Halisi
JF-Expert Member
- Jan 16, 2007
- 2,802
- 613
Jamani hii habari imenishitua sana, nadhani huko CCM mambo si shwari na hili ni gazeti la serikali.
HabariLeo: Gwiji la habari Tanzania | Kundi la wabunge CCM lasuka zengwe la EPA
HabariLeo: Gwiji la habari Tanzania | Kundi la wabunge CCM lasuka zengwe la EPA
Kundi la wabunge CCM lasuka zengwe la EPA
Halima Mlacha
Daily News; Tuesday,November 04, 2008 @21:45
Rais Jakaya Kikwete amesema hajaridhishwa na uamuzi wa Wizara ya Nishati na Madini wa kusubiri kwanza uamuzi wa mahakama juu ya mgogoro wa kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), ndipo ibadilishe mitambo ya umeme ya IPTL kutoka kwenye dizeli na kutumia gesi.
Kutokana na kutoridhishwa huko, ameiagiza Wizara hiyo kuanza mchakato uliosimamishwa mara moja wa kuibadilisha mitambo hiyo na kutosubiri uamuzi huo, kwa kuwa si rahisi kupatiwa ufumbuzi wa kisheria katika muda mfupi wakati suala la kuibadilisha mitambo hiyo ni muhimu zaidi.
Akizungumza jana Dar es Salaam katika uzinduzi wa mtambo mpya wa gesi asilia wa kuzalishia umeme unaomilikiwa na Tanesco, Rais Kikwete alisema tayari ameshazungumza na Waziri William Ngeleja, na kumpatia maagizo ya kuanza mchakato huo.
Nafahamu kuwa mchakato wa kubadilisha mitambo hii ya IPTL ulishaanza, lakini ulisimamishwa kwa sababu ya utashi wa kisheria, sasa nimezungumza na Waziri anasema wanasubiri kwanza uamuzi wa mgogoro huo ndio mitambo hiyo ibadilishwe, sijaridhika, alisema Rais Kikwete.
Alisema iwapo Wizara hiyo itasubiri uamuzi huo, hali ya mitambo hiyo na umeme kwa ujumla itakuwa ni mbaya, kwa kuwa uamuzi wenyewe utachukua muda mrefu, kwani mpaka sasa yameanza kusikilizwa mashauri madogo madogo pekee na kesi ya msingi bado.
Rais Kikwete alisema IPTL ambayo serikali haichukui umeme kwake kwa muda wa miaka miwili sasa, ilikuwa ikiiuzia umeme Tanesco kwa gharama kubwa kutokana na mitambo yake kutumia dizeli, hivyo ikibadilishwa na kutumia gesi gharama itapungua mara tano ya sasa.
Akizungumzia mtambo huo wa gesi wa umeme, Rais Kikwete alisema hiyo ni moja ya juhudi za serikali kupitia Tanesco za kutafuta ufumbuzi wa mitambo ya dharura ambayo utalifanya shirika hilo liache kutegemea mitambo ya maji ambayo ilisababisha mgawo wa umeme mwaka 2006.
Hakuna aliyesahau yaliyotokea 2006, mgawo ule ulikuwa ni mkubwa na wa kihistoria Tanzania, yote hiyo ni kutokana na kutegemea mabwawa, lakini sasa tunaegemeza nguvu katika kutafuta njia mbadala na huu mtambo ni moja ya njia hizo, alisema Kikwete.
Alisema katika mwaka huo wa 2006 kutokana na hali kuwa mbaya, serikali iliamua kukodisha mitambo ya dharura ili kukabiliana na hali hiyo, akitoa mfano wa Dowans, lakini pia ilijiwekea malengo ya kujenga mitambo yake yenyewe ya gesi asilia na mafuta.
Alisema nia hiyo inaanza kutimia na kutia moyo, kwa kuwa pamoja na mtambo huo wa Ubungo ambao utazalisha megawati 103, pia mtambo wa Tegeta wenye megawati 45 unaendelea na utakamilika mwakani, kugeuza mitambo ya IPTL na kuwa gesi na mradi wa kusambaza mitambo vijijini ambao uko katika utekelezaji.
Alisema mitambo ya kusambaza umeme vijijini tayari imenunuliwa na itaanza kufungwa Loliondo, Kigoma, Kasulu, Kibondo na Sumbawanga na kwamba serikali imeweka mpango wa kuhakikisha kila wakala wa umeme vijijini anakuwa na fedha za umeme.
Hata hivyo, aliisisitizia Tanesco kuwa karibu na kujenga ushirikiano wa dhati na wabia wa umeme, kwa kuwa miradi mingi ya umeme ina gharama kubwa na inahitaji msaada wao. Aliwataja baadhi ya wafadhili kama Sweden, Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB), Benki ya Dunia na Marekani kwa mchango wao.
Pamoja na hayo, Rais Kikwete aliwataka wananchi kuwafichua wahalifu wote wanaohujumu miundombinu ya Tanesco hasa ya usafirishaji umeme kama vile nguzo, wizi wa mafuta ya transfoma na nyaya na kulitaka shirika hilo kuweka zawadi kwa ye yote atakayemfichua mhalifu wa aina hiyo.
Eti utakuta mtu anaiba vyuma vya umeme na kuuza kwenye vyuma chakavu huyu ni stupid, ni ujinga kabisa na wote wanaofanya hivyo ni wajinga, tushirikiane tuwafikishe kwenye mikono ya sheria, alisema. Aidha, aliitaka Tanesco kuwa makini katika kushughulikia malalamiko ya wananchi, kwani tayari ameshapokea ujumbe mfupi wa simu kutoka kwa mwananchi ambaye analalamikia kelele na moshi wa mitambo hiyo mipya.
Msipoangalia wanaweza hata kuandamana kwa hili, alisema. Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Dk. Idris Rashid, alisema mtambo huo wa Ubungo wenye mashine 12 aina ya 20B34SG zilizotengenezwa na Kampuni ya Wartisila na kuchangia asilimia 15 hadi 20 kwenye gridi ya taifa na uliogharimu Sh bilioni 99.4, ni moja ya miradi sita ya umeme ya Tanesco ambayo iko nayo mbioni kufunguliwa.
Aliitaja miradi hiyo kuwa ni kituo cha umeme cha megawati 200 cha Kinyerezi, kituo cha megawati 60 cha mafuta mazito Mwanza, kituo cha makaa ya mawe cha megawati 200 Kiwira, kituo cha nishati ya upepo cha megawati 50 cha Singida na kituo cha megawati 200 hadi 300 cha Mnazi Bay.
Alisema mipango iliyopo kwa sasa ya shirika hilo ni kufunga njia za umeme za msongo zenye kilovolti 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga kilometa 650, msongo wenye kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Arusha kilometa 500, msongo wenye kilovolti 400 kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam na wanafikiria iwapo miradi hiyo itafanikiwa, kuuza umeme nchini Kenya.
Kwa upande wake, Waziri Ngeleja alisema suala la mitambo ya IPTL ameshapokea maelekezo na fedha zilizokusanywa dola za Marekani milioni 20 zitatumika kuanza mchakato wa kuibadilisha mitambo hiyo. Serikali kupitia Ngeleja, ilibaini kwamba imekuwa ikitapeliwa kwa kuilipa zaidi IPTL) kinyume na makubaliano na hivyo suala hilo lilipelekwa Mahakama Kuu ambako kesi bado inaendelea.
IPTL yenyewe hivi karibuni ilisema iko tayari kufanya mabadiliko hayo iwapo itaruhusiwa na gharama ya umeme kwa Tanesco itakuwa ni dola za Marekani milioni 2.5 sawa na Sh bilioni tatu kwa mwezi. Kuhusu deni lililopo ambalo ni zaidi ya Sh bilioni 80 za capacity charge wanatarajia suluhisho lake mwakani.