Mafisadi waombe msamaha!

Kamundu

Platinum Member
Nov 22, 2006
6,606
8,744
Kwa kuwa pesa ni ya wananchi basi ni vyema hao mafisadi ili watambuliwe kuwa ni raia wema waombe msamaha kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kurudisha pesa walizopata kidanganyifu. Bila hi9vyo watapigwa mawe na wananchi na kuishi kwa wasiwasi kila siku


Kamati ya Kashfa ya EPA yaficha siri
Yashindwa kujibu maswali muhimu



na Mwandishi Wetu



MIEZI miwili baada ya kuanza kazi ya kuchunguza wizi uliotokea kupitia akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA) ya Benki Kuu (BoT), timu iliyopewa kuifanya kazi hiyo imeshindwa kutoa taarifa ya kina kuhusu hatua ambayo upepelezi huo umefikia.
Zaidi ya hayo, taarifa ya timu hiyo iliyotolewa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali jana, Johnson Mwanyika, ilishindwa kujibu maswali muhimu kuhusu upelelezi huo unaoendelea.

Licha ya kushindwa kujibu maswali hayo muhimu, yakiwemo maswali yaliyoibuka baada ya taarifa ya mwisho iliyoeleza kuwa baadhi ya fedha zilizoibwa katika akaunti hiyo zimeanza kurudishwa, taarifa ya Mwanyika inaweza kuzusha maswali mengine magumu ambayo yatahitaji majibu na ufafanuzi wa kina kutoka kwa timu hiyo.

Kubwa ambalo watu wengi wanataka kulifahamu hivi sasa ni majina ya watu walioamua kurudisha fedha walizochota kwa hila katika akaunti ya EPA. Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustapha Mkullo, alishaueleza umma kuwa kiasi cha sh bilioni 50 zilikuwa zimesharudishwa na baadhi ya watu ambao kampuni zao zilitumika kuchota mabilioni hayo kutoka EPA.

Aidha, watu walitaka baada ya kutajwa kwa watu hao, wachukuliwe hatua za kisherisa mara moja kwa sababu kurejesha kwao fedha ni namna ya kukiri kuhusika kwao katika wizi huo, na hakuna ushahidi mwingine mkubwa unaoweza kutakiwa kuwatia hatiani zaidi ya wao wenyewe kukiri kuiibia serikali kupitia akaunti hiyo.

Lakini katika taarifa yake ya jana, Mwanyika si tu alishindwa kujibu maswali hayo, bali alitoa maelezo ambayo nayo yanazusha maswali kadhaa.

Kimsingi, alichoeleza Mwanyika katika taarifa yake ni kuwataka Watanzania wawe na subira, wakati timu iliyoteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuchunguza suala hilo, ikiongozwa na yeye mwenyewe, ikifanya kazi zake.

Akisisitiza umuhimu wa Watanzania kuwa na subira wakati kazi hiyo ikifanyika, Mwanyika alisema katika taarifa yake kuwa timu hiyo imepewa miezi sita kuikamilisha kazi hiyo na hivi sasa imepita miezi miwili tu tangu kazi hiyo ianze.

“Tunapenda kuukumbusha umma na wanahabari kuwa timu imepewa miezi sita ya kufanya kazi na hatimaye kuwasilisha taarifa kwa Mheshimiwa Rais. Huu ni mwezi wa pili tangu timu ianze kazi yake. Kwa msingi huo, timu inawasihi umma na wanahabari kuwa na subira, kwani wahenga walisema subira yavuta heri.

Hata alipojaribu kutoa taarifa mpya kuhusu kinachofanywa na timu hiyo kwa sasa, Mwanyika alizunguka na kutoa taarifa ambayo inazusha maswali mengine.

Mwanyika alisema kuwa ‘pamoja na majukumu mengi iliyopewa, kwa sasa timu imejikita katika kufanya uchunguzi wa kitaalamu na wa kina,’ bila kueleza kinagaubaga huo uchunguzi wa kina unaofanyika ni upi, wakati kazi ya kuichunguza akaunti hiyo ilishafanywa na Kampuni ya Ernst & Young.

Aidha, Mwanyika hakueleza uchunguzi huo unalenga kubaini kitu gani wakati waliochukua fedha hizo tayari wameshaanza kurejesha, na tayari kiasi cha sh bilioni 50 zilikuwa zimesharejeshwa hadi kufikia mwisho wa wiki mbili zilizopita.

Ili kuhalalisha kukwepa kutoa taarifa kwa umma kuhusu uchunguzi huo kama ilivyoagizwa na Rais Kikwete wakati alipotangaza kuundwa kwa timu hiyo, Mwanyika alisema kuwa kazi ya uchunguzi ndiyo inawakwamisha kutoa taarifa hizo.

“Kwa msingi huo, pamoja na fedha zinazorudishwa, ni vyema umma na wanahabari wakafahamu kuwa kazi ya uchunguzi haijafika mwisho na kwa sasa timu inaona ni vyema kutotoa taarifa ambazo zitaathiri kazi ya uchunguzi inayoendelea,” alisema Mwanyika na kuendelea kuuomba umma na wanahabari kuwa na subira wakati kazi hiyo ikiendelea.

Hata hivyo, Mwanyika alivihakikishia vyombo vya habari na wananchi kuwa kazi ya uchunguzi inaendelea vizuri na timu inapata ushirikiano mzuri kutoka kwa makampuni na wamiliki wanaohusika na upotevu wa fedha za EPA.

Akitoa ufafanuzi kuhusu maswali na malalamiko ya kutokamatwa kwa waliohusika, ambao tayari wameanza kurudisha fedha, Mwanyika, kwa mara nyingine tena, alishindwa kutaja majina.

Alitoa kauli ya jumla na kueleza: “Tunapenda kuueleza umma kwamba uchunguzi wetu hadi hivi sasa unaonyesha kwamba wahusika wakuu ni makampuni.”

Akijitetea katika hilo, Mwanyika, ambaye uwepo wake katika timu hiyo ulishalalamikiwa huko nyuma, alisema kuwa kisheria, makampuni hayo ni mtu, yaani ‘Legal Person’.

“Hata hivyo, makampuni hayo ni tofauti na mtu wa kawaida. Kampuni katika maana hii, inajitegemea yenyewe,” alifafanua na kuongeza:

“Kwa msingi huo, ikiwa kampuni imefanya kosa, kuna utaratibu wa kufuata kisheria. Kazi inayofanyika hivi sasa ni uchunguzi wa kina kuhusu maafisa wa makampuni hayo ili kufahamu ni kitu gani kilichosababisha hali hiyo kutokea.”

Alisema kuwa uchunguzi huo bado unaendelea na ndio utakaoiwezesha timu kujua hatua za kisheria zitakazochukuliwa.

Timu hiyo iliundwa na Rais Kikwete Januari 8, mwaka huu, ikimjumuisha Mwanyika, Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

Pamoja na mambo mengine, timu hiyo ilikabidhiwa jukumu la kuchunguza na kuchukua hatua za kisheria kwa makampuni na watuhumiwa wa upotevu wa fedha katika akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA) kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Taarifa iliyotolewa jana na Mwanyika, ni ya tatu tangu timu hiyo ianze kazi ya kuchunguza sakata hilo ambalo liliibuka bungeni na kuzimwa kabla serikali haijaamua kumwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuipa kazi kampuni ya kimataifa kufanya ukaguzi wa EPA.

CAG aliiteua Kampuni ya Ernst & Young kuifanya kazi hiyo na iliwasilisha ripoti yake mwishoni mwa mwaka jana na kubainisha kuwa kiasi cha sh bilioni 133 zilikuwa zimeibwa na kampuni 22 kupitia akaunti hiyo.

Taarifa hiyo ilimfanya Rais Kikwete kutengua uteuzi wa aliyekuwa Gavana wa BoT, Daudi Ballali, na kuteua timu hiyo na kuitaka kwamba pamoja na uchunguzi itakaoufanya, ihakikishe fedha zilizoibwa kupitia akaunti hiyo zinarejeshwa na wahusika kuchukuliwa hatua za kisheria.
 
Hapa napinga na wewe kabisa, waombe msamaha alafu iweje? sheria inasema mwizi aombe msamaha na kurudisha alichoiba jamani?
Hawa wanatakiwa kufikishwa kwenye vyombo vya sheria na kushughulikiwa kulingana na sheria zinavyosema
au kuna njia nyingine kama tumekuwa kila siku tukiwapiga mawe na kuwachoma vibaka kila siku wanaoiba simu za pesa setu (http://www.ippmedia.com/ipp/alasiri/2008/03/10/110095.html) basi tufanye hivi kwa hawa jamaa kwa sababu serikali imeshindwa kuwachukulia sheria, na inaendelea kuwakumbatia, kwani na hawa si wezi tu kama wezi wengine? na hawa ndo wanaosababisha hali yote hii mbovu tunayoiona Tanzania

wapigwe mawe na kuwachoma moto kama serikali imeshindwa kuwachukulia hatua, basi wananchi wajichukulie sheria mikononi kama wanavyofanya kwa wezi wengine.

NAUNGANA NA WEWE REVEREND. HII INCHI NI YA SHERIA TO. THE RULE OF LAW.
 
Mwandishi wetu,
Tumeona kweli kwamba wewe ni mwandishi wao-mafisadi.
Eti nini?Nchi ya matabaka,waliochini ya sheria na walio juu ya sheria.
Usitulishe hila!!Wananchi tumechukia,waambie waliokutuma kwamba vibaka wote waliojela tena wengi kwa kesi za kubandikiwa waachiwe kama viongozi wa ujambazi waliotajwa walivyo nje hadi leo.Hii inataka kuwa nchi ya namna gani!
HILO SOMO TUMELIKATAA.
 
Kwa kuwa pesa ni ya wananchi basi ni vyema hao mafisadi ili watambuliwe kuwa ni raia wema waombe msamaha kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kurudisha pesa walizopata kidanganyifu. Bila hi9vyo watapigwa mawe na wananchi na kuishi kwa wasiwasi kila siku


it sounds odd, je wale waliiba kuku, sh 50,000/=, yule Afisa mtendaji wa kijiji aliye fukuzwa kazi jukwaani kwa kutotoa taarifa ya michango ya ujenzi wa sekondari siyo Watanzania? kwanini kuwe na matabaka!! hapana Bw.Kamundu, wanatakiwa kushtakiwa, kufilisiwa, kufukuzwa kazi nk.
 
Back
Top Bottom