LIWALO NA LIWE! (A food for Thought)

Ingefurahisha zaidi kama mwandishi angeiweka kwa gazeti ili Wadanganyika wengi waisome!
 
LIWALO NA LIWE!

Na tazama, hata ilipotimia mwezi wa Juni wa mwaka, Baraza lile la saba lilikutana tena kwa ajili ya Baraza la nane. Nao wakakutana kuzungumzia mustakabali wa taifa teule la wana wa nchi. Nchi ya nadharia ya asali na maziwa. Ni kwa namna gani asali na maziwa vigawanywe sawa sawia miongoni mwa wana wan nchi.

Ndipo aliposimama msimamizi mkuu wa fedha za wana wan chi akiwa na mkoba wenye makadirio ya namna gani asali na maziwa vigawanywe. Naye huyu ni mrithi wa msimamizi wa awali ambaye kwa mujibu wa Jemedari Mkuu aliwatabiria, yeye na wahanga wenzake ya kuwa ile dhoruba ingewapitia mbali, lakini haikuwa hivyo.

Naye mwana wa mkulima, akiwa ndiye mkuu wa mawaziri wa Taifa la wana wa nchi, Yule ambaye wana nchi katika Baraza la saba hawakuamini alichowafanyia, kwa upole wa mamba aliyeshiba, alifuatilia hatua kwa hatua yale yote yaliyoletwa mbele ya Baraza. Na kwa unyenyekevu uliofunikwa kwa ngozi safi ya mwanakondoo, aliyapatia maelezo masuala yote yale yaliyoelekezwa katika uwanda wake. Alitamalaki mimbarini kwa mbwembwe na madaha.

Nao wanabaraza walio upande wake kinasaba wakammiminia sifa na kumpelekea maombi kwa njia ya vinubi na vinanda na vigelegelena kusihi, wakiwa chini ya nyao zake kwamba awakumbuke wana wa Kaya zao ya kwamba nao wanasihi kwa unyenyekevu wa nafsi na roho na mwili, ya kuwa wakumbukwe kwa namna itakavyompendeza Jemedari Mkuu, kwenye mgawanyo wa asali na maziwa.

Asali na maziwa ambavyo ni urithi wa nchi. Urithi uliotapakaa Kusi na Kaskazi na Mashariki na Magharibi. Urithi ulioenea toka chini ya ardhi na juu ya ardhi na juu ya maji na kwenye vilindi vya maji. Urithi uliojipambanua katika mazao ya nchi yakiwemo dhahabu na almasi na vito na na gesi na mafuta na wanyama na ardhi safi na misitu. Naam, urithi ambao wawakilishi wa Kaya wanauomba kwa unyenyekevu mkuu ili kuugawanya kwa wana wa nchi. Nao wawakilishi wakiisha kuahidiwa kufikiriwa kutekelezewa maombi yao, hupiga makofi wakiwa na imani katika kusubiri kufikiriwa kusikilizwa kutekelezewa ahadi zao ambazo msimu uliotangulia wa mgawanyo wa urithi wa asali na maziwa, waliomba pia na wakaahidiwa kufikiriwa kusikilizwa kutekelezewa ahadi zao.

Na ilipofika siku ya Jumatano ya wiki katika muendelezo wa vikao vya Baraza, kama ilivyo ada alisimama mkuu wa mawaziri na nyuma ya mimbari alisimama kwa unyenyekevu akisubiri kujibu na kutoa ufafanuzi na kupangua hoja, na kuomba huruma kwa naibu mkuu wa Baraza juu ya maswali toka kwa wanabaraza, juu ya mgawanyo wa urithi wa asali na maziwa.

Ndipo aliposimama mwanabaraza, mwakilishi wa wana wa Kaya yake na kwa niaba ya wana wa nchi ili kuomba mwongozo kupitia kanuni ya 68 (7) ya juzuu ya Baraza. Naye kwa niaba ya wana wa nchi alitaka kujua kupitia kwa naibu wa mkuu wa Baraza kwenda kwa mkuu wa mawaziri, hatua za serikali ya wana wa nchi ilizochukua juu ya mgomo wa matabibu.


Naye mkuu wa mawaziri akasema, “Chombo cha kutoa haki kiliwaonya matabibu wasigome, na waende kwenye mabaraza ya habari kueleza nia yao ya kuacha kugoma. Nayo serikali ikaendelea kuwa sikivu, lakini matabibu hawakusikia… kauli ya serikali ni ya kuwa matabibu waheshimu amri ya ya chombo cha kutoa haki… tutatoa kauli sahihi ya serikali kesho. Tumeamua kulitaarfu Baraza lako Tukufu maana kwa kweli serikali inafanya kila lililowezekana na sasa watu husema LIWALO NA LIWE!

Ikawa ilipotolewa kauli hiyo, mioyo ya wana wa nchi ikazizima kwa hofu na taharuki na jazba na hasira na kukata tamaa juu ya kile alichosema mkuu wa mawaziri. Nayo kauli yake ni kauli ya serikali.

Na katika kuwaongezea wana wa nchi uchungu na kukata tama na sononeko na woga, habari mbaya zikasambaa, bega kwa bega na kauli ya serikali, ya kuwa kiongozi wa Jumuiya ya matabibu amepatikana akiwa nusu mfu kwa kusulubiwa na watu na kisha wakautosa mwili wake wenye majeraha na maumivu kando ya msitu akiwa ameviringishwa kamba. Naye alipopatikana na kuonekana, hakika alionekana kuwa na maumivu mno! Mavazi yake yaligandamana na madonda. Mwili wake ulitapakaa damu. Uso wake walimpiga kiasi cha kumpotezea sura, maana ulivimba sana. Naam, walimpa mateso, na kumdhihaki, ya kuwa, kwa kuwa wewe ni kiongozi wa matabibu, nawe upate adha ya kile mnachogomea kutoa, yaani tiba kwa wana wa nchi.

Nao wenzake walipopata habari walimtafuta na kumchukua kwa huruma na upole na majonzi na masikitiko, huku wakilia na kuapiza na kuonya na kulaani kauli ya mkuu wa mawaziri, ambayo ni kauli ya serikali, ya kuwa liwalo na liwe!

Na katika kuyatafakari hayo, ile sauti ya awali ikavuma tena kama mwangwi kondeni. Ikapenya ndani ya mioyo kama upanga ukatao kuwili. Ikaleta maumivu makali kama uchungu wa mama wakati wa kuzaa. Ikarudisha kumbukumbu zote za madhila waliyowahi kufanyiwa wana wa nchi. Nchi ya urithi wa asali na maziwa. Urithi unaomegwa na watu wa mataifa toka ng‟ambo ya mbali. Sauti yenye maneno ya kuhuisha fikra na mwamko wa kuhimiza wana wa nchi kuamkua toka lindi la mawazo yaliyo mapumziko. Toka katika mawazo ya wanaofisadi. Mawazo ya watu wenye kuleta falsafa ya umasikini katika nchi. Sauti ikawa inasema;

Ee mkuu mfalme wa kisasi Mfalme wa kisasi uangaze! Mwenye kuhukumu nchi, ujitukuze Uwape wenye kiburi stahili zao.

Mkuu hata lini wasio haki,
Hata lini wasio haki watashangilia? Ee mkuu wanawaseta watu wako Wanawatesa warithi wako

Nao husema, mkuu haoni
Mfalme wa wote hafikiri


Enyi wajinga miongoni mwa watu, fikirini
Enyi wapumbavu, lini mtakapopata akili?

Aliyelitia sikio mahali pake asisikie? Aliyelifanya jicho asione? Awaadhibuye mataifa asikemee? Amfundishaye mwanadamu asijue?

Lakini mkuu amekuwa ngome kwetu
Na Mfalme wetu mwamba wetu wa kukimbilia
Naye atawarudishia uovu wao
Atawaangamiza katika ubaya wao

Naam, mkuu, Mfalme wetu atawaangamiza.

Nayo madhila ya kukosa tiba ni mengi. Nayo yanawapata wana wa nchi walio na uwingi wa uduni. Waitegeao serikali yao Tukufu yenye wingi wa nadharia za urithi wa asali na maziwa. Urithi ambao unasomeka katika vitabu na katika vinywa vya wakuu wa mabaraza na mamlaka za nchi. Urithi ambao Baraza la saba linajaribu tena kukaa na kuangalia vipaumbele vya kumegewa. Na kwa kuwa afya ni sehemu ya vipaumbele. Na kwa kuwa pia Baraza lililopita na lilolopo hayajaweza kusema na shida za sehemu ya afya, na kwa vile afya imeonekana na watu wote kuwa ni sehemu iliyo muhimu kabisa, Ndipo walipokusanyika matabibu waliofika hapo kwa ahadi za kuona pepo ya urithi wa asali na maziwa. Nao wasitimiziwe kile ambacho Jemedari Mkuu aliahidi kukitimiza, maana imeandikwa katika Yoshua bin Sira (38:1-15);

Umheshimu tabibu kwa kadiri ulivyo na haja naye, na kwa heshima iliyo haki yake,
kwa kuwa Bwana amemuinua kweli kweli. Kwa maana ni kutoka kwake aliye juu, tabibu alivyoupata ufundi wake,
hata na kwa mfalme atapokea ada.
Maarifa yake tabibu yatamwinua kichwa chake,
naye atasimama ni mkuu machoni pa wakuu. (na kuendelea).

Ikawa hivyo. Wana wa nchi wakiwa wanasononeka na yale yanayotokea, kwa shingo upande wakaimeza kwa uchungu kauli ya mkuu wa mawaziri, ya kutolea maelezo mgomo wa matabibu wanaoshughulika na afya zao. Kwa kuwa waliahidiwa kwa kinywa cha mkuu mwenyewe, mbele ya kadamnasi ya wana wa nchi na mbele ya wawakilishi wa Kaya za wana wa nchi ya kuwa kesho serikali itatoa kauli rasmi, wana wa nchi walifutika sime zao alani. Sime za machungu na maumivu ya mioyo iliyokosa matumani ya ahadi za maisha bora kwa kila mwana wa nchi.

Napo kesho ilipowadia, Baraza Tukufu lilikaa tena ili kuendeleza ya siku iliyotangulia. Pamoja na kwamba yalikuwako na mengine mengi ya kutolea maamuzi na ufafanuzi juu ya mgawanyo sahihi, suala la afya liliendelea kutamalaki kila kona ya pande za nchi na ndani ya mioyo na


vinywa na vichwa na masikio wa watu, kadhalika miongoni mwa wanabaraza. Nao kila mmoja kwa nafasi yake akangoja kwa shauku na kihoro na hamu ya kutaka kusikia ni nini kauli sahihi ya serikali yao Tukufu juu ya hatima ya mgomo wa matabibu.

Hata mkuu wa mawaziri alipoijongelea mimbari, mkuu wa Baraza alitoa ruhusa kwa wanabaraza kuelekeza hoja zao kwake-yaani mkuu wa mawaziri.

Miongoni mwa wanabaraza walioelekeza vilio vyao na maombi na sala na shutuma na kero za wana wa Kaya zao, alisimama mmoja baada ya ombi lake kupitishwa na mkuu wa Baraza. Naye akamsihi kwa hoja na busara ya kuwa ni kwa nini asiseme „sasa imetosha‟ kwa uongozi wake dhaifu juu ya suala la malalamiko ya matabibu. Hoja hiyo ikaonekana kuwa unyonya mbele ya upepo mkali wa kisulisuli. Hoja iliyoongezewa kasi ya kupeperushwa na mkuu wa Baraza kwa kumsihi mkuu wa mawaziri aitupilie mbali.

Ni katika muono huo wa kuendelea kuona ni kipi sahihi cha kufanya kunusuru hali tete inayofuka mfano wa joto la tanuru, ndipo akasimama yule mwanabaraza ambaye ilimpasa kutolewa nje ya Baraza na askari wa Baraza kutokana na kudhaniwa kuvuka mipaka ya kanuni zilizomo ndani ya juzuu la Baraza. Kwa unyenyekevu na hekima akaomba mwongozo kupitia kanuni ya 116 ya juzuu. Naye akaeleza kwa kina na weledi na ufafanuzi na hoja, kuwa, ikimpendeza yeye mkuu wa Baraza, atoe mamlaka kwa kamati ya Baraza yenye kuwiwa na kero za jamii za wana wa nchi, ili iweze kutatua tatizo la mgomo wa matabibu.

Ikawa yule mwanabaraza akiisha kusema hayo, alikaa akisubiri majibu ya mkuu wa Baraza.
Naye kwa mamlaka na kwa mkato akajibu, “Nitatoa maelezo baadae!”

Napo muda bila kusonga sana mkuu wa Baraza akasema, tena kwa mvumo wa ukali, kuwa yaliyoko mikononi mwa chombo cha kutoa haki hayana budi kuachwa humo! Na kwamba si heri kuinukia suala la mhimili mwingine wa mamlaka. Na kama likiwapo jambo lingine kama hilo lenye kuleta uchochezi juu ya suala lililo nje ya mamlaka ya Baraza, na liachwe! Na kwa hiyo haitampasa tena Waziri wa afya kulitolea maelezo. Ndipo aliposema tena kwa kupaza sauti ili wanabaraza wote wamsikie na wafumbe vinywa vyao, kuwa KAULI YA WAZIRI HAITATOLEWA! SHAURI LIKO MIKONONI MWA CHOMBO CHA KUTOA HAKI, NA LIMEFUNGWA!

Na kwa kauli dhaifu ya mkuu wa mawaziri na inayoashiria kushindwa kutekeleza majukumu na hatimaye kuwashukia wanyonge kwa ghadhabu zilizopotoka, hakika isifike siku. Siku ambayo nao wana wa nchi watasema, LIWALO NA LIWE!

.
 
Damu ya Ulimboka iliyomwagika na iwe chachu ya mageuzi katika sekta ya afya
 
Back
Top Bottom