Manispaa idara ya mazingira tendeni haki

ikipendaroho

JF-Expert Member
Jul 26, 2015
3,903
3,850
Sote tunafahamu ukweli wa kwamba Manispaa zote nchi nzima zimerudi kufanya kazi karibuni tu baada ya uchaguzi na nyengine kuchelewa zaidi hasa Manispaa za Ilala na Kinondoni kwa hapa Dar Es Salaam!

Kinachonisikitisha ni kuona watunza mazingira wengi wao kina dada katika kazi za usafi wa barabara wakiwa na vifaa duni na visivyokidhi haja kama mafagio, sare pamoja na vitendea kazi muhimu ambavyo vinalazimika kuwepo kama sheria ya afya na usalama kazini (Health and safety legislation).

Utaona kina dada hawa wanatumia ufagio ule ambao unatumika kusafishia jikoni kwa kusafishia barabara kwa urefu wa kilomita 1. Ni sawa na kumpa mtu kijiko cha chai ajaze maji kwenye ndoo ya lita 20. Hii haisababishi utendaji mbovu tu lakini pia upotevu wa muda katika kutekeleza majukumu na kwa maana hiyo fedha za walipa kodi.

Yote tisa, kilichonitia hamasa zaidi kuandika hapa ni kuona dada hawa hawapewi hifadhi ya ulinzi wa maisha yao kwa kuachiwa kufanya kazi katika mazingira mabovu kwa gharama ya maisha yao. Utaona hawa dada wanasafisha bara bara ( usiku ama mchana kweupe) ikiwa hawajavaa kabisa ama wamevaa sare zenye reflectors ambazo hazing'ai (fake).

Pia hawana cones za kuweka barabarani kutahadharisha na kuzuia gari zisiwafikie. Mbona wanaotia viraka bara bara wanapewa zana zote hizi za kujilinda? Tusiwadharau hawa watunza mazingira kwani ni watu muhimu katika jamii kama walivyo walimu na madaktari. Tusisubiri mpaka mmoja wao akapoteza maisha barabarani na ndio tukaanza kuchukuwa hatua za kuwalinda.

Mnaohusika najua mko humu na ujumbe utawafikia. If we can save one life, then it's worth the cost.

Tusijaribu kukata kona kwenye maisha ya binadamu. Kateni bajeti ya semina magari ya V8 ili mnunuwe zana za kuwalinda hawa wenzetu. Tahadhari kabla ya hatari.
 
Back
Top Bottom