Ndugu Zangu,
Kwanza kabisa , niweke wazi, kwamba kwa staili yangu nilichokoza kwa makusudi mjadala ili kutengeneza mwelekeo wa mjadala ambao ungetusaidia kuyafanya mawili haya;
Mosi, kuumiza vichwa vyetu kujadili nini haswa maana ya mdahalo na hususan mdahalo wenye kuhusu masuala ya msingi ya kitaifa. Kufanya kazi ya kuitafuta tofauti ya kimsingi kati ya mdahalo na mahojiano. Hilo nilijaribu kuliandika kwa msisitizo katika majibu yangu katika baadhi ya posti zenu.
Pili, nilitarajia, baada ya kukaikamilisha kazi hiyo ya kwanza, wengi wetu tungejikita kwenye kujadili issues zilizozungumwa na Dr Slaa usiku ule wa Jumamosi. Nilishangaa, kuwa wengi wakaelekea kwenye kuniachia mimi niifanye kazi hiyo. Sikufanya hivyo, kwa makusudi kabisa. Ningefanya hivyo, mjadala huu ungemalizika jana usiku kwa watu kuandika thanks zao. Tusingejifunza mengi.
Tukija kwenye issues, Dr Slaa alipata fursa nzuri sana ya kujieleza. ( Niligusia hilo kwenye moja ya majibu yangu ya posti ). Hata hivyo, kwa mtazamo wangu, Dr Slaa angefanya vema zaidi kama angepambanishwa na mtu kama Profesa Lipumba. Na hapo, umma ungeweza kumpa alama za ziada. Na laiti JK naye angeingiza timu, basi, tungeshuhudia mdahalo wa karne kati ya Profesa Lipumba, Jakaya Kikwete , Dr Slaa na akina Hashim Rungwe na wenzake. Ni katika hali kama hizo, wapiga kura tunasaidiwa kupeperusha pumba na kubaki na mchele. Niliandika, kuwa ni mkakati wa kimakosa kwa CCM kuamua kutoshiriki midahalo. Maana, huko twendako wataihitaji na kuna watakaowashangaa watakapoonyesha hitaji hilo.
Sababu kubwa ya kuwepo walau wagombea wawili kwenye mdahalo ni ukweli, kuwa wapiga kura tungepata fursa ya kusikia sera mbili tofauti au majibu mawili tofauti kwa swali moja. Hapo, tungeweza kujua nani bora zaidi.
Format ya maswali ingekuwa ni yale maswali magumu yanayohusu most controversial issues of our time. Issues kama uharibifu wa mazingira, ufisadi, mikataba mikubwa ya uwekezaji,. Rasilimali za nchi kama madini, Uongozi bora na maadili ya viongozi( Tuna mfano wa Rais aliyefungua kampuni binafsi na kwa kutumia anwani ya Ikulu)
Tuna issues kama za kuwepo au kutokuwepo kwa wagombea binafsi, Katiba, Uraia wa nchi mbili, upigaji kura kwa Watanzania walio nje, mishahara ya Wafanyakazi, nafasi ya wakulima katika uchumi wan chi (Kilimo kwanza), maradhi (UKIMWI na Malaria). Bila kusahau Kushuka kwa elimu na utitiri wa international schools na academies zilizo chini ya viwango. Na mengineyo mengi.
Kuna pia maswali ambayo hayakuulizwa usiku ule. Moja ni hili la itikadi. Mathalan, Dr Slaa na CHADEMA wanasimama katika itikadi gani kwa sasa katika kutekeleza sera zao? Na kama Jakaya Kikwete, Profesa Lipumba na wengine wangekuwapo, nao wangeulizwa swali hilo.
Mwisho, nasikitika kuwa huenda wagombea wengine wa Urais mbali ya Profesa Lipumba , hawatapata nafasi ya kufanya mahojiano kama wenzao wa CHADEMA, CUF na labda CCM. Nafikiri hawatendewi haki akina Hashim Rungwe , Kuga Mziray na mwenzao Muta wa TLP kama nao hawatapata hata robo saa tu ya mahojiano.
Huko twendako, tuwe na matayarisho ya mapema ya midahalo ya kitaifa inapofikia wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu au masuala mengine makubwa ya kitaifa, kama vile Katiba mpya. Kuwepo na taasisi huru na zenye kuaminika na umma zitakazoratibu midahalo hiyo. Kuwepo na kalenda ya midahalo. Mgombea atakayeshindwa kuhudhuria katika tarehe husika ilihali amepewa mwaliko, basi, huyo itakuwa imekula kwake kama wanavyosema mitaani siku hizi.
Nihitimishe kwa kuwashukuru nyote. Nimesoma kila kilichoingizwa kwenye mjadala huu. Kuna mlionishambulia kwa matusi, nimeyasoma matusi yenu, mengine yamenivunja mbavu. Kuna mliotoka nje ya mada na kunishambulia mimi binafsi badala ya kuikabili hoja iliyowasilishwa. Hilo nalo ni pungufu la kawaida. Na kwa kuchokoza mjadala huu kuna wanaojisikia nimewakwaza, basi, haikuwa dhamira yangu. Sijaufunga mjadala.
Ahsanteni Sana.
Iringa,
Jumatatu, Oktoba, 25, 2010