Bunge laipiku serikali mgomo wa madaktari

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,268
33,040
headline_bullet.jpg
Madaktari waafiki kukutana nalo, Kamati yake yaanza kazi
headline_bullet.jpg
Huduma za matibabu bado mbaya Muhimbili, KCMC



Bunge(20).jpg

Bunge


Sakata la mgomo wa madaktari bado linaendelea kuinyima serikali usingizi, baada ya jana kutoa tamko la mgomo huo bungeni bila ya mwafaka kupatikana, Bunge limeamua kujitosa kusaka ufumbuzi wa suala hilo.

Bunge limeamua kuubeba msalaba huo kwa kulipeleka suala hilo katika Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii ili pande zinazohusika zikutanishwe mbele ya kamati hiyo kutafuta mwafaka.

Baada ya kusomwa taarifa hiyo ya serikali na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hadji Mponda, baadhi ya wabunge walionyesha shauku kubwa wa kutaka ijadiliwe na wabunge ili kutoa maoni yao.

Hata hata hivyo, shauku ya wabunge ilizimwa na Naibu Spika, Job Ndugai, ambaye alisema pamoja na unyeti wa suala hilo kuwa na maslahi mapana ya umma na kuweko haja ya kujadiliwa, lakini kanuni ya Bunge namba 47 ambayo iliwasilishwa hairuhusu matamko ya serikali yanayosomwa bungeni chini ya kaununi hiyo kujadiliwa na wabunge.

"Waheshimiwa wabunge nafikiri hali hii sasa inatupa angalizo huko tuendako tukipata fursa ya kupitia kanuni zetu tujua cha kufanya," alisema.
Ndugai alisema pamoja na kanuni hiyo kuzuia mjadala wa wabunge, kutokana na athari zake kwa umma anaamuru lipelekwe kwenye Kamati ya Bunge ya Ustawi wa Jamii inayoongozwa na Margareth Sitta, ambako madaktari na serikali watakutanishwa na kila mmoja kusikilizwa hoja zake ili kupata suluhu ya haki.

“Hapa tumeusikiliza upande mmoja wa serikali si busara tuakaanzaa kujadili na kutoa uamuzi kabla ya kuusikiliza upande wa madaktari ambao nao una madai yake, kwa kuwa hawawezi kuja hapa kujieleza, naamuru suala hili liende katika kamati. Ni vyema kwanza tukalijua vizuri tatizo hili kwa kusikiza pande zote kabla ya kurukia kutoa uamuzi,” alisema. Ndugai.

Ndugai alisema kuwa hata taarifa ya serikali iliyowasilishwa na Dk. Mponda hakugusia kabisa madai ya madaktari kwamba ndani ya wizara yake kuna viongozi waandamizi waliopewa majukumu ya kuisimamia wizara lakini hawana uwezo na wamejaa jeuri na dharau kwa madaktari.
Alisema ili kupanua mjadala huo hata wabunge ambao si wajumbe wa kamati hiyo wanaruhusiwa kushiriki ili watoe maoni yao.

Aliagiza kamati hiyo kulishughulikia haraka tatizo hilo na baada ya hapo taarifa yake ipelekwe kusomwa bungeni na kama itaonekana ipo haja ya wabunge wote kuijadili itatolewa nafasi.

Wakati suala hilo likiwa linashughulikiwa na kamati, alitoa wito kwa madaktari wote waliogoma kurudi kazini kuhudumia wagonjwa.

“Naungana na serikali kutoa rai madaktari warejee kazini wakati madai yao yakishughulikiwa na tunaaomba ushirikiano wao katika hili,” alisisitiza.

Awali kabla ya Ndugai kutoa mwongozo huo, baada ya serikali kumaliza kusoma taarifa yake, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika; Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe, walisimama kwa nyakati tofauti na kuomba mwongozo wa Spika wakitaka taarifa hiyo ijadiliwe bungeni kutokana na unyeti wake.

Awali, akisoma taarifa ya serikali juu ya mgomo huo, Waziri Mponda, alisema mgomo huo si halali kwa mujibu wa sheria ya ajira inayokaataza wafanyakazi wa sekta muhimu kugoma.

Akisoma taarifa hiyo ndefu mbele ya wabunge ambayo kwa asilimia kubwa inafanana na ile iliyotolewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Dk. Mponda alieleza kuwa tangu mgomo huo uanze serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kuutatua ikiwa ni pamoja na kutaka kuzungumza na madaktari, lakini hawaonyeshi dhamira ya kutafuta suluhu kwa njia ya mazungumzo.

Akieleza hatua ambazo serikali imechukua tangu Waziri Mkuu alipotoa tamko la kusitisha mgomo, Dk. Mponda, alisema serikali imeunda kamati ya kushughulikia maazimio yaliyowasilishwa kwa Waziri Mkuu ili iyachambue na kutoa maoni na mapendekezo yatakaayosaidia kumaliza mgogogro wa watumishi wa sekta ya afya.

Alisema kamati hiyo imeshaanza kazi na inaundwa na wajumbe kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na wizara yake. Wengine wanatoka Wizara ya Fedha, Chama cha Wafanyakazi wa Sekta ya Afya na Serikali Kuu (Tughe), mwakilishi wa madaktari na mwakilishi wa wauguzi.

Alisema kamati hiyo imepatiwa hadidu za rejea zinazoainisha masuala ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi na kwamba itafanyakazi kwa muda wa wiki mbili na kutoa taarifa yake kwa serikali.

“Serikali imedhamiria kwa dhati kulitatua tatizo lililopo mbele yetu, kwa mantiki hiyo, tunawasihi madaktari, wataalamu wengine wa sekta ya afya na waadau wote wa sekta hiyo kutoa maoni kwenye kamati hii ili kupata namna bora ya kutatua mgogoro uliojitokeza na kuepuka migogoro mengine kama hiyo siku zijazo,” alisema.

Aliyataja madai ya madaktari kuwa ni kuongezewa posho ya kuitwa kazini, kupatiwa nyumba za kuishi na malipo kwa ajili ya udhamini kwa madaktari wanaochukuwa maafunzo ya uzamili.

Mengine ni ongezeko la asilimia 30 la posho ya mazingira hatarishi na ongezeko la mshahara kwa daktari anayeanza kazi kutoka Sh. 957,700 hadi Sh. 3,500,000 kwa mwezi. Dk. Mponda, alisema serikali imeshaanza kushughulikia baadhi ya mambo hayo, lakini akasema mengine hayawezi kutatuliwa haraka kutoka na uwezo wa bajeti ya serikali.

KCMC HALI SIO NZURI

Wakati huo huo, hali ya utoaji huduma katika hospitali ya Rufaa ya KCMC bado si ya kuridhisha kutokana na asilimia kubwa ya madaktari kuendelea na mgomo huku wagonjwa wa nje wakiambiwa kuwa hakuna huduma kutokana na madaktari waliopo kuwa wachache na kuzidiwa na kazi.

Uchunguzi uliofanywa hospitalini humo umeonyesha kuwa hali bado si shwari kwani madaktari waliopo kwenye mafunzo ya vitendo wapatao 80, wanaendelea na mgomo huku kazi zikifanywa na madakatari bingwa ambao hawazidi 25 pamoja na madaktari wa chache ambao wanaosomea shahada za uzamili.

Jitihada za viongozi wa dini na serikali kufika hospitalini hapo kwa lengo la kufanya kikao cha dharura na madaktari walio kwenye mgomo juzi, hazikufanikiwa kwani walikataa kuhudhuria kwa madai kuwa msingi wa madai yao ni baina ya serikali na madaktari na si viongozi wa dini na madaktari.

Akizungumza na NIPASHE jana, Mwenyekiti wa kamati ya mpito kwa ajili ya kushughulikia madai ya madaktari Tanzania tawi la hospitali hiyo, Mugisha Nkoronko, alisema hawakuhudhuria kikao cha viongozi hao juzi kwa kuwa mfumo wa mazungumzo ungekuwa wa kati ya muumini na kiongozi wake wa dini.

“Tunajua Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu, Dk. Alex Malasusa, alimuita mmoja wa madaktari na kuongea naye kwa kina na kumsihi awafikishie ujumbe wenzake ili warejee kazini maana athari za mgomo zinaonekana wazi wazi, lakini msimamo wao ni kutorejea hadi serikali itakapotaka kutatua madai yetu ya msingi ambayo ni nane na yapo mezani kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,” alisema.

Kuhusu kauli ya serikali bungeni, alisema Dk. Haji Mponda ameupotosha umma kwa kutueleza kuwa hali ni shwari katika hospitali hiyo bila kujua ukweli wa mambo ilihali
huduma hakuna na kliniki zilizopo zinafanya kazi kwa kusuasua huku madaktari bingwa wakizidiwa na kazi.

“Tunaumia sana tunavyoona wananchi wetu wanateseka kwa kukosa huduma, lakini serikali ndio imesababisha haya yote kwani haitaki kwenda kwenye tatizo la msingi, badala yake wanatumia nguvu kuturudisha kazini ilihali tuna madai ya msingi, ambayo hayajajibiwa na anayepashwa kujibu ni serikali,” alisema Nkoronko.

NIPASHE ilifika hospitalini hapo kuonana na Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali hiyo, Dk. Moshi Ntabaye, ambaye kupitia Katibu muhutasi wake alisema kuanzia sasa si msemaji wa hospitali hiyo na kama waandishi wanahitaji ufafanuzi wa jambo lolote wawasiliane na Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini wa KKKT, Dk. Martin Shao, ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya hospitali hiyo. Hata hivyo, alipotafutwa Askofu Shao kupitia simu ya mkononi, alisema yupo kwenye kikao.

MADAKTARI TAYARI KUKUTANA NA WABUNGE

Kamati ya muda ya kushughulikia madai ya madaktari pamoja na jumuiya ya madaktari imeridhia kukutana na Kamati ya Huduma za Jamii ya Bunge.

Mwenyekiti wake, Dk. Ulimboka Stephen, alisema jana kuwa kwa kuwa suala hili ni la muhimu na la dharura, mkutano wa jumuiya ya madaktari utafanyika leo kabla ya kukutana na kamati ya Bunge.

Dk. Ulimboka alisema: “Hata kama tumekatazwa kufanya mikutano, lazima mkutano huo utafanyika na endapo wakituzuia basi mengi zaidi ha haya yanaweza kutokea, hivyo naiomba Serikali ituruhusu kufanya mkutano huo.”

Ulimboka aliongeza kuwa kauli ya Waziri Mponda bungeni jana ilijaa upotoshaji mkubwa kwa jamii na wabunge kwani ilikuwa inapendelea upande mmoja wa serikali.

"Si kweli kuwa huduma zinaendelea kama kawaida katika hospitali zilizotajwa mfano KCMC, taarifa za jana zinaonyesha kuwa hali ilikuwa mbaya sana kiasi cha kusitisha huduma zote kasoro huduma ya magonjwa ya ngozi, hali iliyomlazimu Askofu Mkuu wa KKKT kufika hospitalini hapo kuwasihi madaktari,” alisema na kuongeza:

“Si kweli kuwa madaktari bingwa walikataa kwenda mikoani, ukweli ni kuwa taratibu hazikufuatwa kabisa badala yake kejeli na ubabe vilitumika huku madaktari bingwa wengi kati yao wakihamishwa, suala la bima ya afya kwa watumishi wa afya hajalitolea tamko lolote, suala la uwajibishwaji wa watendaji wa Wizara ya Afya akiwemo yeye amelikwepa kabisa.”

Jana jioni wakati Bunge likiahirisha shughuli zake, Mwenyekiti wa Kamati ya Ustawi wa Jamii, Margaret Sitta, aliitisha kikao cha dharura cha kamati yake, na inaelezwa kuwa wameanza kazi ya kushughulikia mgogoro wa madaktari.

MUHIMBILI SIO SHWARI

Huduma katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) katika Kitengo cha Kliniki kwa akina mama imezidi kuzorota, hali iliyosababisha kushuka kwa maudhurio ya wagonjwa.

Ofisa Habari wa MNH, Aminieli Aligaesha, alisema mahudhurio ya wagonjwa katika kitengo cha Kliniki yameshuka kwa kiwango kikubwa kutokana jamii kutopeleka wagonjwa wao hospitalini hapo.
“Awali kabla ya mgomo wa madaktari, tulikuwa tunapokea wagonjwa zaidi ya 1,000 kwa siku, lakini kwa sasa tunapokea wagonjwa 250 tu kwa siku,” alisema Aligaesha.


Imeandikwa na Abdallah Bawazir, Dodoma; Salome Kitomari, Moshi na Gwamaka Alipipi, Dar.




CHANZO: NIPASHE
 
hii inadhilisha kwamba mhimili mkuu wa nchi ambao ni serikal imeshndwa kutatua mgomo huo,na ni aibu sana na inatia uchungu mno,utafikiri hatna serkal,
 
Mapambano bado yanaendelea,mpaka kieleweke
Pole kwa wote walioumia na mapambano haya
 
Nimeona pale moi pamefungwa kabisa, ili kutimiza uteklezaji wa ilani ya ccm 2010-15.
 
1 Reactions
Reply
Back
Top Bottom