CHADEMA inakimbia, tutafika?

Josh Michael

JF-Expert Member
Jun 12, 2009
2,523
78
WATANZANIA wenzangu, kwamba ni chama gani cha upinzani kinakua kwa kasi kubwa hivi sasa kuliko vingine, hilo si swali tena.

Wiki iliyopita nilifafanua jinsi Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kinavyokua kwa kasi na kilivyo na nafasi ya kuzidi kukua kwa kasi kuliko Chama cha Wananchi (CUF) na vingine vya upinzani.

Moja ya sababu kuu zinazoifanya CHADEMA kukua kwa kasi kisiasa ni haiba yake kitaasisi pamoja na haiba ya viongozi wake kisiasa, kama nilivyofafanua wiki iliyopita.

Je, ni haiba tu inayoifanya CHADEMA ikue kwa kasi kuliko CUF? Tuvitazame tena vyama hivi kwa muono wa kigezo cha pili cha ajenda ya chama, tukilenga itikadi na sera za vyama husika, kabla sijahitimisha tathmini juu ya vyama hivi kwa kigezo cha oganaizesheni na utafutaji wa raslimali za kufanyia siasa.

Kwa muhtasari, CHADEMA ni chama kinachoamini katika itikadi ya mrengo wa kati kwa mujibu wa madhumuni yake na sera zake.

Ukipitia madhumuni yake ya kiuchumi utaona kuwa chama hiki kinaamini katika kukuza na kuimarisha uchumi wa nchi kwa kutumia rasilimali za nchi bila kuathiri uhuru wa taifa na kuhakikisha kuwa umma kwa ujumla unanufaika na rasilimali hizo.

CHADEMA inaamini katika kujenga na kuimarisha uchumi wa soko huru ama soko la kijamii, utakaoheshimu na kulinda haki na mali za watu, biashara huru na sekta ya watu binafsi bila kupoka mamlaka ya umma katika maeneo nyeti.

Inaamini katika soko huru na si soko holela. Inaona kuwa umiliki wa rasilimali na mali miongoni mwa wananchi utawapa uhuru zaidi hivyo kuweza kujenga chama na baadaye taifa lenye kutoa fursa, ambapo kila mtu bila kujali asili na hali yake anaweza kutimiza na kufanikiwa kadiri ya vipaji vyake.

Imani ya chama hiki ni kuwa, itikadi ya mrengo wa kati ikifuatwa, basi taifa litaepukana na mzigo wa kuwa na serikali kubwa ambayo ni mzigo kwa walipa kodi, tofauti na muundo wa kiserikali ya kijamaa ambao serikali kuu inakuwa pana na yenye mikono kila mahali na kuwa mzigo kwa wananchi.

Kwa itikadi hii, CHADEMA inajitofautisha na CCM inayojinasibu kufuata itikadi ya ujamaa, ingawa ukweli ni kuwa hata ujamaa wenyewe haufuatwi.

Kwamba CCM haifuati siasa ya ujamaa na kujitegemea, hilo ni suala linalothibitishwa na hali halisi ya sera za soko holela zinazoendelea kufuatwa na chama hicho kikongwe nchini, huku maneno ya muasisi wake, hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, yakithibitisha hivyo.

CCM ililizika Azimio la Arusha lililobeba itikadi ya ujamaa na kuanzisha Azimio la Zanzibar lililobeba sera za soko huri (holela), zinazokumbatia watu wachache na kukandamiza maskini walio wengi.

“Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi iliketi Unguja na kubadili Azimio la Arusha bila ya kupata maoni ya wananchi, na walikuwa na haki ya kufanya hivyo maana sera yenyewe ni yao.

“...Tatizo lao ni kwamba, jambo lenyewe walilifanya kwa hila na janjajanja na mpaka leo wanaendelea kuwadanganya wananchi kwamba sera ya CCM ni ujamaa na kujitegemea,” alisema Mwalimu Nyerere katika kitabu chake cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania (1992).

Kwa mtazamo wa kifalsafa, CHADEMA inaamini kuwa “Nguvu na mamlaka ya umma” (People’s Power) katika kumiliki, kuendesha, kubuni na kuendeleza mawazo, rasilimali, uchumi na siasa za nchi, ndiyo itakayolikomboa taifa hili maskini.

Kwamba, nguvu na mamlaka kwa umma ndio msingi na chimbuko la kuundwa kwa dola ya nchi na kuwa umma ndio wenye madaraka ya mwanzo na mwisho katika kuamua hatima ya nchi na taifa pasipo kuingiliwa, kudanganywa au kughilibiwa na viongozi, watawala ama wageni.

Kwa mtazamo wa kisera, sera kuu ya CHADEMA ni sera ya mfumo mpya wa utawala, ambayo pamoja na mambo mengine inakusudia kuanzisha utawala wa majimbo.

Sera hii ndiyo hasa inayoonekana kukipa chama hiki sifa ya kuwa chama mbadala, kutokana na kutoa mtazamo na muongozo mbadala juu ya kulikomboa taifa hili kutoka kwenye umaskini.

Dira ya sera mpya ya utawala ya CHADEMA, almaarufu sera ya majimbo, ni kuwa na taifa linaloendelea kwa haraka na kwa usawa, lenye haki, umoja na mshikamano wa kweli.

Dhumuni kuu la sera hiyo ni kujenga mfumo na muundo wa utawala unaotoa nguvu na mamlaka zaidi kwa umma katika kujiongoza na kutumia rasilimali zao kwa usawa kujiletea maendeleo.

Baadhi ya malengo makuu ya sera hii ni kupunguza ukubwa wa serikali kuu kimuundo na kimajukumu pamoja na gharama zake za uendeshaji na kuachia rasilimali nyingi kutumika moja kwa moja kwa maendeleo ya wananchi.

Sera hiyo inalenga kurahisisha uongozi wa nchi kwa kuiunganisha mikoa kuwa majimbo ambayo viongozi wake watapatikana na kuongoza kwa ridhaa ya wananchi.

Inalenga kupunguza urasimu wa kufikia maamuzi na kuongeza ufanisi na usimamizi wa karibu zaidi katika utoaji huduma kwa jamii chini ya tawala za majimbo.

Inakusudia kuondoa matabaka kwa kuweka mgawanyo mzuri na matumizi mazuri ya rasilimali kati ya eneo moja la nchi na jingine.

Aidha, sera hiyo inakusudia kuimarisha mfumo na muundo wa Serikali za Mitaa kwa kuingiza ngazi ya mkoa katika muundo huu, na kuondoa migongano ya kiutendaji kati ya Serikali Kuu na mamlaka za Serikali za Mitaa kwa pande zote kufanya kazi katika eneo moja la kijiografia na katika jamii ile ile moja.

Kama nilivyoeleza wiki kadhaa zilizopita, ni muhimu na pengine ni lazima kwa chama kinachotaka kuchukua dola kuwa na sera kuu ambayo ni mbadala wa sera za chama kilicho madarakani, vinginevyo hakuna sababu za msingi kwa chama hicho kuungwa mkono, ikiwa sera zake ni sawa tu na sera za chama kinachotaka kukiondoa madarakani.

Kwa sera hiyo ya mfumo wa utawala, CHADEMA imeweza kujipambanua kama chama mbadala kuliko CUF ambayo nilishafafanua kwa mifano dhahiri jinsi sera zake zinavyofananafanana na zile za CCM.

Ili kuona ni kwa kiasi gani sera hiyo ya mfumo mpya wa utawala inaifanya CHADEMA kuwa chama mbadala, ni vema kutilia maanani yafuatayo:

Mosi, nchi yetu imeendelea kuwa moja ya nchi maskini sana duniani licha ya kuwa taifa huru kwa miaka 47 sasa.

Muda huu ungetosha kabisa kulifanya taifa hili pamoja na watu wake wapige hatua kubwa kimaendeleo.

Kinyume chake kipindi cha miaka 47, kimethibitisha kwamba sera na mikakati mingi ya maendeleo ya jamii na kiuchumi imejaribiwa na kukwama au kuleta mafanikio kidogo na ya taratibu mno.

Hata sasa Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA) hauonekani kubadili hali ya maisha ya watu kwa kasi inayostahili.

Nchi imepewa mikopo na misaada mingi sana tangu uhuru na hata kufutiwa madeni lakini bado ni maskini.

Kukwama na kusuasua kwa sera na mikakati mingi ya kimaendeleo tena ndani ya kipindi kirefu kabisa cha miaka 47 sasa, kunaibua haja ya msingi ya kuutazama upya mfumo wa sasa wa utawala.

Pili, taifa limekuwa likiendelea taratibu mno na wakati huo huo kukiibuka matabaka kati ya walionacho na wasionacho na kutoa dalili mbaya kwa mustakabali wa amani, umoja na mshikamano wa taifa hili.

Hili pia linaibua haja ya kuutazama upya mfumo wa sasa wa wa utawala kama walivyofanya CHADEMA katika sera yao hiyo.

Tatu, ufisadi na rushwa vimekuwa ni moja ya matatizo makubwa na ya muda mrefu ndani ya serikali, hali inayoibua haja ya kuutazama upya mfumo wa sasa wa utawala ili kuweza kujenga udhibiti wa kutosha dhidi ya matatizo haya, kama ilivyofanya CHADEMA.

Nne, mfumo wa sasa wa utawala ulishaonyesha udhaifu mkubwa tangu miaka ya mwanzoni baada ya uhuru lakini hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa hazijaweza kuondoa kiini cha tatizo.

Mathalani, kutekelezwa kwa Mpango wa Madaraka Mikoani, na Mipango ya Maboresho ya Serikali za Mitaa, vyote havijaweza kupeleka nguvu na mamlaka kwa umma vya kutosha wala kuongeza ufanisi wa kutosha katika kuwaongoza watu.

Tano, mfumo wa sasa wa utawala ulirithiwa na kuigwa na viongozi kutoka katika mfumo wa utawala wa kikoloni, ukaandikwa kwenye katiba na katiba hiyo kupitishwa na viongozi tu.

Wananchi hawakupewa haki yao ya kuelimishwa na kutoa maoni. Hili pia linaibua haja ya wananchi kupewa haki ya kuandika katiba yao pamoja na mambo mengine, itabainisha kwa ridhaa yao namna bora ya jinsi wanavyotaka kujiongoza.

Sita, Tanzania yetu ni nchi kubwa sana. Ina ukubwa wa kilometa za mraba laki tisa na arobaini na tano elfu (945,000 km2).

Ukubwa huu ni zaidi ya ukubwa wa nchi za Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Lesotho na Swaziland zikichanganywa pamoja.

Tanzania inakadiriwa kuwa na watu milioni 40 ikiwa ni nchi ya 38 kati ya nchi 195 za dunia kwa wingi wa watu.

Katika Afrika, Tanzania ni ya saba kwa wingi wa watu ikizidiwa na Nigeria (yenye watu zaidi ya milioni 132), Misri (zaidi ya milioni 79), Ethiopia (zaidi ya milioni 75), Kongo (zaidi ya milioni 63), Afrika Kusini (zaidi ya milioni 44) na Sudan (yenye watu takriban milioni 41).

Ukubwa huu wa nchi unajenga hoja za kuwa na mfumo mbadala wa utawala utakaochochea ufanisi na maendeleo ya haraka kwa kupeleka madaraka karibu zaidi na wananchi badala ya kila kitu kuidhinishwa, kutekelezwa na kusimamiwa na utawala wa serikali kuu ulio katika eneo moja tu la nchi (Dar es Salaam).

Pia, ukubwa huo wa nchi unaonyesha haja ya msingi ya kuwa na mfumo mbadala wa utawala utakaotoa kwanza uhuru kwa watu kutumia rasilimali zinazopatikana katika maeneo yao kujiletea maendeleo na wakati huo huo kufidia maeneo yatakayoonekana kupungukiwa rasilimali, badala ya rasilimali kutoka pembe zote za nchi kulimbikizwa Dar es Salaam.

Kwa kigezo cha oganaizesheni, ukuaji wa CHADEMA unaonekana kwenda kasi kuliko uwezo wake wa kioganaizesheni wa kupokea wanachama wapya na kuwaratibu kwa manufaa yake ya kisiasa.

Kwa sababu hiyo, idadi ya wanachama wa CHADEMA si kubwa sana kulinganisha na idadi ya mashabiki na wapenzi wa chama hicho waliotapakaa katika mikoa, wilaya na vijiji mbalimbali nchini, bila kuwa na kadi za uanachama.

“Wakati CHADEMA ikikadiriwa kuwa na wanachama 900, 000 nchi nzima, hali halisi inaonyesha kuwa kuna Watanzania wengi zaidi wanaokiunga mkono chama hicho, hasa katika mikoa ya Mara, Mwanza, Kilimanjaro, Kagera, Shinyanga, Kigoma, Rukwa, Arusha, Iringa, Mbeya na Dar es Salaam, lakini hawana kadi za chama hicho na wengine hawajui wapi pa kuzipata. Huu ndio udhaifu mkubwa wa CHADEMA.”

Hata hivyo, mikutano yake almaarufu ’Operesheni Sangara’, imeonekana kufanikiwa kukijenga chama hicho na kukiweka karibu zaidi na wananchi hasa kwenye mikoa yote ya Kanda ya Ziwa.

Kwa kigezo cha utafutaji na utumiaji wa raslimali au fedha kwa ajili ya kugharamia shughuli za kisiasa, CHADEMA inaonekana tena kuifunika CUF kwa sababu zifuatazo:

Mosi, wakati CUF inapata ruzuku ya serikali ya sh milioni 128 kwa mwezi, CHADEMA inapata ruzuku ya sh milioni 72 tu, lakini hekaheka za siasa za CHADEMA, kama kufanya kampeni kwa helikopta na kuendesha operesheni sangara kwa kishindo, zinaonyesha dhahiri jinsi chama hicho kinavyotumia vema ruzuku yake ndogo kulinganisha na CUF yenye ruzuku kubwa ambayo kwa muda mrefu imeonekana kuelekeza nguvu zake nyingi Zanzibar.

Pili, kwa mtazamo wa utafutaji, mazingira yanaonyesha kuwa viongozi wa CHADEMA ndio wamekuwa mahiri zaidi katika kutafuta wafadhili wa kukisaidia chama hicho kiufundi na kirasilimali kutoka ndani na nje ya nchi kuliko hali halisi inavyoonekana kwa upande wa CUF.

Mathalani, CHADEMA leo inaonekana kufaidika kwa kuwa mwanachama wa Umoja wa Kimataifa wa Vyama vya Kidemokrasia Duniani (IDUA) na ule wa Afrika (DUA).

Hatua ya Mbowe kuzindua mpango wa kusajili wanachama na kuchangisha fedha kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu (SMS), ni goli jingine la kisiasa ambalo CUF imefungwa na CHADEMA.

Kwa upande mwingine, hatua hiyo sawa na ile ya kutumia helikopta, inaifanya CHADEMA kuzidi kuonekana kuwa ni chama cha kizazi kipya, cha kisasa, kinachoendeshwa kisomi, kikimbia kisayansi na kiteknolojia.

Sasa naitangaza CHADEMA kuwa chama chenye sifa nyingi za kuiondoa CCM madarakani kuliko CUF na vyama vingine vya upinzani, huku nikiwasihi Watanzania wenzangu hususan wale wa Tanzania Bara, kukiunga mkono chama hiki, tukiwa na mtazamo sahihi kwamba, CHADEMA ndiyo itakayoturahisishia azima yetu ya kuing’oa CCM na hatimaye kuunda serikali itakayojali wananchi kikamilifu.

Kwa upande wa Watanzania wenzetu wa Zanzibar, nachukua fursa hii kuitangaza CUF kuwa chama mbadala katika eneo hilo, huku nikiwasihi kukiunga mkono.

Natoa wito kwa viongozi wa CUF na CHADEMA kuheshimu hali hii halisi ya nguvu za vyama vyao kisiasa na kurudi kwa nia njema kwenye meza ya ushirikiano wa kisiasa, wakiwa na ajenda moja tu, nayo ni CHADEMA kuisaidia CUF Zanzibar na CUF kuisaidia CHADEMA Bara. Hima waache siasa za wivu na ushindani usio na tija. Wakifanya hivyo, Tanzania yetu itakuwa mikononi mwetu, CHADEMA itafika, CUF itafika, sote tutafika...inshaalah tutafika kwa pamoja.
 
CHADEMA ndio Chama ambacho Kipo tayari kwa ajili ya kuchukua uongozi ndani ya Tanzania, Kwa wale wote wapenda demokrasia watajitahidi kuwapa support CHADEMA, Kama serikali dhaifu basi na vyama vyetu ni dhaifu, Huwezi kusema kuwa vyama vya upinzani ni dhaifu huku serikali ikawa imara
 
Umeonesha wazi kuwa wewe ni shabiki mkubwa wa chadema,siwezi kukuamini kwa jinsi ulivoweka wazi ushabiki kuliko hali halisi,na uzuri kuwa tunakujua kuwa wewe ni chadema so lazma uta-base kwa chadema kama ulivoonesha.. Ningefurahi angetokea mtu neutral ili aweze kutufafanulia baina ya vyama hivi vya upinzani.. hata mimi ninaweza kutoa sababu kuwa Cuf ndio ipo tayari kuchukua dola na naweza nikakupa point nzuri tu,lkn yatakuwa ni yale yale kuwa na mimi ninaweza ku-base kwa Cuf. umeweka mbele sana ushabiki.lkn Haki yako mkuu. Respect..
 
Mkuu Josh Michael
Naomba kutofautiana na wewe pale unaposema CHADEMA ni chama kinachokuwa kwa kasi kuliko cha cha CUF.
Mosi CHADEMA si chama cha siasa kama unavyotaka kutudanganya.CHADEMA ni NGO ya kina Mbowe,Mtei na Ndesamburo.Kwamba CHADEMA inakuwa sina tatizo na kukuwa kwa NGO tatizo langu liko kwa baadhi ya watu kama wewe Joshi kuudanganya umma wa Tanzania kwamba CHADEMA ni chama cha upinzani kilicho tayari kuchukua dola.
 
Mkuu Josh Michael
Naomba kutofautiana na wewe pale unaposema CHADEMA ni chama kinachokuwa kwa kasi kuliko cha cha CUF.
Mosi CHADEMA si chama cha siasa kama unavyotaka kutudanganya.CHADEMA ni NGO ya kina Mbowe,Mtei na Ndesamburo.Kwamba CHADEMA inakuwa sina tatizo na kukuwa kwa NGO tatizo langu liko kwa baadhi ya watu kama wewe Joshi kuudanganya umma wa Tanzania kwamba CHADEMA ni chama cha upinzani kilicho tayari kuchukua dola.
Shida moja kubwa ni kwamba nyinyi mulilishwa sumu wakati ule wa Uchaguzi mkuu wa CHADEMA, CHADEMA ni chama Mbadala toka wa CCM na pia kipo tayari kuchukua Dola, Wewe binafsi unajua hivyo na ndio maana unapata shida sana katika kujua na kuona kasi ya chadema inawapa shida sana, Inawezekana kabisa wewe unayesema hivi ni KADA maarufu sana
 
its true CHADEMA wakipewa nchi wapo likely kufanya mapinduzi ya kiuchumi kuliko walivyo CCM,watanzania tafadhali tujaribu kuthubutu kufanya changes,kwanini tunapenda saaana kukunbatia kitu cha zamanii.aliekuambia CCM ikidondoka nchi itakufa nani?40 plus yrs inatosha kwa CCM,lets try then mwanzoni Katiba ibadilike kuwa chama kikiboronga out!
 
its true CHADEMA wakipewa nchi wapo likely kufanya mapinduzi ya kiuchumi kuliko walivyo CCM,watanzania tafadhali tujaribu kuthubutu kufanya changes,kwanini tunapenda saaana kukunbatia kitu cha zamanii.aliekuambia CCM ikidondoka nchi itakufa nani?40 plus yrs inatosha kwa CCM,lets try then mwanzoni Katiba ibadilike kuwa chama kikiboronga out!
CCM wanatumia kuogopesha watu na watu, Ila cha Umuhimu hapa ni kwamba mtu yoyote ile kwamba kama ukiona kuwa vyama dhaifu sana katika Nchi basi jua kwamba hata serikali pia ni dhaifu, vyama imara hujenga serikali imara
 
JOSH MICHAEL NI CHADEMA,meshakujua na nikifuatilia post zako na comments zako..ila ni haki yako ya kokatiba..punguza tu bias, tukiwa tunachangia humu...mfano kuiponda UDOM tu eti kisa CCM imekijenga, wakati ni maendeleo ya taifa kwa ujumla..
 
Shida moja kubwa ni kwamba nyinyi mulilishwa sumu wakati ule wa Uchaguzi mkuu wa CHADEMA, CHADEMA ni chama Mbadala toka wa CCM na pia kipo tayari kuchukua Dola, Wewe binafsi unajua hivyo na ndio maana unapata shida sana katika kujua na kuona kasi ya chadema inawapa shida sana, Inawezekana kabisa wewe unayesema hivi ni KADA maarufu sana

Hivi CHADEMA walikuwa na uchaguzi mkuu au bado mnataka kudanganya wadanganyika !!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!.Mkuu Josh unajua maana ya uchaguzi au unataka kutuchekesha ule si uchaguzi wala CHADEMA haijawahi kufanya uchaguzi pale walikuwa wanamzuga msajili wa vyma.
Nimekwambia CHADEMA ni NGO umeshindwa kuleta hoja kupinga madai yangu unakimbilia uchaguzi mkuu ambao haukuwepo.

Mkuu wacha propaganda zako za kitoto eti mimi ni kada maarufu sana na wewe ni mwana NGO nini !.
 
hatuhitaji chama chenye picha ya NGO na ukabila, hili jambo walieleze vizuri ili watanzania tuwe na imani nao
 
tunahitaji chama ambacho hakina alama ya u NGO au ukabila, CHADEMA walisahihish ili, maana siyo siri kila mtanzania anahisi chadema ni NGO na ni chama cha kikabila...ili watanzania tuwe na imani nacho..naomba comment yangu isifutwe
 
Hivi CHADEMA walikuwa na uchaguzi mkuu au bado mnataka kudanganya wadanganyika !!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!.Mkuu Josh unajua maana ya uchaguzi au unataka kutuchekesha ule si uchaguzi wala CHADEMA haijawahi kufanya uchaguzi pale walikuwa wanamzuga msajili wa vyma.
Nimekwambia CHADEMA ni NGO umeshindwa kuleta hoja kupinga madai yangu unakimbilia uchaguzi mkuu ambao haukuwepo.

Mkuu wacha propaganda zako za kitoto eti mimi ni kada maarufu sana na wewe ni mwana NGO nini !.
Demokrasia siyo lazima wote waende kuchaguliwa bali hata michakato nayo demokrasia. CCM wanatumia mwanya wa uchanguzi mkuu kwa ajili ya kuweka watu wao. Demokrasia ni kwa ajili ya kukubali, kukaa na kuongea kwa ajili ya nani afae kuchaguliwa kuwa mwenyekiti, ila Ni demokrasia ya kweli ipo ndani ya CHADEMA. Inawezekana wewe ukawa Kada ndio maana upo formative kama hivyo mzee wangu
 
Is the payment system anounced recently working for now? Code number pls watu wanataka kuchangia hapa wamekosa code number
 
Demokrasia siyo lazima wote waende kuchaguliwa bali hata michakato nayo demokrasia. CCM wanatumia mwanya wa uchanguzi mkuu kwa ajili ya kuweka watu wao. Demokrasia ni kwa ajili ya kukubali, kukaa na kuongea kwa ajili ya nani afae kuchaguliwa kuwa mwenyekiti, ila Ni demokrasia ya kweli ipo ndani ya CHADEMA. Inawezekana wewe ukawa Kada ndio maana upo formative kama hivyo mzee wangu

Mkuu wangu Josh unatakakuzuga Zitto kugombea nafasi ya mwenyekiti atakuwa alitumwa na CCM ?.Hii habari ya Zitto kutumwa na CCM imeniacha hoi.
 
chadema ni chama kilichofulia na hatuwezi kuikabidhi nchi yetu tupendayo kwa kanda moja tu ya nchi hii wa kaskazini hili kamwe watanzania halipo
 
chadema ni chama kilichofulia na hatuwezi kuikabidhi nchi yetu tupendayo kwa kanda moja tu ya nchi hii wa kaskazini hili kamwe watanzania halipo
Ukiona Chama cha Upinzani kimefulia basi jua hata serikali iliyopo madarakani nayo imefulia, hivyo kutokuwa na accountability sehemu zote
 
Kwanza nilikipenda CUF nikagundua wao ni udini kwa sana alafu mawe kwa mawe, vile vile viongozi wao ni "visiki vya mpingo" vinavyorutubishwa kwa "mafao ya muafaka" yanayoletwa na "chokochoko za muungano".

Nikahamia CHADEMA (Chagaz development machine?) huko nikagundua kwamba Democracy alishaondoka baada ya kubakwa mchana kweupe na wazee wa chadema, vile vile nikagundua kwamba viongozi wa juu na wazee wa chama hiki wana DNA zinazofanana, na matumizi ya fedha ndani ya chama yanaandikwa kwa chaki nyeusi, na kutimuana ni kawaida kwenye uongozi wa juu.

Sasa nimebaki njia panda, upande moja kuna chama cha mawe, upande mwingine kuna chama cha mafisadi, na upande mwingine kuna chama cha ukabila. Kama ndo hivi basi ni bora jinamizi likujualo!
 
Back
Top Bottom