nice 2
JF-Expert Member
- Aug 10, 2011
- 747
- 520
- Kila mkutano alianzisha na kusimamia ajenda
- Wengi walidandia kwa kuunga mkono au kupinga
KUNA namna nyingi za kuelezea taswira ya Bunge na wabunge katika mikutano yake minne ndani ya mwaka 2012, uliokwisha. Unaweza kulielezea Bunge na wabunge kwa kutazama aina ya hoja zilivyoendeshwa ndani ya chombo hicho nyeti nchini.
Lakini pia Bunge linaweza, kwa kadiri ya fursa za mijadala, kupambanua uwezo binafsi wa kila mbunge. Kwa mfano, nani mbunge hodari ‘kudandia' hoja na hata kuiteka na kuiboresha. Nani mbunge hodari wa kuvuruga hoja zenye maslahi kwa taifa, na zaidi, nani mbunge hodari kutohudhuria vikao vya Bunge.
Nani mbunge mahiri katika kushauri pale ushauri wa kibunge unapohitajika katika masuala nyeti na tata nchini. Lakini mbali na hapo, nani mbunge wa kufoka zaidi, yaani nguvu nyingi hoja za msingi chache katika dakika za kujieleza kwake ndani ya Bunge.
Safari ya Bunge na wabunge katika mwaka 2012 imekwisha na sasa ni safari mpya ya 2013. Wabunge wamejipanga vipi, tutarajie nini hasa kwa manufaa ya taifa kutoka kwao? Ili angalau kutabiri ya mwaka 2013 ni vizuri kupitia ya muhimu katika 2012.
Itakumbukwa kwamba mkutano wa 12 wa Bunge ulihitimishwa Novemba 2012, kwa aina yake. Siku mbili za mwisho za mkutano huo zilichangamsha vikao vya Bunge kutokana na aina ya hoja zilizowasilishwa na kujadiliwa. Zilikuwa hoja zinazogusa moja kwa moja maslahi ya wananchi na nchi kwa ujumla.
Hoja ya Mbunge wa Kawe (CHADEMA) Halima Mdee, kuhusu masuala ya ardhi sambamba na hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) Zitto Kabwe, kuhusu Watanzania waliotorosha mabilioni ya fedha na kuzificha huko ughaibuni na hasa nchini Uswiss, ndizo zilizochangamsha mno uhitimishaji wa mkutano wa Bunge kwa mwaka 2012.
Hizo bado hoja viporo, serikali imeahidi Bunge kwenda kuzifanyia kazi na bila shaka, namna zitakavyotua kwa mara nyingine bungeni mwaka huu wa 2013 itategemea na utekelezaji wa serikali.
Licha ya kwamba Zitto na January Makamba (kabla Makamba hajateuliwa naibu waziri Mei 2012) walipata kung'ara bungeni katika sakata la kupinga wabunge kuongezewa posho za vikao, lakini Zitto kwa ujumla wake, Zitto anang'ara zaidi kwenye masuala mbalimbali aliyoyaibua bungeni, akiwa na rekodi ya kuanzisha hoja zinazoungwa mkono kwa sehemu kubwa ya Bunge na hata kwa wananchi mitaani.
Kwa mfano, katika mkutano wa kwanza wa Bunge mwaka 2012 (mkutano wa sita), Zitto akiwa ametoka kwenye matibabu nchini India, aliwasilisha bungeni hoja ya zao la mkonge.
Katika hoja hiyo alitaka serikali kuwekeza vya kutosha kupitia wakulima wadogo wadogo ili kuongeza uzalishaji wa mkonge nchini. Alitaka Tanzania irejee kuwa taifa la kwanza duniani kwa kuzalisha mkonge mwingi zaidi kuliko mataifa yote duniani.
Itakumbukwa kwamba hoja hii ilipingwa na wabunge kupitia Mbunge wa Korogwe Mjini, Yusuph Nassir. Hata hivyo, Zitto aliamua kufanya ziara ya kisiasa mkoani Tanga kuipeleka hoja yake kwa wananchi na hatimaye katika vikao vya Mkoa wa Tanga (RCC), uamuzi wa kutekeleza hoja hiyo ulifikiwa rasmi.
Mkuu wa Mkoa wa Tanga alitangaza kauli mbiu ya "Tanga ni Mkonge na Mkonge ni Tanga" na kuanza mara moja kulipa stahili za wafanyakazi wa zamani wa Mamlaka ya Mkonge Tanzania na hatimaye kuanza kuangalia upya ardhi iliyotengwa kwa mashamba makubwa ya mkonge na kuigawa kwa wananchi, wakulima wadogo wadogo.
Mkutano wa saba wa Bunge ulikuwa mkutano wa kihistoria kwani kwa mara ya kwanza, kusudio la hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu wa Tanzania liliibuka.
Katika historia ya Uhuru wa Tanganyika na Muungano wa Tanzania, haijapata kutokea mbunge kutoa hoja ya kutaka kumng'oa Waziri Mkuu kwa kutokuwa na imani naye.
Zitto alisimamia hoja hii, akiunganisha makundi ya wabunge ili kupata sahihi 75 zilizounga mkono hoja yake. Chama chake (CHADEMA) kina wabunge 48 tu na kama Zitto angekuwa hana kipaji cha ushawishi basi ingekuwa vigumu kupata angalau sahihi za wabunge 70 zilizotakiwa ili hoja iweze kuwa hoja.
Hoja hii ilikuwa na mafanikio makubwa sana na kati ya matokeo yake ni Rais Jakaya Kikwete kufanya mabadiliko makubwa ya Baraza la Mawaziri katika kile kilichoweza kutafsiriwa kuwa ni kumwokoa Waziri Mkuu lakini pia kuimarisha utendaji kazi wa serikalini bungeni na nchini kwa ujumla.
Mawaziri wanane waliondolewa na Rais Kikwete kupata fursa ya kuteua mawaziri wapya na hivyo kupata timu ya wachapa kazi ambao ni pamoja na Waziri Dk. Harrison Mwakyembe, Balozi Khamis Kagasheki na Prof. Sospeter Muhongo.
Kulikuwa na maneno kwamba Zitto alitumwa na Rais Kikwete kutoa hoja hii, jambo ambalo Zitto binafsi alilipinga vikali. Maneno haya yanatokana na ukaribu unaodaiwa kuwapo kati ya Zitto na Kikwete, jambo ambalo licha ya kuleta wasiwasi wa kisiasa lakini wakati mwingine ukaribu huu ulisaidia sana kukamilisha suala la Katiba.
Gazeti hili la Raia Mwema liliwahi kuandika namna ambavyo Zitto alitumia uhusiano wake mzuri na wazee wastaafu kama Jaji Joseph Warioba na Dk. Salim Ahmed Salim kwa upande mmoja na ukaribu wake na Rais Kikwete kwa upande mwingine, kuhakikisha CHADEMA wanaingia kwenye mchakato wa kuandika Katiba, baada ya kususia kujadili Muswada wa Sheria Mabadiliko ya Katiba bungeni.
Lakini mkutano wa nane wa Bunge pia ulikuwa mkutano uliotishia heshima ya Zitto kimaadili. Zitto alihusishwa na kundi la wabunge walioonekana kumtetea aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO, William Mhando.
Mhando alisimamishwa kazi TANESCO na baadaye kuachishwa rasmi kazi hiyo baada ya Bodi ya TANESCO kujiridhisha kuwa alijihusika katika ukiukwaji wa maadili kwa kutoa biashara kwa kampuni ya mkewe.
Ingawa Spika alitoa uamuzi wake kwamba wabunge hawakujihusisha na rushwa, lakini Zitto anapaswa kuwa makini sana siku za usoni kutojihusisha na watendaji ambao maadili yao ni ya shaka.
Licha ya suala hili, Zitto pia alifanikisha kuandikwa kwa sheria ya fedha 2012, akiwa amefanikiwa kuandika na kupitisha mapendekezo yake ya sheria ya kulinda viwanda vya ndani vya nguo na maziwa.
Vile vile sheria ya nyongeza ya mitaji (capital gains) kwa kampuni zinazouziana rasilimali za nchi na pia sheria ya kulinda haki za wasanii ambapo kwa sasa, kazi zao zitalindwa kwa mujibu wa wigo wa taratibu za kodi.
Mkutano wa tisa ambao ndio mkutano wa mwisho kwa mwaka 2012, ulimalizika kwa kishindo kwa Zitto kuibuka shujaa wa kupambana na mafisadi watoroshaji wa fedha za kigeni za nchi.
Zitto alifanikiwa kuunganisha wabunge bila kujali itikadi zao za vyama kupitisha hoja binafsi iliyotaka serikali kuchukua hatua dhidi ya mabilioni ya fedha yaliyofichwa Uswiss.
Licha ya juhudi za Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Frederick Werema, kutaka kuilainisha hoja hii, hoja ilipita kwa kishindo na kuweka historia ya moja ya mabunge katika Afrika yaliyoamua kuchukua hatua dhidi ya utoroshaji wa fedha na kufichwa ughaibuni.
Nilizungumza na Zitto mwenyewe wakati fulani mwaka jana kuhusu mafanikio ya kazi zake za kibunge katika mwaka 2012 naye alinijibu na nadhani ni vizuri nikanukuu kwamba- "Kwanza ifahamike kuwa hoja ya mabilioni ya Uswiss ni hoja ya kwanza binafsi iliyowasilishwa na kupitishwa na Bunge tangu nimekuwa Mbunge.
"Nimefurahi kufanikisha juhudi hizi za kupambana na ufisadi. Watu waone kuwa hawana pa kujificha wakiiba mali ya umma. Pili, ili mbunge afanikiwe katika kazi za ubunge lazima ajisomee.
"Tatizo la wabunge wengi, hasa wabunge vijana wanaendekeza sana starehe na kusahau majukumu yao ya kibunge. Mimi tangu nimekuwa mbunge sijawahi kufika Mnadani (eneo la nyama choma-Dodoma), lakini kuna wabunge bila kujali uzito wa kazi, kila Jumamosi wapo Mnadani.
"Wanashinda kwenye baa kunywa na kutafuta wanawake. Huwezi kuwa mbunge bora kama Dodoma kwako ni nyakati za starehe badala ya kazi. Tatu, kutokukata tamaa. Mwanasiasa mahiri anakomazwa na misukosuko. Nashukuru sana wabunge wenzangu kuniunga mkono.
"Hata hivyo, suala la hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu kwangu inabakia hoja ya kihistoria kuliko nyingine yoyote katika maisha yangu ya kisiasa.
Natumai wachambuzi wa mambo ya siasa wataweza kuiandika historia hiyo."
Source: Raia Mwema - Kwangu, Zitto mbunge wa kipekee mwaka 2012
My Take: Naungana mkono na muandishi wa makala hii, na kumuombea kwa Mungu bw. Zitto aendelee kufanya vizuri kwa maendeleo ya taifa letu mwaka 2013