CHADEMA yaishutumu CCM kuanza kampeni Igunga

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Na Moses Mabula, Igunga

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Wilaya ya Igunga mkoani Tabora kimekishutumu vikali Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kuanza kampeni za ndani
katika maeneo mbalimbali jimboni humo.

Sikuchache zilizopita Msajili wa Vyama vya siasa nchini, Bw. John Tendwa alipiga marufuku vyama vya siasa ambavyo vilikuwa vimeanza shughuli za kisiasa jimboni humo ambazo zinatafsiriwa kama kampeni kabla ya muda.

Mkurugenzi wa Sera na Utafiti wa CHADEMA, Bw. Waitara Mwikabwe alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari jinsi hali ilivyo kwa sasa.

Alisema CCM kimeanza kampeni mapema katika sehemu mbalimbali jimboni humo
sambamba na kutoa rushwa kwa wananchi ili wachague mgombea wake na kueneza lugha za vitisho kwa wananchi kuwa wakichagua mgombea wa CHADEMA wakamatwa na kufungwa jela.

Alieleza kuwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Kamati ya Ulinzi na Usalama zinashiriki kwa kiasi kikubwa katika kutoa vitisho kwa wananchi kwa maslahi ya CCM.

Bw. Waitara alimshutumu Msimamizi wa Kampeni wa CCM, Bw. Mwigulu Nchemba kuwa ni mmoja ya watu wanaoeneza rushwa vijijini kwa kurubuni vijana na kushawishi makundi ya watu na kutoa pesa ili kukisafishia njia chama hicho.

Alisema Bw. Nchemba amekuwa akitoa pesa na kununua kadi za wapigara na kushusha bendera za CHADEMA na kutundika za chama chake.

Alisemsa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU)
wilayani Igunga 'haipo na haifanyi kazi' kwani matukio mengi yamekuwa
yakifanywa na hakuna hatua inayochukuliwa.

Nchemba akanusha tuhuma

Kwa upande wake, Bw. Nchemba alipoulizwa na Majira alikana tuhuma hizo akisema huo ni uongo na ni ishara kuwa CHADEMA wameanza kuweweseka.

"Kwa jinsi nilivyopanga safu, na kwa jinsi wanavyoanza kuweweseka afadhali wasiweke kabisa mgombea maana wanakwenda kushindwa vibaya," alisema Bw. Nchemba ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi.

Alisema hajashusha wala kugusa bendera ya CHADEMA kwa kuwa ana mzio nayo ila inawezekana wananchi wameziteremsha wenyewe baada ya kutambua ukweli.

Kuhusu tuhuma za kutoa rushwa alisema hajafanya hivyo, na wala fedha zenyewe hana kwa kuwa hajatumiwa fedha na chama.

"Hawa wanalalamika kana kwamba Igunga ni sawa na darasa la watu 45, ile ni wilaya ina kata zaidi ya 20 na vijiji zaidi ya 90, hapo rushwa utampa nani utamwacha nani?" alihoji.

Kampeni rasmi za kuwania ubunge wa Igunga ulioachwa wazi na Bw. Ropstam Aziz aliyejiuzulu zinatarajiwa kuanza kutimua vumbi Septemba 7, mwaka huu mpaka Novemba Mosi mwaka huu. Uchaguzi utafanyika Novemba 3.
 
Back
Top Bottom