Zak Malang
JF-Expert Member
- Dec 30, 2008
- 5,404
- 233
Maalim Seif ajitosa tena urais Zanzibar
SIKU moja baada ya mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kutangaza nia yake ya kugombea urais wa Muungano, katibu wake, Maalim Seif Sharif Hamad ametangaza rasmi nia ya kugombea urais wa Zanzibar.
Maalim Seif, ambaye aliwahi kuwa Waziri Kiongozi wakati wa utawala wa Aboud Jumbe, atakuwa akiwania urais wa Zanzibar kwa mara ya nne tangu mfumo wa siasa za vyama vingi urejeshwe.
Maalim Seif, ambaye alikuwa akitarajiwa kugombea tena na ambaye hatarajiwi kuwa na mpinzani, amesema anasubiri muda wa kuchukua fomu utangazwe kwa mujibu wa chama chake ili achukue.
Mimi nadhani kuna haja ya kuvunja ukimya. Ni kweli kabisa mimi ambaye ni mwanachama halali wa CUF nakusudia kugombea urais wa Zanzibar kwa mara nyingine, alisema Maalim Seif.
Maalim Seif alisema anachoomba ni afya njema na kwamba hivi sasa yuko ngangari kuingia katika mapambano hayo ya urais wa Zanzibar.
Wakati wowote muda wa kuchukua fomu ukitangazwa nitachukua fomu na kusubiri ridhaa ya wanachama katika mkutano mkuu unaotarajiwa kufanyika Juni mwaka huu, alisema Maalim Seif.
Kwa mara zote tatu ambazo amegombea urais wa Zanzibar maalim Seif amekuwa akishindwa kwa ushindi mwembamba na wapinzani wake kutoka CCM, matokeo ambayo yamekuwa yakipingwa na CUF na kufanya hali ya kisiasa visiwani humo kuwa tete kwa muda mrefu.
Awali akisoma maazimio ya kikao cha Baraza Kuu la CUF kilichomalizika juzi usiku, Profesa Lipumba alisema kikao kiimepitisha ratiba ya mchakato wa kura za maoni za kuwapata wagombea wa nafasi za urais, ubunge, uwakilishi na udiwani Tanzania Bara na Zanzibar.
Baraza linatoa wito kwa wanachama wote wa CUF kuheshimu na kufuata matakwa ya katiba ya chama na kanuni za uchaguzi wakati wa zoezi zima la kupiga kura ya maoni na hivyo kuhakikisha kuwa demokrasia ya ndani ya chama inaimarika, alisema Profesa Lipumba.
Alisema baraza limeridhika na maandalizi ya mkutano mkuu maalum wa CUF uliopangwa kufanyika mwezi Juni mwaka huu, kwa ajili ya uteuzi wa wagombea wa urais wa CUF.
Baraza pia limeridhia uamuzi wa mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kuwa miongoni mwa wanachama watakaogombea nafasi ya urais wa Muungano katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Lengo kuu ni kuwapatia Watanzania uongozi makini chini ya chama mbadala CUF na makini hapa nchini.
Baraza linatoa wito kwa wanachama wengine wa CUF wenye sifa na uwezo kujitokeza kutangaza nia zao na kuchukua fomu za kugombea nafasi ya urais wa Muungano na Zanzibar, alisema Lipumba.
Lipumba alimvaa Rais Jakaya Kikwete, akimtaka kutoingia mitini katika mijadala ya moja kwa moja ya wagombea urais kupitia vyombo vya habari.
Tunataka mwaka huu Rais Kikwete asiingie mitini... aje tukutane katika mijadala ya televisheni baina ya wagombea kama wanavyofanya Wamarekani na Uingereza na sio aende pekee katika TV, alisema Profesa Lipumba.
Tunataka Watanzania wajue ubovu wa rais wao ili waweze kufanya maamuzi mazito katika uchaguzi huu kwa kukingoa chama tawala, alisema Lpumba.
Profesa Lipumba alisema CUF inaunga mkono madai ya msingi ya wafanyakazi yaliyotolewa na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta) na kuitaka serikali kuboresha maslahi yao.
Baraza kuu limesikitishwa sana na kauli za vitisho, aibu na kufitinisha wafanyakazi na wananchi kwa serikali kutoa habari na taarifa zisizo na ukweli kamili ili kuwapaka matope viongozi wa Tucta, alisema profesa Lipumba.
Mheshimiwa rais amepewa dhamana kubwa na wananchi ya kuwaongoza na kuwatatulia matatizo yao pale yanapojitokeza, lakini kwa kitendo chake cha kukurupuka na kuwahukumu hadharani viongozi wa Tucta si cha kuwatendea haki hata kidogo Watanzania hasa ikizingatiwa dhamana kubwa waliyompa.
Lipumba alisema baraza kuu la CUF limeona haikuwa busara kwa mheshimiwa rais kutumia jukwaa la wazee wa vijiweni wa CCM, ambao si wafanyakazi, kuelezea matatizo ya wafanyakazi.
Baraza linalaani vitisho alivyovitoa rais kwa wananchi na wafanyakazi nchini na vinaonyesha namna serikali ya CCM inavyokosa uvumilivu na uchungu kwa watu wake na kushindwa kuheshimu uhuru wa wananchi kutoa sauti zao, alisema Lipumba.
Vitisho vya aina yoyote katika zama hizi za demokrasia havikubaliki hata kidogo na vinapaswa kulaaniwa na kupigwa vita na wapenda amani na haki wote nchini, kwani vikiachwa vinaweza kuipeleka nchi yetu pabaya.
Alisema baraza linawaomba wafanyakazi na wananchi kwa ujumla nchini wavumilie vitisho na kashfa walizofanyiwa na Rais Kikwete, badala yake wavigeuze kuwa changamoto kwao kwa kuweka nguvu zaidi za kudai haki zao bila ya kuchoka.
Lipumba alisema katika kufikia hatima njema ya maridhiano ya CUF na CCM Zanzibar baraza kuu linaitaka Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kurekebisha mapungufu makubwa yaliyojitokeza katika zoezi la uandikishaji visiwani humo.
Hadi sasa, katika majimbo yaliyokusanywa takwimu tu, zaidi ya Wazanzibari 15,000 wenye haki ya kuandikishwa katika daftari la wapigakura wamenyimwa haki hiyo ya kikatiba, alisema Profesa.
Source: Nipashe