Historia haijafikia tamati

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,005
Historia haijafikia tamati

Jenerali Ulimwengu Aprili 23, 2008
Raia Mwema~Muungwana ni Kitendo

KUKOSEKANA kwa mwelekeo ndani ya chama si ugonjwa wa Chama cha Mapinduzi (CCM) peke yake. Ni kweli kwamba kwa muda mrefu hicho ndicho kilichokuwa chama pekee nchini, lakini hili halikukifanya kiwe pekee kupoteza dira miongoni mwa vyama vya nchi za Bara la Afrika.

Kwa hakika katika makala zangu za mwanzo kabisa za mfululizo huu nilikwisha kutoa rai kwamba vyama karibu vyote vya nchi za Kiafrika, hata vile vilivyoanza vikiwa na mwelekeo ulioeleweka, havina tena maaana yo yote ya kifalsafa na kiitikadi.

Katika mazingira yetu mapya (ya “vyama vingi”) ugonjwa uliokuwa wa chama-tawala umeambukizwa kwa vyama vilivyozaliwa kuanzia mwaka 1992 na kuendelea.

Navyo vimeanzishwa, na vimeendelea kufanya kazi zake, bila kuwa na misingi yo yote ya kifalsafa.

Hali hii si ya kushangaza, si hapa kwetu wala duniani. Kwa muda mrefu kidogo,(labda miongo miwili hivi) dunia imekuwa ikiambiwa kwamba sasa tumefikia tamati ya historia, na kwamba masuala makuu yote yaliyosababisha malumbano, mifarakano na mapigano na vita kuu, sasa yametatuliwa kimsingi, na kilichobaki ni vijineno vyepesi vyepesi ambavyo havina uzito mkubwa katika mahusiano miongoni mwa binadamu, kati ya matabaka na wala baina ya mataifa.

Hii ndiyo injili iliyohubiriwa na baadhi ya wasomi wazito katika utetezi wa hali ilivyokuwa baada ya “Vita Baridi” kwisha na Marekani na nchi za Magharibi kupata ushindi dhidi ya himaya ya Sovieti. Kazi imekwisha, tumeshindwa, twendeni nyumbani, kwani hatuna cha kujadili tena.

Maana ya mtazamo huu ni kwamba hatuna budi kukubali hali kama ilivyo na wala tusijisumbue kujaribu kuibadilisha kwa sababu hata tungetaka tunsingeweza kuibadilisha.

Kila kitu kimekwisha kuamuliwa, matatizo yote yametatuliwa, na sasa tunachohitaji ni kujipanga upya katika himaya mpya iliyotamalaki duniani chini ya diktat (imla) mpya ya Marekani, hali ambayo imebatizwa jina la pax americana, au amani kama ilivyopangwa na Marekani.

Kwa maneno mengine, tunachoambiwa ni, “Kubalini yaishe. Tumeshindwa nanyi mmeshindwa. Hamna chenu tena, na wale watakaojidai kufurukuta tutawashughulikiwa kwa nguvu zetu zote, nao watajuta. Baadhi yenu mtakaodiriki kupinga ukweli huu usiopingika tutawanyima misaada, na baadhi yenu mnatakaozidisha ukorofi tutawachapa.

Tunao uwezo wa kiuchumi, kisiasa, kidiplomasia, kijeshi na kiutamaduni na ninyi hamna uwezo wo wote. Mnaweza kufanya nini bila sisi?”

Watawala wetu walio wengi katika nchi nyingi za Afrika wameikubali injili hii bila kuisaili. Hakuna wanachofanya bila kuzungumiza “wafadhili” na miradi mingi ambayo ingekuwa na manufaa makubwa kwa wananchi imekuwa ikiwekwa pembeni kwa muda mrefu kwa sababu eti “hajapatikana mfadhili”. Wafadhili wanatafutwa hata pale ambapo rasilimali zetu wenyewe zingetosha kabisa bila kumsubiri ye yote.

Ujuha huu ndio unaotufanya tuachie mali zetu zichukuliwe na wageni kwenda kuwaneemesha watu wao ughaibuni wakati watu wetu wanaendelea kuishi maisha ya mbwa nchini mwao. Ndivyo hivyo tulipofikia hali ya nchi za Kiafrika zenye rasilimali kubwa sana ndizo pia zinazoongoza kwa kuwa na raia hohe hahe.. Nigeria, Angola, Kongo, na nyingine.

Ndivyo hivyo tulipofikia mahali nchini Tanzania kwamba watawala wetu wala hawajui ni kiasi gani cha dhahabu kinachimbwa nchini na kupelekwa nje. Kisa? Wafadhili wanajua, na wakijua inatosha. Ujuha mkubwa kuliko huo unatoka wapi.

Na hao “wafadhili” wanawapongeza na kuwasifu watawala wetu kwa kuwa “wamefungua milango”, “wanaheshimu wawekezaji” na “wanainua uchumi wa nchi”.

Kiwango cha ujuha wa watawala wetu kinatisha. Tangu serikali ya “awamu ya tatu” (Sijui kwa nini wanaziita awamu, kwani binafsi naona awamu moja ndeeefu ya umasikini usio na maelezo) tumekuwa na serikali zilizojaa mawaziri na makatibu wakuu na watawala wengine wenye digrii za uzamili na udaktari wa kila aina. Hawa wamesoma hapa nchini na katika vyuo vikuu vya pembe zote za dunia, na wanapozungumza katika semina utadhani wana akili.

Lakini mara nyingi wanachofanya wakiwa wamekabidhiwa madaraka ya uongozi ni ujuha mtupu. Au ni ujuha kweli? Inawezekana si ujuha kwa upande wao, bali ni ujuha kwa upande wetu, sisi tunaoendelea kuwapa madaraka, tena kwa kuwapigia kura wakati tumekwisha kuona mara kadhaa, na kwa muda mrefu, kwamba maslahi yao hayapatikani katika utumishi kwa wananchi bali katika kushibisha matumbo yao.

Sasa, inapotokea, kama inavyotokea leo, kwamba wakubwa wa dunia walioshinda “Vita Baridi” ambao wanatuambia kwamba “tukubali yaishe,” wakakutana na watawala wetu wanaosaka nafasi za uongozi kwa udi na uvumba, na haya makundi mawili yakakubaliana jinsi watakvyozitafuna nchi zetu, ujue tumeliwa.

Ubia baina ya wakuu wa dunia na wakuu wetu, ubia huu haramu ndicho kiama chetu wananchi wa kawaida na hatimaye mataifa yetu yote.

Nimewaona watawala wetu wanavyovaa tabasamu paaana wanaposifiwa na wakuu wa nchi za Magharibi, kama mtoto wa shule ya msingi anavyotabasamu anaposifiwa na kutolewa mfano na “hedi masta” wake. Na kweli, uhusiano kati yetu na hao wakubwa ni huo huo, wa mtoto wa shule na “hedi masta”. Kila anachosema sisi hatuna budi kusema “Yessah.”

Huku tukitabasamu tabasamu zetu za kijuha, mali zetu zinayoyoma. Madini yetu yanasafirishwa nje ya nchi kwa bei ya bure, si kwa kutoroshwa na wageni, bali kwa kusindikizwa na watawala wetu wenyewe. Wakuu wetu, hao hao wenye digrii na digrii, wanaingia mikataba ya kitoto, si kwa sababu hawajui wanalolifanya, bali kwa sababu hao wameingia ubia na mabeberu ambao kimsingi wamewanunua na kuwageuza wapagazi wao.

Fikiria hili; Kampuni la kibeberu linahitaji kuwekeza katika sekta fulani nchini. Ili kampuni hilo likubaliwe kuwekeza linahitajika lifuate taratibu kadhaa, ikiwa ni pamoja na kujali mazingira, kujali maslahi ya wananchi watakaoathirika na uwekezaji huo, kuzingatia viwango vya kodi na vile vya mapato mengine yaliyowekwa na Bunge, n.k.

Hasara zinazoweza kutokana na kutokujali mazingira labda hazipimiki katika mizania ya fedha, lakini zinaweza kuwa kubwa, zisizotabirika na za muda mrefu. Lakini katika eneo la mapato ya serikali hasara zinazotokana na kutokujali kwa watawala wetu zinapimika kwa sababu vipo viwango vinavyotambulika kimataifa.

Kwa kila mkataba wa “uwekezaji” uliotiwa saini katika kipindi cha miaka 20 iliyopita tunaweza kukadiria ni kiasi gani cha fedha nchi imepoteza kutokana na huo ujuha usiokuwa ujuha wa watawala wetu na maofisa wao, ambao kwa kupewa “shangingi” moja ambalo bei yake haizidi shilingi milioni 80 watagawa bure kwa wageni mali za Taifa zenye thamani ya shilinggi bilioni 500.

Huu si ujuha bali ni ugonjwa wa akili.

Katika hali ya nchi zetu zilizoelemewa na umasikini, ujinga na maradhi, hali kama hii haiwezi kuachiwa iendelee kwa sababu tu tumeambiwa kwamba huu ndio mwisho wa historia na masuala yote makuu yamekwisha kushughulikiwa. Hatuwezi kukubali ujuha kama huu uendele kwa kuegemea mantiki-kilema.

Lakini inaelekea watawala wetu wanakubali ujuha huu uendelee, alimradi wakuu wanawasifu na kuwamwagia “misaada”!.

Ndiyo maana Rais Benjamin Mkapa alikuwa haelewi ni kwa nini watu wa ndani wanamsakama wakati wakuu wa nchi za nje wanamsifu. Kana kwamba hao ndio waliomchagua!

Itaendelea wiki ijayo.
 
Historia haijafikia tamati

Lakini inaelekea watawala wetu wanakubali ujuha huu uendelee, alimradi wakuu wanawasifu na kuwamwagia “misaada”!.

Ndiyo maana Rais Benjamin Mkapa alikuwa haelewi ni kwa nini watu wa ndani wanamsakama wakati wakuu wa nchi za nje wanamsifu. Kana kwamba hao ndio waliomchagua!


Ni mishindo mikubwa ya aina yeyote ile itakayo wafanya viongozi wetu wazinduke toka kwenye usingizi wa kijuha...!

Mfano bila kuona mtu kama Ben akiwajibishwa kwa kukiuka MIIKO ya uongozi, wengine wataendelea kupiga usingizi wa pono na kujitakasa kila kukicha kuwa ni wasafi.

Kishindo au vishindo sahihi vinaweza kuwabadili hata kuku kuwa Mwewe! Ilimradi uwe mshindo wa nguvu.

Mshindo wa Bom la Nuk' uliwafanya wajapan kubadilika kutoka upiganaji wa vita kuu ya pili na kuwa wapenda amani na wategeneza magari na kuedeleza tech' ya electronics.

Kishindo kwa mfano cha kumshitaki Mkapa au fisadi mwingine na akafungwa Segerea...Kingeplelekea uponaji wa FIKRA na kupata viumbe wapya wapenda taifa lao nk.

Bora viongozi walioko madarakani wa_control shock kwa kuwashitaki mafisadi walioko hadharani hivi sasa...kwani bila hivyo shock zitawafuata ambazo hazijatathminiwa na kwa namna isiyotabirika na kwa namna hii zinaweza kuwa na uharibifu mkubwa kwani lazima mshindo utatokea tu, mshindo utakao simamisha ujuha uliopo na unaoendelea..... hili halizuiliki!!
 
Back
Top Bottom