Basi latekwa, abiria waporwa

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
WATU saba wamejeruhiwa baada ya basi walilokuwa wakisafiria kutekwa na abiria kuporwa vitu mbalimbali na majambazi.

Kamanda wa Polisi mkoani Tabora, Liberatus Barlow, alisema tukio hilo limetokea juzi saa saba usiku kati ya eneo la Mambali na Igombe mpakani mwa Nzega na Manispaa ya Tabora.

Alisema katika tukio hilo, watu hao walipanga mawe barabarani kwenye barabara iendayo Tabora kutokea Nzega na kulizuia basi la Sabena lililokuwa likitokea Dar es Salaam kwenda Tabora.

Dereva wa basi hilo lenye namba za usajili T535 AXC aliyejulikana kwa jina la Salum Ally, alipigwa risasi sehemu za makalio yake na kujeruhiwa.

Mbali ya dereva huyo, watu wengine pia walijeruhiwa na kulazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Tabora, ya Kitete, ingawa wengine kwa kupatwa na mshtuko.

Waliojeruhiwa ni Fatma Athuman (28), Johari Yona (28), Masaga Mayunga (24), Shaban Mrisho (29), Shukuru Kidika (20) na Jackson Peter.

Kamanda Barlow alisema simu 20 ziliporwa na watu hao pamoja na mali zingine ambazo thamani yake haijajulikana, na hadi sasa, hakuna mtu anayeshikiliwa wakati Polisi ikiendesha msako kuwatafuta watu hao waliokimbia baada ya tukio.

Naye Grace Chilongola kutoka Mwanza, anaripoti kuwa wananchi wamewaua watu wawili kwa kuwapiga mawe na kisha kuichoma moto miili yao kwa tuhuma za ujambazi.

Watu hao ambao ni wanaume wawili wanaokadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 20 na 25,
wanatuhumiwa kufanya ujambazi katika Kijiji cha Igombe, Wilaya ya Ilemela jijini Mwanza.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Simon Sirro aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi saa 9 alasiri na miili ya watu hao imehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa ya Sekou Toure kwa uchunguzi zaidi.

Alisema polisi inaendelea na uchunguzi kubaini ukweli wa mauaji hayo ambapo uchunguzi wa awali hauoneshi uhakika wa watu hao kuwa majambazi kutokana na kutokamatwa na kitu chochote.

“Haijathibitika kama walikuwa majambazi kwa sababu hawakukutwa na kitu, hivyo Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo,” alisema Kamanda Sirro.

Alisema dada wa marehemu amefika kutambua maiti ya ndugu zao, lakini majina yao hayajafika polisi na kwamba ni wenyeji wa Mkoa wa Mara.

Katika tukio jingine, abiria aliyekuwa akisafiri na kivuko cha mv Orion kinachofanya safari zake kati ya Kamanga, Sengerema na jijini Mwanza amejitosa katika ziwa Victoria na kuhofiwa kufa maji.

Sirro alisema abiria huyo ambaye ni mwanamume alipanda kivuko saa 11.30 jioni akitokea Kamanga kuja jijini Mwanza.

Haikufahamika mara moja sababu zilizomfanya ajitose majini.

Hata hivyo mfuko wake wa rambo aliouacha ulipopekuliwa, ulikuwa na jina la Masanja Elias (23) mhitimu wa Chuo cha Ualimu Dodoma.

Alisema Polisi kwa kushirikiana na wavuvi wanaendelea kuusaka mwili wake.
 
  1. Hivi saa saba usiku basi la abiria linaruhusiwa kutembea?
  2. Kwa nini matukio haya yasikomeshwe kabisa? Au hadi siku atekwe mama Salma ndo wahusika watapata mbinu mpya ya kudhibiti haya matukio!
 
Back
Top Bottom