Madai ya 7 ya chadema kutoka kwenye tamko

Maishamapya

JF-Expert Member
Nov 3, 2010
1,279
375
Haya ndiyo madai ya CDM kutoka kwenye tamko lililosomwa na Mh. Mbowe jana kwenye maziko ...



Ili tutimize majukumu yote haya, tunahitaji kuhakikisha kwamba mambo yafuatayo yanafanyika:
  1. Serikali hii iwajibike kwa wananchi kama ilivyotamkwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Waziri wa Mambo ya Nchi Shamsa Vuai Nahodha na Inspekta Jenerali wa Polisi Saidi Mwema wajiuzulu mara moja ili kuwawajibisha kama viongozi na wasimamizi wa juu kabisa wa Jeshi la Polisi la Tanzania. Aidha, kujiuzulu kwao kutapisha uchunguzi huru na wa kina wa matukio yote yaliyosababisha wananchi wetu kuuawa, mamia kujeruhiwa na mamia mengine kukamatwa bila sababu yoyote na kuwekwa rumande na baadaye kufunguliwa mashtaka ya uongo ya jinai;
  2. Inspekta Jenerali wa Polisi Saidi Mwema, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha Andengenye na wale wote walioamuru au kutekeleza amri ya kuvunja maandamano na mkutano halali wafunguliwe mashtaka ya jinai kwa matumizi mabaya ya madaraka na kwa kusababisha mauaji ya wananchi wasiokuwa na hatia;
  3. Fidia stahili ilipwe kwa mujibu wa sheria husika za nchi kwa ndugu na/au jamaa wa wale wote waliouawa kutokana na vitendo vya Jeshi la Polisi la Tanzania na kwa wale wote walioumizwa kwa namna yoyote ile na/au kuharibiwa mali zao kutokana na vitendo hivyo;
  4. Mashtaka ya uongo ya jinai yaliyofunguliwa dhidi ya viongozi wa ngazi zote wa CHADEMA, wanachama, wafuasi na wananchi wengine wote waliokumbwa na kumba kumba ya Jeshi la Polisi la Tanzania yafutwe bila masharti yoyote kwa sababu maandamano na mkutano wa hadhara uliozuiliwa yalikuwa halali kwa mujibu wa sheria husika za nchi yetu. Tunasisitiza katika jambo hili kwamba viongozi, wanachama na wafuasi wetu wote waliokamatwa na kufunguliwa mashtaka haya hawatahudhuria mahakamani tena kuhusiana kesi iliyofunguliwa dhidi yao hata kama kwa kufanya hivyo kutafanya wakamatwe na kurudishwa tena gerezani;
  5. Kwa vile uchaguzi wa viongozi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha ndio chanzo cha mauaji ya wananchi na kwa kufahamu utaratibu haramu uliotumika kumpata Meya wa Jiji hilo, matokeo ya uchaguzi huo yafutiliwe mbali na uchaguzi mpya uitishwe haraka iwezekanavyo kwa kufuata sheria husika za nchi yetu;
  6. Haki ya vyama vya siasa na wananchi kufanya maandamano ya amani kama inavyotambuliwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iheshimiwe na kutiliwa nguvu zaidi kwa kufuta vifungu vya Sheria ya Jeshi la Polisi nay a Vyama vya Siasa vinavyoruhusu Jeshi la Polisi la Tanzania kuzuia na/au kusitisha maandamano ya amani. Badala yake, sheria ziweke wazi wajibu wa Jeshi la Polisi la Tanzania kulinda maandamano ya amani na mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na/au ya wananchi;
  7. Tume huru ya uchunguzi ya kimahakama (Judicial Commission of Inquiry) itakayoundwa na majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania iundwe ili kufanya uchunguzi huru, wa kina na wa wazi wa matukio yote yaliyopelekea Inspekta Jenerali wa Polisi na/au Jeshi la Polisi la Tanzania kupiga marufuku maandamano ya amani na mkutano wa hadhara na baadaye Jeshi la Polisi la Tanzania kufanya vurugu zilizosababisha mauaji ya wananchi wasiokuwa na hatia. Tunapenda kusisitiza kuundwa kwa tume huru ya kimahakama kwa sababu historia ya tume nyingine ambazo zimeundwa kwa utaratibu wa Rais kuteua watu anaowataka inaonyesha kwamba zimefanya kazi zao za uchunguzi mafichoni bila kushirikisha wadau wengine na bila wananchi kufahamu kitu kinachoendelea. Matokeo ya tume nyingi za namna hiyo ni kwamba ripoti zake mara nyingi zimepuuzwa na/au kufichwa na watawala. Tume ya uchunguzi ya kimahakama hufanya kazi zake kwa uwazi na huruhusu wananchi kuhudhuria na/au kushiriki moja kwa moja katika kazi za tume kama mashahidi na/au kwa kuhoji mashahidi wengine wanaotoa taarifa kwenye tume hiyo;
Katika kuhakikisha kwamba madai yetu yanatekelezwa, CHADEMA inaelekeza viongozi, wanachama na wafuasi wetu mikoani na Wilayani kuandaa maandamano ya amani nchi nzima ili kulaani mauaji ya wananchi wa Arusha na kudai utekelezaji wa madai haya. CHADEMA Makao Makuu itatuma maafisa wa ngazi za juu wa chama, wakiwemo Wabunge na Wajumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA kushiriki katika maandamano hayo kwa ngazi za mikoa na wilaya ili kuyaongezea nguvu na hamasa.

Nionavyo mimi kwa mkazo huo (hasa dai la 4) ... ni sawa kabisa wasihudhurie mahakamani
 
Back
Top Bottom