Chunya yatumia mitumbwi kuhesabu watu [sensa]

sir.JAPHET

JF-Expert Member
May 18, 2012
699
133
Alhamisi, Agosti 30, 2012 | Na Pendo Fundisha, Chunya | Gazeti la Mtanzania

HALMASHAURI ya Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya imeanza kutumia usafiri wa boti na mitumbwi kwa ajili ya kuwafikia wananchi waishio kando kando ya mito na pembezoni mwa Ziwa Rukwa kwa ajili ya kuhakikisha wanahesabiwa katika mchakato wa Sensa ya Watu na Makazi.

Akizungumza mjini hapa jana, Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Deodatus Kinawilo, alisema Serikali imeamua kutumia usafiri wa boti na mitumbwi katika kuhakikisha jamii yote ya wafugaji na wakulima inafikiwa.

Alisema kutumika kwa vifaa hivyo kumesaidia mchakato wa Sensa kuendelea vizuri kutokana na wananchi wote kuhesabiwa ikiwa ni haki yao ya msingi licha ya jamii ya wafugaji kutoa sababu mbalimbali kwa nia ya kutaka kukwepa kuhesabiwa.

Aidha, alisema mbali na kutumia vifaa hivyo, pia walikabiliwa na changamoto kwa jamii ya wafugaji kujaribu kukwepa kuhesabiwa, huku wakitoa sababu mbalimbali ambazo zote zimetatuliwa.

"Wafugaji walijaribu kukwepa kuhesabiwa kwa kutoa sababu mbalimbali, lakini tulifanya jitihada za kutoa elimu na hivyo limefanikiwa," alisema Kinawiro.

Alisema siku za mwanzo mpango wa kuwahesabu ulikuwa mgumu, lakini sasa wafugaji wameanza kuelimika kwa kujua umuhimu wa Sensa.

Kwa upande wake, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Malangali, Kata ya Totowe wilayani Chunya, Bahati Mwangula, alisema Agosti 26, jamii ya wafugaji iligoma kwa stahili yake ya kutohesabiwa kwa sababu za kuugua na hali hiyo iliwapatia wakati mgumu makarani wa Sensa.

Alisema baada ya kugundua changamoto hiyo viongozi wa kijiji, mtaa na kata walilazimika kushirikiana na makarani wa Sensa kupita nyumba hadi nyumba kwa ajili ya kutoa elimu ya kushiriki kuhesabiwa.

Hata hivyo, Diwani wa Kata ya Totowe, Godian Wangala, alisema maeneo mengi ya wafugaji yamekuwa na tatizo hilo na wengine kukimbia makazi yao kutokana na wingi wa mifugo waliyonayo.
 
Back
Top Bottom