BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,006
Hatima yake bungeni wiki ijayo
na Mwandishi Wetu
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
na Mwandishi Wetu
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
JINAMIZI la shutuma limeendelea kumwandama Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, kudai kiongozi huyo alipoteza dira na kuifanya nchi ielekee kusikojulikana.
Aidha, Lipumba alisema kiongozi huyo hakuwa na mtazamo wa muda mrefu, jambo ambalo hata viongozi wengi wa sasa wameangukia katika mkumbo huo.
Anatoa sababu za viongozi hao kuingia huko kwa kushiriki kwa kasi kubwa katika vitendo vya ufisadi bila kujali masilahi ya taifa.
Kauli hiyo ya Lipumba dhidi ya Mkapa imekuja huku kukiwa shinikizo kubwa kutoka kwa baadhi ya wananchi na wabunge kutaka kiongozi huyo aondolewe kinga ili aweze kupelekwa mahakamani kwa tuhuma za matumizi mabaya ya madaraka.
Profesa Lipumba alitoa kauli hiyo juzi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Mbeya Vijijini uliomalizika hivi karibuni na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuibuka na ushindi.
Alisema kiongozi anapokosa dira ya kuona mbali humfanya ajione ana uwezo wa kufanya kila kitu kwa muda huo, bila ya kufikiri kuwa jambo analolifanya litakuwa na madhara kwa taifa au litakuja kumletea matatizo pindi aondokapo madarakani.
Mkapa hakuwa na dira ya mbali, ndiyo maana yeye na viongozi wenzake walijihusisha katika mambo ya kifisadi na hivi sasa baadhi yao ndio wanaanza kuumbuka kwa kupelekwa mahakamani, alisema Profesa Lipumba.
Alisema sifa kubwa ya kiongozi ni kujenga misingi imara ya maendeleo ya muda mrefu, lakini si kufikiri namna ya kutapanya rasilimali za taifa kama inavyoonekana hivi sasa.
Tupo njia panda, hatujui tuendako, kwani viongozi wamejisahau kiasi cha kujikuta wanabomoa misingi ya maendeleo badala ya kuijenga nchi kama wengi tulivyotarajia, alisema Profesa Lipumba ambaye kitaaluma ni mchumi.
Wakati Lipumba akimchambua Mkapa, hatima ya kuondolewa au kutokuondolewa kinga kwa kiongozi huyo wa awamu ya tatu inatarajiwa kujulikana kuanzia kesho katika vikao vya Bunge vinavyoendelea mjini Dodoma iwapo hoja ya kufanya hivyo itawasilishwa.
Habari ambazo Tanzania Daima Jumapili imezipata zinadai kuwa kuna mgawanyiko mkubwa miongoni mwa wabunge kuhusu suala hilo, huku idadi kubwa ikionekana kumkingia kifua.
Baadhi ya wabunge wanaodaiwa kumkingia kifua, wakiwemo wa kambi ya upinzani, inadaiwa wanafanya hivyo ili kumnusuru kiongozi huyo na wengine wanaoshiriki kwa namna moja au nyingine kwa matumizi mabaya ya madaraka.
Tayari Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo Ndesa Pesa (CHADEMA), alionyesha nia ya kutaka kuwasilisha hoja binafsi bungeni akitaka kinga ya Mkapa iondolewe, lakini katika siku za hivi karibuni amenukuliwa akisema hataiwasilisha hoja hiyo katika kikao kinachoendelea hivi sasa.
Pamoja na Ndesamburo kuripotiwa kutoiwasilisha, bado mbunge yeyote anaweza kujitokeza kuwasilisha hoja hiyo ambayo ili ipite itahitaji uungwaji mkono wa wabunge wasiopungua theluthi mbili.
Jambo kubwa lililopo hivi sasa ni kuelekeza macho bungeni kuona kama kuna mbunge atajitokeza kuwasilisha hoja hiyo inayosubiriwa kwa hamu kubwa na baadhi ya watu.
Wakati kukiwa na joto hilo, wiki iliyopita Mkapa aliwaonya viongozi kuacha siasa za majungu, fitina, chuki, ukabila na udini, kwani wasipofanya hivyo Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 utakuwa mgumu na kuna hatari taifa likaingia katika machafuko.
Onyo hilo alilitoa mkoani Iringa alipokuwa kwenye harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).
Alisema katika kipindi cha miaka mitatu aliyo nje ya uongozi, ameshuhudia mambo hayo kwa kiwango kinachomtia woga.
Wakati Mkapa akitoa onyo hilo, baadhi ya viongozi wa kidini wakitumia majukwaa mbalimbali ya kidini, wamejitokeza hadharani wakimtetea, kwa kudai ni kiongozi anayestahili heshima kubwa, kwa kuwa amelifanyia taifa mambo mengi mazuri, ikiwemo kukuza uchumi wa taifa.
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya siasa wanabashiri kuwa kujiingiza kwa viongozi hao kunalifanya sula hilo kuchukua mkondo wa kidini zaidi kuliko kisiasa kama ilivyokuwa hapo awali.
Wachambuzi hao wanadai kuwa, suala la Mkapa kufanywa kuwa la kidini, kuna kila dalili la kuligawa taifa kwa misingi ya kidini, hasa kuhusu utawala wa sasa unaoongozwa na Rais Jakaya Kikwete.