Gazeti la mwananchi limekuja na report inayofafanua vizuri jinsi mawaziri wenye tamaa wanavyoweza kumvuruga rais aliyepo madarakani kwa kujijenga wao binafsi badala ya kumsaidia rais kutumikia wananchi.
=======
Tuanze hapa; kuna tofauti kubwa kati ya ndoto na tamaa. Mwenye kuota huwa na subira, huamini wakati wake sahihi utafika. Aliyejawa tamaa, huona zamu yake inachelewa.
Kuelekea Uchaguzi Mkuu Kenya Agosti 2022, yapo majina mawili yanatawala; Raila Odinga na William Ruto. Kuna mmoja ana ndoto, mwingine ni mwenye tamaa kubwa. Nitafafanua!
Raila ana ndoto, ndio maana mwaka hadi mwaka anagombea urais, anashindwa, lakini anabaki na subira. Ruto ana tamaa. Ikawa sababu ya kutoelewana na Rais Uhuru Kenyatta, kisa ukaribu wake na Raila.
Uhuru na Raila walipofanya maridhiano na kufanikisha Mpango wa Ujenzi wa Daraja (BBI), kwa ajili ya kuzika uhasama wa kisiasa, Ruto akakasirika. Akaona Uhuru anataka kumbeba Raila kwenye uchaguzi ujao Kenya.
Wakati Uhuru alikuwa akijitetea kuwa ukaribu wake na Raila sio wa kisiasa, bali ni kwa masilahi ya Kenya na Wakenya. Ruto hakuelewa maelezo hayo. Ni kwa sababu fikra zake zilikuwa zinawaza urais kuliko chochote.
Hapo ndipo kwenye elimu ya msingi; kwamba mtu mwenye tamaa ya urais, hata akiwa sehemu ya Serikali yenye Rais mwingine, hufanya mambo kwa ajili ya kujisafishia njia kwenda Ikulu kuliko kuitumikia nchi inavyopasa.
Huu ndio ujumbe ambao nimekusudia kumfikishia Rais Samia Suluhu Hassan. Ndani ya Serikali anayoiongoza, Baraza la Mawaziri, anaweza kuwa na maadui, ingawa hawatajipambanua mbele yake. Inawezekana akawaamini lakini watamwangusha.
Rais Samia anatakiwa kuwabaini mawaziri wenye tamaa ya urais na kuwaweka kando, kisha ajitenge nao kabisa. Hawatamsaidia yeye kama rais na taifa, bali siku zote itakuwa kujionesha ili kujisafishia njia ya kushika mpini.
Akumbuke jinsi watu walivyoshughulikiana nyakati za mwisho wa urais wa Alhaj Ali Hassan Mwinyi, vita ikawa kubwa kuelekea kumrithi Rais wa Tatu, Benjamin Mkapa, vivyo hivyo wakati wa kumpokea kijiti Rais wa Nne, Jakaya Kikwete.
Hili sio la Tanzania tu, mfano upo kwa Uhuru na Ruto, hawaelewani. Rais wa Pili wa kidemokrasia Afrika Kusini, Thabo Mbeki, alivurugana na Makamu wake, Jacob Zuma. Mbeki Rais, halafu kuna msaidizi wake anautaka urais, pakachimbika. Mbeki akalazimishwa kujiuzulu. Zuma akaingia.
Rais akiwa na msaidizi mwenye tamaa ya urais, hawezi kuwa na uaminifu wa kuitetea serikali. Machoni kwa rais anaweza kutoa kila aina ya sifa, pembeni atamponda kiongozi wake kwamba hawezi kazi.
Kipo kiburi hujengeka kwa mwenye kuusaka urais. Hujiona yeye ndiye anayeweza kazi kuliko hata aliyepo madarakani. Na kwa kawaida huwezi kumwongoza mtu anayejiona ana uwezo mkubwa kuliko wewe.
Suala la rais kufanya kazi na wapinzani wake ndani ya Serikali anayoiongoza, lipo pia kwenye kitabu cha “Team of Rivals: The Political Genius of Abraham Lincoln” – “Timu ya Wapinzani: Maarifa ya Kisiasa ya Abraham Lincoln.”
Mwanahistoria wa Marekani, Doris Kearns Goodwin, kupitia kitabu hicho, aliandika kuhusu serikali iliyoundwa na Rais wa 16 wa nchi hiyo, Abraham Lincoln, kwamba alifanya kazi na watu ambao walikuwa na ndoto ya kupata urais.
Washindani wa Lincoln wa kisiasa ambao walikuwepo kwenye Baraza la Mawaziri aliloliunda ni Waziri wa Fedha, Salmon Chase, Waziri wa Mambo ya Nje, William Seward, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Edward Bates. Hao ni kuwataja kwa uchache.
Shida kubwa kwa mawaziri wenye uchu ya urais ni kutengeneza makundi. Utakuta mpaka Serikali inapita vipindi vyenye joto kali, kisa makundi ya wasaka madaraka. Rais Samia akitaka uongozi wake usipitie joto hilo, ajitenge na asiwape nafasi wote wenye tamaa ya urais. Waliopo awatoe.
Urais hauji kwa nguvu
Uongozi huletwa na Mungu, japo jitihada hazikatazwi. Samia hakuwahi hata kujitokeza kugombea urais, lakini leo ndiye Amiri Jeshi Mkuu. Alipewa nafasi kwa kuwa mgombea mwenza, akawa Makamu wa Rais, kisha ikampendeza Mungu kumtwaa Rais John Magufuli.
Mwinyi (baba) na hata mwanawe, Hussein Mwinyi, hawakuwahi kujipambanua popote kutaka urais, lakini utulivu wao uliwezesha kupendekezwa. Hata Mkapa, hakupata kujionesha mwenye tamaa ya urais, lakini muda ulipofika aligombea na kupata. Kadhalika, Magufuli.
Kikwete, mwaka 1995, hakutaka kujitokeza kugombea urais. Alitaka kutulia na uwaziri.
Chanzo: Mwananchi
Inasikitisha pale mwandishi wa gazeti kubwa kama Mwananchi anakosa kujua na kutafiti historia kuwa 1995 JK aligombea urais na akaingia mpaka 3 bora. Kwa kumbukumbu majina yaliyopenya 3 bora ni
Jakaya Kikwete (akiwa Waziri wa Fedha)
Benjamin Mkapa (akiwa Waziri wa Sayansi na Elimu ya Juu) na
Cleopa Msuya (Akiwa Waziri Mkuu)
Benjamin Mkapa aliibuka kidedea kwenye Mkutano Mkuu na kupeperusha bendera ya CCM wakati wa Uchaguzi mkuu.
1995-2005 Jakaya Kikwete alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje na aligombea tena 2005.
Kwa wanaokumbuka, mwaka 2005 waliogombea wakipenya 3 bora ni
Jakaya Kikwete (akiwa waziri wa mambo ya nje)
Dr. Salim Ahmed Salim (huyu ndiye pekee hakuwa waziri)
Prof. Mark Mwandosya (akiwa waziri wa Usafiri na uchukuzi)
2015 Wagombea Urais wengi wanakumbuka walikuwa mawaziri na waliopenya 3 bora wawili walikuwa mawaziri wa JMT na mmoja akiwa waziri tokea Zenji.
Bila shaka ni ngumu kupima tamaa/shauku ya moyo wa mtu kuutaka Urais, japo kwa vitendo unaweza kupima kiu kwa yule anafanya kampeni mapema kama mkakati wa kutaka kurithi kiti cha Urais.
JK bila shaka aliutaka urais toka 1995 au kabla ila sidhani kama alihusika na kumkwamisha Rais wake BWM aliempa uwaziri wa mambo ya nje.
Hali kadhalika Benard Membe (akihudumu kama waziri wa mambo ya nje akiwa anagombea) aliepenya 5 bora (2015), January Makamba (aikuhudumu kama Naibu Waziri wa Sayansi na Technology) aliepenya 5 bora (2015); pamoja na kuwa na "uswahiba" na JK sidhani kama walimkwamisha kwenye kumtii boss wao ambae ni JK; bila shaka hawa walianza mapema mikakati ya chini chini hata kufikia hatua ya kupewa adhabu ya Kamati ya maadili ya Kamati Kuu ya CCM.
Changamoto anayopitia Madam President SSH ni kuupata Urais kwa "kudra za mungu" nanukuu maneno ya SSH akizungumza katika moja ya mikutano yake na wanawake.
SSH anakumbana na upepo wa watu ambao walijiandaa na 2025, ambao huenda waliogopa kufanya kampeni za chini-chini wakati wa JPM.
JPM was the Supreme President ambae bila shaka kila waziri chini yake aligwaya kumkwamisha au hata kujaribu kupenyeza "rupia" ili 2025, wajumbe wampe kura.
Kukosa "subra" ya hao waliotaka kurithi nafasi ya JPM 2025, kama wapo kwenye cabinet, bora madam SSH awatimue ili wasimharibie kama wanamharibia; na kama wako nje ya cabinet, basi madam anaweza kuzidi kujiimarisha.
Ila nadhani ni mapema sana kuanza kampeni kwani 2025 bado ni mbali na ndani ya mwaka miaka hii hatuwezi jua nini kitatokea.
Nataka kuamini Oct 2014 ni wacheche sana waliweza kudhani JPM atapeperusha bendera ya Urais kwa tiketi ya CCM;
Nataka kuamini March 17, 2020 ilikuwa haipo akilini kwa SSH kama mwaka mmoja baadae anaweza kuwa mbele ya TV kuutangazia umma na dunia kuwa boss wake ameaga dunia na yeye anajukumu la kuwa CinC.
Tuombeane kwa Mungu tuishi kwa amani, wenye shauku/tamaa iliyopitiliza wasitie utaifa wetu rehani kwa tamaa zao.
Wale wenye madaraka wawatumikie wananchi wa utii kwa boss wao Mhe. Rais na utii wa Watanzania kwa utumishi uliotukuka.
Mungu ibariki Tanzania, tuombeane uzima na afya njema.
Uchaguzi wa CCM 2022 utatupa kujua mengi kama timu za ushindi zitaanza kuandaliwa kama ilivyokuwa 2012 na 2002-2003.