CCM: Mbio za urais, makundi vinatutesa

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797


Saturday, 26 November 2011 07:45
gamba-vip.jpg
Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama akitoa taarifa kwa waandishi wa habari, jana, juu ya maazimio yaliyotolewa kwenye mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho uliofanyika kwa siku mbili mkoani Dodoma.Kulia ni Makamu Mwenyekiti Bara Pius Msekwa Picha na Edwin Mjwahuzi

CHASEMA KUJIVUA GAMBA,VITA YA UFISADI VIKO PALEPALE

Neville Meena na Habel Chidawali, Dodoma

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kwa mara ya kwanza kimekiri hadharani kuwa mbio za Urais wa mwaka 2015 ni miongoni mwa mambo yanayokitikisa na sasa kinachukua hatua za kuwadhibiti makada wake wenye nia hiyo ili harakati zake zisikiathiri.Kadhalika, CCM kimesema dhana ya kujivua gamba kiliyoiasisi iko palepale na kwamba utekelezaji wake unaanza mara moja kwa kuwachukulia hatua wanachama wake wote wanaotuhumiwa kwa rushwa na ufisadi.

Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama aliwaambia waandishi wa habari jana Mjini Dodoma kuwa si vibaya makada wa chama hicho kuanza kufikiria urais wa 2015 lakini tatizo ni njia ambazo zinatumika katika harakati hizo.“Sisi hatuna shida na watu hao kwa kuwa ni haki yao, lakini lazima watumie njia sahihi ambazo hazitaleta shida kwa chama na tumeona iko haja ya kutengeneza mfumo mzuri wa kupata mgombea urais ambaye hatatokana na fedha isipokuwa akubalike kwa uwezo wake wa kujenga hoja, itikadi yake na kile anachokiamini,” alisema Mukama.

Mukama alikiri kuwa mbali na mbio za urais 2015, pia CCM kinateswa na siasa za makundi ambayo yamekuwa yakitumika kushambuliana, kinyume cha maadili yake.Alisema CCM kinachukua hatua za kukabiliana na makundi ambayo misingi yake hujengwa katika chaguzi za ndani ya chama, na kwamba watahakikisha hilo halitokei wakati wa uchaguzi wake unaotarajiwa kufanyika mwakani.

“Kwa maneno ambayo tuliyatumia tulisema, hii kansa ya kupangana safu inaweka mtu ambaye hata sifa wala hana habari kabisa na matatizo ya wananchi, wala haumii lakini anapanga safu… lazima tuondokane na kansa hii ili tupate viongozi wanaojali na wanaohangaika na maisha ya wavuja jasho wa nchi hii,” alisema.

Kujivua gamba
Kuhusu suala la kujivua gamba, akimaanisha kuchukua hatua dhidi ya watuhumiwa wa makosa mbalimbali ukiwemo ufisadi na rushwa, Katibu Mkuu huyo alisema kati ya maazimio 26 yaliyotolewa na NEC Aprili mwaka huu, Azimio namba 27 “linahitaji kutekelezwa haraka iwezekanavyo.”

“Dhana hiyo ya kukipatia chama chetu sura mpya ndiyo iliyopewa jina la kujivua gamba na Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa imekwishatengeneza mpango wa utekelezaji wa uamuzi huo,’’ alisema Mukama.Alisema katika kikao chake kilichomalizika juzi, NEC imeamua kuwa viongozi wa CCM wanaotuhumiwa kwa ufisadi ndani ya chama walipaswa kujipima na kujitafakari wenyewe na ikibidi wachukue hatua jambo ambalo halijatekelezwa hadi sasa.

Alisema Azimio hilo liliwalenga viongozi katika ngazi zote za chama kuanzia taifa hadi tawi na kilichokusudiwa ni kujenga utamaduni wa kusimamia maadili ya viongozi na wanachama wake.

“Takriban miezi saba baada ya Azimio hilo kupitishwa, bado hatujapata mwitikio wa kuridhisha kutoka kwa viongozi wa ngazi yoyote wa chama chetu ambao ni walengwa wa azimio,’’ alisema na kuongeza:“Bila shaka sasa wakati umefika wa chama kutekeleza ile sehemu ya pili ya azimio husika kwa kuwawajibisha wahusika, lakini utekelezaji wake hauna budi ufanyike kwa kufuata utaratibu uliowekwa ndani na kanuni za CCM za uongozi na maadili.’

’Msingi wa mpango wa kujivua gamba umejengwa katika azimio la NEC linalosema: “Viongozi wanaotuhumiwa kwa ufisadi watafakari, wajipime na kuchukua hatua wao wenyewe kwa maslahi ya chama, wasipofanya hivyo, chama kiwawajibishe bila kuchelewa.”Lakini tangu kupitishwa kwa mpango huo Aprili mwaka huu, ni kada mmoja tu, Rostam Aziz aliyechukua hatua za kujiuzulu Ubunge wa Jimbo la Igunga na Ujumbe wa NEC huku wengine wakiwa kimya.

Mukama alisema sehemu ya pili ya azimio hilo inayosema: “Wasipofanya hivyo chama kiwawajibishe bila kuchelewa,” ndiyo msingi wa NEC kurejesha suala hilo kwa Kamati Kuu na kwamba sasa litafanyika katika ngazi zote.Alisema NEC imeziagiza kamati za siasa kupitia kamati za ulinzi usalama na maadili kwa ngazi zote kuanza mara moja, mchakato wa kutekeleza azimio hilo kwa mujibu wa kanuni na taratibu za chama.

Alisema NEC iliagiza kazi hiyo kufanyika haraka bila kuchelewa na baada ya kukamilika kwa kazi hiyo, taarifa zipelekwe kwenye vikao vya kikatiba vya uamuzi kwa hatua za utekelezaji.

Alisema chama hicho kitahakikisha kwamba ajenda hiyo haitekwi na makundi yanayokinzana na kwamba lengo zima ni kuhakikisha kwamba CCM kinaongeza uwezo wa kusimamia mambo yake na Serikali zake zote.

“Lazima kifike mahali (CCM), kiwe na uwezo wa kuzisimamia na kuhakikisha kwamba Serikali zinatekeleza matakwa ya wananchi na siyo vinginevyo, ndiyo maana watu wanajiunga na vyama kwani huwa wanatarajia watapata utetezi,” alisema Mukama.

Kuhusu vurugu na migomo ya vyuo vikuu CCM kiliagiza Serikali kuchukua hatua za haraka kukabiliana na hali hiyo na kuitaka kusimamia sheria inayokataza uendeshaji wa shughuli za kisiasa katika taasisi za elimu nchini.

Kimetaka wanafunzi na watumishi wabanwe ili waendeshe shughuli hizo nje ya taasisi husika.Kuhusu suala la Nishati nchini, Mukama alisema NEC imeiagiza Serikali kuhakikisha kuwa inapunguza bei za mafuta na hasa ya taa ambayo yanatumiwa na wananchi wengi wenye kipato cha chini.

Juzi, Mawaziri Wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye, waliwashambulia kwa maneno makali wajumbe wawili wa Sekretarieti ya CCM kwamba wamekuwa wakikivuruga chama na kusababisha mgawanyiko uliopo kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakisimamia mpango wa kujivua gamba.

Lowassa aliyejiuzulu Uwaziri Mkuu, kutokana na kashfa ya Richmond ndiye aliyekuwa wa kwanza kuzungumzia suala hilo wakati wa mjadala wa hali ya siasa, pale alipowataja Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Tanzania Bara, John Chiligati kwamba wamekuwa wakitukana watu ovyo kwa fedha wanazopewa na CCM.Kwa mujibu wa taarifa hizo, Lowassa alitumia zaidi ya dakika saba kumshambulia Nape kwamba amekuwa akifanya mambo nje ya utaratibu na kwamba mwenendo huo umekuwa ukikibomoa chama badala ya kukijenga.

Sumaye alisimama na kuhoji sababu za chama hicho kunyamazia ukiukwaji wa taratibu ambao umekuwa ukifanywa na watendaji hao.
 
Mukama ana wakati mgumu sana kuliko wakati mwingine wwt katika utumishi wake!!EL hawatamvua gamba maana yeye si gamba ni ngozi ambayo ina gamba hivyo hawamuwezi kabisa,wataishia kubadilisha tungo zao na semi tata,ili kupoteza muda!labda AC anaweza kujivua gamba na si EL
 
Nadhani hii ni kisingizio tu. Kwa nini isiwe mbio za ubunge au Udiwani if that is the case?
 
Kwa wenye ufahamu huu ndio mwanzo,kwa kuwa kanuni ya kuepusha mashua ya CCM na dholuba ya Wananchi ni kujivua gamba na kubaki na watu wenye roho na nafsi ya kweli ya kuwahudumia watu na si watu kuwahudumia wao.

Kokoliko kumekucha ndio mwanzo tena taaaaaaaaarrrrrrrrrratiiiiiiiiiiiiiiiiiiibuuuuuuuuuuuuuu.
 
Hawa wazee wa CCM wamezoea kulelewa,akitokea mtu kama NAPE mwenye nia nzuri na chama,wanaanza kulia lia,NAPE GO ON ILA UTUMIE AKILI SANA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom