NGOJA TUUFUFUE
HOTUBA YA MWISHO YA MTUME MUHAMMAD (s.a.w)
Siku ya 9 ya Mwezi wa Dhulhijja, mwaka wa 10 Hijriya, baada ya kuonesha kwa vitendo jinsi hijja itakavyotekelezwa na umma wake na baada ya kukamilisha wajibu zote zinazohusu hija, Mtukufu Mtume (s.a.w) alitoa Hotuba yake ya Kuaga, katika mlima Arafat, mahali ambapo leo kuna Masjid Namirah:
“Enyi watu!
Yasikilizeni maneno yangu kwa umakini! Hakuna ajuaye…huwenda mwaka huu ukawa wa mwisho kwangu kuwa hapa pamoja nanyi!
Enyi watu!
Kama ambavyo siku hizi, miezi hii na mji huu ni vitukufu, vivyo hivyo, uhai wenu, mali zenu na staha zenu ni vitukufu. Ni haramu kuvikiuka.
Enyi Waislamu!
Kesho, mtakutana na Mola wenu na kuhesabiwa kwa yale mnayoyatenda leo! Msirejee kinyumenyume kwenye mila zenu za zamani na kuchinjana nyinyi kwa nyinyi baada yangu! Jueni kwamba nitawatangulieni na kuwasubiri kwenye Birika (la Kawthar)! Nitajifakhiri kwa idadi yenu juu ya umma nyingine! Angalieni msinishushe chini (kwa kuangukia katika dhambi)!
Enyi Waislamu!
Kila mwenye amana ya mtu airejeshe kwa mwenye nayo! Kila aina ya riba imefutwa; iko chini ya migu yangu. Bali mtu anatakiwa kurejesha mkopo. Usidhulumu wala usidhulumiwe! Sasa kujihusisha na riba kumeharamishwa kwa amri ya Mwenyezi Mungu. Mambo yote yenye kuchukiza, yaliyokuwa yakifanywa katika zama za Ujahiliya, sasa yako chini ya miguu yangu. Riba ya kwanza ninayoifuta ni ile ya (ami yangu) Abbas ibn Abdulmuttalib.
Enyi Maswahaba!
Uhasama wa enzi za Ujahiliya, nao umefutwa moja kwa moja. Taasubi ya kwanza ninayoifuta ni ile ya Rabia, mjukuu wa AbdulMuttalib.
Enyi watu!
Leo shetani amepoteza nguvu yake ya kurejesha ushawishi na mamlaka yake katika hii ardhi yenu. Lakini, bado ataendelea kufurahi iwapo mtamfuata katika mambo ya upuuzi, mbali na yale ambayo nimeyafuta. Jiepusheni nayo pia ili kuilinda dini yenu!
Enyi watu!
Chungeni haki za wanawake! Amilianeni nao kwa upendo na huruma! Ninawausieni kumcha Mwenyezi Mungu kuwahusu wanawake! Mmewachukuwa wanawake kama amana ya Mwenyezi Mungu; staha na heshima yao kwa jina la Mwenyezi Mungu! Mna haki juu ya wanawake, nao wana haki juu yenu! Haki mliyonayo juu ya wanawake ni kwamba wasiruhusu yeyote kuikanyaga heshima ya familia yenu! Haki ya wanawake juu yenu ni kuwa mnatakiwa kuwapa, kihalali, matumizi na mavazi. Hairuhusiwi kwa mwanamke kutoa kitu katika mali ya mumewe na kumpa mtu bila ruhusa yake.
Ama kuhusu watumishi wenu, walisheni katika vile mnavyokula nyinyi wenyewe na muwavike katika vile mnavyofaa nyinyi wenyewe. Wakifanya kitu ambacho hamuwezi kuwasamehe, basi waacheni waondoke! Lakini msiwaadhibu; kwa maana, nao ni waja wa Mwenyezi Mungu.
Enyi waumini!
Sikilizeni maneno yangu na myazingatie vizuri! Muislamu ni ndugu wa Muislamu; hivyo Waislamu wote ni ndugu. Hairuhusiwi kudhulumu haki ya ndugu yako katika dini, labda kama ataitoa kwa ridhaa yake mwenyewe.
Enyi Maswahaba!
Msizidhulumu nafsi zenu! Nafsi zenu zina haki juu yenu pia!
Enyi watu!
Mhalifu ni mwenye kuwajibika kwa kosa lake yeye mwenyewe. Mtoto hatabeba adhabu ya kosa la baba! Wala baba hatawajibika kwa uhalifu wa mwanaye!
Enyi watu!
Mwenyezi Mungu amempa kila mwenye kustahiki, haki yake (katika Qur’an)! Mwenye kurithi hahitaji wosia! Kitanda atakachozaliwa mtoto, hapo ndipo kwake. Mzinifu atanyimwa. Ghadhabu na laana ya Mwenyezi Mungu, Malaika na Waislamu wote itamkuta yule mwenye kudai kuwa katika nasaba tofauti na ile ya baba yake au mtumishi asiye na fadhila anayedai kuwa anatoka kwa mtu mwingine tofauti na bwana wake! Mwenyezi Mungu haikubali toba na ushuhuda wa watu hao.
Enyi watu!
Mola wenu ni Mmoja! Vivyo hivyo baba yenu ni mmoja; nyote ni watoto wa Adam, na Adam anatokana na udongo. Mwenye thamani zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule mwenye taqwa zaidi. Mwarabu hana ubora juu ya asiyekuwa mwarabu, isipokuwa kama atakuwa na taqwa.
Enyi watu!
Hakika zama ambazo zimeendelea kuzunguka, zimerejea katika awamu ambapo Mwenyezi Mungu aliumba mbingu na ardhi. Mwaka una miezi kumi na mbili. Kati yake kuna minne mitukufu (haram). Mitatu kati yake ni yenye kufuatana, ambayo ni Dhil-qadah, Dhil-hijjah na Muharram, na wa nne ni Rajab ((baina ya Jamadi’al-Akhir na Shaban). Mwaka huu, miezi mitukufu imerejea katika zama zake za kale. Msimu wa hijja umesadifiana na siku ya kumi ya Dhil-hijjah.
Enyi Waumini!
Ninakuachieni amana, ambayo mkishikamana nayo hamtapotea kamwe. Amana hiyo ni Qur’an, Kitabu cha Mwenyezi Mungu.
Enyi watu!
Muabuduni Mwenyezi Mungu! Tekelezeni swala tano za kila siku! Fungeni swaumu wakati wa mwezi wa Ramadhan na mtii maamrisho yangu! Hivyo mtaingia Peponi.
Enyi watu!
Tahadharini na kupindukia hali ya kiasi! Kupindukia katika dini ndiyo sababu iliyowafanya waliokuwa kabla yenu kuangamia! Jifunzeni taratibu za hijja kutoka kwangu! Huwenda nisiweze kukutana nanyi tena hapa, baada ya mwaka huu! Wale waliopo wafikishe maneno yangu kwa wale ambao hawapo! Huwenda yule aliyefikishiwa akayaelewa vizuri zaidi na kuyalinda maneno yangu kuliko mfikishaji.”
Baada ya kusema maneno hayo, aliwauliza maswahaba zaidi ya laki moja na elfu ishirini waliokuwepo hapo: “Enyi watu…kesho mtaulizwa kuhusu mimi; mtasema nini?”
“Tunashuhudia kuwa ulitekeleza wajibu wako kama Mjumbe wa Mwenyezi Mungu, ukatuonya na kutuusia”, umati wa waumini ulisema kwa pamoja.
Kufuatia ushuhuda huo wa Waumini, Mtukufu Mtume (s.a.w) akauliza mara tatu: “Je nimefikisha?” Maswahaba wote wakatoa kauli za ushuhuda, ndipo alipoinua mikono yake juu na kumuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu awe shahidi:
“Shuhudia ewe Mola wangu! Shuhudia ewe Mola Wangu! Shuhudia ewe Mola wangu!”
(REJEA: Muslim, Hajj, 147; Abu Dawud, Manasiq, 56; Ibn Majah, Manasiq, 76, 84; Ahmad, V, 30; Ibn Hisham, IV, 275; Hamidullah, al-Wasaiq, uk. 360)
***************************
MAZINGATIO
Hotuba hii ya Kuaga ni sheria zinazoratibu mahusiano ya kijamii, mukhtasari wa mafunzo ya Uislamu na, wakati huo huo, ni mizani ya mwenendo na haki za binaadamu. Kabla ya uundwaji wa Azimio maarufu la Haki za Binaadamu, La Fayette, mwanafalsafa maarufu wa Kifaransa anayetambulika kuwa miongoni mwa waasisi na nguzo muhimu ya Mapinduzi ya Ufaransa ya mwaka 1789, baada ya kufanya utafiti wa kina kuhusu mifumo mbalimbali ya kisheria duniani, hatimaye alikutana na Hotuba ya Mwisho ya Mtukufu Mtume (s.a.w); na alipoiona kuwa inawakilisha misingi ya haki na uadilifu kwa wanadamu wote, akalazimika kukiria: “Ewe Muhammad Mwenye ukuu…! Umefikia kilele cha juu kabisa cha uadilifu kiasi kwamba hakuna mtu aliyekifikia na hakuna atakayekifikia!”
Katika Hotuba hiyo, Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w) anaainisha kanuni ambazo wanadamu wanatakiwa kuzijua ili pasiwepo na udhuru kwa kutozijua. Umati mkubwa uliokuwepo uliwezesha yaliyomo katika Hotuba hiyo kuwafikia wanadamu wote.