GE2025 Kwa nini Zanzibar inapiga Kura tofauti na Bara?

Matukio, Taarifa, Habari na Mijadala ya Wananchi WAKATI wa Mchakato wa Uchaguzi Mkuu 2025

Waufukweni

JF-Expert Member
Joined
May 16, 2024
Posts
4,393
Reaction score
14,500
Tanzania ipo katika maandalizi ya uchaguzi mkuu Oktoba 29, ambapo Wananchi kote nchini wanatarajiwa kushiriki kuwachagua viongozi wa ngazi mbalimbali. Zikiwa zimesalia siku chache kabla ya siku ya kupiga kura, ni muhimu kuelewa upekee wa visiwa vya Zanzibar ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ingawa Zanzibar ni sehemu ya Muungano, ina mfumo wa kisiasa na kiutawala unaojitegemea kwa kiasi fulani. Hii ni matokeo ya historia yake ndefu na utambulisho wake ambao umeunda nafasi maalum ya visiwa hivyo ndani ya taifa.

Zanzibar ina Serikali yake, Rais wake na Tume yake ya Uchaguzi, kwanini uchaguzi wake ni watofauti na watanzania nzima?

Kwa karne nyingi, Zanzibar ilikuwa kitovu cha biashara katika eneo la Bahari ya Hindi — maarufu kwa viungo vya chakula na marashi lakini pia kwa kusikitisha biashara ya utumwa. Wakati huo, walowezi wa Kiarabu walijenga mamlaka makubwa, na dini ya Kiislamu ikasambaa bara kupitia visiwa hivyo. Mfumo wa kitabaka uliibuka, Waarabu wakawa tabaka la juu lenye utajiri na madaraka, huku Waafrika wengi wakibaki katika tabaka la chini.

Mwaka 1964, serikali ya Jamshid bin Abdullah al-Said, Sultan wa mwisho wa Zanzibar ilipinduliwa na chama cha Afro-Shirazi (ASP), tukio lililomaliza rasmi utawala wa Waarabu lakini pia likasababisha vifo vya maelfu ya watu.

Serikali mpya chini ya uongozi wa Aman Abeid Karume ilikumbwa na changamoto za utulivu na upweke wa kimataifa. Wakati huo, upande wa Tanganyika, Rais Julius Kambarage Nyerere alihofia taifa lake kuhusishwa moja kwa moja na siasa za Vita Baridi.

Ili kudumisha utulivu na mshikamano, viongozi hao wawili waliamua kuunganisha nchi zao Aprili 1964, na kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (JMT).


Licha ya muungano huo, Zanzibar iliendelea kuwa na Rais wake, Serikali yake na mamlaka fulani ya ndani. Hadhi hiyo maalum imeendelea hadi leo, na ndiyo inayofanya siasa za Zanzibar kuwa na sura tofauti na zile za Bara.

Mfumo wa Uchaguzi Zanzibar​

Zanzibar ni sehemu ya Muungano, lakini inaendeshwa kwa mujibu wa Katiba yake ya mwaka 1984 na chini ya usimamizi wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).
Wakati wa uchaguzi mkuu, mpiga kura wa Zanzibar hupiga kura tano ambazo ni:
  1. Rais wa Muungano,
  2. Wabunge wa Muungano,
  3. Diwani,
  4. Rais wa Zanzibar,
  5. Wawakilishi wa Baraza la Wawakilishi.
Kwa upande wa Bara, mpiga kura hupiga kura tatu pekee — kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mbunge, na Diwani.

Aidha, Zanzibar imekuwa na utaratibu wa kupiga kura mapema kwa baadhi ya makundi maalum, jambo ambalo halitekelezwi upande wa Bara.

Upekee huu wa mfumo wa uchaguzi unadhihirisha nafasi ya kipekee ya Zanzibar ndani ya Muungano — mchanganyiko wa historia, utambulisho na mamlaka ya ndani ambayo yameunda taswira ya kisiasa ya visiwa hivyo hadi leo.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…