Bunge lashutumiwa kukalia hoja nyeti

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Tumaini Makene na Grace Michael

PAMOJA na mkutano wa nne wa Bunge la 10 kumalizika kwa kutimiza moja ya majukumu yake ya kikatiba ya kuisimamia serikali ambapo imeunda kamati teule kufuatilia tuhuma za ufisadi katika sakata la Bw. David Jairo, bado Bunge hilo limeendelea 'kukalia' hoja mbalimbali, zinazoonekana kuibua masuala mazito nchini, hasa zile ambazo baadhi ya wabunge wamekuwa wakiwabana viongozi wa serikali.

Mbali ya kukalia hoja hizo binafsi za wabunge, mkutano wa nne pia umeendelea kuliweka kiporo suala nyeti la mjadala wa uandikwaji wa katiba mpya nchini, ambapo suala hilo lilikuwa katika ratiba ya vikao vya mkutano huo uliomalizika mwishoni mwa juma lililopita, lakini muswada uliopaswa kuwasilishwa, uliondolewa baadaye na kamati ya uongozi, inayohusika katika kupanga ratiba za vikao vya Bunge na masuala ya kujadiliwa katika mkutano husika.

Imeelezwa na Kaimu Katibu wa Bunge, Bw. John Joel kuwa kamati hiyo iliona kuwa suala hilo ni nyeti na hivyo halikupaswa kujadiliwa katika muda mfupi wa mkutano huo wa nne ambao ulikuwa na masuala mengi ya kibajeti, hivyo wabunge waingepata muda wa kutosha kuujadili muswada huo kwa kina, ikaonekana ni vyema urudishwe kwenye kamati husika ya bunge, ili wadau mbalimbali nchini waendelee kutoa maoni yao.

Zitto na Baraza la Mawaziri

Bw. Zitto Kabwe ni Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini ambaye aliibua tuhuma nzito bungeni dhidi ya Baraza la Mawaziri ambalo alisema limekuwa likifikia maamuzi kutokana na kurubuniwa.

Bw. Zitto alitoa tuhuma hiyo kwa kujiamini na akaenda mbali zaidi kwa kusema kuwa hawezi kutafuna maneno kwa kuwa anaamini anachokisema kuwa baraza hilo ndivyo linavyofanya kazi.

Tuhuma hiyo aliziibua wakati akichangia Azimio la Serikali linalohusu kuongeza muda wa uhai wa Shirika Hodhi la Mali za Mashirika ya Umma (CHC), ambapo alipingana moja kwa moja na azimio hilo ambalo lilitaka kuongezwa muda wa miaka mitatu kwa CHC.

"Jamani tulikubaliana vingine kabisa katika Kamati na leo kilicholetwa hapa ni kitu kingine, Kamati ya Fedha na Uchumi ilijadili na kutaka shirika hili lipewe muda zaidi kutokana na majukumu yaliyo mbele yake lakini hiki kilicholetwa hapa ni kitu kingine...wabunge kataeni haya maamuzi ya baraza la mawaziri kwa kuwa yametokana na kurubuniwa na watu wenye lengo la kuua CHC kwa ajili ya maslahi yao," alisema Bw. Zitto.

Kutokana na tuhuma hizo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI),George Mkuchika aliomba mwongozo kwa spika akitaka Bw. Zitto athibitishe kauli yake hatua iliyomfanya Bi. Makinda kumpa muda wa siku saba kuthibitisha tuhuma hizo.Pamoja na Bw. Zitto kuwasilisha ushahidi wake kama alivyotakiwa, lakini mpaka sasa hakuna kilichofanyika juu ya tuhuma hizo.


Chadema na Spika Makinda

SAKATA la Chama cha Demokrasia (CHADEMA) na Spika wa Bunge Bi. Anne Makinda nalo limewekwa kiporo mpaka sasa.

CHADEMA walimshtaki Bi. Makinda katika Kamati ya Kanuni ya Bunge ambapo walilalamikia kitendo cha kuendesha Bunge kwa upendeleo hasa katika mijadala mbalimbali ambapo walidai anaipendelea serikali.

Hata hivyo Bi. Makinda alikaririwa na vyombo vya habari likiwemo Majira akisema: "Niko tayari kuhojiwa, kwa kuwa nafahamu kuwa kila jambo linalofanyika ndani ya bunge linafuata kanuni na huo ndio utaratibu hivyo mambo ya bungeni lazima yamalizikie bungeni," alisema Spika Makinda.

Katika hilo, Bi. Makinda alisema kuwa asingeruhusu kujadiliwa kwa mambo waliyohoji kwa kuwa jambo likiwa mahakamani haliwezi kujadiliwa bungeni na ikifanyika hivyo itakuwa ni kuingilia mhimili mwingine.

Hoja nyingine ambayo mtoaji wake aliambiwa na kiti awasilishe ushahidi kuthibitisha kauli yake ni ya Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, ambaye alitoa tuhuma nzito juu ya ufisadi wa matumizi mabaya kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, akimtuhumu kuwa hawezi kutekeleza kwa vitendo yale ambayo amekuwa akiyasema, hasa katika kupunguza gharama za matumizi kwa serikali.

Akichangia hotuba ya bajeti ya serikali kwa mwaka 2011/2012, Mchungaji Msigwa alimtuhumu Bw. Pinda kuwa alitumia ndege mbili za serikali kwenda Iringa kufungua barabara, ambapo pia msafara wake uliokuwa na magari yapatayo 50 alifunga barabara za Dar es Salaam-Morogoro na Iringa kwa takriban masaa matano, hivyo kuzuia shughuli za kiuchumi na kijamii.

Pia mbunge huyo alitoa tuhuma kwa serikali kuwa imekuwa ikiua watu na kuwajeruhi kwa kipigo katika maeneo mbalimbali nchini, akitolea mifano ya mauaji ya wananchi katika Mgodi wa North Mara huko Nyamongo (Tarime), mauaji ya watu watatu huko Arusha, wakati wa maandamano ya amani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na kipigo walichopewa baadhi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu Dodoma, hadi wengine wakalazwa hospitalini kwa kujeruhiwa.

Hoja hizo ya Mchungaji Msigwa ambayo ni kati ya hoja zilizoibua 'utaratibu, mwongozo, taarifa' katika mkutano ulioisha, iliilazimisha serikali kuingilia kati kupitia kwa Waziri William Lukuvi, ambaye kwa kutumia kanuni ya 64:(1) (b )ya Kanuni za Kudumu za Bunge, inayosema mbunge yeyote hatazungumzia jambo ambalo haliko kwenye mjadala, akimtaka mbunge huyo kuthibitisha kauli yake.

Hoja nyingine ya Mchungaji Msigwa ilihusiana na ukiukwaji wa sheria ya mafao ya wanasiasa wastaafu, ambapo alituhumu kuwa Spika wa Bunge la 9, Bw. Samuel Sitta anaendelea kukaa katika nyumba ya spika akidai imekodishwa kwa dola 8,000 za Marekani takriban milioni 12 kwa mwezi, akisema kitu hicho si stahili yake, suala ambalo hata hivyo lilizimwa na Spika Anna Makinda, akimzuia Waziri Mkuu Pinda asilijibu swali hilo katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo.

Mchungaji Msigwa akizungumza na Majira jana, alishikilia msimamo wake kuwa anao ushahidi wa hoja zake hizo na kuwa yuko tayari kuutoa wakati wowote akihitajiwa, akiongeza kusema kuwa sheria ya mafao ya viongozi wastaafu wa kisiasa haizungumzi juu ya spika mstaafu kupewa nyumba na serikali, isipokuwa gari moja na dereva ambavyo bunge litalazimika kuvihudumia kwa matengenezo, lita 70 za mafuta.

Kitu kingine kinachoibua mkanganyo mkubwa katika suala hilo na pengine kulazimisha taifa kuangalia mfumo mzima wa mafao ya wastaafu na stahili za watumishi wa serikali, watendaji na wanasiasa, ni kuwa sasa Bw. Sitta 'analazimika' kupata mafao hayo ya bunge, lakini pia stahili zake kama waziri, kwa maana ya gari la serikali, nyumba na kama anaishi katika nyumba yake binafsi, serikali inatakiwa kumlipa fedha za fidia ya gharama za nyumba.

Hoja nyingine ambayo nayo imeonekana kulaliwa na haijulikani itatolewa maelezo lini ni juu ya tuhuma alizotoa Mbunge wa Singida Mashariki, Bw. Tundu Lissu Mbunge wa Singida, akisema kuwa Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Elimu), Bw. Kassim Majaliwa alisema uongo bungeni, kulidanganya bunge juu ya michango wanayochangishwa wananchi.

Akijibu swali Namba 313, Bw. Majaliwa alisema kuwa michango mbalimbali wanayochangishwa wananchi nchini wamekuwa hawalazimishwi kwa serikali kutumia nguvu, bali wanashirikishwa kuiibua, kupanga na kuendesha miradi wao wenyewe, lakini Bw. Lissu aliliambia bunge kuwa kwa majibu hayo, waziri huyo alilidanganya bunge na kuwa angeweza kuthibitisha uongo huo siku hiyo hiyo kwa maandishi.

Pamoja na kupewa muda wa takribani masaa mawili awe tayari amewasilisha usahidi wake, mpaka mkutano wa bunge unamalizika hakukuwa na kauli yoyote kuonesha kuwa ushahidi ulipokelewa na kuwa tayari unafanyiwa kazi, pengine kwa uharaka ule ule wa kuombwa kuthibitisha.

Akizungumza na Majira jana, Kaimu Katibu Mkuu wa Bunge, Bw. John Joel alisema kuwa hoja za Bw. Zitto, Bw. Lema na Bw. Lissu zimeshawasilishwa kwa spika, ambapo kanuni zinamwelekeza kuzisoma na kujiridhisha nazo kwanza kabla hajaamua kuziweka wazi bungeni, ambapo iwapo mbunge husika atashindwa kuthibitisha kauli yake aliyotoa bungeni katika hoja yake hiyo, atakabiliwa na adhabu.

Lakini katika hali ambayo inaibua changamoto kwa kanuni za bunge, Bw. Joel alisema kuwa kanuni hizo 'ziko kimya' pale ambapo mbunge atafanikiwa kuthibitisha katika hoja yake 'ukweli' wa kile alichokisema bungeni, hatua zipi zitachukuliwa dhidi ya mtu huyo. Mjadala unaweza kuwa mkubwa mathalani katika hoja ya Bw. Zitto, ambaye alilituhumu Baraza la Mawaziri kuwa lilishawishiwa katika uamuzi wake, hivyo akiweza kuthibitisha bunge litaliwajibishaje baraza hilo.

"Spika hana limit (ukomo wa muda) katika kuzipitia na kuziwasilisha hoja hizo bungeni, lakini ni lazima ajiridhishe kuwa kilichowasilishwa kiko katika mfumo fulani...kama ikibainika kuwa mbunge alidanganya basi atapewa adhabu, ziko adhabu kadhaa...ndiyo maana si vizuri kukimbilia kuzipeleka bungeni kwa suala ambalo spika anakuwa hana uhakika nalo, lazima spika ajitosheleze.

Alipoulizwa juu ya hatua gani zitachukuliwa kwa upande wa pili, iwapo mbunge mto hoja ataweza kuthibitisha kauli yake, Bw. Joel alisema: "kanuni ziko kimya katika suala hilo...lakini kwa mfano kama aliyetuhumiwa ni waziri kuwa alilidanganya bunge, spika anaweza kumwambia afute kauli yake hiyo. Lakini ndiyo maana hata juzi umemsikia spika akisema tumemaliza mzunguko wa kanuni zetu, hivyo zinapaswa kuangaliwa upya."

Akizungumzia juu ya 'kesi' iliyofunguliwa na CHADEMA kwa Kamati ya Kanuni, ikihoji uadilifu wa Spika Makinda katika kusimamia masuala ya msingi ya kitaifa, hasa pale serikali inapobanwa bungeni kutoa majibu, ambapo amedaiwa kuwa amekuwa akitumia madaraka yake vibaya kuiokoa serikali, hivyo kuwakwaza wabunge kutimiza wajibu wao wa kikatiba, Bw. Joel alisema kuwa tayari imeshawasilishwa kwa kamati hiyo, ambayo itakaa wakati wowote, kupitia hoja za chama hicho.

"Spika na Naibu Spika si kwamba wanajiuzulu nafasi zao katika kamati hiyo, kinachotokea ni spika kutokuwa mwenyekiti, yaani hatakalia kiti chake cha uenyekiti wakati wa kusikiliza hoja hiyo, kwa kuwa anaweza kuhitajika kuleta maelezo ya kujitetea, hivyo spika na naibu wake wote hawatakuwemo wakati wa kikao," alisema Bw. Joel.
 
Mimi siamini Kama Tanzania tuna bunge ni pango la wezi tu, tumewatuma bungeni wakatusemee matatizo yetu wao wanakua watetezi waserekali
 
Spika hana limit (ukomo wa muda) katika kuzipitia na kuziwasilisha hoja hizo bungeni, lakini ni lazima ajiridhishe kuwa kilichowasilishwa kiko katika mfumo fulani...hapa tutasubiri mpaka tusahau!
 
Back
Top Bottom