Kinachoviponza vyama vya upinzani katika chaguzi

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,006
Kinachoviponza vyama vya upinzani katika chaguzi

Selemani Rehani
Raia Mwema
Novemba 25, 2009

MWAKA 1992 tuliamua kurejea katika mfumo wa vyama vingi vya siasa. Ni miaka 17 sasa toka tuingie katika mfumo wa vyama vingi. Chaguzi tatu zimekwishafanyika katika mfumo huu wa vyama vingi. Tunaweza kabisa kufanya tathmini ya kukua kwa uwezo wa vyama vya siasa, na hasa vyama vipya vya upinzani.

Uchaguzi wa kwanza katika mfumo wa vyama vingi 1995, Chama tawala cha CCM kilipata viti 186, CUF viti 24, NCCR MAGEUZI viti 16, CHADEMA viti 3, UDP viti 3 na TLP kiti 1.

Mwaka 2000, CCM walipata viti 202, CUF viti 17, NCCR MAGEUZI kiti 1, CHADEMA viti 4, UDP viti 3 na TLP viti 4. Mwaka 2005, CCM walipata viti 208, CUF viti 19, NCCR MAGEUZI hawakupata hata kiti kimoja, CHADEMA viti 4, UDP kiti 1 na TLP kiti 1.

Matokeo ya urais: Mwaka 1995 mgombea wa CCM kwa nafasi ya urais alipata 59.22%, NCCR –MAGEUZI alipata 21.83%, CUF ilipata 5.02%, CHADEMA alipata 6.16% na UDP ilipata 3.32%.

Matokeo ya urais mwaka 2000: Mgombea wa CCM kwa nafasi ya urais alipata 65.3%, NCCR –MAGEUZI alipata 3.6%, CUF alipata 11.2%, CHADEMA alipata 4.2% na UDP alipata 4.4%.
Matokeo ya urais mwaka 2005: mgombea wa CCM kwa nafasi ya urais alipata 80.28%, (Huu ulikuwa ni ushindi wa kishindo), NCCR –MAGEUZI alipata 0.49%, CUF alipata 11.68%, CHADEMA alipata 5.88%.

Takwimu hizi zinatueleza kuwa kwa kutumia kigezo cha kuungwa mkono katika chaguzi hizo juu, tunaweza kusema kuwa vyama vya upinzani vimekuwa vikiendelea kudorora kwa kufanya vibaya sana katika chaguzi hizi. Kwa upande mwingine Chama tawala CCM kimekuwa kikiongeza ushawishi wake na kufanya vizuri katika chaguzi kwa kuongeza idadi ya kura na viti bungeni.

Takwimu hizo pia zinaonyesha kuwa bunge letu bado linatawaliwa na chama kimoja. Iwapo bunge la namna hili linaweza kuisimamia serikali na kuhakikisha kuwa inafanya kazi yake, ni suala la mjadala.

Lakini mara nyingi bunge la namna hili hukabiliwa na changamoto kubwa katika kuisimamia serikali, hasa ukizingatia ukweli kuwa wabunge wana “wajibu kwa chama chao na kwa serikali inayotokana na chama chao”. Changamoto hii inakuwa ni ngumu sana kukabiliana nayo hasa pale inapokuwa hakuna mipaka kati ya chama na serikali.

Kwa nini vyama vya upinzani vimeendelea kufanya vibaya katika chaguzi mbalimbali? Swali hili si rahisi sana kulijibu na halina jibu moja. Hilo linathibitishwa na ukweli kuwa yamekuwepo maelezo kadha wa kadha yanayoeleza sababu za vyama vya upinzani kushindwa vibaya katika chaguzi.

Muhimu ni kuwa na uchambuzi wa kisayansi na tuwe objective ili tuweze kujua sababu hasa za dhati zinazosababisha hali hii. Tutakapofanya hivyo, basi ndipo tunaweza kupata dawa na ndipo tutaweza kupata majawabu ya kweli ya matatizo haya. Hili litatuwezesha kuwa na vyama imara vya upinzania, ushindani wa dhati na demokrasia kukua zaidi.

Wapo wanaoamini kuwa vyama vya upinzani huwa vinaibiwa kura. Hii ni hoja teketeke sana na haina mashiko yoyote. Mpaka sasa hatujawahi kupewa ushahidi wa dhati kabisa unaoonyesha kuwa kura huwa zinaibiwa wapi? Katika hatua gani ya uchaguzi? Na namna gani? Haya huwa ni madai tu yanayotolewa bila ushahidi wowote.
Tunafahamu kuwa wagombea na vyama vya siasa huwa na mawakala wao ambao wajibu wao ni kuangalia zoezi zima la uchaguzi na upigaji kura ikiwa ni pamoja na zoezi la kuhesabu kura na hutakiwa kutia saini karatasi ya matokeo iwapo wanakubaliana na matokeo ya uchaguzi.

Kama ni kweli kuna wizi wa kura kwa nini mawakala hawa wasikatae kutia saini zao? Na kwa nini wasitoe maelezo yanayojitosheleza kueleza wizi unafanyika wapi na vipi? Kwa ushahidi ambao hauna shaka yoyote? Na kwa nini wasitoe takwimu zao ambazo wamekusanya?

Hoja hii haina ushawishi na hasa ukingalia takwimu hapo juu utaona kuwa tofauti ya kura za CCM kwa mfano mwaka 2005 ni kubwa sana - 80.28% dhidi ya chama kinachoshika nafasi ya pili 11.68? Hii ni tofauti kubwa sana, na ni ushindi mkubwa sana kwa chama tawala.

Aidha wanaoshikilia hoja hii hawajatueleza je katika yale majimbo machache wanayoshinda huwa inakuwaje wanashinda? Kwa nini huko wizi huwa hautokei?

Lakini kubwa zaidi ni kuwa vyama vya upinzani hushindwa hata kusimamisha wagombea kwa asilimia mia moja katika chaguzi mbalimbali. Hilo limejitokeza hata katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliomalizika hivi karibuni.

Tutazame mifano michache. Mwaka 1995 CCM kilisimimasha wagombea 232 ikiwa ni 100% CUF wagombea 171 ikiwa ni 73.7%, TLP wagombea 55 ikiwa 23.7%, NCCR MAGEUZI wagombea 191 ikiwa ni 82.3%, CHADEMA wagombea 153 ambao ni 65.9% na UDP wagombea 119 ambao ni 51.3%.

Mwaka 2000 CCM kilisimimasha wagombea 231 ikiwa ni 100%, CUF wagombea 138 ikiwa ni 59.7%, TLP wagombea 112 ikiwa 48.5%, NCCR MAGEUZI wagombea 93 ikiwa ni 40.3%, CHADEMA wagombea 66 ambao ni 28.6% na UDP wagombea 66 ambao ni 28.6%.

Kila chama kina haki ya kusimamisha wagombea kwa asilimia 100 katika kila uchaguzi, lakini vyama vya upinzani havijaweza kufikia lengo hilo. Uwezo wa kusimamisha wagombea una umuhimu wa pekee. Unaonyesha uwezo wa raslimali, oganizesheni nzuri na kukomaa kwa chama na muhimu zaidi, chama kinaonyesha kuwa kina mtandao nchi nzima.

Chama kinapokuwa na wagombea kutoka katika baadhi tu ya mikoa kinaonyesha kuwa bado hakijawa na sura ya kitaifa, na hivyo wapiga kura wanaweza kabisa wasikiamini kukipa dhamana ya kuongoza dola.

Uchache wa idadi ya wagombea ni kigezo kimojawapo cha jinsi chama kilivyojikita katika jamii kiasi cha kuweza kujitokeza. Kwa uzoefu wa Tanzania sura inayojitokeza ni kuwa wakati chama tawala kimekuwa kinasimamisha wagombea kwa asilimia mia moja, vyama vya upinzani kwa ujumla wao na kimoja kimoja vimekuwa vikipungukiwa na uwezo huo.

Katika baadhi ya majimbo wagombea wa chama cha tawala wamekuwa wakipita bila kupingwa. Hii si dalili nzuri katika ujenzi wa demokrasia.
Wapo wanaosema kuwa vyama vya upinzani vinashindwa vibaya kutokana na kutokuwepo katiba inayokidhi mfumo wa vyama vingi. Katiba tuliyo nayo sasa haijakidhi mfumo wa vyama vingi.

Ni kweli kuwa mfumo wetu wa sasa haujaweza kuweka mazingira ya uwanja kuwa sawa kwa vyama vyote vinavyoshindana. Hoja hii inaweza kuwa ya msingi. Kwani mara nyingi vyama vya upinzani huwa havitendewi sawa kulinganisha na chama tawala. Vyombo vya habari vya serikali na binafsi hutoa nafasi kubwa sana kwa chama tawala.

Mara nyingi unaweza kusikia chama cha upinzani kimekataliwa kufanya mkutano au maandamano. Vyombo vingine hujkuta vinaegemea sana kwa chama tawala na kuvinyima fursa sawa vyama vya upinzani.

Katiba inaweza kuwa inachangia katika kushindwa vibaya, kwa mfano mkuu wa mkoa ambaye ni mwanachama wa chama tawala na pengine ni mbunge itakuwa ni vigumu sana kuonekana haegemei upande wowote katika kuvihudumia vyama vya siasa. Hivyo hivyo kwa wakuu wa wilaya, wakurugenzi na watumishi wengine wa serikali.

Pamoja na uzito wa hoja hii ya katiba, ni ukweli pia hata kama tungekuwa na katiba ya namna gani, vyama vya upinzani visingeweza kushinda uchaguzi iwapo vinashindwa hata kusimamisha wagombea wa kutosha katika majimbo yote. Hii ni changamoto kubwa kwa vyama vya upinzani.

Tunacho chama kikubwa lakini hakina mbunge hata mmoja upande wa bara. Viongozi na wanachama wa vyama vya upinzani wanapaswa kuitafakari hali hii na kufanya juhudi za makusudi kuirekebisha.

Ni imani yangu kuwa kama matatizo mengine yaliyopo katika vyama vya upinzani yakitafutiwa ufumbuzi, basi inawezekana kabisa kwa vyama vya upinzani kupata ushindi katika katiba hii ambayo labda haikidhi mazingira ya mfumo wa vyama vingi.

Ushahidi wa hilo ni viti vichache ambavyo wapinzani wameweza kuvipata kwa kutumia katiba hii hii. Ni maoni yangu kuwa iwapo vyama vya upinzani vingeweza kuwa na oganizesheni nzuri, vikajenga hoja madhubuti kwa wananchi, uongozi imara, umoja na mshikamano na kuepuka migogoro, vingejenga imani vingeweza kuwashawishi wananchi na vingepata ushindi angalau wa kuridhisha.

Siamini kabisa kuwa vyama vya upinzani vinashindwa kwa sababu eti havina sera nzuri. Sina hakika kama watanzania wanachagua kwa kulinganisha sera za vyama mbalimbali.

Ninaamini kuwa sera za vyama vya siasa, pamoja na chama tawala hazifahamiki miongoni mwa wapiga kura wengi, hasa vijijini. Hivi ukimuulza mwanachi wa kawaida, kwa mfano, sera ya maji, au ya elimu ya chama chochote, anaweza kuwa na jibu?

Nachelea kusema hata wasomi wengi hawajui sera mbalimbali za vyama vya siasa. Ni namna gani watanzania wanachagua ni suala la utafiti wa kina.

Zipo sababu za msingi hasa zinazosababisha kushindwa vibaya kwa vyama vya upinzania. Mtazamo Hasi : Kama nilivyowahi kusema katika makala yangu iliyopita, ni sababu mojawapo. Wakati tunaingia katika mfumo wa vyama vingi msisitizo mkubwa uliwekwa katika upande mweusi wa athari mbaya za vyama vingi.

Watu waliaminishwa kuwa vyama vingi vitaleta vita, ukabila na magomvi. Upande wa pili wa shilingi wa faida za vyama vingi haukupewa msisitizo kabisa. Matokeo yake ni wananchi wengi kuamini kuwa vyama vingi ni vita na vurugu. Hali hii bado haijabadilika na hasa kwa wananchi ambao hawapati taarifa. Hiyo ilichangangiwa na kukosekana kwa elimu ya uraia juu ya mfumo wa vyama vingi kama ilivyopendekezwa na Tume ya Nyalali.

Waanzilishi wa vyama vya upinzani : Wengi wao walikuwa ni viongozi ambao walikuwa chama tawala wakatolewa au kufukuzwa kwa sababu moja au nyingine. Kuingia katika vyama vya upinzani huku wakiwa wametoka kwa sababu ya matatizo fulani kuliwaondelea kuaminika miongoni mwa wananchi.

Propaganda ambayo ilienezwa ni kuwa hawa wamejiunga na upinzania baada kuwafukuzwa kutokana na madhambi yao. Ingekuwa vyema kama waanzilishi wangekuwa ni watu ambao hawana doa katika jamii, ila wameamua kujiunga na upinzani kwa sababu wanaamini kuwa vyama hivi vina sera na programu nzuri kwa maneno mengine vina visheni ambayo nao wanaikubali.

Migogoro isiyokwisha ndani ya vyama vya upinzani: Baada ya vyama hivi kuanzishwa, si vyote lakini vingi viligubikwa na mizozo na migogoro isiyokwisha. Baadhi ya migogoro hii ilichukua muda mrefu sana. Na kwa kiasi kikubwa migogoro hii ilikuwa ni ya kugombea uongozi na ruzuku. Ikajotokeza dhana ya kupandikizwa mamluki.

Lakini kama ninavyosema ni yale yale ya kushindwa kuukabili ukweli na kujisahihisha. Kwa nini mamluki wapandikzwa upande mmoja tu? Pia tabia ya baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani kuhamahama, kutoka chama kimoja kwenda chama kingine, nayo ilidhoofisha upinzani na kuufanya ukose imani miongoni mwa wananchi.

Viongozi ambao walikuwa upinzani na walikuwa wakikutukana chama tawala katika majukwa, ghafla wakarudi katika chama tawala na sasa wanawatukana wapinzania. Hali hii si tu inadhoofisha upinzani bali pia inadhalilisha mfumo mzima wa siasa nchini kwetu.

Tabia ya kuhamahama miongoni mwa viongozi wa upinzani tena wa ngazi za juu umeonyesha kuwa kinachotafutwa ni madaraka tu. Upinzani pia umekuwa ukifanya makosa kusubiri wale waliotemwa na chama tawala katika kinyanganyiro cha uchaguzi wa ndani na kuwapokea wao na kuwasimamisha kugombea nafasi mbalimbali. Hili nalo linaleta sura mbaya kwa upinzani.

Migogoro hii ni ya zamani na kwa kiasi kikubwa imepungua lakini ilidhoofisha sana upinzani na kuondoa imani ya wananchi kwa vyama vya upinzani. Ni wazi kuwa wananchi walijiuliza; iwapo wanagombana wenyewe kwa wenyewe je tunaweza kuwamini kuwapa dola?

Hata kwa vile vyama vichache ambayo havikuwa na migogoro kama CHADEMA viliathirika kwani kwa bahati mbaya vyama vyote vya upinzani huwekwa kundi moja na kama ni kosa la chama kimoja huwa ni la vyama vyote.

Aidha zimekuwepo juhudi za makusudi za kuibua imani zisizo za kweli (myths) dhidi ya vyama vya upinzani vinavyoonekana kuelekea kufanya vizuri katika kukuza uwezo wake. Kumekuwepo na dhana kuwa vyama au chama fulani ni cha kabila fulani au ni chama cha fujo na vurugu, hii imesaidia kupunguza ukuaji wa uwezo wa vyama fulani vya upinzani.

Vyama vya upinzani vimeshindwa kuongeza au kupata wafuasi kutoka katika makundi kama ya wafanyakazi, wakulima, au makundi ya matajiri walioibuka katika miaka ya hivi karibuni. Chama tawala kimeweza kuongeza kundi la wafanyabiashara matajiri ambao wamejiunga pamoja na watawala kwa faida ya pande hizo mbili. Juhudi za kutenganisha siasa na biashara hazina budi kuungwa mkono.

Katika zama tulizo nazo pesa imekuwa ni nyezo muhimu sana ya kupata uongozi. Wenye pesa wanaweza kuwanunua wananchama na kura na wasio na pesa wakakosa wananchama na kura zao.

Katika mazingira ya namna hii ambapo pesa ndicho kigezo pekee cha kupata wananchama na kura za wapiga kura Chama tawala kitaendelea kuwa na mapato makubwa zaidi ikilinganishwa na vyama vya upinzani na hivyo kuendelea kuwapo madarakani.

Vyama vya upinzani vimekosa mshikamano, hivyo basi kudhoofisha nguvu za kuweza kupata wafuasi wengi zaidi na kuwashawishi wananchi wengi zaidi. Vyama vya upinzania vimeshindwa kujikita katika jamii hasa vijijini ambako ndipo asilimia kubwa ya watanzania wanaishi huko.

Zipo sababu nyingi zinazopelekea shughuli za vyama vya upinzani kutojulikana huko vijijini ikiwa ni pamoja na kuwapo kwa mfumo mbaya wa upashanaji habari kupitia vyombo vya habari.
Vyombo vya serikali bado vinakabiliwa na changamoto ya kuweza kutoa habari ambazo haziegemei upande wowote. Pili, vyombo vingi vya habari vimejazana kwenye miji mikubwa. Lakini kibaya zaidi ziko sheria ambazo zinafanya utangazaji na usambazaji wa habari hapa nchini kuwa mgumu ikiwa ni pamoja na sheria ya utangazaji namba 6 ya mwaka 1993 inayozitaka redio na TV kutangaza masafa aslimia 25 ya nchi.

Demokrasia ndani ya vyama vya upinzani bado ni changamoto kubwa. Hiki ndio kimekuwa chanzo cha migogoro mingi ndani ya vyama hivi. Vyama hivi vinaongozwa na utashi na uwezo wa watu binafsi kuliko taratibu, mila na desturi za vyama hivyo. Maamuzi mengi yanafanywa na viongozi bila kufuata taratibu na kwa kweli maamuzi hayatabiriki, kwani itategemea kiongozi anaegemea wapi.

Katiba za vyama vyote pamoja na chama tawala zinawapa madaraka makubwa mno viongozi wa vyama hasa wenyeviti ngazi ya Taifa wakiwa na uthibiti mdogo kutoka kwa wananchama wa kawaida au viongozi wa chini. Vikao vinafanyika katika ngazi za juu tu na maamuzi yanafanywa na vikao vya juu na kutelemshwa chini katika ngazi za chini (top down).


Kama vyama vya upinzani vitajitazama upya na vitazingatia haya niliyoyagusia, hakika vina uwezo wa kukibwaga Chama Cha Mapinduzi au hata kuwa tu na wabunge wa kutosha bungeni kiasi cha kulichangamsha zaidi bunge letu.

Selemani Rehani ni mwandishi mwalikwa (guest writer) wa safu hii. Mwandishi wa kawaida wa safu hii, Johnson Mbwambo yupo likizo vijijini.


srehani@hotmail.com 0756 209666 0756 209666
 
Katika kuukuza upinzani nchini ili uwe na nguvu zaidi, naona ipo haja ya Registrar wa political parties kupewa meno zaidi kama wanavyotaka kufanya huko Unguja, ili chama either kikubali matokeo ya uchaguzi au kama kinapinga basi kiende Mahakamani na sio chama kujitangazia chenyewe kuwa kimeshinda lakini eti kimeibiwa kura. Utoto huu ukome kwa uchaguzi wa mwakani, kwani is costing us a lot!!!
 
Matokeo ya urais: Mwaka 1995 mgombea wa CCM kwa nafasi ya urais alipata 59.22%, NCCR –MAGEUZI alipata 21.83%, CUF ilipata 5.02%, CHADEMA alipata 6.16% na UDP ilipata 3.32%.

mwaka 1995 CHADEMA haikuwa na mgombea urais.

Matokeo ya urais mwaka 2000: Mgombea wa CCM kwa nafasi ya urais alipata 65.3%, NCCR –MAGEUZI alipata 3.6%, CUF alipata 11.2%, CHADEMA alipata 4.2% na UDP alipata 4.4%.

mwaka 2000 CHADEMA haikuwa na mgombea urais.

sasa kama ameanza kwa kupotosha na mhariri kaamua kuibandika makala bila kuihariri mnataka hayo mengine yaaminiwe?
 
Matokeo ya urais: Mwaka 1995 mgombea wa CCM kwa nafasi ya urais alipata 59.22%, NCCR –MAGEUZI alipata 21.83%, CUF ilipata 5.02%, CHADEMA alipata 6.16% na UDP ilipata 3.32%.

mwaka 1995 CHADEMA haikuwa na mgombea urais.

Matokeo ya urais mwaka 2000: Mgombea wa CCM kwa nafasi ya urais alipata 65.3%, NCCR –MAGEUZI alipata 3.6%, CUF alipata 11.2%, CHADEMA alipata 4.2% na UDP alipata 4.4%.

mwaka 2000 CHADEMA haikuwa na mgombea urais.

sasa kama ameanza kwa kupotosha na mhariri kaamua kuibandika makala bila kuihariri mnataka hayo mengine yaaminiwe?
Asante ndugu kwa kutukumbusha na mimi naongeza mwaka 1995 CHADEMA ilikuwa inawaunga mkono NCCR MAGEUZI na mwaka 2000 wakawaunga mkono CUF na katika makubaliano baadhi ya majimbo wasimamishe mgombea mmoja ndio maana unaona vyama hivyo vilivyoungana havikusimamisha wagombea kwa 100%
 
uchu wa madaraka kwa viongozi wa vyama vya upinzani,wanakuwa wagombea wa kudumu kiasi kwamba wanatia wasiwasi.
 
Good info Bubu, huwa nawaambia wanaokataa vyama vya upinzani visikosolewe ni kuwadanganya!!! actually matokeo ya siasa chafu za CCM ni watu kutovipigia kura hivi vyama.Njia pekee ni vyama vya upinzani kuwa clean katika kila kitu.

Hapo juu hata kama wakiunganisha nguvu bado sana,labda miujiza itokee.

Kazi ipo kubwa sana kuwaaminisha wananchi kuwa wapinzani wanaweza, na hii ni wapinzani kuwa kweli wapinzani.....sio 'compromiser'....wala negotiators....wala kujikombakomba CCM...


Wakati kuna maendeleo ya mawasiliano tangu 1995 mwaka waliofanya vizuri, trend ilitakiwa kuongezeka ila inashuka vibaya.

mwaka 95' urais wapinzani walipata 21% kwenye kura ya urais(wa kwanza), miaka 10 baadae 11%. trend ya 95 ingeendelea basi kulikuwa na uwezekano mwaka 2005 wapinzani wangeshika nchi, lakini wapi

Hii inaonyesha

1.Upinzani kamili utatoka CCM
2. Vyama bado havina ushawishi.kazi ugomvi, ruzuku, n.k
3.wapinzani hawajatumia nguvu ya mawasiliano

KUNA TATIZO


sad!
 
Kwanza kabisa Vyama vya upinzani viondoe Tamaa na Uchoyo wa Kijinga Vijikusanye katika Vyama VIWILI au VITATU tu ili viwe na Nguvu ya kuikabili CCM sasa hivi vipo 16 ukitoa CCM. Mgawanyiko wao unaipa CCM nguvu za kutawala hasa ukichukulia kuwa ndio chama pekee kilichokuwepo na hivyo kimejichimbia vya kutosha.Baada ya kujikusanya/kujiunga wafanye kazi ya kuwaelimisha Wanachi/Wapigakura VIJIJINI narudia VIJIJINI kwani huko ndiko kura ziliko na ndiko kunakohitajika elimu ya mchanganuo kwa Mwananchi ajue THAMANI ya KURA yake na asiiuze kwa chupa ya POMBE au kwa KILO YA SUKARI.Bila shaka Elimisho hilo lipite mijini pia. Ikiwa wataendelea na TAMAA waliyonayo ya kila Mmoja kufikiria Tumbo lake watasota mpaka Kiama kiwakute. Takwimu zilizotolewa hapo zinaonyesha BAYANA kabisa kuwa Vyama vya Upinzani vitaendelea KUFUA JAZI ya CCM. Cha kuwaokoa ni Kubadili MTAJI kwa kuunganisha Nguvu. Mnapambana na NYANGUMI si PAPA au KIDAGAA. MPIRA MNAO Nyinyi Kuucheza juu yenu. (kila la heri)
 
uchu wa madaraka kwa viongozi wa vyama vya upinzani,wanakuwa wagombea wa kudumu kiasi kwamba wanatia wasiwasi.

sidhani kama ni uchu wa madaraka mkuu, wanaingia kwenye uchaguzi wakijua watashindwa, hawajiulizi njia za kushinda. wanataka kula ruzuku, sifa na allowance za hapa na pale! wahuni tu(ashakum si matusi)
 
CCM: Chama cha mafisadi
Chadema: Chama cha ndiy mzee kutoka kilimanjaro (goup and assocites)
CUF: Chama cha Maalim seif

Bottom line chagua mtu makini hakuna hata chama moja makini bongo, ni vikundi vya wapuuzi na wachuuzi
 
Back
Top Bottom