Kila mtu akijitetea kutumia katiba itakuwaje..

Rugas

JF-Expert Member
Jan 8, 2009
1,048
196
Naona kama kuna mambo hayaeleweki kwenye katiba yetu ya nchi.....

We hebu ona mashoga wanajitetea na kuomba haki yao kwa kutumia katiba ya nchi..

Mwishowe hata wala unga watataka watambuliwe kwa kutumia katiba hii hii....

Soma sehemu ya habari hii kutoka mwananchi la leo..


Watetezi wa haki za mashoga waandamwa...

WATETEZI wa haki za mashoga na wasagaji nchini, walioishtaki Tanzania kwenye Kamati ya Haki za Binadamu Umoja wa Mataifa (UN), wakidai kuwa haki zao hapa nchini zinakiukwa wakati katiba inaruhusu haki sawa kwa wote wamekumbana na upinzani mkali.


Viongozi wa dini na wanaharakati wengine wamepinga madai hayo wakisema shughuli za mashoga ni kinyume na mapenzi ya Mungu na ukiukaji wa misingi ya utu wa binadamu.


Maoni hayo yamekuja baada ya watetezi hao kuwasilisha ripoti yao UN, ikieleza kile wanachodai kuwa sheria za hapa nchini zinazuia uhuru wao katika suala la mahusiano kwa watu wenye jinsia moja.


Ripoti hiyo ambayo imetumwa na taasisi tatu zisizo za kiserikali ambazo ni Centre for Human Rights Promotion inayojitaja ya Afrika Mashariki, International Gay and Lesbian Human Rights Commission (IGLHRC) na Global Rights inaeleza kuwa, wana matumaini kuwa ripoti hiyo itatoa mwanga kwa jamii juu ya malalamiko yao dhidi ya serikali ili hatimaye wafikiriwe.


Wawakilishi wa watetezi hao wametaja majina yao kwenye ripoti hiyo kuwa ni Julius Kyaruzi ambaye ni mratibu LGBTI Tanzania, Monica Mbaru mratibu wa programu IGLHRC; na Stefano Fabeni, mkurugenzi wa LGBTI Initiative na Global Rights.


Taasisi hizo zimedai kuwa, Tanzania bado ina sheria ambazo zinapinga uhuru binafsi wa mtu na kutengeneza matabaka kwa kufanya hisia za mtu kuwa hazikubaliki kisheria na siyo hisia halisi.


Baada ya ripoti hiyo kutolewa mwezi huu na kuwasilishwa kwa vyombo vya habari wanaharakati wa haki za binadamu na viongozi wa dini hapa nchini, wamekuwa na maoni tofauti kuhusu madai hayo.


Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), Ananilea Nkya amesema kuwa, kama watu hao wanataka haki zao zitambuliwe wajitokeze hadharani kwanza ili jamii iwajue.


“Tunatakiwa tuwajue, hivyo ni vizuri wakajitokeza na siyo kujificha,” alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mtandao wa Jinsia nchini (TGNP), Usu Mallya alisema kuwa watu hao wana haki kwa kuwa jamii ina mifumo mbalimbali ya maisha.

“Misingi ya katiba inatambua uhuru wa kila mtu, hivyo wana haki kama kikundi na jamii inahitaji kulitambua hilo,” alisema Mallya.


Alisema jamii inatakiwa kutambua mahitaji yao, kama ilivyoweza kutambua mahitaji ya watu wengine nchini.


“Kwenye jamii kuna watu tofauti ni kama watu wenye ukimwi, jamii ilivyokuwa haitaki kuwapa nafasi lakini elimu imeonyesha ni jinsi gani mambo yanavyoweza kubadilika,” alisema.


Mkurugenzi wa Kituo cha Haki za Binaadamu (LHRC) Francis Kiwanga alisema kuwa, LHRC inafanya utafiti jinsi gani suala hilo linaweza kushughulikiwa.

Alisema kama watu hao wanataka wakubaliwe inabidi jamii iulizwe kwa kuwa ni suala ambalo ni tete.


“Ni suala tete, hivyo watu waulizwe na wabunge wahusishwe ili kuangalia sheria inasemaje katika hilo,” alisema.


Alisema hata hivyo, suala hilo ni gumu kukubalika katika jumuiya ya Afrika.


Askofu Mkuu Msaidizi wa Kanisa Katoliki, jimbo la Dar es Salaam, Methodius Kilaini alisema kama watu hao ingekuwa ni walemavu wanataka kutambuliwa haki zao ingekuwa sawa, lakini kwa hilo wanalolitaka haiwezi kukubalika.


“Kama ni walemavu wanataka tuwatambue sawa, lakini kwa sisi hatuwezi kukubali, ni kitu ambacho hakikubaliki na hakiwezi kutambuliwa kwa kuwa Mungu ameumba jinsi mbili na itabaki kuwa hivyo,” alisema Kilaini.


Alisema kuwa suala la usawa ambalo wanadai limekiukwa kutokana na katiba kuruhusu, ni kitu ambacho hawaelewi kwa kuwa usawa unaoelezewa kwenye katiba ni wa jisia ya kike na kiume na siyo ya uhusiano wa kimapenzi kwa watu wa jinsi moja.


“Usawa hauwezi kupinga uhalisia, mwanamke atabaki kuwa mwanamke na mwanamume atabaki kuwa mwanamume kama Mungu alivyoumba,” alisema.


Kilaini alisema kuwa katiba inatambua hivyo na haitambui mwanamume kujigeuza kuwa mwanamke na mwanamke kujigeuza kuwa mwanamume.


Katika ripoti yao taasisi hizo tatu zimetaka marekebisho yafanyike katika sheria ya makosa ya jinai (Penal Code) ambayo inazuia masuala hayo kwa kuyafanya kuwa jinai.


Hata hivyo, Msemaji wa Wizara ya Sheria na Katiba, Omega Ngole alikiri kuona ripoti ya watetezi hao wa mashoga, na kufafanua kuwa sheria za nchi siyo tu zipo kwa ajili ya kulinda haki za watu wote, bali pia kulinda utu wa mtu.
 
Back
Top Bottom