Mkurugenzi wa zamani Wanyamapori asota hotelini miezi saba
Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Chuo cha Kimataifa cha Usimamizi na Uhifadhi wa Wanyamapori Mweka (CAWM), Emmanuel Severe, anaishi hotelini kwa miezi saba sasa tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo kutokana na ukarabati wa nyumba aliyopangiwa kiushi kutokukamilika.
Kabla ya uteuzi huo, Severe alikuwa ni Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori kabla ya Waziri wa Maliasili na Utalii wa wakati huo, Profesa Jumanne Maghembe, kumhamishia chuoni hapo.
Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa Severe amekuwa akiishi chumba namba 209 katika Hoteli ya Kilimanjaro Crane ya mjini Moshi.
Gharama za kuishi katika Hoteli hiyo kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu zimefikia Sh9,924,000 ambazo zinahusisha Sh60,000 kwa siku zikiwa ni gharama za chumba na gharama nyingine za chakula.
Ukarabati wa nyumba hiyo aliyokuwa akiishi mtangulizi wake, Deogratius Gamassa, umechukua muda mrefu kutokana na ukosefu wa fedha kutoka serikalini.
...Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, alipoulizwa sababu za wizara yake kutoa pesa kwa mafungu hali inayosababisha ukarabati wa nyumba hiyo kuchelewa, alisema suala la utoaji wa fedha ni la kiutendaji ambalo hawezi kulizungumzia.