Bilionea Asigwa
JF-Expert Member
- Sep 21, 2011
- 16,515
- 28,504
Wahalifu wa mitandao wamedaiwa kuingilia akaunti za wateja wa Benki ya Biashara ya Standard Chartered na kuiba fedha kiasi ambacho hakijajulikana.
Mkuu wa Uhusiano na Masoko wa benki hiyo, Joanita Mramba alisema wamechukua hatua ikiwamo kuzuia kadi za kutolea fedha na kuanza mchakato wa kutengeneza kadi mpya ili kudhibiti wizi huo.
“Kwanza kabisa nawahakikishia wateja wetu fedha zao ziko salama na wasiwe na wasiwasi waendelee kufurahia huduma ya benki yetu.
Alisema tukio hilo lilianza kujitokeza mwanzoni mwa wiki iliyopita na benki iliwataarifu wateja wake kwa simu kuwa kuna jaribio la kuingilia akaunti zao ili kuibiwa fedha zao.
Mkazi wa Kimara, Method Makumvi aliyekumbwa na mkasa huo alisema alibaini kuwa ameibiwa baada ya kukosa fedha kwenye akaunti yake jana.
“Nilifika katika moja ya mashine za ATM, iliyopo Mwenge, kutoa fedha ya mafuta ya gari langu.Bahati mbaya sikukuta kitu na akaunti ilikuwa na kiasi cha Sh800,000,” alisema Makumvi.
Aliongeza kuwa baada ya kubaini tukio hilo alikwenda moja tawi la benki hiyo maeneo ya Shoppers Plaza na kuwaelezea mkasa huo.
“Wahudumu wa benki waliniambia siyo mimi pekee niliyekumbwa na mkasa huu. Wakanishauri nijaze fomu kwa ajili ya kuzipata fedha zangu zilizokuwa katika akaunti,” alisema.
Kutokana na tukio hilo, Makumvi alielezwa na wahudumu wa benki hiyo kuwa wameamua kuzuia kadi za ATM za wateja wote na kuamua kutoa kadi mpya lengo likiwa ni kupambana na wizi huo.
Source: Mwananchi.
My take: Wateje wa Standard Chartered mkaangalie taarifa za akaunti zenu.