Hadithi: Umslopogazi na Nada

Hadithi: Umslopogazi na Nada

Lycaon pictus

JF-Expert Member
Joined
Jan 31, 2021
Posts
10,884
Reaction score
18,824
Mwandishi: H. Rider Haggard, 1892.

Install app ya Maktaba Sauti kutoka playstore uweze kusoma na kusikiliza vitabu mbalimbali.


71t4uSJv+LL._UF1000,1000_QL80_FMwebp_.webp


Utangulizi
Miaka mingi imepita—wakati wa baridi, kabla ya vita vya Wazulu, kulikuwa na mzungu aliyekuwa akisafiri kupitia Natal. Jina lake si muhimu kwa sababu hahusiki na hadithi hii. Alikuwa ameambatana na mikokoteni miwili iliyojaa bidhaa alizokuwa akizipeleka Pretoria. Hali ilikuwa ya baridi na hakukuwa na nyasi za kutosha kuwalisha ng’ombe waliovuta mikokoteni na hilo lilifanya safari kuwa ngumu sana. Alikuwa ameshawishika kufanya safari sababu ya nauli kubwa aliyotoza kwenye ule msimu, mapato ya nauli yalitosha kufidia hasara zozote ambazo angeweza kupata.

Alifanya safari yake na kila kitu kilimuendea vyema hadi alipopita mji mdogo wa Stanger, mahali ambapo zamani palikuwa na Duguza, yaani boma la Chaka. Mfalme wa kwanza wa Wazulu na mjomba wa Cetywayo. Usiku uliofuata baada ya kupita Stanger hali ilibadilika na kuwa ya baridi kali, wingu jeusi liliziba anga na kuzuia mwanga wa nyota.

‘Nisingekuwa Natal ningesema kuwa theluji nyingi itaanguka,’ alijiambia mzungu. ‘Huko Scotland mara nyingi anga kama hili hutokea kabla ya theluji.’ Akakumbuka kuwa hakujakuwa na anguko la theluji nyingi katika Natal kwa miaka mingi. Basi alikunywa mvinyo kidogo na kuvuta tumbaku, kisha akajilaza kwenye hema alilojenga chini ya mkokoteni mkubwa.

Usiku aliamshwa na baridi kali na kilio cha ng’ombe wake ambao alikuwa amewafunga. Alitoa kichwa kwenye hema na kuangalia nje. Nchi ilikuwa nyeupe kwa theluji, na hewa ilijaa theluji ikipeperushwa na upepo huku na kule.

Aliruka huku akiwa amejikunyata kwenye nguo zake, akawaita makafiri waliokuwa wamelala kwenye mikokoteni yake mingine. Waliamka wakitetemeka kwa baridi huku wamejitanda mablanketi toka kichwani hadi miguuni.

‘Harakisheni vijana,’ aliwaita kwa kizulu. ‘Harakisheni, mnataka ng’ombe wafe kwa theluji na upepo? Wafungueni ng’ombe na wapelekeni katikati ya mikokoteni; itawakinga kidogo. Aliwasha taa na kuingia kwenye theluji.

Kazi ilikuwa ngumu lakini mwishowe waliikamilisha. Haikuwa rahisi kwa mikono ya makafiri iliyokufa ganzi kufanya kazi ya kuwafungua ng’ombe. Mikokoteni ilipangwa na kuweka nafasi katikati, kwenye nafasi hii waliwekwa ng’ombe thelathini na sita na kufungwa. Mzungu akarudi kitandani na wale wenyeji wakajipasha kwa mvinyo na kuingia kulala kwenye mkokoteni wa pili na kujifunika turubai.

Kwa kitambo kidogo kulikuwa na utulivu, zilisikika tu kelele za ng’ombe wakigugumia.

‘Theluji ikiendelea hivi itabidi niwafungulie ng’ombe,’ alijisemea mzungu. ‘Hawawezi kuvumilia baridi hii.’

Haukupita muda mkokoteni wake ukatingishika sana; sauti za kamba kukatika na kwato zikasikika. Aliangalia nje tena. Aliona ng’ombe wakikimbilia gizani, wakitafuta mahali pa kujificha na baridi. Ndani ya dakika moja wakawa wametokomea kabisa. Hakukuwa na cha kufanya zaidi ya kusubiri hadi asubuhi.

Kukakucha, ardhi yote ilijaa theluji. Hakukuwa na dalili zozote za kuonyesha walikokwenda, alama zote za kwato zilikuwa zimefukiwa na theluji iliyoanguka. Mzungu akaita baraza la watumishi wake makafiri. ‘Tufanye nini?’ aliuliza.

Mmoja alisema hili na mwingine akasema kile, lakini wote walikubaliana kuwa wanatakiwa kusubiri mpaka theluji iyeyuke.

‘Au mpaka tugande tufe, nyie wapumbavu!’ alifoka mzungu, alikuwa na hasira maana alikuwa amepoteza ng’ombe wa thamani ya paundi mia nne.

Basi mzulu mmoja aliyekuwa amekaa kimya kwa muda mrefu akaongea. Alikuwa ni dereva wa moja ya mikokoteni. ‘Baabaangu,’ alimwambia mzungu. ‘Ni hivi, hakuna anayejua walikokwenda au kama wapo hai au wamekufa, lakini kwenye lile boma.’ Akaelekezea kwenye nyumba Fulani zilizokuwa juu ya kilima kama umbali wa maili mbili, ‘Anaishi mganga aitwaye Zweete. Ni mzee—mzee sana lakini ana maarifa, kama kuna mtu anayeweza kukuambia ng’ombe wako walipo basin i yeye.

‘Hekaya tu!’ alijibu mzungu. ‘Lakini kwa sababu bomani kutakuwa na joto kuliko hapa tutaenda kumuona Zweete. Bebeni chupa ya pombe naugoro kiasi kama zawadi. Baada ya saa moja akawa amefika ndani ya nyumba ya Zweete. Mbele yake alisimama mzee mmoja mzee sana, alibaki kama furushi la mifupa tu. Alikuwa haoni macho na mkono mmoja, mkono wake wa kushoto ulikuwa mweupe na uliojipinda.

‘Unahitaji nini kutoka kwa Zweete mzungu?’ aliuliza mzee kwa sauti nyembamba. ‘Hauniamini wala haiamini hekima yangu; sasa kwa nini nikusaidie? Lakini nitakusaidia japokuwa ni kinyume na sheria zenu na unatenda kosa kutaka msaada wangu. Nafanya hivyo ili kukuonyesha kuwa uganga wa kizulu ni wa kweli, nitakusaidia. Ninajua unachotafuta babaangu. Unataka kujua walipo ng’ombe wako baada ya kukimbia kwenda kutafuta mahali pa kujikinga na baridi, sivyo?’

‘Ndivyo mganga,’ alijibu Mzungu. ‘Una masikio marefu.

‘Ndiyo babaangu, nina masikio marefu japo wanasema kuwa nimekuwa kiziwi. Nina macho makali pia, japo siwezi kuona sura yako. Ngoja nisikilize, ngoja niangalie!’

Kwa kitambo kidogo alikuwa kimya, akiyumbisha mwili mbele na nyuma, kisha akasema: ‘Una shamba babaangu, huko karibu na mji wa Pine, sivyo? Na kama umbali wa saa moja hivi kutoka kwenye shamba lako anaishi kaburu mwenye vidole vine tu kwenye mkono wake wa kulia. Kwenye shamba la kaburu kuna korongo ambalo miti ya kifauongo imeota. Ng’ombe wako utawapata kwenye korongo hilo, ndiyo, safari ya siku tano kutoka hapa. Watume watu leo nao utawapata wote kasoro watatu waliokufa kwenye theluji. Sihitaji malipo yoyote! Sifanyi maajabu ili nilipwe. Kwa nini nifanye hivyo na mimi ni tajiri?’

Mzungu alibeza, lakini alituma watu. Siku ya kumi na moja aliowatuma walirudi wakiwa na ng’ombe wote kasoro watatu. Katika zile siku kumi na moja alizokaa kwenye boma la Zweete waliongea hadi usiku mwingi.

Katika siku ya tatu alimuuliza Zweete ilikuwaje mkono wake wa kushoto ni mweupe na umesinyaa, na Nada na Umslopogazi aliowataja mara kadhaa ni nani? Basi mzee yule akamsimulia kisa kinachosimuliwa kwenye kitabu hiki. Alimsimulia kila siku hadi kikaisha. Kisa chote hakijaandikwa hapa sababu mengine yanaweza kuwa yalisahaulika au yalionekana kuwa hayana umuhimu. Pia haijawezekana kwa mwandishi kupata maneno mazuri ya kuelezea kisa kama ambavyo msimuliaji angetaka. Maana kiukweli alikuwa kama anaigiza kuliko kusimulia hadithi. Aliposimulia kifo cha shujaa alionyesha ishara za kuchoma kwa fimbo yake. Hadithi ilipokuwa ya huzuni alionyesha majonzi na hata kulia. Na zaidi ni kuwa alikuwa na sauti nyingi, kila mhusika wa kwenye hadithi alikuwa na sauti yake. Mzee huyu alionekana kuishi tena katika nyakati za kale.

Mzungu yule alijitahidi kadri awezavyo kuiweka hadithi ya Zweete kama alivyosimuliwa. Na kwa sababu hadithi ya Nada—yungi yungi na wahusika wote ilimgusa sana ameamua kufanya hata zaidi, ameichapisha ili watu wengine waweze kuisoma.

Basi baada ya kusema hayo tumuache Zweete, ambaye alikuwa na jina jingine pia, aendelee na hadithi.
 
1. Unabii wa mtoto Chaka

Babaangu unasema nikusimulie habari za Umslopogazi, mmiliki wa shoka liitwalo Mleta Kilio, ambaye aliitwa Bulalio Mchinjaji, na habari za mapenzi yake kwa Nada, mwanamke mzuri kuliko wote katika Uzulu. Ni habari ndefu, lakini kwa vile upo hapa kwa siku nyingi, na katika maisha yangu inanibidi kusimulia hadithi hiyo. Kaza moyo babaangu maana nitakayosimulia ni ya kutia simanzi. Na hata sasa nikimfikiria Nada machozi yananitoka.

Babaangu, unafahamu mimi ni nani? Haufahamu. Unadhani mimi ni mganga mzee aitwaye Zweete. Watu wengi wamedhani hivyo kwa miaka mingi. Ni wachache tu ndiyo wamefahamu ukweli, maana ni siri niliyoitunza sana. Hata wakati huu wa utawala wa mzungu, na Malkia akiwa ndiye mtawala wangu lakini bado mkuki wa assegai unaweza kupenya moyo wangu iwapo watu watafahamu jina langu la kweli.

Angalia huu mkono baba yangu—siyo huo ulioharibiwa na moto; angalia huu mkono wangu wa kulia. Unauona? Mimi kipofu siuoni. Hata hivyo moyoni mwangu nauona kama vile ulivyokuwa hapo zamani. Nauona ukiwa mwekundu wenye nguvu—mwekundu sababu ya damu ya wafalme wawili. Sikiliza babaangu—inama nikunong’oneze. Mimi ni Mopo—nimeona mshtuko wako; umeshtuka kama kikosi cha nyuki kilivyoshtuka pale Mopo alipopita kati yao akiwa na assegai mkononi iliyolowa kwa damu ya Chaka iliyokuwa ikitiririkia ardhini polepole. Mimi ndiye Mopo niliyemuua Mfalme Chaka. Nilimuua nikiwa pamoja na wanawafalme Dingaan na Umhlangana; lakini pigo langu ndilo lililomtoa uhai, na bila mimi asingeuawa. Ni Dingaan, mimi na mtu mwingine ndiyo tulimuua.

Utasema, ‘Dingaan alikufa karibu na mto Pongola’

Ndiyo ndiyo, Dingaan alikufa, lakini siyo pale; alikufa kwenye mlima wa mzimu; amelala kwenye matiti ya Mchawi wa Mawe ambaye amekaa milele akisubiri mwisho wa dunia. Lakini nami pia nilikuwepo kwenye mlima wa mzimu. Wakati huo miguu yangu ilikuwa na kasi, na kisasi kilinifanya nisilale usiku. Nilisafiri mchana kutwa, usiku nilimpata. Nikiwa na mtu mwingine tulimuua—ah!ah!

Kwa nini nakusimulia haya? Yanahusiana vipi na mapenzi kati ya Umslopogazi na Nada? Nitakuambia. Nilimchoma mkuki Chaka sababu ya dada yangu Baleka, mama ya Umslopogazi, na kwa sababu aliwaua watoto na wake wangu. Mimi na Umslopogazi tulimuua Dingaan kwa sababu ya Nada, aliyekuwa ni binti yangu.

Baba yangu kuna majina makubwa kwenye simulizi hii. Wengi wameishayasikia majina hayo: majeshi ya Wazulu yaliyaita majina hayo yalipokuwa yakipiga kelele za vita. Nilihisi milima ikitikisika na maji yakitetema kwa sauti hizo, lakini wako wapi leo? Kimya kimewameza na mzungu anayaandika majina yao kwenye vitabu. Nilifungua malango nao wamepita na kwenda zao. Nilikata kamba zilizowaunganisha na dunia nao wakaanguka. Ha! ha! Wakaanguka! Pengine mpaka sasa bado wanaanguka, pengine wanarudi kwenye maboma yao yenye ukiwa wakiwa kama nyoka. Natamani ningewajua nyoka hao ili niwaponde kwa kisigino. Mbali huko sehemu za chini, kwenye makaburi ya wafalme—kuna shimo. Ndani ya hilo shimo imelala mifupa ya Chaka, mfalme aliyekufa kwa sababu ya Baleka. Mbali huko kwenye nchi ya Wazulu kuna korongo kwenye Mlima wa Mzimu. Kwenye sakafu ya korongo hilo kuna mifupa ya Dingaan, mfalme liyekufa kwa sababu ya Nada. Alikuwa ni mnene na korongo lilikuwa refu sana; alipofika chini mifupa yake ilivunjika vipandevipande. Nilikwenda kuiona baada ya ndege na wanyama wala mizoga kufanya kazi yao. Nilicheka mara tatu, kisha nikaja mahali hapa kufa.

Mambo hayo yote yalitokea zamani sana, nami bado sijafa; japo natamani kufa na kufuata njia ya Nada. Pengine nimebaki hai ili kukusimulia hadithi hii babaangu, na labda utawasimulia wazungu ukipenda. Nina miaka mingapi? Sifahamu. Ila ni mingi sana. Kama Chaka angekuwa hai, angekuwa na umri kama wangu. Katika walio hai hakuna hata mmoja niliyemfahamu nilipokuwa mvulana. Ni mzee sana hivyo natakiwa nikusimulie haraka. Nyasi zinanyauka na kipupwe kinakuja. Ndiyo, hapa ninavyoongea baridi inachoma moyo wangu. Nipo tayari kulala milele, lakini pengine nitaamka tena wakati wa majira ya kuchipua.

Nitaanza mwanzo kabisa. Kabla Wazulu hawajawa kabila kubwa—mimi nilizaliwa katika kabila la Langeni. Hatukuwa kabila kubwa, hapo baadaye wanaume wetu wote wenye nguvu walikuja kuwa kikosi kimoja tu katika jeshi la Chaka, pengine walikuwa elfu mbili au elfu tatu hivi, lakini wote walikuwa majasiri sana. Lakini sasa wote wamekufa, na wake na watoto wao pia—hakuna tena kabila hilo. Wamepotea kama mwezi upoteavyo. Nitakueleza jinsi walivyopotea polepole. Kabila letu liliishi kwa amani katika nchi nzuri tambarare. Nimeambiwa kuwa Makaburu, ambao tuliwaita Amaboona ndiyo wanaoishi huko sasa.

Baba yangu, Makedama ndiye alikuwa Chifu wa kabila letu. Alijenga boma lake kwenye kilima, mimi sikuwa mtoto wa mke wake mkubwa. Jioni moja nilipokuwa mvulana wa urefu wa kufikia mabega ya mtu mzima tulitoka na mama yangu kwenda kuangalia ng’ombe wakiingizwa zizini. Mama yangu aliwapenda sana wale ng’ombe. Alikuwepo ng’ombe mmoja aliyekuwa na rangi nyeupe usoni aliyemfuata mama yangu huku na kule. Mama alikuwa amembeba Baleka, dada yangu. Wakati huo Baleka alikuwa bado mtoto mdogo. Tulitembea mpaka tukawakuta vijana waliokuwa wakiingiza ng’ombe. Mama alimwita ng’ombe mwenye sura nyeupe na kumpatia majani ya mahindi aliyokuja nayo. Vijana waliendelea kuwaingiza ng’ombe wengine lakini yule mwenye sura nyeupe alibaki na mama. Alisema kuwa atampeleka zizini atakapokuwa anarudi. Mama aliketi na kumnyonyesha Baleka, ng’ombe aliendelea kula nami nilicheza kuwazunguka. Tukamuona mwanamke mmoja akitujia kutokea nyikani. Alitembea kama mtu aliyechoka sana. Mgongoni mwake alikuwa amebeba mikeka. Alikuwa anaongozwa na kijana wa kama umri wangu, lakini yeye alikuwa mrefu na mwenye nguvu zaidi. Kilipita kitambo kidogo kabla ya mwanamke yule kutufikia na kuketi kwenye nyasi, maana alikuwa amechoka sana. Kwa jinsi nywele zake zilivyotengenezwa tuligundua kuwa hakuwa mtu wa kabila letu.

‘Habari zenu!’ alisalimia mwanamke yule.

‘Njema,’ alijibu mama. ‘Unatafuta nini?’

‘Chakula na nyumba ya kulala. Nimesafiri kutoka mbali sana.’

‘Unaitwa nani na umetoka wapi?’ aliuliza mama yangu.

‘Jina langu ni Unandi: ni mke wa Senzangakona, natoka kabila la Zulu.’

Kuna kipindi kulikuwa na vita kati yetu na Wazulu. Katika vita hiyo Senzangakona aliua mashujaa wetu kadhaa na kuchukua ng’ombe wetu wengi. Kwa hiyo mama yangu alipomsikia Unandi akitamka vile alipandwa na hasira.

‘Unathubutuje kuja hapa na kuniomba chakula na makazi ewe mke wa mbwa wa kizulu!’ Aling’aka mama yangu. ‘Nenda zako. La sivyo nitawaita wasichana waje wakutandike na kukufukuza kutoka nchi yetu.’

Mwanamke yule, ambaye alikuwa ni mrembo sana. Alisubiri hadi mama yangu amalize kutamka maneno yake ya hasira, kisha polepole akasema, ‘Ng’ombe wako maziwa yanamdondoka. Hautatupatia hata kibuyu cha maziwa mimi na kijana wangu?’ kisha akatoa kibuyu kutoka kwenye mizigo yake na kutupatia.

‘Siwezi?’ alijibu mama yangu.

Macho ya mwanamke yule yalijaa machozi. Lakini mvulana alikunja mikono yake kifuani na kukunja sura kwa hasira. Alikuwa ni kijana mzuri mwenye macho makubwa meusi. Lakini alipokasirika macho yake yaligeuka na kuwa kama anga kabla ya mvua ya radi.

‘Mama,’ alisema. ‘Hatutakiwi hapa kama ambavyo hatutakiwi huko tulikotoka. Acha twende kwa Dingiswayo; Wamtetwa watatulinda.’

‘Sawa, twende zetu mwanangu.’ Alisema Unandi. ‘Lakini ni mbali, nasi tumechoka. Tutaanguka njiani.’

Moyo wangu ukaingiwa na huruma sababu ya mwanamke yule na mwanawe. Kwa kweli walionekana wamechoka sana. Bila ya kumwambia mama yangu, nilinyakua kibuyu na kukimbilia kwenye korongo dogo ambalo nilifahamu kulikuwa na kisima. Nikarudi na kibuyu kilichojaa maji, mama yangu alijaribu kunikamata, maana alikuwa na hasira sana, lakini nilimchenga na kumpatia yule kijana kibuyu. Mama yangu aliendelea kumtupia maneno mwanamke yule, akisema kuwa mikosi imeifikia nyumba yetu sababu ya mume wake, na kuwa anahisi mikosi zaidi itatujia sababu ya kijana wake, roho yake imemwambia hivyo. Ooh babaangu! Roho yake ilimwambia kweli kabisa. Kama Unandi na kijana wake wangekufa siku ile, nchi nzuri ya watu wangu leo hii isingegeuka pori, na mifupa yao isingelala kwenye korongo kubwa huko karibu na boma la Setshwayo.
 
Mama yangu aliendelea kuongea. Mimi na ng’ombe mwenye sura nyeupe tulitulia kimya, Baleka alikuwa akilia kwa sauti. Kijana wa Unandi alipopokea kibuyu cha maji hakumpatia mama yake, alikunywa theluthi mbili peke yake. Nadhani angekunywa yote kama kiu yake isingepoa. Alimpatia mama yake yaliyobaki naye akayanywa yote. Baada ya hapo kijana yule akatupatia tena kibuyu, mkono wake mwingine alikuwa ameshika fimbo fupi.

‘Unaitwa nani?’ aliniuliza kama vile tajiri anavyoongea na mtu mdogo na maskini.

‘Mopo,’ nilijibu

‘Na kabila lenu linaitwaje?’

Nilimjibu kuwa kabila letu linaitwa Langeni.

‘Vizuri sana Mopo. Sasa nitakwambia jina langu. Jina langu ni Chaka, mwana wa Senzangakona, na watu wangu wanaitwa Amazulu. Na nitakwambia jambo jingine zaidi. Leo hii mimi ni mdogo, na watu wangu ni wachache. Lakini siku moja nitakuwa mkubwa mpaka kichwa changu kitafika mawinguni; utaangalia juu lakini hutaniona. Sura yangu itakutia upofu; itang’aa kama jua. Na watu wangu watakuwa wakuu pamoja nami, wataila dunia yote. Nitakapokuwa mkuu pamoja na watu wangu, na kuishinda dunia yote hadi sehemu za mbali za watu kuweza kusafiri—nitalikumbuka kabila lako, kabila la Langeni, watu ambao walikataa kunipatia mimi na mama yangu kikombe cha maziwa pale tulipokuwa na njaa. Unakiona kibuyu hiki; kwa kila tone la maji litakaloweza ingia humu basi damu ya mtu mmoja lazima imwagike—damu ya jamaa zako. Lakini kwa sababu umenipatia maji wewe sitakudhuru. Wewe Mopo peke yako, nami nitakufanya kuwa mkuu chini yangu. Utanawiri pembeni yangu. Lakini ni wewe pekee ndiye sitakudhuru; hata unifanyie kosa gani, hilo naapa. Lakini huyo mwanamke.’ Alisema huku akimnyooshea mama yangu kidole, ‘ni afadhali kwake akifanya haraka na kufa mapema ili nisije kumuonyesha uchungu wa kifo cha polepole. Nimemaliza.’ Aliuma meno na kutunyooshea fimbo yake.

Mama yangu alikaa kimya kwa kitambo kidogo, kisha akasema. ‘Kijana fedhuli, anaongea kama mwanaume kweli. Ndama anayeunguruma kama fahali. Nitamfunza adabu—kijana wa nabii mwovu!’ Hapo mama yangu alimuweka Baleka chini na kuanza kukimbia kumfuata yule kijana.

Chaka alisubiri kimya kabisa. Mama yangu alipomkaribia, aliinua fimbo yake ghafla na kumpiga nayo kwa nguvu kichwani hadi akaanguka. Baada ya hilo akacheka na kugeuka kuondoka na mama yake.

Basi babaangu hayo ndiyo maneno ya kwanza niliyoyasikia kutoka kwa Chaka. Yalikuwa ni maneno ya kinabii, na yalikuja kuwa kweli. Na hata maneno yake ya mwisho niliyoyasikia yalikuwa ya kinabii pia, na nafikiri yatakuja kuwa kweli. Hata sasa naona yanaanza kuwa kweli. Kuhusu maneno aliyoniambia juu ya kukua kwa Wazulu. Je hawakukua? Aliniambia pia juu ya kuanguka kwao; na kweli walianguka. Je Wazungu hawajikusanyi hata sasa ili kumshambulia Setshwayo, kama vile tumbusi wanavyokusanyika kumzunguka ng’ombe aliyekaribu kufa? Leo Wazulu hawana nguvu ya kuweza kuwakabili. Bila shaka maneno yake ya kinabii yatatimia. Wimbo wangu ni wimbo wa watu walioandikiwa kuangamia.

Lakini kuhusu hayo maneno mengine ya kinabii, nitayazungumza wakati ukifika.

Nilimfuata mama yangu. Wakati huo alikuwa ameketi huku mikono yake ipo usoni mwake. Damu kutoka kwenye jeraha la fimbo ilimtiririka hadi kwenye ziwa lake, nilimfuta kwa kutumia nyasi. Alikaa vile kwa kitambo kidogo, wakati huo huo mtoto aliendelea kulia na ng’ombe alipiga kelele akitaka kukamuliwa. Mwishowe alitoa mikono usoni na kuniambia.

‘Mopo mwanangu, niliota ndoto. Niliota nimemuona Chaka aliyenipiga na fimbo; alikuwa mkubwa kama jitu. Alitembea kupita milima na nyanda, macho yake yaliwaka kama radi, kwenye mkono wake alikuwa na mkuki mwekundu kwa sababu ya damu. Alikamata watu kwa mikono yake na kuwachanachana. Aliyasigina maboma yao kwa miguu. Mbele yake kulikuwa na nchi nzuri ya kijani. Nyuma yake kulikuwa na nchi nyeusi kama vile imechomwa moto. Niliwaona watu wetu. Walikuwa wengi na walionawiri na waliojaa vicheko. Wanaume walikuwa ni mashujaa na wanawake warembo; walikuwa na mamia ya watoto. Kisha nikawaona tena. Walikuwa mifupa, maelfu ya mifupa kwenye eneo lenye miamba. Chaka alisimama juu ya mifupa yao na kucheka mpaka dunia ikatikisika. Kisha nikakuona wewe ukiwa mwanaume mtu mzima. Kati ya watu wetu ni wewe pekee uliyebakia. Ulimnyemelea Chaka kwa nyuma, pia pamoja nawe walikuwepo watu wengine wa ukoo wa kifalme. Ulimchoma kwa mkuki naye akaanguka na kuwa mdogo tena; alianguka na kukulaani. Lakini ulimpigia kelele masikioni mwake kwa kulitaja jina, jina la dada yako Baleka—kisha akafa. Twende nyumbani, usiku umeingia.

Basi tukaamka na kuelekea nyumbani. Lakini niliingiwa na hofu, hofu kuu.


Itaendelea.
 
2. Mopo aingia matatani

Sasa nitakuambia jinsi mama yangu alivyotimiza kile alichoambiwa na Chaka—yaani kufa haraka. Pale ambapo alichapwa na fimbo ya Chaka pakatokea kidonda kisichopona. Kisha kikatunga usaha na kuchimba hadi kikaufikia ubongo. Siku moja mama yangu akaanguka na kufa, nililia kwa uchungu sababu nilimpenda sana. Nilipata uchungu nilipoona mwili wake wa baridi na mkavu, usiojibu haijalishi niliita kwa nguvu kiasi gani. Tulimzika mama yangu na akasahaulika. Kila mtu alimsahau isipokuwa mimi—hata Baleka hakumkumbuka, maana alikuwa bado mdogo sana. Kuhusu baba yangu—alioa binti mwingine na kuridhika. Baada ya hapo sikuwa na furaha tena. Kaka zangu walinichukia sababu nilikuwa mwerevu kuliko wao, nilijua kutumia assegai vizuri na mwenye mbio kuliko wao. Basi walinifanyia maneno ya hila kwa baba yangu naye akanichukia. Lakini mimi na Baleka tulipendana maana sote tulikuwa wapweke, alining’ang’ania kama mmea utambaao unavyoung’ang’ania mti pekee nyikani. Japokuwa nilikuwa mdogo lakini nilijifunza jambo hili: kuwa na busara ni kuwa na nguvu, japokuwa wale wanaobeba assegai ndiyo wanaoua, lakini yule anayeongoza pambano kwa kutumia akili ni mkuu kuliko anayeua. Nilijionea kuwa watafuta wachawi na waganga walikuwa watu walioogopwa. Kila mtu aliwatii. Wanaume kumi wenye mikuki walimkimbia mganga mmoja japokuwa alikuwa na fimbo tu mkononi. Basi nikadhamiria kuwa mganga. Maana wao pekee ndiyo walioweza kuwaua waliowachukia kwa kutoa neno tu. Basi nikajifunza ujuzi wa uganga. Haikuwa rahisi. Nilikaa na njaa nyikani, nilifanya mambo yote uliyosikia kuhusu waganga na zaidi. Kuna busara katika uganga na uongo wetu, nawe unafahamu vyema, vinginevyo usingekuja hapa kuniuliza kuhusu ng’ombe wako waliopotea.

Mambo yaliendelea hivyo hadi nilipofika umri wa miaka ishirini na moja, mtu mzima. Wakati huo nilikuwa nimeishajifunza yote niliyoweza kujifunza peke yangu, basi nikaamua kujiunga na mganga mkuu wa kabila letu, aliitwa Noma. Alikuwa mzee sana na mwenye jicho moja. Lakini alikuwa ni mwenye akili sana. Nilijifunza mbinu mbalimbali kutoka kwake, lakini mwishowe akaanza kunionea wivu hivyo akanitegea mtego. Kuna tajiri mmoja kutoka kabila la jirani alikuwa amepoteza ng’ombe wake. Akafika kwa Noma ili amsaidie kuwapata. Noma alijaribu mbinu zake lakini hakuweza; maono hayakumsaidia. Basi yule tajiri akapatwa na hasira na kutaka arudishiwe malipo aliyotoa. Lakini Noma hakuwa tayari kurudisha hivyo kukatokea malumbano ya maneno. Yule tajiri alisema atamuua Noma, Noma naye kasema atamroga.

‘Amani jamani, amani.’ Nilisema, maana nilikuwa naogopa kutatokea umwagikaji wa damu. ‘Niruhusuni nione kama nyoka wangu ataniambia ng’ombe waliko.’

‘We ni kijana tu,’ alisema tajiri. ‘Kijana anajua nini kuhusu uganga?’

‘Hilo tutapata jibu lake hivi punde,’ nilisema na kuchukua mifupa mkononi mwangu.

‘Iache hiyo mifupa,’ alifoka Noma. ‘Hatutawahangaisha nyoka wetu sababu ya huyu mtoto wa mbwa.’

‘Mwache ajaribu,’ alisema yule tajiri. ‘Na kama ukijaribu kumzuia nitafanya mwanga wa jua uingie ndani yako kwa mkuki wangu.’ Alisema hayo na kuinua assegai yake.

Basi nikafanya haraka; nikarusha mifupa ardhini. Tajiri alikaa mbele yangu na kujibu maswali niliyomuuliza. Nafikiri baba yangu unafahamu haya mambo—wakati mwingine mganga anakuwa anafahamu mahali viliko vitu vilivyopotea, maana masikio yetu ni marefu. Na wakati mwingine roho yake humwambia, kama tu alivyoniambia kuhusu ng’ombe wako. Lakini siku ile nyoka wangu alifanya kazi yake. Sikujua chochote kuhusu ng’ombe wa bwana yule, lakini roho yangu ilikuwa pamoja nami na nikawaona ng’ombe wale. Nikamwambia kila kitu kuwahusu, rangi zao, umri na kila kitu. Pia nilimwambia walikokuwa, na jinsi mmoja wao alivyotumbukia mtoni na kufa, miguu yake ya mbele ikiwa imejifunga kwenye mizizi ya miti. Nilimwambia yote kama roho yangu ilivyoniambia.

Bwana yule akaridhika; akasema kuwa kama maono yangu yatamsaidia kupata ng’ombe wake basi malipo aliyopewa Noma nichukue mimi, akawauliza watu waliokuwapo—ambao walikuwa wengi; iwapo jambo hilo ni sawa nao wakamjibu kuwa ni sawa kabisa na watahakikisha linafanyika. Lakini Noma alikaa kimya na kuniangalia kwa jicho kali. Alijua kuwa nimefanya uganga wa kweli hivyo alikuwa na hasira sana. Lilikuwa jambo kubwa. Ng’ombe waliopotea walikuwa wengi, na kama wangepatikana kule nilikosema basi watu wangeanza kufikiri kuwa mimi ndiye mganga nguli zaidi. Muda ulikuwa umeenda na mwezi ulikuwa bado haujatoka, hivyo yule tajiri akasema kuwa atalala katika boma letu na asubuhi na mapema ataondoka nami kwenda sehemu niliyosema ng’ombe wake wako. Baada ya hayo akaenda kulala.

Mimi pia nikaelekea kwenye kibanda changu na kulala. Ghafla nikashtuka usingizini nikihisi uzito kifuani kwangu. Nilijaribu kuinuka lakini kitu fulani cha baridi kikanikwaruza shingoni hivyo nilirudi chini na kuangalia vizuri. Niliangalia mlangoni na kuona kuwa ulikuwa wazi. Mwezi mkubwa ulikuwa umeishatoka, ulionekana kama mpira wa moto. Mwanga wake uliangukia juu ya uso wa Noma aliyekuwa amekaa mkabala nami, akinitazama kwa jicho lake moja, mkononi ameshika kisu. Kisu hicho ndicho nilichohisi kikinikwaruza shingoni.

‘We kinyago niliyekuchonga mwenyewe unataka kunimaliza!’ alisema Noma. ‘Unaagua kazi iliyonishinda! Ngoja nikuonyeshe ninavyowafanya watu wa aina yako. Kwanza nitakata mzizi wa ulimi wako ili usiweze kupiga kelele. Kisha nitakukata vipande vipande pole pole. Asubuhi nitawaambia watu kuwa mizimu imekufanyia hivyo sababu ulidanganya. Nitakutoa mikono na miguu. Kisha!’—akaanza kukikandamiza kisu kidevuni mwangu.

‘Nisamehe mjomba. Nisamehe.’ Nilisema, maana nilijawa na uoga na nikaanza kusikia maumivu ya kisu. ‘Nisamehe mjomba. Nitafanya kila utakacho.’

‘Utafanya hili nikuambialo. Utaenda kuwaswaga ng’ombe wa yule mshenzi na kuwapeleka sehemu nyingine na kuwaficha huko?’ Akaniambia kuhusu bonde fulani ambalo ni watu wachahce sana walilifahamu. ‘Ukifanya hivyo nitakuacha hai na kukupatia ng’ombe watatu. Lakini ukikataa au kufanya ujanja wowote basi ninaapa kuwa nitafanya kila njia kukuua.’

‘Nitafanya hivyo mjomba.’ Nilijibu. ‘Kwa nini hukuniambia mapema? Ningejua kama unataka kumdhulumu ng’ombe wake nisingefunua waliko. Nilifanya vile kwa kuogopa kuwa utanyang’anywa malipo.’

‘Kumbe si mwovu kama nilivyodhani,’ alisema. ‘Haya amka na ufanye kama nilivyokuagiza. Urudi saa mbili baada ya mapambazuko.’ . . . . . .
 
Niliamka. Nikawaza iwapo nimshambulie, lakini sikuwa na silaha, naye alikuwa na kisu. Na hata kama ningemshinda na kumuua watu wangesema nimemuua nao wangeniua. Basi nikafanya mpango mwingine. Nilipanga kwenda sehemu niliyowaona ng’ombe kwenye maono, lakini sitawapeleka eneo la siri aliloniambia. Nitawapeleka moja kwa moja bomani na kumchongea Noma kwa Chief, ambaye alikuwa ni baba yangu,na watu wote. Lakini nilikuwa bado kijana, sikujua moyo wa Noma ulivyo. Hakuwa amekuwa mganga hadi uzeeni hivi hivi tu. Alikuwa katili—mwenye hila kama mbweha na mkali kama samba, alikuwa amenipanda kama mti, lengo lake ni kunipunguza matawi mara kaa mara ili nisiwe mkubwa sana, lakini sasa nimekuwa mti mkubwa kumzidi—basi akapanga kuning’o kabisa.

Nilielekea kwenye kona ya kibanda changu—wakati huo wote Noma ananiangalia. Nilichukua rungu langu na ngao. Nikaanza safari, nilitembea polepole mpaka nilipotoka nje ya boma. Baada ya hapo nikaanza kukimbia huku nikiimba ili kuitisha mizimu.

Kwa muda wa saa nzima nilisafiri eneo tambarare, baada ya hapo nikakutana na kilima kilichokuwa na pori. Humo chini ya miti kulikuwa na giza hivyo nikaanza kuimba kwa sauti zaidi. Baada ya kitambo kidogo nikaikuta njia niliyodhani kuwa itakuwa ni ya nyati, nikaifuata. Nikaendelea nayo na kutokezea kwenye eneo la wazi ambalo mwanga wa mwezi ulipenya. Nikakaa kidogo na kuchunguza. Nyoka wangu hakunidanganya, kulikuwa na harufu ya ng’ombe. Basi nikaenda haraka hadi nikakuta bonde dogo ambalo kulikuwa na kijito. Mahali hapa njia ya ng’ombe ilikuwa pana zaidi; walikuwa wameangusha vichaka na kukanyagakanyaga nyasi. Kisha nikakiona kidimbwi—kidimbwi nilichoonyeshwa na nyoka wangu. Pembeni ya kidimbwi nikamuona ng’ombe akielea, miguu yake imenaswa kwenye mizizi. Yote yalikuwa kama nilivyoona kwenye maono.

Niliendelea mbele kuchunguza zaidi. Mwanga wa alfajiri ulimulika kitu, zilikuwa ni pembe za ng’ombe. Nilipoendelea kusogelea mmoja wao aliamka, akapiga chafya na kujikung’uta umande uliomjaa mwilini. Kwenye ukungu na mwanga hafifu alionekana mkubwa kama tembo.

Niliwakusanya wote. Jumla walikuwa ng’ombe kumi na saba. Niliwaswaga kuelekea nyumbani. Nilipofika njia panda ya kuelekea eneo nililopaswa kuwaficha ng’ombe tayari jua lilikuwa limeishatoka. Lakini sikuwa na nia ya kwenda huko. Lengo langu ni kwenda na ng’ombe mpaka bomani na kuwaambia watu wote kuwa Noma ni mwizi. Nilikaa chini mahali hapo ili kupumzika kidogo, maana nilikuwa nimechoka sana. Nilipoanza tu kukaa nikasikia kelele, nilipotazama nikaona kundi la watu wakishuka kilimani kuja nilipo, Noma akiwaongoza na pembeni yake yule tajiri. Nilisimama na kutulia tuli, nimepigwa na bumbuwazi. Walianza kunikimbilia wakipiga kelele huku wameinua fimbo na mikuki.

‘Yule pale! Yule pale!alipiga kelele Noma. ‘Kijana nilimkuza mwenyewe, akajitia werevu na kutaka kuniletea aibu. Niliwaambiaje? Sikuwaambia kuwa ni mwizi! Nafahamu mbinu zako zote Mbopo mwanangu! Mnaona! Anaiba ng’ombe. Alifahamu walikokuwa, na sasa anawachukua kwenda kuwaficha. Watamfaa sana kama mahali, si ndiyo kijana wangu?’ Basi Noma akawa ananifuata huku fimbo yake kainua juu. Nyuma yake yule tajiri naye akija mbio huku kafura kwa hasira.

Nikawa kama nimechanganyikiwa, vitu vyote vilionekana kama vinaelea. Hali kama hiyo hunikuta mara zote ninapolazimika kupigana. Nilitamka neno moja tu, ‘Muongo’ kisha nikamkimbilia kupambana naye. Noma alinipiga na fimbo yake, lakini nilijikinga kwa ngao yangu ndogo na kurudisha mapigo. Pigo langu lilimpata vyema kichwani. Pale pale akaanguka miguuni pangu amekufa. Nilipiga tena kelele na kumkimbilia yule tajiri. Alirusha mkuki lakini ulinikosa. Naye nikampa pigo. Alijaribu kujikinga kwa ngao lakini haikusaidia. Akaanguka chini hajitambui. Sijui kama alikufa au la, lakini nadhani aliishi. Watu walipoendelea kushangaa yaliyotokea niligeuka na kukimbia kama upepo. Walinikimbiza huku wakinitupia mikuki na kujaribu kunikamata lakini hawakuweza. Nilikimbia kama swala waliyeamshwa na mbwa kutoka usingizini. Sauti zao ziliendelea kufifia hadi zikawa hazisikiki tena na nikajikuta peke yangu.

Itaendelea. . . .
 
3. Mopo aelekea nyumbani

Nilijitupa kwenye nyasi na kuhema mpaka pumzi iliponirudia; baada ya kupata nafuu nikaenda kujificha kwenye matete karibu na bwawa. Nilikaa hapo siku nzima nikitafakari. Nitafanya nini? Nimekuwa mbweha nisiye na shimo. Kama nikirudi nyumbani hakika wataniua, maana wanajua mimi ni mwizi. Damu yangu itamwagwa kulipa ya Noma. Basi likanijia wazo la Chaka, mvulana niliyempatia maji ya kunywa miaka mingi iliyopita. Nilikuwa nimemsikia, jina lake lilifahamika nchini. Tayari hewa ilikuwa imejaa jina lake. Hata miti na nyasi vililitaja. Maneno aliyoyasema, na maono ya mama yangu vilianza kuwa kweli.

Kwa msaada wa wa kabila la Umtetwa alikuwa amepata cheo cha baba yake, Senzangakona; alikuwa amelifukuza kabila la Amakuabe na sasa alikuwa vitani na Zweete, chifu wa kabila la Endwande. Aliapa kwamba atawapiga Waendwande na kuwasagasaga kiasi kwamba hakuna mtu atakuja kuwaona tena.

Nikawa nimekumbuka ahadi ya Chaka kuwa atanifanya kuwa mtu mkubwa, na kuwa nitanawiri pembeni yake. Basi nikaamua kuamka na kumuendea. Pengine ataniua. Lakini hata nikiendelea kukaa hapa hakika nitauawa. Lakini moyo wangu ukawa mzito. Kuna mtu mmoja nimpendaye sana duniani—dada yangu Baleka. Baba yangu alikuwa amemfungisha uchumba kwa Chifu wa kabila la jirani, lakini nilifahamu vyema kuwa Baleka hakutaka ndoa hiyo. Pengine nikimwambia kuwa ninaondoka atatoroka pamoja nami—nitajaribu kufanya hivyo.

Nilisubiri mpaka giza lilipoingia. Hapo niliamka kutoka kwenye matete na kuelekea nyumbani. Nilisimama kidogo kwenye shamba la mahindi, nikachuma na kuanza kuyala maana nilikuwa na njaa sana. Nilijaza tumbo langu mahindi mateta. Niliendelea na safari hadi nikafikia boma la baba yangu. Baadhi ya jamaa zangu walikuwa nje wakiongea kando ya moto. Nilinyata polepole na kuwasogelea kama nyoka ili nisikie walichokuwa wanaongea. Kama nilivyodhani, walikuwa wakiniongelea na kuniita majina yote mabaya. Walisema kuwa ningeliletea kabila laana kwa kumuua mganga mkubwa kama Noma. Na kuwa watu wa yule tajiri watadai fidia kwa kumpiga kwangu. Pia nikasikia kuwa baba yangu ametoa amri kuwa wanaume wote wa kabila letu kesho wanisake na kuniua popote watakaponikuta. ‘Mtawinda lakini hamtarudi na chochote nyumbani,’ niliwaza. Wakati huo huo mbwa aliyekuwa karibu na moto alianza kunusanusa hewani. Sikujua ni mbwa yupi kati ya wengi tuliowafuga. Nilipoingia bomani nilikuwa nimesahau kabisa habari za uwepo wa mbwa, hayo ndiyo madhara ya kukosa uzoefu babaangu. Mbwa aliendelea kunusa na kuunguruma huku akiangalia uelekeo niliokuwepo, nilianza kuingiwa na hofu.

‘Kwanini mbwa anaunguruma?’ alisema mwanaume mmoja. ‘Nenda kaangalie.’ Lakini alieambiwa alikuwa anavuta ugoro hivyo hakutaka kuamka. ‘Mwache mbwa mwenyewe aende akaone.’ Alisema huku akipiga chafya. ‘Kuna faida gani ya kufuga mbwa kama unatakiwa wewe mwenyewe ndiye ukamate mwizi.’

‘Nenda,’ alisema yule mtu wa kwanza akimwambia mbwa. Mbwa akatoka mbio akibweka, nikamuona. Alikuwa ni mbwa wangu aliyeitwa Koozi, mbwa mzuri sana. Sikujua cha kufanya. Lakini baada ya kuninusa akaacha kubweka na kuanza kunilamba usoni. ‘Kimya Koozi!’ nilimnong’oneza. Akakaa kimya na kulala pembeni yangu.

‘Mbwa ameenda wapi?’ alisema mwanaume wa kwanza. ‘Amerogwa! Maana ameacha kubweka na harudi.’

‘Ngoja tukaone,’ alisema mwenzake huku akiinuka, mkuki mkononi.

Sasa hofu ikaniingia tena. Maana nilihisi nitakamatwa. Nikaamua kukimbia. Lakini kabla sijakimbia nyoka mkubwa mweusi alipita katikati yao na kuelekea kwenye nyumba. Waliruka kwa uoga kisha wote wakaanza kumfuata nyoka yule huku wakisema kuwa ndiye aliyemfanya mbwa abweke. Ile ilikuwa roho yangu babaangu, ilichukua umbo la nyoka ili kuokoa maisha yangu.

Walipoondoka nilipita njia nyingine huku Koozi akinifuata. Mwanzoni nilifikiria kumuua ili asije kunisaliti kwa kupiga kelele, lakini nilipotaka kumpiga na kirungu kichwani aliikaa chini huku akitikisa mkia. Basi nikaamua kwenda naye. Mpango wangu ulikuwa ni huu. Kwanza kuingia kwenye kibanda changu na kuchukua mkuki na blanketi langu la ngozi, kisha nikaongee na Baleka. Niliwaza kuwa kibanda changu kitakuwa hakina mtu maana ni mimi pekee hulala mule, na nyumba za Noma zilikuwa hatua kadhaa upande wa kulia. Nilifika kwenye uzio wa matete uliozunguka nyumba. Hakuna mtu aliyekuwa langoni, wala halikufungwa kwa miba kama ilivyokuwa kawaida. Ilikuwa ni kazi yangu kufunga geti, nami sikuwepo. Nilimuacha mbwa nje, nikapenya kimya kimya ndani na kufikia kibanda changu. Kilikuwa hakina mtu, hata sauti ya kuhema haikusikika. Nikaingia ndani na kuanza kutafuta mkuki wangu, kibuyu cha maji na mto wangu wa mti, ulikuwa umechongwa vizuri sana hivyo sikutaka kuuacha. Nilivipata vyote. Nikaanza kutafuta kirago changu cha ngozi. Katika kupapasa nikawa nimeshika kitu fulani cha baridi. Katika kuchunguza zaidi nikangundua kuwa ni sura ya mtu—sura ya maiti, maiti ya Noma. Mtu niliyemuua na sasa maiti yake ipo kibandani mwangu ikisubiria mazishi. Niliingiwa na hofu kubwa, maiti ya Noma gizani ni hatari kuliko Noma aliye hai. Nikaamua kuondoka haraka.

Kabla sijaondoka nikasikia sauti za wanawake nje. Nilizitambua vyema, zilikuwa sauti za wake wawili wa Noma. Mmoja wao alikuwa anasema kuwa anakuja kibandani kukaa karibu na maiti ya mumewe. Sasa nikawa nimenaswa. Kabla sijafanya chochote niliiona mwanga ukififia sababu mtu alikuwa ameuziba mlangoni, nikasikia sauti ya mwanamke mnene akihema, alikuwa ni mke wa kwanza wa Noma, tayari akawa yupo ndani na kuchuchumaa karibu na maiti na hivyo kunizuia kutoka. Akaanza kuomboleza huku akinilaani vikali. Hakufahamu kama nimo mle ndani nikiyasikia asemayo. Sababu ya hofu akuli yangu ikafanya kazi haraka.Nikakumbuka kuwa Noma alikuwa mwenye hila nyingi sana. Basi nikapanga afanye hila moja kwa mara ya mwisho. Nilichuchumaa na kupitisha mikono yangu kwenye makwapa yake na kumuinua kiasi cha kumfanya awe kama ameketi sakafuni. Mwanamke yule alisikia sauti naye akafanya kelele za mshtuko.

‘Kimya we kikongwe!’ Nilisema kwa sauti ya Noma. ‘Hautaki niwe na amani hata sasa nikiwa nimekufa?’

Alishtuka na kurudi nyuma, akaanza kuvuta pumzi ili apige kelele kubwa.

“Yaani unataka kupiga kelele?’ nilisema. ‘Basi nitakufundisha kunyamaza.’ Niliisukuma maiti ya Noma juu ya mke wake.

Hapo akili zikamruka mwanamke yule, sijui kama alizipata tena lakini alikaa kimya kabisa. Nikanyakua kirago changu—ambacho baadaye nilikuja kugundua kuwa ni blanketi la noma, lilikuwa blanketi bora sana lililotengenezwa na mafundi wa kibasuto kwa kutumia ngozi za paka—thamani yake fahari watatu. Nikakimbia huku nikufuatwa na Koozi.

Boma la baba yangu, chifu Makedama lilikuwa kama umbali wa hatua mia moja. Nililazimika kwenda huko sababu ndiko alikolala Baleka. Sikuthubutu kupita getini sababu mlizi alikuwepo hapo muda wote. Basi nikakata uzio wa matete kwa mkuki wangu na kwenda kwenye nyumba ambayo Noma alilala na dada zake wa kambo. Nilifahamu upande wa nyumba aliolala, basi polepole sana nikaanza kukata nyasi za zilizotumika kujengea kuta za nyumba ile. Ilichukua muda mrefu maana nyasi zilikuwa nene. Baada ya kukaribia kumaliza nikasimama. Nikawaza kuwa inawezekana Baleka amebadili upande wa kulala nami nitamuamsha msichana mwingine. Nilikaribia kukata tamaa na kuamua kutoroka peke yangu—nikasikia sauti ya msichana akilia upande wa pili. Nikatambua kuwa ni Baleka anamlilia kaka yake. Basi niliweka mdomo pale nilipokata na kunong’ona:-

‘Baleka dada yangu! Baleka usilie, ni mimi Mopo. Usiongee kitu. Njoo nje taratibu, uje na blanketi lako.’

Baleka alikuwa mwerevu sana. Hakupiga kelele kama ambavyo wasichana wengine wangefanya. Alielewa alichotakiwa kufanya. Baada ya kutulia kidogo alitoka kibandani, akiwa ameshika blanketi lake.

‘Unafanya nini hapa Mopo?’ alisema kwa kunong’ona. ‘Watakuua!’

‘Shhhh!’ nilisema. Kisha nikamueleza mpango wangu na kumuuliza kama ataondoka nami au atarudi ndani.

Itaendelea. . . .
 
Alifikiria kidogo kisha akasema, ‘Nitaenda nawe kaka yangu. Maana ni wewe pekee ninayekupenda kati ya watu wetu. Lakini naamini huu ndiyo utakuwa mwisho wangu—unanipeleka kwenye kifo.’

Wakati ule sikuyafikiria sana maneno yake, lakini hapo baadaye yalinirudia. Basi tukatoroka pamoja na Koozi, baada ya muda kidogo tukawa tukikimbia nyikani, tukielekea nchi ya Wazulu.



4. Kutoroka kwa Mopo na Baleka

Tulisafiri usiku kucha, hadi mbwa alichoka. Ilipofika mchana tulijificha kwenye shamba la mahindi maana tuliogopa kuonekana. Ilipokaribia mchana tulisikia sauti, tulipochungulia tuliona kundi la watu wa baba yangu likipita, wakitutafuta. Walienda kwenye boma la karibu kuuliza kama tumeonekana, baada ya hapo hatukuwaona kwa kitambo kirefu. Usiku tuliendelea na safari; lakini kama vile ilipangwa, tulikutana na bibi kizee mmoja, alituangalia kwa udadisi lakini hakusema kitu. Baada ya hapo tulisafiri usiku na mchana, tuliogopa yule bibi utawajulisha wanaotutafuta iwapo ataonana nao. Kwenye jioni ya tatu tulikuta mashamba ya mahindi yaliyokuwa yamevurugwa. Katikati ya mahindi yaliyovurugwa tuliona mwili wa mtu mmoja mzee sana, ulikuwa umejaa majeraha ya mikuki kama vile miba kwenye mwili wa nungunungu. Tulishangaa kidogo kisha tukaendelea. Mbele tukakutana na boma la mwenye mashamba, lilikuwa limechomwa moto. Tulilichunguza zaidi, aaah, tyliona hali ya kuhuzunisha sana, lakini baada ya muda tukazoea kuona hayo. Kila mahali kulitapakaa maiti za watu—wazee, vijana, wanaume, wanawake, watoto na watoto wanyonyao—wamelala katikati ya nyumba zilizochomwa moto, miili yao imejaa majeraha ya mikuki. Ardhi ilikuwa nyekundu kwa damu zao—jua la jioni nalo lilifanya miili yao ionekane myekundu. Ilikuwa kama nchi yote imepakwa damu na Mzimu Mkuu, Umkulunkulu. Baleka alipoona hayo akaanza kulia; alikuwa msichana dhaifu na tulikuwa hatujala kitu zaidi ya nyasi na mahindi mabichi.

‘Adui atakuwa amepita hapa,’ nilisema. Nilipokuwa nasema hayo nikasikia sauti ya kukoroma kutoka kwenye uzio wa matete. Nilienda kutazama. Nikamkuta mwanamke mmoja, amejeruhiwa vibaya lakini bado mzima. Mbali kidogo naye ilikuwepo maiti ya mwanaume, na pembeni yake maiti nyingine za watu walioonekana ni wa kabila tofauti, inaonekana mwanaume yule ambaye maiti yake ilikuwa pembeni ya mwanamke alikufa akipambana. Mbele ya mwanamke kulikuwa na miili ya watoto watatu, mwili mwingine wa mtoto mdogo ulikuwa maungoni mwake. Nilimuangalia tena mwanamke yule, naye akagugumia. Alifumbua macho na kuniona nikiwa na mkuki mkononi.

‘Niue haraka!’ alisema. ‘Haujatosheka tu kunitesa?’

Nilimwambia kuwa nilikuwa mgeni na sipo pale kumuua.

‘Niletee maji, kuna chemichemi pale nyuma ya boma.’

Nilimwita Baleka akae na mwanamke yule kisha nikaelekea kwenye chemichemi na kibuyu changu. Kulikuwa na maiti kwenye chemichemi. Nilizotoa, na baada ya maji kuwa masafi kidogo nilijaza kibuyu na kurudi kwa yule mwanamke. Alikunywa kwa pupa na nguvu zikaonekana kumrudia kidogo—maji yakampa uhai.

‘Nini kimetokea?’ niliuliza.

‘Wanajeshi wa Chaka chifu wa Wazulu ndiyo waliotufanyia hivi. Walituvamia alfajiri ya leo tulipokuwa tumelala vibandani mwetu. Niliamshwa na kelele za mauaji. Nilikuwa nimelala na mume wangu, huyo hapo, na watoto. Sote tulikimbilia nje, mume wangu alibeba mkuki na ngao. Alikuwa mtu jasiri. Kabla hajafa aliua mashetani watatu Wakizulu. Alikufa kishujaa! Baada ya kumuua walinikamata na kuwaua wanangu, wakanichoma kwa mikuki mpaka walipohisi kuwa nimekufa. Baada ya hayo wakenda zao. Nadhani walitushambulia sababu chifu wetu alikataa kupeleka watu kumsaidia Chaka katika vita yake na Zweete.’

Aliacha kuongea. Akatoa kilio na kufa.

Dada yangu alilia, nami pia nilishikwa na huzuni. ‘Aaah Mzimu Mkuu utakuwa mbaya sana, kama sivyo basi haya yasingetokea,’ hivyo ndivyo nilivyofikiri wakati huo babaangu, lakini sasa nina mtazamo tofauti. Nafahamu kuwa bado hatujaipata njia ya Mzimu Mkuu. Nilikuwa kuku wakati huo babaangu, lakini baada ya muda nikazoea kuona yale. Hayakunihuzunisha tena, hata kidogo. Wakati ule wa Chaka mito ilitiririsha damu, ilitulazimu kuangalia maji kama masafi kabla ya kunywa. Watu walijifunza kufa bila kelele. Lakini haijalishi kitu, maana kufikia leo wengi wao wangekuwa wamekufa.

Usiku ule tulipumzika kwenye boma moja. Lakini hatukuweza kulala usingizi maana tulisikia sauti za Itongo, mizimu ya watu waliokufa—ikiitana. Ilikuwa ni sahihi ifanye vile, wanaume walikuwa wanawatafuta wake zao na mama wakiwatafuta watoto wao. Tuliogopa kuwa itachukizwa na uwepo wetu pale hivyo tulikumbatiana na kutetemeka. Koozi naye alitetemeka, na mara kwa mara alipiga kelele. Lakini ilionekana mizimu ile haikutuona, kulipokaribia kupambazuka vilio vyao vilianza kupungua.

Mwanga wa kwanza ulipotoka tuliamka na kupita katikati ya maiti kuelekea nyikani. Wakati huu njia ya kuelekea kwenye boma la Chaka ikawa inaonekana kirahisi, maana tuliona yalimopita majeshi yake na ng’ombe waliowapora, na wakati mwingine tulikutana na maiti za wanajeshi waliouawa kwa sababu majereha yao yaliwafanya wasiendelee na safari. Tulivyoendelea na safari nilianza kupata wasiwasi juu ya uamuzi wa kwenda kwa Chaka. Kwa yale tuliyoona nilianza kuingiwa na wasiwasi kuwa pengine atatuua. Lakini hatukuwa na kwa kwenda, basi nikaamua kuwa tutaendelea kwenda tuone kitakachotokea. Tulikuwa dhaifu sana kwa njaa, Baleka alisema kuwa ni afadhali tukae chini na tufe ili tusiendelee kuteseka. Basi tukaketi kando ya chemichemi, lakini sikuwa tayari kufa wakati ule japo kiukweli Baleka alikuwa sahihi, ingekuwa afadhali kufa. Tulipoketi Koozi alienda kwenye kichaka kilichokuwa karibu, akarukia kitu fulani na tukasikia purukushani, nikakimbia kwenda kuona. Alikuwa amemkamata swala aliyekuwa amelala pale, alikuwa mkubwa kama yeye tu. Nilimchoma swala yule kwa mkuki na kupiga yowe la furaha, maana sasa tulikuwa na chakula. Baada ya swala yule kufa nilimchuna, tukakata vipande vya nyama, tukaviosha na kula nyama mbichi maana hatukuwa na moto wa kupikia. Haifai kula nyama mbichi lakini tulikuwa na njaa sana hivyo hatukujali, chakula kile kilitupa nguvu tena.

Tulipomaliza kula tulinawa kwenye chemichemi, tulipokuwa tunanawa Baleka aliangalia juu kilimani na kutoa kilio kikali cha uoga. Kwenye kilele cha kilima kulikuwa na kikundi cha wanaume sita waliokuwa na silaha. Watu wa kabila langu, wa baba yangu Makedama ambaye bado alikuwa anaendelea kututafuta—kutukamata au kutuua. Walipotuona walipiga kelele na kuanza kutukimbilia. Nasi pia tuliruka na kuanza kukimbia kama swala maana uoga ulikuwa umeipa nguvu miguu yetu.

Mbele yetu ardhi ilikuwa tambarare kisha ilishuka kuelekea kingo za mto Umfolozi Mweupe ambao ulikuwa umejipindapinda nyikani kama nyoka. Upande wa pindi nchi iliinuka tena. Hatukujua kilichokuwako baada ya kupita kilima cha ng’ambo ya pili, lakini tulidhani kuwa ndiko yaliko makazi ya Chaka. Tulikimbia kuelekea mtoni, tungeenda wapi? Askari wakitufuatia nyuma. Walianza kutukaribia maana walikuwa na nguvu na hasira iliwajaa sababu ya kusafiri umbali mrefu. Tuliukaribia mto. Ulikuwa ni mpana na umejaa, unakotoka maji yake yalienda kasi sana, yakijipigapiga kwa kasi kwenye mawe yaliyokuwa chini yake. Unakoelekea kulikuwa na maporomoko makubwa ya maji ambayo mtu yeyote ambaye angetumbukia asingeweza kupona. Katikati ya sehemu hizo mbili kulikuwa na bwawa lenye maji matulivu lakini mkondo wake ulikuwa na nguvu.

‘Tutafanya nini kaka?’ alisema Baleka

‘Kuna mawili, kufa kwa mikuki au kujaribu bahati yetu mtoni.’

‘Ni rahisi kufa maji kuliko kwa chuma.’ Alijibu.

‘Vyema,’ nilisema. ‘Basi nyoka wetu na roho za mababu wetu ziwe pamoja nasi! Walau tunaweza kuogelea.’ Nilimuongoza mpaka kando ya bwawa. Tulitupa mablanketi na vitu vyetu vingine isipokuwa mkuki ambao niliushika kwa meno—tukajirusha bwawani. Maji yalitufika kifuani; mara tukawa hatuwezi tena kukanyaga chini—tulipiga mbizi kuelekea katikati ya mto, Koozi akiwa mbele.
 
Mara tukawaona wanajeshi wakitokea ukingoni. ‘Mnaogelea siyo,’ alipiga kelele mmoja wao. ‘Mtazama, na msipozama tunapajua mahali pa kuvukia, tutawakuta na kuwaua—hata kama itatubidi kwenda mpaka kwenye ukingo wa dunia ili kuwakamata tutafanya hivyo.’ Alisema hivyo na kuturushia mkuki ambao ulipita kati yetu kama muale wa mwanga.

Alipokuwa anaongea sisi tulizidi kuogelea kwa nguvu zaidi. Tukakutana na mkondo mkali lakini tuliushinda maana tulikuwa waogeleji wazuri.

Ilikuwa tufike ng’ambo ya pili kabla mkondo haujatuchukua kwenda kufa maporomokoni. Tukawa tumekaribia ng’ambo ya pili lakini pia mkondo ulikuwa umetuchukua karibu sana na maji yanayofoka. Tulipambana kwa nguvu zetu zote. Baleka alikuwa msichana shujaa na aliogelea kishujaa sana lakini mkondo ulimchukua kuliko mimi. Nilipata jiwe la kuweka miguu, nilipoangalia nyuma nilimuona akiwa kama hatua nane toka nilipo, karibu na maji yenye hasira. Sikuweza kurudi kumfuata, nilikuwa taabani. Ilionekana kuwa atachukuliwa na maji maporomokoni. Lakini Koozi alimuona. Aliogelea kumfuata, alipomfikia akabweka na kugeuka kurudi ukingoni. Baleka alimshika mkia. Alikuwa ni mbwa mwenye nguvu, Baleka naye alipiga maji kwa miguu na mkono wake mwingine. Polepole walikaribia ukingoni. Waliponikaribia nilinyoosha mpini wa mkuki wangu naye aliushika. Nilimvuta hadi ufuoni, akajilaza huku akivuta pumzi kwa nguvu.

Baada ya askari kuona kuwa tumevuka, waliturushia maneno ya vitisho kisha wakaanza kukimbia kuelekea uelekeo wa chini wa mto.

‘Amka Baleka,’ nilisema. ‘Wameenda kuangalia sehemu ya kuvukia.’

‘Niache nife,’ alisema.

Nilimlazimisha kuamka na baada ya muda pumzi ikawa imemrudia. Tulipanda ukingo kwa kasi kadri tulivyoweza. Tuliendelea kutembea tukipanda kwa muda wa saa mbili, mwishowe tukafika juu ya muinuko, kwa mbali tuliona boma kubwa.

‘Kaza moyo,’ nilisema. ‘Ona kule, boma la Chaka.’

‘Nimeona kaka, lakini kitu gani kinatungoja kule? Kifo kipo mbele yetu na nyuma yetu—tupo katikati ya kifo.’

Baada ya kutembea kwa muda kidogo tukakutana na barabara inayotoka kwenye kivuko cha Umfolozi kuelekea kwenye lile boma tuliloliona, tuliifuata hiyo hadi tukawa umbali wa kama nusu saa kutoka kwenye boma. Tulipoangalia nyuma, lo! Askari watano wanatujia—mmoja alizama walipokuwa wanavuka.

Tulianza kukimbia tena. Lakini wakati huu tulikuwa dhaifu zaidi nao wakawa wanatukaribia haraka. Wazo la kumtumia mbwa likanijia. Alikuwa mkali na angemrarua yeyote ambaye ningemuelekezea. Nilimwita na kumwambia cha kufanya, nilijua huo ndiyo utakuwa mwisho wake. Naye alielewa vyema. Alianza kuwakimbilia askari huku akibweka na nywele za mgongoni zimemsimama. Walijaribu kumuua kwa mikuki na marungu lakini aliwakwepa, akiwauma na kuwazuia wasiendelee na safari. Mwishowe mtu mmoja alimpata kwa rungu. Mbwa alimrukia mtu yule na kumkamata koo. Aling’ang’ania koo la mtu yule. Walibiringika pamoja huku na kule mpaka mwishowe walipokufa pamoja. Ah! Yule alikuwa mbwa hasa. Siku hizi hakuna mbwa kama yule. Baba yake alikuwa mbwa wa kikaburu. Amewahi kumuua chui peke yake. Basi huo ndiyo ulikuwa mwisho wa Koozi.

Wakati hayo yakitokea sisi tuliendelea kukimbia. Sasa tukawa tupo umbali wa hatua kama mia tatu tu kutoka kwenye lango la boma. Ndani ya boma kuna kitu kilikuwa kinaendelea maana tulisikia kelele na kuona vumbi. Wale askari wanne walimuacha mwenzao na mbwa waliokufa na kutujia kwa kasi sana. Niliona wazi kuwa sasa watatukamata, maana Baleka hakuweza tena kwenda kwa kasi. Wazo likanijia, ni mimi nimemleta hapa hivyo natakiwa kufanya kila niwezalo kuokoa maisha yake. Iwapo atalifikia boma bila mimi basi ataishi, Chaka hatamuua msichana mdogo na mzuri.

Wakati huu Baleka alikuwa kama kipofu kwa kuchoka na hofu. Hakujua lengo langu. Aliendelea kujikongoja kuelekea kwenye lango la boma. Mimi nilikaa chini kwenye nyasi ili kupata pumzi, nilikuwa najiandaa kupambana na askari wanne hadi kifo. Moyo ulinidunda na nilisikia damu ikipita kwenye mishipa ya masikioni. Walipokaribia nilisimama—mkuki mkononi na hofu yote ikanitoka.

Wanaume wale walikuwa wanakimbia wawili wawili. Wakiachiana nafasi kati yao, Katika wale wawili wa kwanza mmoja alikuwa kama hatua tano au sita mbele ya mwenzake. Alipiga kelele na kunikimbilia huku kainua mkuki na ngao. Mimi sikuwa na ngao, mkuki tu. Lakini nilikuwa mjanja na askari yule alijiamini kupita kiasi.

Nilimsubiria hadi aliponikaribia na kutaka kunichoma na mkuki. Hapo kwa ghafla niliinama na kuinuka kwa nguvu nikiwa ndani ya ngao yake, mkuki wake ukanikwaruza hapa begani—unaona hili kovu, lipo hadi leo. Mkuki wangu! Uliingia penyewe. Ulimpata sawia. Alianguka na kugaragara chini, vumbi lilimfunika kabisa. Lakini sasa sikuwa na silaha. Mkuki wangu ulikuwa ni mdogo tu kwaajili ya kurusha. Ulivunjika vipande viwili na nikawa nimebaki na mpini tu. Askari yule mwingine alikuwa ananijia. Akili ikanijia, niliinama chini na mwili wangu uliikumba miguu ya mtu yule aliyejiandaa kunichoma mkuki. Alianguka kama mzigo. Kabla hajatua chini nilikuwa nimeishahepa. Mkuki wake ukamtoka. Niliuokota. Alipokuwa anajaribu kuamka nikamchoma mkuki wa mgongoni. Yote yalifanyika ndani ya sekunde chache sana. Baada ya hilo nikaanza kukimbia. Sikuwa na nguvu ya kupigana na wale wawili waliobakia, ujasiri uliniisha.

Kama hatua mia mbili mbele yangu Baleka aliendelea kujikongoja kama mtu aliyekunywa bia kupita kiasi. Nilipomfikia alikuwa amebakiza kama hatua arobaini hivi kufikia lango la boma. Lakini hapo nguvu zilikuwa zimemuisha kabisa. Alianguka hajitambui kabisa. Nilisimama pembeni yake. Kama si wale wawili kusimama kuwaangalia wenzao waliokufa hakika ningeuawa. Baada ya kuwaangalia wenzao wakaanza kutufuata, wamefura kwa hasira. Wakati huo huo lango la boma likawa linafunguliwa. Kikundi cha wanajeshi kikatoka kikimkokota mfungwa. Nyuma yao alikuwepo mwanaume aliyeonekana ni mkuu wao, alikuwa amevaa ngozi ya chui mabegani, alikuwa akicheka kwa sauti. Aliambatana na wapambe kama watano au sita hivi. Nyuma yao kulikuwepo tena kundi la askari.

Wanajeshi wale waliona kuwa kuna mauaji yanaendelea. Walikimbia kutufuata na wakati huo huo wale wauaji nao wakawa wanatufikia.

‘Nyinyi ni nani?’ walifoka. ‘Mnathubutuje kufanya mauaji kwenye lango la boma la Tembo? Hapa ni tembo tu ndiye anaruhusiwa kuua.’

‘Sisi ni wana wa Makedama,’ walijibu wale waliotukimbiza. ‘Tunawafuatilia hawa waovu waliofanya uovu na kuua kwenye boma letu. Si mmeona! Na sasa wenzetu wawili wamekufa kwa mikono yao, na wengine wamelala wamekufa huko njiani. Tunaomba kuwaua’

‘Muombeni hilo Tembo,’ walisema wanajeshi waliotoka bomani. ‘Muombeni ili asiwaue nanyi pia.’

Wakati huo yule chifu mrefu akawa amesikia yaliyosemwa na kuona damu. Alikuwa mkuu sana kwa kumtazama japo alionekana ni kijana. Alikuwa mrefu kuliko wengine wote, kifua chake kilikuwa kikubwa kama cha watu wawili. Uso wake ulikuwa mkali lakini wenye kuvutia. Alipopatwa na hasira macho yake yalikuwa kama moto.

‘Ni nani hawa wanaothubutu kutimua vumbi kwenye lango la boma langu?’ alisema kwa hasira.

‘O Chaka, O Tembo!’ alisema kapteni wa askari huku akiinama mbele yake. ‘Watu hawa wanasema kuwa hawa wawili ni waovu, wamewafuatilia ili kuwaua.’

‘Vyema,’ alisema. ‘Waacheni wawaue waovu.’

‘O chifu mkuu! Ahsante sana Chifu mkuu!’ walisema wale watu wa kabila langu.

‘Nimewasikia,’ alisema. Alimgeukia kapteni na kusema, ‘Wakishawaua wahalifu wapofusheni macho na kuwaachia watafute njia ya kwao maana wamethubutu kuinua mikuki yao kwenye lango la Wazulu.’ kisha akacheka. ‘Chifu mkuu. Nimwenye busara,’ walisema wanajeshi wake. ‘Hukumu zake ni kama jua, zinaangaza na kuunguza.’

Lakini wale watu wa kabila langu walilia kwa uoga, hawakutaka hukumu ya namna hii

‘Wakateni na ndimi zao pia,’ alisema Chaka. ‘Nchi ya Uzulu haiwezi kuvumilia hizo kelele hata siku moja! Mimba za ng’ombe zisije kuharibika, haya nyie wageni tekelezeni. Msichana yuko pale amelala hajiwezi. Muueni! Mnasita nini? Kama mnataka muda wa kutafakari siyo! Basi nitawapatia. Askari wachukueni watu hawa na wapakeni asali kisha wafungeni juu ya kichuguu. Kufikia kesho watakuwa wameishafanya maamuzi. Lakini kabla ya hilo waueni hawa mbweha wawili waliokuwa wanakimbizwa,’ alisema maneno hayo ya mwisho huku akielekeza kwangu na Baleka. ‘Wanaonekana kuchoka na wanatamani kulala.’

Basi kwa mara ya kwanza nikaongea maana wanajeshi walianza kutusogelea ili kutuua.

‘O Chaka,’ nilipaza sauti, “Mimi ni Mopo na huyu ni Baleka dada yangu.’

Kicheko kikubwa kilitoka kwa wale waliokuwepo.

‘Vyema sana Mopo na dada yako Baleka,’ alisema Chaka huku akitabasamu. ‘Asubuhi njema kwenu Mopo na Baleka, Usiku mwema pia.’

‘O Chaka,’ nilirukia. ‘Mimi ni Mopo mwana wa Makedama wa kabila la Langeni. Ni mimi niliyekupatia kibuyu cha maji miaka mingi iliyopita, sote tulipokuwa bado wadogo. Uliniambia nikujie utakapokuwa mkuu. Uliahidi kuwa utanilinda na hutanifanyia ubaya. Basi nimekuja nikiwa na dada yangu. Nakuomba uyakumbuke maneno yako ya zamani.’

Nilipokuwa ninaongea uso wa Chaka ulibadilika na alisikiliza kwa makini sana. ‘Wanaongea ukweli,’ alisema Chaka. ‘Karibu Mopo. Utakuwa mbwa kwenye numbani mwangu na utakula kutoka mikononi mwangu. Lakini sikusema chochote kuhusu dada yako. Sasa kwa nini asiuawe iwapo niliahidi kulipa kisasi juu ya kabila lenu lote isipokuwa wewe tu?’


Itaendelea. . . .
 
‘Sababu ni mzuri ee chifu!’ Nilijibu kwa ujasiri, ‘Pia sababu ninampenda, ombi langu kwako ni umuachie maisha yake.’

‘Mgeuzeni huyo binti nimuone,’ alisema Chaka. Askari wake walimgeuza naye akauona uso wa Baleka.

‘Kwa mara nyingine mwana wa Makedama haujaongea uongo. Nimekubali ombi lako. Naye pia atalala kibandani kwangu, atakuwa mmoja wa dada zangu. Haya nisimulie yaliyokupata. Ongea ukweli tu.’

Basi nikaketi na kumsimulia kisa changu chote. Hakuchoka kusikiliza. Nilipomaliza hakuongea chochote zaidi ya kusema anatamani mbwa Koozi asingeuawa, kwamba kama angekuwa hai angemuweka juu ya nyumba ya baba yangu, Makedama na kumfanya kuwa Chifu wa kabila la Langeni. Kwa Wazulu ilikuwa ni ishara mbaya sana kwa mbwa kupanda juu ya paa.

Akamgeukia kapteni wa askari wake. ‘Nimebadili mawazo yangu. Msiwatese hao askari wa Langeni. Mmoja auawe na mwingine aachwe huru. Unamuona huyu, alimuelekezea mtu tuliyemuona akikokotwa kutoka bomani. Mopo huyu ni mtu aliyejithibitisha kuwa ni muoga. Jana boma la wachawi lilishambuliwa kwa amri yangu. Pengine mmeliona wakati mkija huku. Mtu huyu na wenzake watatu walimshambulia mwanaume aliyejaribu kuwalinda mkewe na wanawe. Mtu huyo alipambana kishujaa, aliua wanajeshi wangu watatu. Huyu mbwa aliogopa kukabiliana naye uso kwa uso, alimuua kwa kumrushia mkuki. Baada ya hilo akamchoma mke wake kwa mkuki, lakini hilo si kitu, alipaswa kupambana na mtu yule ana kwa ana. Sasa ninampa heshima. Atapigana na mmoja wa hawa nguruwe kutoka zizi lako,’ alisema hayo na kuunyosha mkuki wake kwa wale watu wa baba yangu. ‘Atakayepona atakimbizwa na kuwindwa kama walivyokuwinda wewe. Nguruwe mwingine nitamrudisha kwao na ujumbe. Haya chagueni wenyewe watoto wa Makedama, nani ataishi.’

Wale watu wa kabila langu walikuwa ni ndugu waliopendana. Kila mmoja alikuwa tayari kufa ili mwenzake awe huru. Basi wote walitoka mbele wakisema watapambana na Mzulu.

‘Nguruwe hawana ustaarabu?’ Alisema Chaka. ‘Basi itakuwa hivi, mnauona huu mkuki? Nitaurusha juu. Kama utaangukia mpini basi huyo mrefu atakuwa huru. Kama ukiangukia ncha basi mfupi atakuwa huru.’ Alirusha mkuki ukawa unazunguka hewani. Kila mtu aliuangalia. Uliangukia mpini.

‘Njoo hapa wewe,’ alisema Chaka akimwita yule mrefu. ‘Nenda haraka kwenye boma la Makedama, kamwambie kuwa Chaka, Simba wa Zulu anasema kuwa ‘Miaka mingi iliyopita kabila lako lilininyima maziwa, leo mbwa wa mtoto wako Mopo anapiga kelele kwenye paa la nyumba yako.’ Haya nenda.

Mtu yule aligeuka. Akampa ndugu yake mkono wa kwa heri na kwenda zake huku akiwa amebeba ujumbe wa laana.

Kisha Chaka akamwita mzulu na yule aliyebaki kati ya waliotufukuza na kuwaamuru wapigane. Walipotoa heshima zao kwa Chaka wakaanza kupambana vikali, mwishowe mtu wa kabila langu alimshinda mzulu. Mara tu baada ya pumzi kumrejea akaanza kukimbizwa auawe, watu watano walichaguliwa kumkimbiza.

Aliweza kuwashinda. Alikimbia na kukwepa kama sungura na kwenda zake salama. Chaka hakuchukizwa na hilo, nadhani aliwaambia wale wanaomkimbiza kuwa waende polepole. Kulikuwa na kitu kimoja kizuri katika ukatili wote wa Chaka, siku zote alijaribu kuokoa maisha ya mtu shujaa, na alifanya hivyo bila kuonekana kuwa amekiuka maneno yake. Kwa upande wangu, nilifurahi kuona mtu wa kabila langu amemuua yule aliyewaua watoto wa mwanamke tuliyemkuta kule nyuma ng’ambo ya mto.
 
Mopo awa mganga wa mfalme

Basi babaangu hayo ndiyo matukio yaliyotokea mpaka mimi na Dada yangu tukaishi kwenye boma la Chaka, Simba wa Wazulu. Pengine utauliza kwa nini nimekukalisha muda mrefu kukusimulia kisa hiki, kisa ambacho hakina tofauti na visa vingine katika maisha, huko mbele utaelewa, kama tu ambavyo mti unazaliwa kutoka kwenye mbegu ndivyo matukio hayo yalivyokuja kumzaa Umslopogazi Bulalio, Umlopogazi Chinjachinja na Nada Mrembo, watu ambao ninapaswa kusimulia kisa cha mapenzi yao. Nada alikuwa ni binti yangu, na juu ya Umslopogazi, wengi hawajui lakini alikuwa ni mwana wa Chaka, mzaliwa wa Baleka dada yangu.

Baada ya Baleka kurudia afya yake kutoka kwenye udhaifu wa safari yetu, baada ya uzuri wake kurudi Chaka akamchukua kuwa mke wake, kuwa sehemu ya wake zake ambao aliwaita ‘dada’ zake. Chaka alinifanya kuwa mmoja wa waganga wake, alipendezwa sana na dawa zangu hata mwishowe akanifanya kuwa mganga wake mkuu. Hiki kilikuwa cheo kikubwa sana, baada ya miaka michache nikawa nimetajirika kwa ng’ombe na wake; lakini pia ilikuwa kazi ya hatari. Kila asubuhi nilipoamka sikujua kama jioni nitaenda kulala nikiwa mzima. Chaka aliua waganga wengi sana, wale ambao hawakuwa waganga wazuri waliuawa. Siku ambazo mfalme hakuwa sawa kiafya au kiakili aliweza kukimbilia mkuki na kumchoma yule aliyemtibu, alimtesa. Mimi niliepuka hayo sababu ya nguvu ya dawa zangu, na pia kwa sababu ya kiapo ambacho Chaka aliniapia nilipokuwa mdogo. Basi ikawa kwamba kila alipo mfalme basi nami nipo. Nililala karibu na nyumba yake, nilikaa nyuma yake kwenye baraza na vitani nilikaa pembeni yake siku zote.

Ah vita! Vita! Vita! Vita! Siku zile tulijua kupigana babaangu! Siku zile maelfu ya tumbusi yalifuata wanajeshi wetu. Fisi walienda sambamba na misafara ya askari wetu kwa makundi, na hakuna aliyerudi na njaa. Kamwe sitasahau vita yangu ya kwanza nikiwa pembeni ya Chaka. Ilikuwa dhidi ya mpinzani wa Chaka. Chifu Zwide alikuwa amemshambulia Chaka kwa mara ya tatu. Chaka alitoka kupambana naye akiwa na vikosi kumi vya askari, kama wanajeshi elfu thelathini hivi.

Kwenye kilima kifupi mbele yetu vilijipanga vikosi vya Zwide. Vikosi kumi na saba. Ardhi ilikuwa nyeusi kwa wingi wao. Manyoya meupe waliyovaa kichwani yalikuwa kama theluji. Sisi pia tulikuwa kwenye kilima ng’ambo yao, katikati kulikuwa na bonde ambalo kijito kidogo kilipita. Usiku mzima mioto ilimulika bonde, sauti za nyimbo za wanajeshi zilisikika kote bondeni. Mapambazuko yakafika, ng’ombe walipiga kelele kwa kuona mwanga, wanajeshi waliamka kutoka vitanda vyao vya mikuki. Waliamka na kutikisa umande kutoka kwenye nywele, mikuki na ngao zao—ndiyo waliamka! Waliokuwa tayari kufa. Walijipanga kulingana na vikosi vyao, wengi kama nyota, na kama nyota, waling’aa. Upepo wa asubuhi ulivuma na kulaza manyoya ya ndege waliyovaa, walionekana kama ambavyo nyasi zenye maua hulala nyikani wakati wa upepo. Jua la Mchinjaji likapanda, mwanga wake ulikuwa mwekundu juu ya ngao nyekundu. Walicheka kwa kufurahia vita. Kifo kitu gani? Je halikuwa jambo jema kufa kwa mkuki? Kifo kitu gani? Haikuwa vyema kufa kwa ajili ya mfalme? Kifo kilikuwa sehemu ya ushindi. Ushindi utakuwa mwali wao usiku ule, ah! Jinsi yalivyo mazuri matiti yake!

Muziki wa vita wenye nguvu za kuwafanya wanaume wawehuke ulianzishwa upande wa kushoto. Ulipokelewa na kikosi baada ya kikosi.

Sisi ni ng’ombe wa mfalme. Tumezaliwa ili tuchinjwe. Wewe pia, wewe ni mwenzetu! Sisi ni Wazulu, watoto wa Simba.Unatetemeka?

Ghafla Chaka akaonekana akipita kukagua vikosi, alifuatana na makapteni wake, washauri na mimi. Alitembea kama dume kubwa la swala. Kifo kilikuwa machoni pake, na kama dume la swala, alinusa hewa huku akienda. Aliinua mkuki wake na ukimya ukatawala.

‘Wako wapi watoto wa Zwide?’ alipaza sauti, sauti yake ilikuwa kama sauti ya fahali.

‘Wale kule ng’ambo baba,’ vilijibu vikosi huku mikuki yote ikielekezwa ng’ambo ya bonde.

‘Hawajaja,’ alisema Chaka. ‘Je tuendelee kuwasubiri hapa hadi tuzeeke.

‘Hapana baba,’ jeshi lilijibu. ‘Tuanze! Tuanze!’

‘Kikosi cha Umkandhlu kipite mbele,’ kikosi cha Umkandhlu kilichokuwa na ngao nyeusi kikapita mbele.

‘Nendeni watoto wangu!’ alipiga kelele Chaka. ‘Adui yule pale. Nendeni na msirudi.’

‘Tumekusikia baba!’ Walijibu wote kwa pamoja na kuanza kushuka kilima kama kundi kubwa la wanyama mwitu wenye pembe za chuma.

Wakavuka kijito. Hapo Zwide naye akaamka. Kelele zilisikika kutoka kwenye vikosi vyake; ncha za mikuki yao iliyopangwa kwa mstari ziling’aa.

Wakakutana. Sauti za migongano ya ngao ilisikika kama ngurumo za radi. Sauti za vita. Walipambana wakirudishana mbele na nyuma. Mwishowe kikosi cha Umkandhlu kikazidiwa—kikarudi nyuma na kuvuka kijito, nusu yao wakiwa wameuawa. Sauti za hasira zilisikika kutoka kwa wanajeshi, ni Chaka pekee ndiye alitabasamu.

‘Fungueni njia! Fungueni njia!’ alipiga kelele. ‘Wapeni WASICHANA wa Umkandhlu nafasi.’ Wanajeshi wa kikosi cha Umkandhlu walipita, vichwa wameinamisha chini.

Baada ya hilo akatoa neno kwa washauri wake, nao washauri wakakimbia kwa Menziwa, jenerali na kwa makapteni. Vikosi viwili vilishuka kilimani. Viwili vingine vilipita kushoto na vingine viwili vikapita kulia. Chaka yeye aliendelea kubaki kilimani na vikosi vitatu vilivyobakia. Ngurumo za mgongano wa ngao ukasikika tena. Ah! Wale walikuwa wanaume: Walipigana, hakuna kukimbia. Walishambuliwa na kikosi baada ya kikosi lakini bado waliendelea kusimama. Waliuawa mamia na baadaye maelfu lakini hakuna aliyegeuka, kila askari chini yake kulikuwa na maiti mbili. Ah babaangu! Kwenye vikosi hivi viwili hakuna aliyepona. Walikuwa ni wavulana tu, lakini walikuwa watoto wa Chaka. Menziwe alilala amekufa na kufunikwa na rundo la mashujaa wake. Siku hizi hakuna wanaume kama wale.

Wote walikufa. Chaka alikuwa bado ameinua mkono wake. Aliangalia kaskazini na kisha kusini. Tazama, kuna mikuki inang’aa kwenye miti. Sasa vikosi vyetu vilimkaribia adui kutokea pembeni. Walichinjwa na wao walichinja. Lakini watu wa Zwide walikuwa wengi na mashujaa, vita ikaanza kutuelemea.

Kisha Chaka akasema neno. Makapteni wakasikia. Wanajeshi wakanyoosha shingo zao kusikia. Ikasikika. ‘Mbele watoto wa Wazulu.’

Kulikuwa ngurumo, kelele za vita zilisikika, mikuki iling’aa na manyoya kichwani yakalala. Kama mto uliotapika, kama mawingu ya tufani—tuliwaangukia rafiki na adui . Walijipanga kutukabili; tukavuka kijito. Watu wetu walijeruhiwa walisimama na kutupungia mikono lakini tuliwakumba, wanafaida gani? Hawawezi kupigana tena. Kisha tukakutana na Zwide, akija kasi kutukabili. Fahali kukabiliana na fahali. Ah! Babaangu, sikujua chochote kilichoendelea. Kila kitu kilikuwa chekundu. Hakika ilikuwa vita! Tuliwafagilia mbali. Kulipotulia hakuna kilichoonekana isipokuwa ardhi ilikuwa nyeusi na nyekundu. Wachache walikimbia, tuliwaruhusu wachache kukimbia, tuliwapitia kama moto; tuliwala kabisa. Tukakaa kumtafuta adui, hakuonekana. Wote walikuwa wamekufa. Zwide hakuwako tena. Tukajitahidi kujikusanya. Vikosi kumi vililiona jua la asubuhi; ni vikosi vitatu tu ndivyo vililiona likizama; vingine vimeenda mahali kusiko na mwanga wa jua.

Hizo ndizo zilikuwa vita zetu enzi zile za Chaka.

Unauliza juu ya kikosi cha Umkandhlu kilichokimbia. Nitakuambia kilichotokea. Tuliporudi bomani Chaka alikikusanya kikosi kile. Aliongea nao kwa upole sana. Aliwashukuru kwa kazi yao, alisema kuwa ni jambo la kawaida kwa wasichana kuzimia na kukimbilia kwenye maboma yao waonapo damu. Lakini alikuwa amewaamuru wasirudi na wao wamerudi! Sasa awafanye nini? Akaziba uso wake kwa blanketi na wanajeshi wakawaua askari wote wa kikosi cha Umkandhlu, karibu watu elfu mbili—waliwaua huku wakiwadhihaki na kuwatukana.

Hivyo ndivyo tulivyowashugulikia waoga nyakati zile. Baada ya hayo, mtu mmoja wa kabila la Zulu alikuwa sawa na watu watano wa makabila mengine. Hatageuka kukimbia hata akishambuliwa na watu kumi. Kaulimbiu yetu ilikuwa ni ‘Pigana ufe, kamwe usikimbie.’ Katika kipindi chote cha maisha ya Chaka jeshi lililoshindwa halikupita tena kwenye lango la Ikulu.

Vita ile ilikuwa ni moja tu kati ya nyingi. Kila mwezi wanajeshi wapya waliandaa mikuki yao, walienda vitani na wachache walirejea, lakini walirejea na ushindi na ng’ombe nyingi. Kabila moja baada ya jingine lilianguka mbele yetu. Wale waliopona kuanguka kwa mkuki walichukuliwa kuunda vikosi vipya. Kwa hiyo, japokuwa maelfu ya askari walikufa kila mwezi bado jeshi letu lilizidi kukua. Baada ya muda hakukuwa na chifu yeyote aliyesimama. Umsuduka alianguka, baada yake Mankengeza. Umzilikazi alikimbilia kaskazini; Matiwane alisagwa kabisa. Tuliingia nchi yake ya Natal. Tulipoingia idadi ya watu wake ilikuwa haihesabiki. Tulipotoka ilikuwa bahati sana kumuona mtu. Tuliangamiza wanaume, wanawake na watoto. Tulisafisha kabisa nchi. Sasa ikaja zamu ya Ufaku, chifu wa Amapondozi. Ah! Yuko wapi Ufaku leo.

Basi iliendelea hivyo siku na siku mpaka Wazulu wenyewe wakawa wamechoshwa na vita, na hata mikuki mikali zaidi ikawa imekuwa butu.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom