Watu watatu wamenusurika kifo baada ya kula chakula kinachosadikiwa kuwa na dawa za kulevya hali iliyosababisha kupoteza fahamu kwa muda wa saa tisa bila kujitambua hali iliyowapa nafasi wahalifu kufanikisha kupora mali mbalimbali ikiwemo TV katika nyumba ya kulala wageni inayofahamika kwa jina la Diana iliyopo mjini Chato mkoa wa Geita.
Wakizungumza na ITV katika hospitali ya wilaya ya Chato walipolazwa kwa matibabu zaidi wagonjwa hao wameonekana kudhoofika kiafya wamesema kuwa walipata mteja ambaye alichukua chumba kimoja kwa ajili ya kulala na baadaye alitoka kwenda kula hotel jirani aliporudi aliyewakarimu kwa kuwapatia chakula aina ya chipsi ambazo zinasadikiwa kuwa na dawa za kulevya na walipokula walianza kuishiwa nguvu.
Akithibitisha kupokea wagonjwa watatu wakiwa hawajitambui Mganga wa zamu katika hospitali ya wilaya ya Chato Dkt Paul Kahindi amesema kuwa uchunguzi wa awali umebaini wagonjwa hao walikula chakula chenye dawa za kulevya ambayo haijafahamika.