Hivi vyeo vina kazi/Tija gani kwa taifa maskini Tanzania

dosama

JF-Expert Member
Dec 25, 2010
912
957
NASEMA kama wewe hujapata cheo katika nchi hii basi ujue una tatizo. Hivi vyeo vyote hivi katika nchi hii bado wewe hujapata hata kimoja? Tangu ubalozi wa nyumba kumikumi hadi hivi vya juu kabisa vya wanaoitwa waheshimiwa? Kama ulikuwa hukuambulia ubunge ina maana hata mkuu hajakuona kwenye hivi vya ukuu wa wilaya vilivyotangazwa juzi-kati? Mie huko simo maana sikuambulia kitu mwanawani.

Eti nasikia kuna wilaya zilikuwa hazina wakuu wa wilaya maarufu kama DC kwa kipindi cha kutosha? Lahahula! Kama wilaya inaweza kuendelea kuwepo bila ukuu wa wilaya mwaonaje tukafanyia upya haya maamuzi ya hawa “marais” wa wilaya? Wahuni huko mitaani wanasema eti hiki cheo wanapewa makada watiifu wa chama kama asante. Nasema hayo ni ya wahuni, sio ya watu wenye heshima zao kama miye Mzee Mzima. Kwenye hili wala sijitoi.

Lakini hebu tuache utani halafu tujiulize vijiswali vya umbea kidogo. Kazi kubwa ya mkuu wa wilaya ni ipi hasa? Nasikia kwenye wilaya kuna halmashauri ya wilaya na nyie wa mijini mna manispaa. Nasikia hizi halmashauri na manispaa zina watu wanaitwa wakurugenzi. Hivi hawa wasingetosha kuendesha wilaya jamani? Wacha nikae kimya maana wengine watadhani nawaonea donge wenzangu. Miye sina nongwa na vyeo, hofu yangu ni gharama zinaweza kuwa kubwa mno kwenye uongozi bila sababu.

Mwaonaje tukiwapa watu kazi watufanyie utafiti ili tuambiwe Ma-DC wanaongeza tija gani katika uzalishaji wa nchi hii? Nasikia mmoja huko kaskazini kasema kazi yake kubwa kabisa ni kukamata wauzaji na wanywaji wa chang’aa, namaanisha gongo ile pombe haramu, msianze kunishangaa kwamba namshangaa huyo DC. Hivi kukamata pombe haramu mgambo si wanatosha? Hao wakiwa chini ya mkurugenzi mbona wanaweza kufanya kazi nzuri tu? Tena si nasikia kila wilaya ina mshauri wa mgambo ambaye ni afande orijino kabisa? Miye simo.

Hata kama basi kwa upendo wetu tumeona ni vizuri hawa watu wakawa na vyeo hivyo, mnaonaje wananchi tukapewa kile kinachoitwa job description yao? Maana yaelekea hata wao wenyewe hawana hakika sana wanapaswa kufanya nini. Usishangae wapo wanaodhani kazi yao ni kudumisha fikra za chama ngazi ya wilaya. Nasikia wote wako darasani huko Dodoma wakifundishwa. Hivi si mngewafundisha kwanza na kuwapa mtihani kabla ya kuwateua ili watakaofeli ile kwao? Wacha tu nikae kimya maana wapo watakaosema nalalamika kwa vile sijaapishwa na mkuu wa mkoa ili niwe na kahimaya kakusimamia katika hii Jamhuri yetu.

Mbona miaka hii mmeamua pia kuongeza wilaya? Katika zama hizi za teknolojia bado tunaogopeshwa na ukubwa wa eneo kijiografia? Kama wakina Nyerere waliweza kuitawala Tanzania yote enzi hizo hakuna hata simu za mkononi za kubipu kwa nini nyie iwe ngumu katika zama hizi za mitandao iwe ya simu, computa na wavuti? Ndio maana nasema kuna watu wanalopoka kwamba hivi vyeo wakati mwingine vinaonekana kama zawadi. Hivi unaanzisha wilaya mpya ili huduma za hospitali ziwe bora zaidi?

Gharama za kuanzisha wilaya mpya si zingepelekwa kwenye huduma za kijamii? Ukiwa na gari la wagonjwa na barabara nzuri mbona ni muhimu kuliko kuwa na jengo linaloitwa hospitali kila wilaya lakini hakuna dawa? Hilo nalo mwabisha enyi wana? Nasema haya mahela ya kujenga makao makuu mapya ya wilaya si yangepelekwa kwenye mashule na mahospitali? Na ukishaanzisha wilaya mpya si wapo na watendaji ambao lazima wawepo? Hao viongozi si ni gharama nyingine? Na ukweli mchungu ni kwamba viongozi si wazalishaji wa moja kwa moja? Hilo mwabisha? Kwenye kula mimi sitii neno msije mkaniona msaliti bure.

Hivi hiki si ndicho kipindi cha kutoa maoni ya katiba mpya? Ngoja nami niwahi nikatoe wazo kwamba kwenye katiba mpya kusiwepo na ukuu wa wilaya na kama upo basi hawa wakuu wa wilaya wagombee kama ilivyo kwa rais wa nchi. Kwani mkuu wa wilaya si ni rais wa wilaya jamani? Kama hivyo ndivyo hamuoni itakuwa raha kuongoza watu waliokuchagua? Kama inawauma sana kufuta hiki cheo basi walau tukitafutie majukumu rasmi halafu watu wagombee wakiweka ahadi zao. Hapo patakuwa patamu mwanangu. Haya ya kulala huna hili wala lile halafu unasikia ghafla umepewa uheshimiwa yafike mahala yaishe.

Nasikia waziri mkuu amewapiga mkwara wakuu hao wa wilaya wasichanganye siasa na kazi yao. Thubutu! Kwani kilichowapa ukuu wa wilaya si ni siasa? Yaani waziri mkuu anataka wamtukane mamba madhali wameshavuka mto? Kwani hajui kuna kurudi? Kama sio siasa mbona yule na yule na huyu wasingeweza kuwa wakuu wa wilaya milele? Ila waziri mkuu ana hoja. Nasema kama imefika mahali tukasema piga ua garagaza lazima hiki cheo kiwepo, basi iwe kama ajira na sharti liwe ni kwamba wakuu wa wilaya wasiwe na chama chochote wanachokishabikia, japo hiyo itakuwa hadharani tu. Moyoni hawakatazwi kuhusudu jembe na nyundo. Miye simo huko, msiniwekee maneno mdomoni.

Inabidi hata hivi vyeo vya kuteuliwa katiba ijayo viwekwe vigezo vya nani anastahili kuteuliwa kuwa nani na kwa nini. Wengi wetu tulishasahau yale ya waziri asiye na wizara maalumu! Nasikia yamerudi siku hizi. Kaka yangu JK ametukumbusha mbali sana. Nasikia Mark Mwandosya ni waziri lakini hana wizara. Kwa nchi maskini kama yetu hizi gharama za mawaziri wa aina hii ni za nini? Hivi kweli kabisa jua lingegoma kuzama kama Mwandosya asingekuwa waziri? Miye sijui lakini simo kwenye hayo yote. Ngoja niake kimya msianze kusema nina roho ya kutu. Simo kabisa!
 
umenena vyema. lakini yote haya ni kwa mujibu wa katiba iliyopo. dawa ni kuyaondoa ndani ya katiba mpya.
 
Ni kweli ma DC ni mfumo tuu wa kikoloni wa kutawaka kwa indirect rule, enzi hizo hakuna simu wa mtandao, mawasiliano yalikuwa kwa barua tuu!. Kwa sasa ma DC ni redundanty, RC na wakurugenzi wanatosha kabisa!. Kwenye katiba mpya, tutawafutilia mbali hawa ma DC!. Kazi yao kubwa ni kuogoza vikao vya kamati za ulinzi na usalama za wilaya ila kiukweli hawa ndio walikuwa kauzibe wakuu kuhakikisha watu hawaamki ili CCM itawale milele!. Sasa watu wameshaanza kuamka, ma DC can't help anymore!.
 
Nasikia kuna Tarafa. Tarafa zina viongozi pia. Naona nchi hii kila mtu aliyemnyenyekevu kwa chama anaweza kuwa kiongozi. Swali, je viongozi wote hao wanafanya kazi gani? TUPIGANIE KATIBA MPYA
 
Back
Top Bottom