Mbunge John Mnyika amezindua huduma ya kutoa Msaada wa Bure wa Kisheria kwa wakazi wa jimbo lake

Donatila

JF-Expert Member
Oct 23, 2014
7,557
21,507
13015645_1065795866800346_905132858619711790_n.jpg


Mbunge wa Jimbo la Kibamba, John Mnyika, amezindua huduma ya kutoa Msaada wa Bure wa Kisheria kwa wakazi wa jimbo lake.

Huduma hii inatolewa kwa ushirikiano wa mashirika mawili - Shirika la Universal Development Initiative (UDI) na Jopo la Wanasheria mahiri liitwalo Justice Voices Tanzania. Huduma hii ijulikanayo kama “Law on Saturday” – ‘Sheria kwa Siku ya Jumamosi’ inasukuma “upatikanaji wa haki sawa kwa wote” kwa kuhakikisha kuwa “umaskini au kuishiwa fedha” haviwi kikwazo kwa mtu kufuatilia na kupata haki yake katika vyombo vya maamuzi ya kisheria.

Inalenga wote kwa shida zote. Iwe ni migogoro ya ardhi, majengo, mirathi, ndoa, kuporwa, kudhulumiwa, kuharibiwa au kutapeliwa mali yoyote ile; iwe ni shida ya kufuatilia stahili au mafao kazini; iwe ni kutozwa gharama zisizo halali kisheria au suala lolote lile linalohitaji utaalam wa kisheria, huduma hii ipo kwaajili hiyo. Tayari wakazi wa jimbo la Kibamba wameanza kujitokeza kwa wingi kupata huduma hii.

Ni huduma endelevu yenye shughuli nyingi muhimu ndani yake. Haishii kutoa msaada wa kisheria kwa mwananchi mmoja-mmoja au vikundi pekee, bali pia kutoa elimu ya kisheria kwa viongozi wa Serikali za Mitaa na Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Kata ili kupunguza, kama si kumaliza kabisa, ukiukwaji mkubwa wa kisheria ambao umekuwa ukifanywa na viongozi hawa na kuwaumiza wananchi. Inakusudia kutoa mafunzo maalum kwa watu muafaka kutoka ndani ya jimbo la Kibamba na kusajili mtandao mpana wa watoa huduma wasaidizi wa kisheria (Paralegals) kwenye jimbo husika.

Hawa wanatarajiwa kuwa msaada mkubwa si katika kutoa usaidizi wa msingi wa kisheria tu, bali pia kufanya usuluhishi wa migogoro mingi ya wananchi ambayo si lazima ifikishwe mahakamani ndipo imalizwe. Msaada wa bure wa kisheria si suala geni duniani. Ni haki ya msingi kwa mujibu wa makubaliano na mikataba mingi ya kimataifa. Tamko la Haki za Binadamu la Kiulimwengu (1948), Mkataba wa Kimataifa juu ya Haki za Kiraia na Haki za Kisiasa (1966), na Mkataba wa Kiafrika wa Haki za Binadamu na Haki za Watu (1918), ni baadhi tu ya mikataba mingi inayosisitiza upatikanaji sawa wa haki kwa watu wote na ambayo Tanzania imeiridhia.

Hata hivyo, Tanzania iliishia kuweka kifungu cha jumla tu kwenye Katiba yake ya mwaka 1977, kwamba “watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki, bila ubaguzi wowote ule, ya kulindwa katika kupata haki mbele ya sheria”. Asiye na uwezo ameachwa ajisomee kifungu hicho kitamu kwenye katiba na kutabasamu, lakini akilazimika kujihangaikia mwenyewe kuinunua hiyo “haki sawa” kwa gharama kubwa asizoziweza, tena kwa kuchuana na mwenye pesa ndipo aipate stahili yake! Ilipasa serikali ibebe jukumu la kuhakikisha wasio na uwezo nao wanakuwa na fursa ya kufukuzia na kupata haki zao kwa mujibu wa sheria.

Kinyume chake, hadi sasa bado hakuna sheria rasmi wala jitihada za msingi za kiserikali za kuwanusuru wananchi maskini na misukosuko ya kupoteza stahili zao kwasababu tu ya udogo wa vipato vyao. Huduma za msaada wa bure wa kisheria ambazo zingeweza kuwanusuru wengi, bado zimekuwa adimu sana nchini. Wananchi wengi hawamudu gharama za kununua haki zao kupitia kwa wale Mawakili Wasomi au kupata muongozo wa kitaalam kutoka kwao.

Mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), ndiyo yamekuwa yakijaribu kutekeleza huduma za kutoa msaada wa bure wa kisheria kwa wananchi. Mashirika haya, hata hivyo, bado hayajaweza kuwafikia mamilioni ya Watanzania wenye uhitaji. Ripoti iliyopita ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), inathibitisha kuwa hadi kufikia mwaka 2014, huduma za msaada wa kisheria kupitia kituo hicho zilikuwa zimewafikia Watanzania 15, 297 tu, huku mashauri ya ardhi yakiongoza kwa asilimia 41 ya mambo yote yaliyotolewa msaada wa kisheria, asilimia 23 mashauri yahusuyo kazi, asilimia 10 mashauri ya ndoa na asilimia 5 ni mashauri yahusuyo Wosia.

Idadi hiyo ya wananchi waliofikiwa na LHRC ikijumlishwa na idadi za watu waliofikiwa na mashirika mengine machache yanayotoa huduma hizi, bado mamilioni ya Watanzania wasio na uwezo wanakuwa wameachwa katika hali mbaya sana ya kuendelea kukandamizwa, kudhulumiwa na kupoteza stahili zao kwasababu tu “Haki imekuwa bidhaa adimu na ghali mno kwao kuweza kuinunua”.

Wakati Taifa likiwa bado kwenye fungate la utumbuaji majipu, ufike wakati sasa tushughulikie na masuala mengine ya msingi na yenye umuhimu mkubwa sana katika kusukuma maendeleo. Ni kweli kuwa rushwa na ufisadi vimekwamisha kwa kiasi kikubwa na kwa muda mrefu nchi yetu kupata maendeleo, lakini bado si kweli kuwa ufisadi na rushwa vikiisha au kupungua basi maendeleo yatatujia. Jitihada za kuleta maendeleo zinapaswa kwenda mbali zaidi ya kutumbua majipu. Tunahitaji sera bora, mikakati makini na organaizesheni thabiti ya kimfumo ndipo nchi hii ipige hatua kubwa kimaendeleo. Umasikini wa nchi yetu hausababishwi tu na rushwa na ufisadi, bali pia na uwezo finyu wa kuvuna na kuzitumia vizuri na kimkakati raslimali zetu; umasikini wetu hausababishwi na uzembe na matumizi mabaya ya madaraka ya kiserikali tu, bali pia na uvivu na uzembe binafsi wa baadhi ya watu; umasikini wetu hauwezi kumalizwa kwa kubana matumizi tu ya kiserikali, bali pia kwa kuhakikisha jitihada za Mtanzania mmoja-mmoja za kujitafutia maendeleo yake hazikwamishwi na dhuluma wala na ukiukwaji mkubwa wa haki za kiraia na haki za binadamu. Kumbe, upatikanaji wa haki sawa kwa wote ni ajenda muhimu si kwa maendeleo ya mtu mmoja-mmoja tu, bali pia kwa maendeleo ya Taifa.

Natamani kuiona serikali hii ikibadilika na kushughulikia masuala mengine mengi na makubwa sana katika kusukuma maendeleo ya nchi hii. Na kwa hili la msaada wa kisheria, natamani kuiona serikali hii ikibadilika na kuurejea haraka mchakato wa kupata Katiba Mpya. Ni kwenye katiba hiyo ndipo kifungu maalum cha kutoa msaada wa bure wa kisheria kinaweza kuingizwa kama suala la lazima; na ni kutokana na katiba hiyo ndipo sheria mahsusi ya kuongoza na kusimamia vizuri utoaji wa huduma za msaada wa bure wa kisheria inaweza kukamilishwa na kuanza kutumika.

Kwa sasa, wakati tukiendelea na fungate letu la utumbuaji majipu, UDI sawa na mashirika mengine machache, ipo tayari kupanua huduma ya msaada wa kisheria. Mawakili na wanasheria wasomi mliopo facebook mnaweza kuwasiliana na UDI kwaajili hiyo, ili nanyi muweze kuingia kwenye jopo la kuwafikia kwa urahisi Watanzania wengi wasiojiweza angalau mara moja kwa wiki. Kuna nguvu katika kujitolea. Ifanyeni sadaka yenu kuu kwa Mungu kuwa ni kutumia utaalamu wenu kunusuru haki za masikini.

Nampongeza John Mnyika kwa kuendelea kuonyesha uwakilishi imara. UDI inawakaribisha wabunge, madiwani, viongozi na Mtanzania yeyote yule mwenye kiu ya kuwasaidia wananchi wenzake, si kwa kutoa msaada wa kisheria tu, bali pia kwa kuibua na kutekeleza programu mbalimbali za kusukuma maendeleo ya watu kupitia UDI au mashirika mengine yenye dhamira kama hii.

Na: Edward Kinabo
 
View attachment 340986

Mbunge wa Jimbo la Kibamba, John Mnyika, amezindua huduma ya kutoa Msaada wa Bure wa Kisheria kwa wakazi wa jimbo lake.

Huduma hii inatolewa kwa ushirikiano wa mashirika mawili - Shirika la Universal Development Initiative (UDI) na Jopo la Wanasheria mahiri liitwalo Justice Voices Tanzania. Huduma hii ijulikanayo kama “Law on Saturday” – ‘Sheria kwa Siku ya Jumamosi’ inasukuma “upatikanaji wa haki sawa kwa wote” kwa kuhakikisha kuwa “umaskini au kuishiwa fedha” haviwi kikwazo kwa mtu kufuatilia na kupata haki yake katika vyombo vya maamuzi ya kisheria.

Inalenga wote kwa shida zote. Iwe ni migogoro ya ardhi, majengo, mirathi, ndoa, kuporwa, kudhulumiwa, kuharibiwa au kutapeliwa mali yoyote ile; iwe ni shida ya kufuatilia stahili au mafao kazini; iwe ni kutozwa gharama zisizo halali kisheria au suala lolote lile linalohitaji utaalam wa kisheria, huduma hii ipo kwaajili hiyo. Tayari wakazi wa jimbo la Kibamba wameanza kujitokeza kwa wingi kupata huduma hii.

Ni huduma endelevu yenye shughuli nyingi muhimu ndani yake. Haishii kutoa msaada wa kisheria kwa mwananchi mmoja-mmoja au vikundi pekee, bali pia kutoa elimu ya kisheria kwa viongozi wa Serikali za Mitaa na Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Kata ili kupunguza, kama si kumaliza kabisa, ukiukwaji mkubwa wa kisheria ambao umekuwa ukifanywa na viongozi hawa na kuwaumiza wananchi. Inakusudia kutoa mafunzo maalum kwa watu muafaka kutoka ndani ya jimbo la Kibamba na kusajili mtandao mpana wa watoa huduma wasaidizi wa kisheria (Paralegals) kwenye jimbo husika.

Hawa wanatarajiwa kuwa msaada mkubwa si katika kutoa usaidizi wa msingi wa kisheria tu, bali pia kufanya usuluhishi wa migogoro mingi ya wananchi ambayo si lazima ifikishwe mahakamani ndipo imalizwe. Msaada wa bure wa kisheria si suala geni duniani. Ni haki ya msingi kwa mujibu wa makubaliano na mikataba mingi ya kimataifa. Tamko la Haki za Binadamu la Kiulimwengu (1948), Mkataba wa Kimataifa juu ya Haki za Kiraia na Haki za Kisiasa (1966), na Mkataba wa Kiafrika wa Haki za Binadamu na Haki za Watu (1918), ni baadhi tu ya mikataba mingi inayosisitiza upatikanaji sawa wa haki kwa watu wote na ambayo Tanzania imeiridhia.

Hata hivyo, Tanzania iliishia kuweka kifungu cha jumla tu kwenye Katiba yake ya mwaka 1977, kwamba “watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki, bila ubaguzi wowote ule, ya kulindwa katika kupata haki mbele ya sheria”. Asiye na uwezo ameachwa ajisomee kifungu hicho kitamu kwenye katiba na kutabasamu, lakini akilazimika kujihangaikia mwenyewe kuinunua hiyo “haki sawa” kwa gharama kubwa asizoziweza, tena kwa kuchuana na mwenye pesa ndipo aipate stahili yake! Ilipasa serikali ibebe jukumu la kuhakikisha wasio na uwezo nao wanakuwa na fursa ya kufukuzia na kupata haki zao kwa mujibu wa sheria.

Kinyume chake, hadi sasa bado hakuna sheria rasmi wala jitihada za msingi za kiserikali za kuwanusuru wananchi maskini na misukosuko ya kupoteza stahili zao kwasababu tu ya udogo wa vipato vyao. Huduma za msaada wa bure wa kisheria ambazo zingeweza kuwanusuru wengi, bado zimekuwa adimu sana nchini. Wananchi wengi hawamudu gharama za kununua haki zao kupitia kwa wale Mawakili Wasomi au kupata muongozo wa kitaalam kutoka kwao.

Mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), ndiyo yamekuwa yakijaribu kutekeleza huduma za kutoa msaada wa bure wa kisheria kwa wananchi. Mashirika haya, hata hivyo, bado hayajaweza kuwafikia mamilioni ya Watanzania wenye uhitaji. Ripoti iliyopita ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), inathibitisha kuwa hadi kufikia mwaka 2014, huduma za msaada wa kisheria kupitia kituo hicho zilikuwa zimewafikia Watanzania 15, 297 tu, huku mashauri ya ardhi yakiongoza kwa asilimia 41 ya mambo yote yaliyotolewa msaada wa kisheria, asilimia 23 mashauri yahusuyo kazi, asilimia 10 mashauri ya ndoa na asilimia 5 ni mashauri yahusuyo Wosia.

Idadi hiyo ya wananchi waliofikiwa na LHRC ikijumlishwa na idadi za watu waliofikiwa na mashirika mengine machache yanayotoa huduma hizi, bado mamilioni ya Watanzania wasio na uwezo wanakuwa wameachwa katika hali mbaya sana ya kuendelea kukandamizwa, kudhulumiwa na kupoteza stahili zao kwasababu tu “Haki imekuwa bidhaa adimu na ghali mno kwao kuweza kuinunua”.

Wakati Taifa likiwa bado kwenye fungate la utumbuaji majipu, ufike wakati sasa tushughulikie na masuala mengine ya msingi na yenye umuhimu mkubwa sana katika kusukuma maendeleo. Ni kweli kuwa rushwa na ufisadi vimekwamisha kwa kiasi kikubwa na kwa muda mrefu nchi yetu kupata maendeleo, lakini bado si kweli kuwa ufisadi na rushwa vikiisha au kupungua basi maendeleo yatatujia. Jitihada za kuleta maendeleo zinapaswa kwenda mbali zaidi ya kutumbua majipu. Tunahitaji sera bora, mikakati makini na organaizesheni thabiti ya kimfumo ndipo nchi hii ipige hatua kubwa kimaendeleo. Umasikini wa nchi yetu hausababishwi tu na rushwa na ufisadi, bali pia na uwezo finyu wa kuvuna na kuzitumia vizuri na kimkakati raslimali zetu; umasikini wetu hausababishwi na uzembe na matumizi mabaya ya madaraka ya kiserikali tu, bali pia na uvivu na uzembe binafsi wa baadhi ya watu; umasikini wetu hauwezi kumalizwa kwa kubana matumizi tu ya kiserikali, bali pia kwa kuhakikisha jitihada za Mtanzania mmoja-mmoja za kujitafutia maendeleo yake hazikwamishwi na dhuluma wala na ukiukwaji mkubwa wa haki za kiraia na haki za binadamu. Kumbe, upatikanaji wa haki sawa kwa wote ni ajenda muhimu si kwa maendeleo ya mtu mmoja-mmoja tu, bali pia kwa maendeleo ya Taifa.

Natamani kuiona serikali hii ikibadilika na kushughulikia masuala mengine mengi na makubwa sana katika kusukuma maendeleo ya nchi hii. Na kwa hili la msaada wa kisheria, natamani kuiona serikali hii ikibadilika na kuurejea haraka mchakato wa kupata Katiba Mpya. Ni kwenye katiba hiyo ndipo kifungu maalum cha kutoa msaada wa bure wa kisheria kinaweza kuingizwa kama suala la lazima; na ni kutokana na katiba hiyo ndipo sheria mahsusi ya kuongoza na kusimamia vizuri utoaji wa huduma za msaada wa bure wa kisheria inaweza kukamilishwa na kuanza kutumika.

Kwa sasa, wakati tukiendelea na fungate letu la utumbuaji majipu, UDI sawa na mashirika mengine machache, ipo tayari kupanua huduma ya msaada wa kisheria. Mawakili na wanasheria wasomi mliopo facebook mnaweza kuwasiliana na UDI kwaajili hiyo, ili nanyi muweze kuingia kwenye jopo la kuwafikia kwa urahisi Watanzania wengi wasiojiweza angalau mara moja kwa wiki. Kuna nguvu katika kujitolea. Ifanyeni sadaka yenu kuu kwa Mungu kuwa ni kutumia utaalamu wenu kunusuru haki za masikini.

Nampongeza John Mnyika kwa kuendelea kuonyesha uwakilishi imara. UDI inawakaribisha wabunge, madiwani, viongozi na Mtanzania yeyote yule mwenye kiu ya kuwasaidia wananchi wenzake, si kwa kutoa msaada wa kisheria tu, bali pia kwa kuibua na kutekeleza programu mbalimbali za kusukuma maendeleo ya watu kupitia UDI au mashirika mengine yenye dhamira kama hii.

Na: Edward Kinabo
jembe mnyika nakuelewa sana..upo vizuri bro
 
Back
Top Bottom