20th January 2011
Polisi adaiwa kumpiga risasi dereva teksi Arusha
Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha linadaiwa kukumbwa na kashfa nyingine, baada ya askari wake mmoja kumpiga risasi ya shingoni dereva wa teksi na kumjeruhi.
Askari huyo ambaye alikuwa amevaa sare za jeshi hilo huku akiwa na bunduki aina ya SMG, alimpiga dereva huyo risasi sehemu ya shingoni
Dereva huyo, Jamal Abdul (32), amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) katika Hospital ya Selian jijini hapa.
Taarifa za tukio hilo zimeeleza kuwa askari huyo ambaye polisi bado wanafanya uchunguzi juu ya tukio hilo, alifika katika eneo la Shivaz, Kaloleni Jumatatu wiki hii majira ya saa 10:00 alfajiri, ambako dereva taksi huyo huegesha gari lake namba T.976 AGZ aina ya Toyota Mark II saloon, na kumtaka ampeleke katika kituo cha Polisi cha Ngarenaro, baada ya makubaliano ya kulipwa Sh. 3,000.
Imeelezwa kuwa baada ya kufika karibu na kituo hicho, askari huyo alimwamuru dareva huyo kusimama na alimtaka ampatie Sh. 7,000 ili ampe noti ya Sh. 10,000.
Wakati dereva huyo akijaribu kutoa noti hiyo 10,000 ,askari huyo aliyekuwa ametoka nje ya gari hilo, ghafla aliikoki bunduki na kumfyatulia risasi moja iliyompata Abdul sehemu ya shingo na kutokeza upande wa pili na kumjeruhi pia katika bega la kushoto.
Kwa mujibu wa maelezo ya dereva huyo aliyekuwa akiongea kwa taabu hospitalini hapo, anamtambua mtu huyo kuwa ni askari polisi na kwamba baada ya kukumbwa na masahibu hayo, aliamua kwenda katika kituo cha polisi Ngarenero, kuomba msaada.
"Chakushangaza mara baada ya kufika kituoni hapo, askari wa waliokuwa zamu siku hiyo waligoma kunifungulia, mlango na kunitaka niende kituo kikuu cha polisi mjini kati kwa ajili ya kupata msaada zaidi," alisema Abdul.
Alisema wakati akiwa na askari huyo wakielekea Ngarenaro, cha kushangaza kila wakati askari huyo alikuwa akiwasiliana na watu kadhaa kwa simu muda wote.
Inadaiwa kuwa baada ya askari huyo kumpiga dereva huyo, alipora gari hilo na kuelekea eneo la Mbauda, ambapo alifanya tukio la uporaji wa fedha katika kituo kimoja cha mafuta akiwa na wenzake.
Habari zaidi zilieleza kuwa baada ya tukio hilo la uporaji, askari huyo na wenzake waliondoka na gari hilo, lakini waliligonga gari aina ya Toyota Hiace eneo la Mbauda na kuamua kulitelekeza gari hilo na kutokomea kusikojulikana wakiwa na mfuko wa fedha.
Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo, walidai kuwa mfuko huo ulikuwa ukidondosha fedha barabarani, huku askari huyo na wenzake wakiendelea kukimbia wakiwa wamevaa sare za polisi na SMG.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha,Thobias Andengenye, alisema kuwa taarifa juu ya tukio hilo amezipata na wanafanya uchunguzi.
"Tutatoa taarifa juu ya tukio hilo, bado tunafanya uchunguzi kubaini ni askari gani alihusika na tukio hilo, maana inawezekana pia siyo askari bali majambazi waliamua kuvaa sare ili kujifanya polisi," alisema Andengenye.
Hata hivyo, familia ya Abdul waliokutwa wodini hapo, ambao hawakutaka kutajwa majina yao, walilalamikia Jeshi la Polisi kwa kushindwa kutoa ushirikiano juu ya tukio hilo, japo wanakiri kuwa baadhi ya viongozi wa jeshi hilo, wamefika hospitalini hapo kumjulia hali majeruhi huyo.
CHANZO: NIPASHE