Mapendekezo ya CUF[bara] hayana baraka za Wazanzibari?

JokaKuu

Platinum Member
Jul 31, 2006
30,441
55,018
Zanzibar kutoka nchi, Mkoa, hadi Jimbo!

Rais kuwa Gavana.

Ni mapendekezo ya Azimio la Katiba ya CUF


Na: Malik Nabwa

Kimya kingi kina mshindo mkubwa! Na ukweli ukidhihiri uongo hukaa chonjo! Nayasema haya nikiwa na dhamira nzima ya kuwa mtu mzima hasutwi lakini hufahamishwa. Pia ni ithibati kuwa lisemwalo lipo kama halipo laja na kilicho mtungini huvuuliwa na kata. Naam! Takriban wiki moja iliyopita niliandika kuhusu makala iliyoanza kwa kichwa ‘’ MAALIM SEIF ATIWE KIKUTINI?’’. Kimsingi sikusema atiwe kikutini bali nilikuwa nauliza suali tu lakini kwa bakhti mbaya wengine hawakunifahamu labda. Na kwa Mujibu wa suali langu nilitegemea sana kusikia kwa wasomaji wetu na wazalendo wote kuwa, ndio au hapana na si vyenginevyo kutokana na zile hoja zilivyofahamika na wenye fahamu zao.

Mada hii ilikuwa funzo kwangu kama muandishi na bila shaka kama si kuwa na ujasiri na umri kusonga kwa kuona mengi ningekwisha vunjika moyo kabisa kuitumikia jamii kupitia mzalendo. Nasema haya kwa mintarafu nzima ya kuwa yaliyonikuta ni ya mnazaa mkubwa na kashfa za mwana hizaya kutoka kwa wasomaji wangu na washabiki wa mzalendo. Naamini sikuwa na nia mbaya lakini nilikuwa na wasi wasi na mwenendo mzima wa Chama cha CUF kutokana na kilivyo na washabiki wake walivyo na wafuasi hadi kufikia kula ahadi ya kuimarisha Muungano ambao hata hao wana CUF wenyewe hawauoni kuwa una umuhimu na tijara kwao. Wenye busara wakasema hiyo ndio Sera ya CUF na nikawaelewa.

Defra, nakumbagana na taarifa ya CUF ikitoa taarifa kutoka kwa Naibu katibu mkuu wa chama hicho Bwana Julius Mtatiro akisema kuwa rasimu mpya ya katiba ya CUF ni kuvunja muungano na kuleta Shirikisho. Shirikisho hilo litazirejeshea nchi zote mbili hadhi zake za kuwa Jamhuri kama ilivyokuwa kabla ya muungano. Kisha Azimio hilo linaendelea kwa kusema kutakuwa na Rais mmoja tu huku nchi zote mbili zikiwa chini ya magavana. Kwa tafsiri hii Zanzibar kutakuwa na Gavana wa visiwa vya Zanzibar na bara kutakuwa na Gavana wake. Na kwa kufanya haya CUF inaona kuwa itakuwa imefikia malengo yake kama chama chenye nia ya kuwakomboa waanchi wa nchi hii.

Jicho langu halina makengeza wala sijapata maruweruwe ya kusoma. Nafahamu wazi kuwa hapa kwa haraka haraka wana CUF hili wenyewe hawataliunga mkono katika hatua za awali ijapo mwisho ikionekana watu wamekuwa wakali sana, iko silaha yao ya Zima moto (Firextinguisher). Namaanisha kuwa iwapo wanachama watalipinga hili kwa kuona hasara zake mapema kama nionavyo mimi bila kuwa makengeza, basi ataletwa kiongozi wao mkuu Seyyid Akbar Hashimiy aje kuuzima moto na atafanikiwa kwa asilimia mia moja na ushei kama alivyouzima moto wa Kibanda maiti baada ya kutangaza kumtambua Dr. Karume. Hakuna sumu isiyo na sumu yake. Akishasema Alhashimiy hili litapita na tuseme lishapita madhal Seyyid Akbar yuhai na amelitaka mwenyewe hakuna mwenye ubavu wa kulipinga.

Haya basi na iwe mzaha hili jambo likubaliwe kule bara na hata CCM na vyama vyengine vikubali lipitishwe kuwa sheria kutokana na hoja binafsi. Au tuseme CUF ishike hatamu ya nchi 2015 na ianzishe mfumo wake huu nchi nzima.Tutakuwa na shirikisho la Tanzania na magavana wetu wa nchi mbili. Nafikiri hii inapendeza sana au vijana husema ‘’imetulia eeh?’’. Tukishakuwa na magavana tunaambiwa tutashirikiana katika mambo fulani muhimu hivi bila kuleta utata kama uliopo sasa katika Muungano. Nahili sibaya naunga mkono. Na kila kitu naunga mkono kuanzia tume huru na kila lililomo katika rasimu zuri na baya.Lakini pia tuombe uhai na uzima mtoto huyu azimio akuwe vizuri na apendwe na kila mtu kuanzia CCM , CHADEMA, CUF, TLP,na wote.

Lakini hofu yangu iko hapa; azimio hili liliogharimu umayamaya wa pesa za wanyonge walipa kodi likiandikwa kwa miaka minne, ni matokeo ya ushauri na ridhaa za wananchi au ni mawazo ya waasisi wa chama tu? Kama ni kutokana na mashauri ya wanachama wote wa CUF na wananchi wapenzi wa CUF basi hakuna tatizo maana likiwa zuri watafaidika wenyewe na likiwa baya hawatakuwa na wakumlaumu. Bighairi ya hivyo, yaani iwapo ni jopo la wenye chama tu walioamua hayo, mimi sioni kuwa wazo hili ni la busara hasa tukiangalia joto lililo vifuani na vichwani mwa vijana wa Kizanzibari wa leo la kutaka utambulisho wao kamili. Utambulisho utakaowatambulisha wao kama ‘’wao’’ na sio ‘’ wao na sisi’’. Nasema hivi kwa kuwa kizazi hiki kipya kinatamani zaidi kuiona Zanzibar mpya iliyo huru na isiyo katika makucha ya Muungano na kwa fikra zangu ndio wafuasi wengi wa chama hichi wanavyotaka. Wengi ya hawa hawakuingia katika CUF kwa kuimarisha muungano bali kujikomboa na madhila yake na hali ngumu za maisha ambazo sababu kubwa ni huo muungano wenyewe kwa imani na fikra zao.

Sasa tukirudi nyuma kidogo, nilipomlaumu Maalim nakusema ana siri nzito na atiwe kikutini watu hawakunielewa hata kidogo kwa kile tunachokiita ushabiki na jazba zilizopindukia uwezo wa fikra na mawazo (Hysteric or maniacal staunch support). Tukiacha hizo jazba na mahabba ,Suali langu jee tuko tayari kweli kuifuta Jamhuri yetu na kuwa na Gavana? Kwa maana ikiwa kutakuwa na mfumo wa gavana bila shaka baraza la wawakilishi halitakuwepo na mengine mengi yaiundayo Zanzibar japo tunaambiwa kutakuwa na katiba yake, sijui,….! maana kimsingi sasa Zanzibar na Tanganyiko zitakuwa majimbo tu kama ilivyo Marekani. Mambo mengi yatabadilika na mabadiliko hayo hayatakuwa ya faida tu bali hasara yake yaweza kuwa mbaya zaidi na ya muda mrefu kupamabana nayo wakati huu ambao wengi wetu tumesharejesha matumaini yetu juu ya nchi yetu na viongozi wetu.

Nakumbuka katika baraza lililopita, Mh. Pinda alilaaniwa na kila mtu kwa kitendo chake cha kutaka Zanzibar ifutwe katika Ramani pale aliposema si nchi. Kitendo hichi kilimpelekea yeye kuitwa haini na kikafuatiwa na hatua ya CCM Zanzibar kukubali maridhiano kwa kile tunachokiita kuinusuru Zanzibar. Maridhiano hayo yameirejeshea hadhi Zanzibar kuwa nchi na kuwa na Serikali moja ya umoja wa kitaifa ambayo kwa sasa ni chaguo la wananchi wa Zanzibar. Wasiwasi wangu ni kuwa vyereje leo CUF wafikie kutoa azimio hili ambalo nionavyo laweza likarudisha tena nyuma hatuwa ya kujifufuwa na kujikomboa kwa sisi Wazanzibari na kuwa na nchi yetu yenye muruwa na mustakabali wake usio tegemezi na huko ndiko tunakotaka tufike, sasa leo hii vyereje na azimio hili?

Kwa fikra zangu Azimio hili litakuwa sawa na ule mchezo wa watoto wa chuoni (madrasa) wa kuwinda ndege na wakimpata wakamchoma. Kisha wakagawiyana kidege hicho kundi zima. Sasa wamo wanaopata kinyondo (Chinjo) yaani kijinofu kiduuchu na wale wanaongoja wapewe mwisho wakitegemea kupata kinachobesabesa lakini huishia kupata mtanda (vumba au harufu tu ) ya kidege hicho au vifupa. Nahofia kuwa tunakataa chinjo na sasa huu tunaochaguwa ni mtanda kabisa. Aheri ya kuudumisja huo muungano wa Serikali tatu kama kuifanya nchi hii iwe jimbo tu na hata si mkoa kama vile CCM ilivyotaka, huku Uzanzibari ukibaki makumbsho ya taifa. Vyovyote iwavyo, pendekezo hili la katiba laweza kuharibu kila kitu badala ya kujenga. Maana imani yangu inipavyo, kuwa na Raisi mmoja na magavana wa kila upande wa mShirikisho ni sawa na kutoka nchi mbili kwenda nchi moja kama ilivyo ilani ya CCM bara. Kumbe hii ndio Sera ya CUF pia? Yakhe sina khabari!

‘(Nabwa ajizoazoa na kunyanyuka)’ Toba sikio, yarabi stara muungu mwema, ngoja ninyanyuke nikanunue hivyo vidagaa nije nile na watoto jua lishatuwa!’

Wakatabahu

Nabwa (Jr.)
 
..sina uhakika kama wa-Zenj walishirikishwa kuandaa mapendekezo ya CUF.

..pia sina uhakika kama wabunge toka Zenj watayaunga mkono mapendekezo hayo yatakapowasilishwa bungeni.
 
Back
Top Bottom