diana chumbikino
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 428
- 368
OKTOBA 14 mwaka huu, Watanzania wanaadhimisha kumbukumbu ya miaka 20 tangu kutokea kifo cha muasisi wa taifa hili, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyefariki dunia Oktoba 14, 1999 katika hospitali ya Mtakatifu Thomas, kule London Uingereza.
Mwalimu Nyerere, licha ya kustaafu urais mwaka 1985 na kufariki miaka 20 iliyopita, bado ameendelea kuishi katika mioyo ya wengi, wakikumbuka kwa uzalendo wake, ubinadamu na hasa kwa kujitolea na kuipenda nchi yake kwa dhati. Ndiyo maana, kila mwaka, kila kona ya nchi, makundi mbalimbali, wakiwemo wasomi, wanasiasa, watafiti na wadau wa mambo mbalimbali, wamekuwa wakiendesha semina, makongamano, mijadala na tafiti mbalimbali zinazomhusu muasisi huyo wa taifa.
Mwaka huu, ukiwa ni wa nne tangu kuingia madarakani kwa serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli, makongamano, midahalo na semina mbalimbali zimekuwa zikiendelea kuhusu kumbukuzi hii muhimu ambayo itafikia kilele chake Jumatatu ijayo ambayo kwa heshima yake, imepewa hadhi ya kuwa siku ya mapumziko kitaifa.
Mwenyekiti wa Umoja wa Wafuasi wa Mwalimu Julius Nyerere, unaohusisha wanasiasa mbalimbali waliofanya kazi karibu na Baba wa Taifa, Paul Kimiti, anazungumza na Nipashe kuhusu mambo mbalimbali kuelekea kumbukizi hii, akichambua ndoto za Mwalimu zinavyoakisiwa kwenye kazi za Rais John Magufuli
MAONI YANAVYOAKISIWA
Mzee Kimiti, ambaye enzi za Mwalimu alikuwa mwalimu wa siasa makao makuu ya chama, mkuu wa mikoa kadhaa na baadaye waziri, anazungumzia jinsi ambavyo ndoto ya kujitegemea ya Mwalimu Nyerere, inavyoshughulikiwa kwa kasi na weledi na Rais Magufuli. “Sisi ambao tulifanya kazi kwa karibu na Mwalimu wakati wa Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, tunafahamu nini hasa ilikuwa ndoto yake.
Mwalimu aliamini kwamba siyo jambo jepesi kwa nchi changa kama Tanzania wakati huo kuweza kuamua kufuata aina moja ya siasa ikiwa tegemezi, ndiyo maana akaanzisha siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, akiamini kuwa kama taifa litajitegemea, kwa mahitaji yake yote muhimu, ni rahisi kuamua aina ya siasa ya kuifuata. “Mwalimu alipenda sana taifa lijitegemee, lisiwe ombaomba kwa sababu siku zote ukiwa unaomba huwezi kuwa huru, ni lazima utafuata matakwa ya anayekupa kile unachokiomba.
Angalia, katika wakati ambao taifa lilikuwa limejitoa kuzisaidia nchi zingine za Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara zipate uhuru wake, lakini bado aliweza kujenga viwanda vya bidhaa mbalimbali karibu kila mkoa, nia yake kuu ikiwa ni kujitegemea.” Anasema Kimiti.
Anakumbusha zaidia kuwa :“Ukiangalia kwa umakini dhana hii, japo Mwalimu alishindwa kuitimiza wakati wa uongozi wake, lakini ni wazi kuwa Rais John Magufuli anaelekea kuitekeleza kwa kwa namna anavyofanya kila njia kuhakikisha kuwa taifa linajikomboa kutoka utegemezi wa mataifa ya nje na kuijengea uwezo wa kuweza kufanya mambo yake yenyewe,” anaongeza.
KAZI ZA NYERERE
Kimiti ambaye ndiye aliyesimamia shughuli zote za mazishi ya Mwalimu Nyerere, yaliyofanyika kijijini kwake, Butiama mkoani Mara, anasema anamtazama Rais Magufuli kama kiongozi ambaye ameamua kwa makusudi kuhakikisha taifa linajitegemea kupitia rasilimali zake. “Mambo anayoyafanya hivi sasa yasingewezekana kwa kutegemea fedha za misaada. Siku zote watu wanaotukopesha hawapendi tujitegemee, wanatupa msaada wa leo ili kesho turudi tena kuwaomba na hivyo kuerndelea kuwa tegemezi.” Anaongeza Kimiti.
Anataja mfano wa ujenzi wa bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere Rufiji, akieleza kuwa mradi huo ukikamilika, taifa litakuwa limepiga hatua kubwa sana kuelekea kujitegemea, kwa sababu viwanda vingi vitakuwa na uhakika wa umeme kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa mbalimnbali. “Ujenzi wa reli ya kisasa ya kutumia umeme, maana yake taifa litaweza kusafirisha abiria na bidhaa kwa wingi ndani ya muda mfupi, na hivyo kuharakisha maendeleo ya taifa kwa watu kuwa huru kupeleka bidhaa kokote wanakotaka kwa wakati.
“Wahisani siku zote wanataka tuwaabudu kwa kila jambo, angalia jinsi serikali ya awamu ya tano inavyofanya jitihada za kujenga vituo vya afya, hospitali kubwa na vifaa tiba nchi nzima. Hii inaondoa hofu ya kuwa na taifa ambalo haliwezi kuwapa tiba raia wake na hivyo kutegemea huduma hizo kutoka nje. “Jambo la kufurahisha sasa ni kuwa vitu vyote hivi vinafanyika kwa kutumia fedha za ndani, kama ambavyo Mwalimu Nyerere alidhamiria.
Serikali imedhibiti mianya yote ya rasilimali kuchotwa na watu wachache kwa faida yao, leo hii kodi inayokusanywa, mapato yanayopatikana kupitia rasilimali zetu mbalimbali, zinaonekana kwa sababu kila mmoja ni shahidi wa namna ambavyo taifa letu linasonga mbele. “Mwalimu hakuruhusu madini kuchimbwa, kwa sababu aliamini wananchi wake hawajaelimika, akatoa fursa ya wanafunzi wote kusoma bure kwa gharama za serikali kuanzia darasa la kwanza hadi chuo kikuu, lengo lake lilikuwa ni kuzalisha wasomi ambao kwa elimu yao, wataweza kusimamia rasilimali za nchi kwa faida ya wote, ” anasema.
Aidha, Mzee Kimiti anasema ujenzi wa reli, bwawa la umeme, hospitali na vituo vya afya vinavyoendelea kujengwa sehemu mbalimbali, vitaifanya Tanzania kuwa taifa la mfano miaka michache ijayo, kwani maendeleo, ni namna ambavyo wananchi wananufaika na huduma zinazotolewa, akitumia msemo usemao “Matajiri wote duniani hawafanyi kazi kwa ajili ya fedha bali wanafanya fedha ifanye kazi kwa ajili yao”. “Maana ya msemo huu ni kwamba ili tuweze kujua thamani ya fedha zetu, ni lazima fedha hizi ziwasaidie wananchi kwa kupata kwa uhakika na kwa wakati kwa huduma zote muhimu ikiwemo elimu, afya na nyinginezo,” anasema Mzee Kimiti na kuongeza kuwa huo ndiyo msingi wa Ilani za Chama Cha Mapinduzi, kama mwongozo wa 1971, Ibara ya 28 inavyotamka kwamba “Kitendo chochote kinachompa mtu uwezo wa kuamua maisha yake na kutawala maisha yake, ni kitendo cha maendeleo, hata kama hakimwongezei afya wala shibe, lakini ni kitendo anachoamua mwenyewe”.
Mzee Kimiti anaongeza : “Sera ambazo Mwalimu Nyerere alizikazania sana ilikuwa , ajira, mishahara na bei za bidhaa. Katika bei, aliamini kwenye ujamaa wa kweli, bei za vitu ni lazima zifanane, zisiwe na tofauti kubwa na hii ndiyo ilipelekea kuanzishwa kwa kampuni za biashara za mikoa maarufu kama RTC. “Aidha Mwalimu hakutaka uwepo wa tofauti kubwa katika mishahara ya watumishi wa umma, hii ni kwa sababu kungekuwa na unyonge miongoni mwa wananchi, kama utaona, Rais Magufuli amepunguza sana mishahara ya watumishi kwa sababu mtu mmoja hawezi kulipwa milioni 40 kwa mwezi wakati mwingine anapata laki tatu.
“Utaona pia dhana ya Mwalimu ya uanzishwaji wa viwanda, alilenga kutoa ajira kwa Watanzania kwa sababu ndizo huchukua watu wengi, kitu ambacho Rais Magufuli anakifanya hivi sasa akihimiza ujenzi wa viwanda kila anapokwenda, akiamini taifa linakwenda katika uchumi wa kati na viwanda’ anasema Kimiti