa baharini kwa sababu unautaka unahodha, wasichojua masikini ni kwamba wewe ndiye unayeijua njia bora, nahodha wanayempigania anawapeleka kwenye mkondo bahari ambapo wasipokuwa makini chombo chao kitapigwa dafrao na kuzama. Laiti wangalijua.
Ndugu Membe, wewe una uzoefu wa zaidi ya miaka 45 kwenye bahari ya uongozi, umeona mengi, unajua mengi, wamekutosa lakini kupiga mbizi unajua. Sasa ni wakati wa kupiga mbizi kuliwahi Tanga jingine la watu wanaojitambua ili kwalo uweze kushirikiana ili safari iendelee salama salmini.
6. Unao uungwaji mkono
Ndugu Membe, kutokana na hali ya kinchi na kutokana na ujasiri wako wa kusimama kidete na kusema pale wengine walipoufyata, umejipatia heshima kubwa mbele ya umma. Kutokana na hilo rightfully umejikusanyia mtaji wa imani ya wananchi mkubwa sana. Na napenda nikwambie, kama utaamua kusimama kidete na kugombea, nchi hii itazizima!. Watu wamechoka kaka, watu wanaugulia maumivu braza. Njoo waziwazi utangaze nia uone nchi itakavyozizima!. Sasa hivi wananchi wanasubiri mtu mzito, jasiri wa kujitokeza na kutamka kuwa yuko tayari kusimama kwenye uchaguzi kumng'oa huyu bwana.
7. Aluta continua victory Asceta
Mwisho nimalizie, kwa kauli ya mwanaharakati aliyepotea, ndugu Ben Saanane, aliyekuwa akipenda kuitumia, akimaanisha victory is certain, na mimi napenda kukwambia, Ushindi upo basi utafute
2020 Twende na Membe
Ni mimi Missile of the Nation (Kombora hatari kabisa la Ulinzi wa Taifa)