Ni juzi tulikuwako, kwa karamu yakufana
Ikiwa bathdei yako, Da! Pati ya kuagana
Ukanita Niko ,Niko, Ati hatuta achana
Niseme si langu fungu, haujakubali mtima
Siamini umeenda, hatutaonana tena
Yote tuliyoyatenda, hayatarudia tena
Popote tulipo kwenda, hatuwezi fika tena
Niseme si langu fungu, haujakubali mtima
Siamini hutofika, kawaida kusalimu
Kwa utani tukicheka, Dah! Hilo tabasamu
Malengo yakipangika, mbeleni ndoa muhimu
Niseme si langu fungu, haujakubali mtima
Ukapanga lake jina, la mtoto tukijaliwa
Kwa wakike Rihanna, wa kiume majaliwa
Ni mipango mingi sana, tulopanga maridhawa
Niseme si langu fungu, haujakubali mtima
Umeniacha na kidonda, kutwa kucha ninakonda
Giza nene limetanda, moyo wangu ulipenda
Pendo leo umeenda, Najua sio kwa kupenda
Ni seme si langu fungu, haujakubali mtima
Moyo wajawa uchungu, hauijui hatima
Kwaheri', Mapenzi yangu, yamebakia yatima
Nisamehe sana Mungu, nizitoapo lawama
Niseme si langu fungu, haujakubali mtima
Ukaandika wosia, nifikie mazikoni
Eti niache kulia, siwezi huo mtihani
We ukiniandikia, pendo ulilia nini?
Mama yote kanitonya, kweli tulipendana
Nenda salama pendo, sisahau abadani
Ulinifunza upendo, uliozidi uzani
Umeacha pengo, pendo, Mpaka nije kwa manani
Kwaheri' mpenzi, Tutaonana baadae