Masala Gomolo:Umevunjika mfupa, njoo uponywe

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,318
33,125




umevunjika.jpg
Mmoja wa wagonjwa wake akionyesha jeraha ambalo linakaribia kupona na POP ambayo alikuja nayo.​


Na Frederick Katulanda
TIBA asilia nchini ina historia ndefu pengine ile inayolingana na historia ya maisha ya wengi.
Kwa bahati mbaya, tiba hiyo imekuwa ikibezwa kuwa siyo sahihi, dhana ambayo ilisababishwa zaidi na ujio wa wageni kutoka Ulaya na kwingineko kunako karne ya 19.

Awali,, Waafrika wengi waliitumia tiba hiyo kama sehemu ya huduma zao kutibu magonjwa mbalimbali.

Ukoloni na mwingiliano ya tamaduni mbalimbali ndizo sababu pia za mabadiliko katika tiba nchini.
Taaluma ya utabibu imepitia mabadiliko mengi kiasi kwamba kwa leo imefikia mahali pa kutumia teknolojia ya kisasa, vifaa vya gharama kubwa huku ile ya asili ikipuuzwa au hata kuachwa.

Lakini, Serikali inatambua matumizi ya tiba mbadala na ndiyo maana imeitungia sheria na kanuni ambazo zinaiongoza tiba hiyo.
Hadi sasa inakadiriwa kuwa takriban asilimia 65 ya wananchi wanatumia tiba asilia katika kukabiliana na maradhi mbalimbali yanayowakabili hasa baada ya wengine kushindwa kupona katika hospitali au tiba za kisasa.

Kwa upande wake mtaalam wa tiba ya mifupa kwa kutumia tiba asilia, Masala Gomolo (72), anaeleza kuwa amekuwa akipokea wagonjwa wengi kutoka sehemu mbalimbali nchini na hata nje ya nchi, wengi wao wakiwa wale ambao wamevunjika mifupa kwa ajali ama majanga mbalimbali.

Gomolo ambaye ni mzaliwa wa Mwakata wilayani Kahama, Shinyanga anaishi katika eneo lenye ukubwa wa ekari mbili huku eneo hilo likiwa limezungukwa na nyumba tisa na kati ya hizo nyumba tatu zikiwa ni maalum kama wodi za wagonjwa.
Mahali hapa ni hospitali maalum ya tiba asilia ya mifupa na ugonjwa wa kupooza ambako wananchi wamekuwa wakikimbilia kwa matibabu ya kuunganishwa mifupa yanafanyika kwa mafanikio.
Mtalaam huyo anaeleza kuwa wagojwa hufika kwa urahisi kutokana na kuwa eneo hilo lipo kando kidogo ya barabara kuu ya Isaka- Kahama, hivyo kuwa rahisi kwa wagonjwa kufika kwa machela ama kwa kujikongoja.

“Wagonjwa ninaowapata hapa kwangu ni wale ambao wamevinjika mifupa, wengi wanakuja na muhogo (bandeji ngumu au POP) baada ya kuwa wamehudumiwa katika hospitali za kawaida.
Wengine wanakuja kwangu na mimi naanza kuwapa tiba, ila wapo na ambao wanakuja wakiwa hawajapita kabisa hospitalini,” anaeleza.

Asili ya Tiba:
Anasema alianza kutoa tiba hii miaka 30 iliyopita baada ya kufundishwa tiba hii na baba yake mzazi, Gomolo Kumba.
Alianza kwa kufundishwa aina ya miti na namna ya kuitumia miti hiyo kwa mifupa ya miguu na mikoni au mifupa ya sehemu nyingine ya mwili.

Ingawa hataji miti hiyo, lakini anaeleza kuwa miti hiyo ni ile ya asili ambayo hupatikana porini ambayo huota kila eneo kulingana na mazingira, huchimba mizizi na mingine magome yake na kusaga kuwa ya unga hivyo huanza kutumika.

“Mgonjwa anapokuja akifika hapa kama amewekewa POP hulazimika kuitoa na kuanza kumwekea dawa, hii ni dawa kali ninapoweka siwezi kugusa kwa mikono eneo la mfupa ulipovunjika. Ninadondoshea tu dawa bila ya kugusa,” anaeleza.
Anaongeza kuwa iwapo ataweza dawa hiyo na kugusa kwa mikono, basi eneo la jeraha ama mahali ambapo mfupa umekatika pakiguswa kwa dawa, huoza.

Matibabu yake:

Kwa wagonjwa ambao wanakuja wakiwa wamevunjika mifupa ama na hawajapitia hospitali kabla ya kuanza kuwatibu cha kwanza huwapatia dawa ya kunywa ambayo huwekwa ndani ya soda aina ya Fanta ikiwa na kazi ya kuwasaidia kuwarejeshea nguvu.

Anaeleza kuwa mgonjwa ambaye huja na POP hulazimika kumwondolea ili iwe rahisi kwake kuweka dawa yake na kubainisha kuwa iwapo mgonjwa ataanza kutumia dawa yake humchukua siku saba mfupa kuunga na kama ana jehara kuwa limepona.
Mbali na kuunga mifupa, pia ameeleza kwamba amekuwa akitibu baadhi ya wagonjwa hasa waliopooza.

Ili kuweka kumbukumbu ya muda anaoanza matibabu na siku za kupona kila mgonjwa anapofika husajiliwa katika rejesta ya wagonja huku ndani akionyesha jina na mahali atokako hata na balozi wa eneo lake.

“Hii hunisaidia kuwa na kumbukumbu ya siku ya kufika kwa mgonjwa, lakini pia kujua anakotoka na iwapo anaweza kutokea jambo basi nijue pia yeye ni wa wapi na ametoka ubalozi gani na nani ninaweza kumpigia simu,” anaeleza.

Hata hivyo, shajara ya wagonjwa anayoitumia ni daftari la shajara ya ufundishaji darasani linalotumika kwa walimu wa shule za msingi.
Inaonyesha kuwa alianza kuitumia Agosti 3, 2004 huku wastani wa mwezi mmoja akiwa anasajili wagonjwa kati ya watatu hadi sita.

Kati ya Agosti 3, 2004 hadi Novemba 18, 2009 anaonyesha kupokea wagonjwa 314 ambao wengi walitibiwa mifupa iliyovunjika.

Wagonjwa waliopo

Nyumbani kwake tulikuta akiwa na wagonjwa sita ambao alikuwa akiendelea kuwatibia. Kati ya hao, mmoja alieleza kuwa alikuwa amefika siku tatu kabla akitokea Tarime, Mara.

Mgonjwa huyo, Samson Sota (21) alisema ni mzaliwa wa Tarime naye ni miongoni wa wagonjwa ambao walikuwa wakiendelea na tiba za mtaalam huyo hapo nyumbani kwake.
Akaeleza kuwa alifika hapo kwa matibabu ya kupooza kiuno na miguu.

“Mimi ni mgeni huku, ni mara yangu ya kwanza kufika hapa Kahama, sikupajua, lakini nililetwa na ndugu yangu ambaye aliponea hapa mguu wake uliovunjika baada ya kupata ajali ya gari. Mimi nimepooza kuanzia kiunoni mpaka huku miguuni siwezi kusimama wale kutembea,” anaeleza.

Anasema alianza kuugua Juni mwaka huu na alipata maumivu makali sana katika kitovu, maumivu hayo yalizidi kukomaa na kusababisha ganzi kiunoni na eneo la kiuno kujawa baridi kali.

Kutokana na hali hiyo alipelekwa Hospitali ya Wilaya ya Tarime kwa matibabu, lakini hali ilizidi kuwa mbaya na hata baada ya kupima daktari na wauguzi walimweleza kuwa hawakuwa wanaona ugonjwa hivyo baada ya vipimo walilazimika kumfanyia x-ray kuangalia tatizo zaidi ambapo pia walimueleza kuwa hawakuona kitu.

“Baada ya majibu hayo na vipimo hivyo ndugu walishauriana na kunileta hapa ambapo nimefika na kuanza matibabu, najisikia nafuu, hali yangu naona kama inaimarika kidogo kila siku. Kwa vile bado naendelea na matibabu, nahisi nitapona,” anaeleza.

Naye Machibya Bundala (13), anaeleza kuwa aliletwa hapo akiwa na POP baada ya kutolewa hiospitali. Yeye anaumwa mguu kutokana na kuvunjika kwa kushambuliwa na ng’ombe akiwa machungani huko Luhumbo Isaka.

“Sikuweza natembea, mpaka nilipowekewa POP hospitalini lakini nilipofika hapa, ilitolewa sikuweza tena kutembea mguu ulikuwa ukinuuma, lakini baada ya kutumia dawa kwa siku tano nilianza kuhisi ni kama mwenye POP kwani niliweza kutembea ingawa kwa msaada wa fimbo,” anaeleza.

Anasema Mungu amemjalia anajiona sasa akiwa amepona, lakini hawezi kutoka hapo kutokana na kuendelea na matibabu.

Wito wa DMO

Gomolo anaeleza kuwa kutokana na tiba yake amewahi kufuatwa na mganga mkuu wa wilaya akiombwa kuchukuliwa ili akafanye kazi katika hospitali ya wilaya, lengo likiwa ni kusaidia wagonjwa ambao wanapata matatizo ya kuvunjika mifupa, lakini kutokana na kutambua tabia za watu anaowahudumia, alisita kuitikia wito huo na kuamua kubaki kwake akielendelea na kutoa tiba.

“Walinifuata na kuniomba niende hospitalini wakanipe kazi lakini niwe sehemu ya kitengo cha x-ray ili inapotokea wagonjwa wanawefika na hali zai ni mbaya niwaone na kama ninaweza kuwatibu niwatibu wakiwa hapo hospitalini, sikukubali jambo hilo hii ni kutokana na ukweli kwamba nilijua iwapo ningefika hapo wagonjwa wengi wasingekuja kwa imani yao ya kukosa huduma, sasa ninapata wagonjwa kutoka Kenya, Rwanda na mikoa ya jirani.
Nikiwa hospitalini nitapokea wa hapo tu,” anaeleza na kuongeza:

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kahama, Eliza Mbwana anasema japo hili ni kweli lilitaka kufanyika, lakini lilikuwa na lengo la kumsogeza karibu ili kuifanyia utafiti tiba yake, lakini kutokana na kugoma basi hawakuwa na namna bora ya kumfanyia utafiti.

Anasema mpango huo ulikuwa ukiendeshwa na mganga mkuu wa wilaya (DMO) aliyepita, hata hivyo alisema kuna haja ya kuangalia upya mpango wa kumtambua mganga huyo kama wilaya ili kuona uwezekano wa tiba yake kusajili kama tiba asilia na kuigira safi kwa vile watu wanaikimbilia.

Pamoja na tiba asili kutumiwa na wananchi wengi, huduma hiyo imekuwa ikitolewa katika mfumo usio rasmi, hali ambayo imekuwa ikichangia na kuifanya isikubaliwe na watu wengi huku baadhi yao wakizizarau hasa wasomi na wenye imani za mapokeo yasiyo ya asili ya Afrika.

chanzo: Gazeti la Mwananchi

Utafiti zaidi na kina kuhusu tiba hii na nyingine, bado ni changamoto kubwa kwa Serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) ambalo kupitia azimio lake la Alma Ata mwaka 1978, limekuwa linazihimiza nchi mbalimbali duniani kuenzi na kuboresha tiba asilia za nchi zao, ikiwa ni sehemu ya huduma za afya ya msingi.


 
fb yaani shortly anamsifia mganga wa kienyeji huko Kahama mwenye uwezo wa hali ya juu kutibu watu waliovunjika mifupa; na anashauri serikali iwekeze ktk kuwaendeleza watu hawa kwani waweza kutoa msaada mkubwa kwa taifa. Lol, umenikumbusha mbaali mazoezi ya kusamaraiz passage!
 
Back
Top Bottom