Magufuli katika nyayo za Kinana

kalulukalunde

JF-Expert Member
May 27, 2016
1,056
1,083
SIKU zinahesabika kabla ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kufanya mkutano wake maalumu, Julai 23.

Pamoja na masuala mengine, Rais mstaafu Jakaya Kikwete anatarajiwa kukabidhi kijiti cha uenyekiti wa chama hicho tawala kwa Rais John Magufuli. Ndani ya miaka 39 ya uhai wake, chama kimepitia kwenye milima na mabonde; kwa maana ya kung’ara na kufifia kwa namna moja au nyingine, hali ambayo kilistuka na kutafuta busara za kujinusuru. Itakumbukwa kwamba, mwaka 2012, Mkutano Mkuu wa Taifa wa CCM ulifanya maazimio kadhaa.

Miongoni mwa maazimio hayo ilikuwa ni kukitoa chama ofisini na kukipeleka kwa wakulima na wafanyakazi wa Tanzania. Baada ya mkutano huo, iliundwa sektretarieti mpya chini ya Abdulrahman Kinana ambayo kazi yake ni kutekeleza maazimio ya chama kukitoa ofisini kwenda kwa wananchi. Katibu Mkuu huyo wa CCM, Abdulrahman aliongoza mkakati huo. Akishirikiana na wajumbe wengine wa Sekretarieti, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye walifanya kazi hiyo kwa uaminifu mkubwa kwa kuzunguka nchi nzima.

Sifa anazopewa za kurudishia chama hadhi yake, ni ukombozi kwa chama tawala ambacho baadhi ya wanachama, wanakiri kwamba ilifika wakati kikatetereka. Alitembea kilometa 193,537 kuzunguka mikoa 31, wilaya 163 na majimbo 239 pamoja na kata 1,938 kuwezesha chama kurudisha nguvu yake. Mikutano ya hadhara 1,918 aliyofanya na miradi 2,671 aliyoitembelea ndani ya miezi hiyo 26, inatajwa kuwa ilikirudishia chama heshima ambayo ndiyo imekiwezesha kiendelee kushika dola baada ya kushinda uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Ndani ya miezi 26 ya ziara hiyo ambazo nilibahatika kushiriki sehemu yake, katika mikakati ya kurudisha chama kwenye misingi ya muasisi wake, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Kinana alikuwa na maono ambayo mengi yameanza kufanyiwa kazi na Serikali ya Awamu ya Tano. Kinana ambaye alikuwa akisikiliza wananchi na kubaini kero zao, udhaifu wa viongozi serikalini na hata sheria kandamizi ambazo hakusita kukemea, kushauri na kutaka chama na serikali kwa ujumla kuyafanyia kazi.

Kusoma kwa wananchi Namnukuu Kinana siku alipohitimisha ziara zake mjini Mwanza. Akiwa kwenye mkutano wa hadhara alisema: Mao katika kuandika historia yake, amefanya mambo mengi. Alisema upo wakati aliulizwa, je umesoma? Akasema amesoma sana na akasema amekwenda zaidi ya chuo kikuu, wakati alikuwa hajasoma. Aliwajibu kwamba, amesoma chuo cha wananchi. Lazima na mimi nikiri kwamba kwenye ziara zangu, nimesoma chuo cha wananchi.

Niwahakikishie, masomo hayo niliyoyasoma nitayafundisha chama na kuhakikisha serikali yangu nayo inajifunza. Wakati Magufuli akisubiriwa kupokea kijiti cha uongozi wa juu katika chama, mambo mengi yaliyotabiriwa, kukemewa, kushauriwa na Kinana chini ya baraka za CCM kilichomtuma afanye ziara, yanaonekana kutekelezwa kwa kiwango kikubwa katika serikali yake ya awamu ya tano.

Taswira inayomwonesha Rais Magufuli akiwa ndani ya nyayo za Kinana kutokana na kufanyia kazi kwa vitendo mambo mengi ambayo Kinana alitamani yafanyike serikalini. Matumizi makubwa serikalini, safari za nje, adhabu kwa watumishi wabadhirifu, sheria mbovu na uongozi thabiti na kero mbalimbali zinazokabili wananchi, ni miongoni mwa mambo mengi ambayo namna ambavyo Kinana aliyazungumzia, ndivyo utekelezaji na utatuzi wake unafanyika sasa chini ya Rais Magufuli.

Kupunguza matumizi Katika mikutano yake, Kinana alikemea sana matumizi yasiyo ya lazima kwa kushauri serikali iachane na sherehe zisizo na maana. Alikuwa akishauri serikali kuwa na utaratibu wa kubana matumizi ili fedha zielekezwe kwenye halmashauri, zifanye maendeleo.

“Siku hizi kuna utamaduni serikali wa kufanya sherehe mara kwa mara, na kwenye sherehe hizo zinaandaliwa na fulana na kofia na zote zinatumia fedha… Serikali iache sherehe na fedha ziende kwa wananchi kutatua shida zao. “Watajenga mahema, wataweka mapambo, wataleta kofia, hiyo yote kuna mtu anapewa ulaji,” ni kauli ninazokumbuka kusikia akihutubia mkutano wa hadhara katika Kata ya Karumwa, wilayani Nyang’hwale katika Mkoa wa Mwanza.

Hatua ya sasa ya Rais Magufuli kubana matumizi kwa kuamua kuahirisha baadhi ya sherehe ni uthibitisho wa ‘utii’ kwa maono ya chama kupitia Kinana. Kama alivyoshauri Kinana, hivi sasa fedha zinazookolewa, zinaelekezwa kwenye maendeleo ya wananchi ikiwemo utengenezaji madawati, matengenezo ya barabara. Safari za nje Miongoni mwa viongozi ambao Kinana aliwanyooshea vidole ni mawaziri wanaohusudu ziara za nje ya nchi hususani Ulaya, kuliko kwenda vijijini kuzungumza na wananchi na kutatua kero zao.

“Lakini waalikwe kwenda Ulaya, wa kwanza kwenda. Waalike kwenye sherehe wa kwanza kufika, chinja kuku wa kwanza kula firigisi lakini matatizo ya wananchi, wa mwisho,” alinukuliwa Kinana akisema. Nakumbuka kwenye mkutano wa hadhara mjini Masumbwe wilayani Mbogwe, Nape aliungana na Katibu Mkuu Kinana, akakemea mawaziri kwa kuwataka wapunguze safari za nje ya nchi wakasikilize wananchi.

Katika kuonesha namna ambavyo Rais Magufuli anatembelea kwenye nyayo za viongozi hao wa chama, baada ya kuingia madarakani, alipiga marufuku safari za nje kwa mtumishi yeyote wa serikali pasipokuwa na kibali cha Ikulu. Kupitia mkakati wa Magufuli wa kubana matumizi, hata safari za nje kwa mawaziri zimebanwa. Sasa wamekuwa wakishuhudiwa wakizunguka mikoani wakizungumza na wananchi.

Wakati huo huo, kero mbalimbali zinazojitokeza katika sekta mbalimbali, zimekuwa zikifanyiwa kazi haraka na mawaziri. Watumishi wabadhirifu Ubadhirifu miongoni mwa watumishi serikalini na wengine kujigeuza miungu watu, ni mambo mengine yaliyoonekana kumkera Kinana ambaye hakusita kukemea na kushauri juu ya hilo. Alitamani sheria ya utumishi inayolinda wabadhirifu, ifutwe.

Aliweka bayana kwamba CCM kimeamua kusimamia na kurudisha misingi iliyoasisiwa na waasisi wa taifa, ikiwa ni pamoja na kutenda haki na kutetea wanyonge. Msimamo wa Kinana kutaka wanachama kuwa wakali dhidi ya ulaji unaofanywa na watendaji ulikwenda sanjari na kutaka watu wa namna hiyo kufukuzwa kazi mara moja na si kumhamishia idara au taasisi nyingine. Akanyooshea kidole sheria Utumishi wa Umma inayolinda wabadhirifu kwa kutoruhusu waadhibiwe papo kwa hapo.

Akashangaa kitendo cha mtu aliyeiba mali ya umma kuundiwa tume za kumchunguza licha ya ushahidi kuwapo na kutosheleza. Alikuwa akihoji mantiki ya utawala bora kuzingatiwa kabla ya kuadhibu wanaoiba mali za umma wakati hao wezi hawaheshimu utawala bora.

“Lakini akishaiba, akitaka kuchukuliwa hatua, anataka ufuatwe utawala bora kwa maana ya kuchunguzwa, kuundiwa tume kabla ya kuchukuliwa hatua.” Msimamo wake ukawa kwamba, mtu anapoiba, afukuzwe, aajiriwe mwingine kwa kuwa wapo wasomi wengi wanaoweza kuziba nafasi hiyo. Msisitizo wake ukawa kwamba, CCM haipo kwa ajili ya kutetea kila jambo linalofanywa na serikali endapo haliko sawa.

Juhudi za Rais Magufuli za kutetea wanyonge zinaendelea kuonekana kutokana na utumbuaji majipu kwa watendaji wanaotuhumiwa kufanya ubadhirifu kwenye ofisi za umma. Wakati akichukua hatua hiyo, wapo watu vikiwamo baadhi ya vyama vya upinzani, ambao wamekuwa wakimnyooshea vidole wakidai anakiuka sheria na taratibu za uwajibishaji watumishi. Sheria ya manunuzi Pamoja na masuala mengine, katika ziara zake, Kinana alishutumu sheria ya manunuzi akisema imejaa urasimu na mianya ya rushwa.

Alishauri Bunge lijalo (la sasa) liifute kutokana na kuwa na kasoro ambazo ni urasimu, rushwa na kuongeza gharama za manunuzi. Akaiita sheria hiyo kuwa ya hovyo na isiyo na tija kwa taifa. Akaishutumu kuleta matatizo ikiwamo kusababisha watu wasiofaa kupewa nafasi katika zabuni mbalimbali na kuacha wanaofaa. Chini ya uongozi wa Rais Magufuli, sheria hiyo tayari imeshafanyiwa marekebisho.

Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Manunuzi wa Mwaka 2016 ulijadiliwa na kupitishwa katika mkutano wa tatu wa Bunge la 11 . Kinachosubiriwa sasa ni kusainiwa na rais. Maovu serikalini yasitetewe Kinana ambaye alihimiza wana CCM kuwa wakali dhidi ya maovu yanayotendeka serikalini kwa kutokubali kutetea serikali na watendaji wanapotenda maovu, ziara zake zote alihimiza utetezi wa haki kwa wanyonge.

Alisisitiza chama kiwe cha kukataa maovu na watu waovu. “Kiwe chama cha kupambana na dhuluma; watu watatuheshimu, ukisema CCM hoyee kila mtu atasema hoyee,” ni miongoni mwa kauli alizokaririwa akitoa kwenye mikutano ya ndani ya chama na ya hadhara. Kwenye mikutano hiyo, Kinana alikiri kuwapo wakati ambao watu walianza kukiona chama cha hovyo kwa sababu ya wakati wote kutetea serikali.

“Mimi nilitakiwa nikija hapa nitoe hotuba nieleze serikali ilivyo nzuri… Siwezi kufanya hivyo, kama mambo yakiharibika, mimi ni wa kwanza kusema halifai, jambo likiwa zuri lazima niseme serikali imefanya vizuri. Wananchi wakionewa lazima niseme mnaonea watu,” alisema Kinana. Tangu Rais Magufuli ashike madaraka, amekuwa akifuata nyayo za Kinana kwa kuainisha uozo mbalimbali uliomo serikalini bila kujali kuwa yeye ni kiongozi mkuu wa serikali hiyo.

Hatua hiyo imekuwa ikienda sanjari na uchukuaji wa hatua mbalimbali dhidi ya wabadhirifu, ikiwa ni pamoja na kuwasimamisha kazi na wengine kufikishwa mahamani. Ahadi hewa Lakini pia Kinana hakuacha kushauri viongozi serikalini akiwataka waepuke kuahidi wananchi mambo mbalimbali ya maendeleo iwapo hawana uhakika wa maandalizi na upatikanaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji miradi husika. Rais Magufuli ni muumini wa vitendo kuliko maneno (ahadi). Katika hotuba zake nyingi, amekuwa akisisitiza nia ya kujenga ‘Tanzania mpya’ .

“Nasema kweli, tena nasema kweli…,” ni kauli ambayo amekuwa akiitumia mara kwa mara kuonesha dhamira yake ya kuhakikisha anayoahidi yanatimia. Mengi ameyatimiza ikiwa ni pamoja na suala la elimu bure, kupambana na ufisadi, kubana matumizi na mengine lukuki. Kero ya kodi Kinana alisema kupitia ziara zake ameona mambo mengi yanayofanyika vijijini yasiyo sahihi kwa wananchi ikiwemo kodi na ushuru wenye kero kwa wanyonge.

Kwenye mikutano yake mingi, alishauri halmashauri na serikali kwa ujumla kuondoa ushuru na kodi kwa wanyonge. Serikali ya awamu ya tano imeshafanyia kazi hilo. Kutokana na maelekezo ya rais, tayari kodi na ushuru mbalimbali unaogusa watu wa kipato cha chini, wakiwemo wakulima umeshafutwa. Hii ni pamoja na ushuru kwenye mazao. Vyeo vya utukufu Kinana alikuwa akikemea kwa nguvu watu wanaopata vyeo na madaraka serikali wakajisahau na kuvigeuza kuwa vya utukufu badala ya kunufaisha wananchi.

“Umezuka ugonjwa wa ‘mheshimiwa’ kwa maana mtu akishapata cheo hata kama alikuwa kwenye jamii, anajiita mheshimiwa. Mtu alikuwa mbunge, rais anamuita anampa uwaziri, anakuwa zaidi ya wananchi.” Akasema wapo watendaji wamejitengenezea serikali zao hadi wanatoza watu ushuru. Kwa upande wake, Rais Magufuli katika kutoa nasaha kwa wateule wake, wakiwemo wakuu wa mikoa, wilaya na makatibu tawala wao, amekuwa akiwasisitiza kutumikia wananchi ipasavyo na siyo vinginevyo.

Viwanda/mashamba Katika suala zima la kufufua viwanda, Kinana alikuwa akihimiza serikali kuwanyang’anya watu waliomilikishwa viwanda na kushindwa kuviendesha. Pia alizungumzia migogoro ya ardhi na kutaka wenye mashamba yanayohodhiwa bila kuendelezwa, pia wahusika wanyang’anywe. Ushauri huo umeshaanza kutekelezwa na serikali awamu ya tano, lengo likiwa kutengeneza taifa lenye viwanda kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na ajira. Wale waliohodhi viwanda walivyobinafsishiwa wameanza kuguswa.

CCM ya Nyerere Kwa upande wa chama, shauku ya Katibu Mkuu huyo wa chama, ilikuwa ni kuona CCM inayosimamia misingi ya muasisi wake, Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere. Nakumbuka katika mikutano mbalimbali aliyofanya, katika kusisitiza kuwa hayuko tayari kutetea serikali iwapo yako mambo maovu yanayotendeka, alikuwa akisisitiza CCM anayoifahamu ni ile inayojali matakwa ya watu.

“Lazima chama kiwe kinachosimamia matakwa ya watu… Iwe ni kimbilio la watu, ndiyo CCM ninayoijua, niliyokua nayo, ambayo mwasisi wake ni Baba wa Taifa, Julius Nyerere,” alikaririwa katibu mkuu huyo wa chama. Changamoto ya mtendaji huyo wa chama ni kujenga CCM yenye nguvu kupita kiasi. Miongoni mwa mambo anayotamani yafanyike, ni halmashauri kuu ya taifa kuwa na nguvu kuliko mtu yeyote, waziri yeyote.

Anasema lazima halmashauri kuu inapaswa kusema namna serikali inavyoendeshwa na yenye kuamua hatma ya mawaziri wavivu, ikiwemo kuwabadilisha. Ni matarajio kwamba, Rais Magufuli atakapopokea kijiti cha uenyekiti wa CCM, ataendelea kuwa ndani ya nyayo hizi za Kinana ndani ya CCM pia. Atachukua fikra na maono mazuri ya Katibu Mkuu, Kinana kuhakikisha chama kinafanya kazi kwa maslahi ya watanzania wote.
 
Back
Top Bottom