JAMAA KUMBE WALIBEBWA
Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Jan Poulsen
Allan Goshashy, Bangui
KOCHA Mkuu wa Taifa Stars, Jan Poulsen alishindwa kujizuia baada ya kushudia kikosi chake kikipokea kipigo kutoka kwa Jamhuri ya Afrika Kati pale alipomshutumu mwamuzi wa mchezo huo kuwa alipewa hongo kuiua Tanzania jijini Bangui.
Poulsen alitoa tuhuma hizo wakati alipokuwa akitoa mtazamo wake kuhusu mechi yake dhidi ya Afrika Kati ambayo ilishudia Taifa Stars ikipokea kipigo cha mabao 2-1.
"Nafahamu nimesema maneno hayo makali kwamba mwamuzi alipokea rushwa na mwizi wa ushindi wa Taifa Stars, lakini ndivyo alivyokuwa mwamuzi," alisema Poulsen.
"Katika mechi nzima mwamuzi alikuwa akiipinga Stars na kuwapendelea wenyeji kwa kuwapa faulo nyingi karibu na goli letu."
Poulsen alisema alishangazwa zaidi na mwamuzi alipokataa bao la pili la Stars ambalo lilifungwa na Athumani Machupa baada kuunganisha krosi ya Mbwana Samata aliyewapiga chenga mabeki wawili katika winga ya kulia na kupiga krosi iliyomkuta mfungaji.
Kutokana na maamuzi mabovu ya mwamuzi, Joseph Lamptey kutoka Ghana, ilifika wakati kocha Poulsen alikuwa akivua koti lake na kulitupa chini kabla ya kuliokota na kulitupa kwa nguvu kwenye benchi la wanalokaa wachezaji wa akiba.
Poulsen alikuwa akionekana akipingana na maamuzi ya mchezo mara nyingi yaliyokuwa yakitolewa na mwamuzi huyo, huku akionyesha ishara mbalimbali za kuonyesha wachezaji wake walikuwa hawatendewi haki uwanjani.
Mara baada ya pambano kumalizika mwamuzi wa mchezo na wasaidizi wake walitolewa uwanjani huku wakiwa wamezungukwa na wanajeshi wengi hadi kwenye vyumba vyao vya kubadilisha nguo, na kujifungia.
Viongozi wa Stars waliokuwepo kwenye msafara huo wenyewe pia, walikuwa wakionekana kutoridhishwa na maamuzi ya mwamuzi na walisimama katika mlango wa kutoka kwenye uwanja kuingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo na walikuwa wakisikika wakimwambia mwamuzi hakuchezesha kwa haki, lakini wakati huo mwamuzi alikuwa akipitishwa na wanajeshi hao kwa haraka.
Akizungumzia kuhusu kiwango kilichoonyeshwa na wachezaji wake, Poulsen alisema anawaonea huruma vijana wake ambao walicheza kwa kujituma ila hawakutendewa haki na mwamuzi uwanjani.
Alisema: "Kipindi cha kwanza vijana wangu walijitahidi, lakini Jamhuri ya Afrika Kati walikuwa wakitumia faida ya kucheza nyumbani na kuleta mashambulizi kwetu , lakini pia uwanja ulikuwa siyo mzuri kwa upande wetu kwa sababu ya utelezi na sisi tulijitahidi wasilisogelee goli letu, ila walipata bao moja, ingawa sisi hatukuwa wazuri katika ushambuliaji katika kipindi hicho."
Poulsen alisema katika kipindi cha pili ilibidi afanye mabadiliko, kwa kumtoa John Boko na kumuingiza Mbwana Samata na alimtoa Mwinyi Kazimoto na kuingia Athumani Machupa ambao walibadilisha mchezo katika safu ya ushambuliaji.
"Wachezaji hawa walipoingia waliongeza nguvu kubwa katika ushambuliaji na kuanza kuisumbua ngome ya Jamhuri ya Afrika ya Kati na Stars ikapata bao la kusawazisha, na baadaye kidogo Machupa akafunga bao la pili ambalo lilikuwa zuri ambalo lingeifanya Stars kuwa mbele 2-1, lakini kwa ajabu lilikataliwa na mwamuzi,"alisema Poulsen.
Kutokana na kupoteza mechi hiyo dhidi ya Jamhuri ya Afrika Kati, Poulsen alisema Stars bado ina nafasi ya kufuzu kushiriki Fainali za Mataifa ya Afrika ingawa inakabiliwa na mechi mbili ngumu dhidi ya Algeria na nyingine dhidi ya Morocco kuweza kujiweka katika nafasi nzuri.
Naye Athumani Machupa ambaye alikuwa mfungaji wa bao hilo la pili la Taifa Stars lililokataliwa alisema anaamini lile ni goli safi na lilikuwa halina kasoro yoyote kwa sababu kila mtu aliyekuwa uwanjani aliona na hata mashabiki wao walikaa kimya zaidi, lakini mwamuzi alilikataa bao lile.
"Mimi nilichokifanya nilikwenda tu kuugusa ule mpira sikumgusa golikipa wala kumchezea faulo kwa sababu yeye golikipa wakati anatoka mimi nilikuwa nilishaugusa mpira siku nyingi upo nyavuni ila kipa wao alichokifanya aliruka na kujiangusha miguuni mwangu na refa akasema kipa ameguswa kwa hiyo ni faulo," alisema Machupa.
Taifa Stars inatarajiwa kuondoka leo nchini Afrika Kati majira ya saa saba mchana kupitia Cameroon halafu Kenya kabla ya kutua Dar es Salaam saa tano na robo usiku.