BARUA MUHIMU: Kwa mpenzi Paranoid Young Man

Asha Abdala

JF-Expert Member
Mar 21, 2007
1,130
44
Kwa mpenzi Paranoid Young Man Fisadi Papa Rostam Aziz

Salaam

Dhumuni la waraka huu ni kutaka kujua hali yako baada ya shoo ya mchezo wa kuigiza uliyoifanya pale Kempinsiki. Kwa kweli nakupungeza kwa kuwa bingwa wa mipasho, unafaa kuwepo kwenye kikosi changu cha mipasho. Baada ya kutuliza kijiba cha roho tembelea hapa: http://ashawazenj.blogspot.com tuendeleze mipasho.

Sasa mpenzi, katika mipasho yako ya leo mbona umeshindwa kutenganisha public issues na private matters? Maana tuhuma dhidi ya ufisadi wako alizotoa swahiba na hasimu wako Mengi zilihusu wewe kuiba mali za umma kupitia Kagoda, Dowans nk!. Zilikuwa ni public interest allegation, wewe katika mipasho yako umetueleza weweeeee masuala private ya mikopo ya Mengi na staili zake za uandeshaji wa biashara.

Halafu Mpenzi, hivi mtu aliyefanya proof reading ya tamko lako hakusoma vizuri? Naona tuhuma za mkopo wa Mengi ulizotoa kuhusu kampuni yake ya Anche Mwedu dhidi ya NBC zilihusu mkopo wa bilioni 5 mwaka 1996. Halafu mwenyewe naona ukaongezea mipasho wewe na kuuita kuwa sasa ni bilioni 28, na ukasema kwamba hizi ndio zimeua NBC na zingejenga shule kibao. Hivi hao NBC wakisema ukweli kuwa hawamdai Mengi bilioni 28 utaweka wapi sura yako? Halafu Mpenzi, kwa maelezo yako inaonyesha kuwa deni la Mengi lilikuwa bilioni 5, je fedha hizo zingetosha kuifilisi NBC na kufanya iuezwe bei chee? Basi si ungetueleza ukweli nini hasa kimeua NBC maana inaelekea mpenzi wewe unajua siri za ndani. Hivi ilikuwaji fisadi mwenzio Mkapa akauza bei chee ile benki? Naona mtindo wako ndio ule ule wa gazeti la Uhuru, ulisoma shule moja na mhariri wake nini, maana naona juzi aliandika kwamba Mbowe alifilisi NSSF kwa kudaiwa bilioni 58, lakini ndani ya habari yenyewe akaandika kwamba alikopa milioni 7 tu, na kwamba huyo mhariri wa uhuru mwenyewe akaongezea maneno yake kuwa sasa zimefikia milioni 200 kwa mahesabu yake mwenyewe ya riba. Naona na wewe mpenzi ndio umefanya propagaganda hizo hizo! Hiyo bilioni 58, ilielezwa wazi kuwa NSSF ilikopesha wengine kabisa sio Mbowe; labda mpenzi na wewe uteueleze mafisadi wengine wenye mabilioni mengi ya NBC. Jamani mpenzi sema basi.

Halafu mpenzi, umeeleza kuwa Mengi alipewa fedha nyingi za CIS. Ukataja kidogo, ukasema ni fedha za kigeni, zikigeuzwa kuwa za kibongo na kuwekewa riba zinakuwa mabilioni. Sasa mpenzi, uliniahidi kuwa leo ungemwaga data. Sasa data gain hizo umeshindwa kusema kiasi hicho cha fedha? Au umetaja fedha za kigeni na kuhitimisha kuwa ni mabilioni ili waliokusikiliza wafikiri wenyewe kuwa ni mabilioni mengi? Huoni kwamba wajanja watakuona kuwa wewe ni mwongo mwongo? Mbele kidogo ukakiri mwenyewe kuwa hasimu wako ameshalipa hayo madeni yake ya CIS kwa barua yake, halafu unasema barua ni ya kughushi. Sasa mpenzi, huoni kama hapa unajitafutia kesi? Mbunge unajua mtu ameghushi, ambalo ni kosa la jinai, umemuacha miaka yote hiyo mpaka baada ya kukuumbua nawe ndio umeamua kumuumbua? Halafu kuthibitisha huo uzushi wako mpenzi unataka ukaguzi huru, hivi unajua nyaraka za fedha zinakaa makabatini kwa miaka mingapi? Unataka ukaguzi wa nyaraka za miaka ya 80 kwa kuwa unajua hazipo? Hebu tueleze ukweli, ni kwa vipi umewaza kuwa hakulipa na barua ni ya kughushi? Au kwa sababu Mengi amesema mwenzako Manji na mafisadi papa wengine wanadaiwa mabilioni ya CIS? Kwanini hujajibu kama fedha hizo za CIS wamelipa au la badala yake unageuza mjadala?

Mpenzi, wewe inalekea na wewe una wivu na uwekezaji wa NICO eeehh. Sasa unadhani walipa kodi wa Tanzania maamuzi ya NICO kuwekeza yanawahusu nini? Mi naona wao yanawahusu zaidi masuala ya EPA/BOT, Dowans nk kwa hiyo sitashangaa kama wakikuzodoa. Au unataka kumchonganisha Bwana Mengi na hao wanahisa 22,000 wa NICO? Maana wamesambaa nchi nzima kama wale wana upatu wa DECI. Lakini mpenzi wanahisa wa NICO huwa wanamikutano yao, na wanajua uwekezaji wa NICO uko zaidi ya hicho kiwanda cha kina Mengi; na wanagawiwa faida kutokana na fedha zao. Sasa watakuamini vipi kwamba wamepata hasara kwa sababu tu ya uwekezaji wa bilioni 2 kati ya mabilioni mengi ambayo NICO imewekeza? Mi naona Mpenzi, hao watu watajitokeza na kukwambia kwamba Mengi hakuamua mwenyewe bali Bodi ndio iliona iwekeze fedha huko.

Halafu Mpenzi, naona umefungua makabati na kukumbusha suala la TanPack, kwamba huo mkopo wa milioni 600 ndio umesababisha kampuni ifilisiwe. Sasa mpenzi huoni kama hapa watu watakuona ni mwongo kabisa? Mpenzi hivi ulikosa kabisa ufisadi wa Mengi unaofanana na tuhuma alizotoa juu yako na Dowans, Kagoda nk? Sasa kwanini usingesubiri kwamba nikueleze mambo ya ndani? Maana hivi sasa watu wataona unatapa tapa kwa kuwa umeshikwa pabaya!

Mpenzi nimekutazama, naona baada ya maneno hayo ukaelekea kuishiwa mipasho. Ukaanza kuzunguzunguka.

Ghafla ukahamia kwenye mambo private, kwamba oooh huyo bwana Mengi hana maadili ya biashara. Sijui kama wanatanzania wataona kwamba hayo nayo yana public interest. Maana wewe umetuhimiwa kwa maadili ya umma!. Halafu naona umekumbusha tena kwamba wewe una rekodi ya maadili ya biashara toka kwenye familia toka mwaka 1852, Aahhh Mpenzi, hujaacha tu majigambo. Mi nilifikiri hili ulilimaliza wakati wa Mtikila. Mwaka 1852 Mpenzi familia yako ilikuwa inafanya biashara gani yenye maadili vile, maana nakumbuka wakati huo kulikuwa na biashara ya kishenzi ya utumwa na kupora mali? Je, hayo ndio maadili ya biashara uliyojifunza mpenzi. Halafu mbona hayo maadili hayajafanya baba Mkwe awe tajiri, manake naona alikuacha kawaida tu. Mi nakumbuka utajiri wako mpenzi uliupata kupitia kufilisi kile kiwanda cha ngozi, na baadaye kwenye makampuni kama Caspian kupitia tenda mbovu mbovu za ujenzi. Halafu ukapata fedha zaidi kwenye masuala ya CIS, EPA nk. Lakini najua hao mabwege watanzania hawayajua hayo, maana niliona wale waandishi pale walikuwa wanatumbua macho hawakuulizi maswali ya maana!

Halafu mpenzi, naona umetaja orodha ndefu ya makampuni binafsi ambayo Mengi aliamua kuyafunga kama Kalamu, Chemical, Body Care, Medicare. Lakini yote hayajafika hata saba. Lakini mbona mi nafahamu Mpenzi Mengi ana makampuni mengine zaidi ya 20 ambayo yanafanya kazi? Sasa huyu mwenzio akijitokeza na kuyataja hayo kueleza ufanisi wake wa biashara utasemaje? Halafu kama makampuni ameyafunga kwa maamuzi yake kwa sababu za kibiashara mbona sio issue? Mimi nilitarajia kwa kila kampuni mpenzi ungeeleza ufisadi aliofanya mpaka akafunga. Hapo ndio naaona mpenzi ungeeleweka zaidi. Lakini mi najua mpenzi wewe kuna makampuni 50 uliyowahi kuyafungua, mengine hewa na mengine ukayafunga. Ila mi nakupongeza mpenzi kwa ujanja wako, maana wewe sikuwezi- huweki jina lako; umenunua Habari Corporation hukuweka jina lako, umeshiriki kwenye Dowans hukuweka jina lako, Kuna Mirambo, hakuna jina lako; kwenye Kagoda ukaweka wafanyakazi wako. We mpenzi sikuwezi, una akili sana. Hivi kwanini huyo Mengi anaweka jina lake badala ya kuweka majina ya paka wake?

Yaani mpenzi umenivunja mbavu kwamba mwenzio Mengi anakwepa kodi; hivi kwanini siku zote hujawaambia TRA? Manake kule bungeni najua huwa wabunge wenzio wanachangia kuhusu ukata wa taifa. Hakikisha huyo jamaa analipa jamani. Halafu mpenzi hongera, siku hizi naona umeajiri wafanyakazi 6,000 na wote unawalipa vizuri. Hebu niambie jamani hao wafanyakazi 6,000 wako kwenye makampuni yapi na yapi na viwango vya mishahara yao? Wala usinitajie majina maana mi sitaki kujua kama hao ni wale watumishi wako kama wakina Ballille na vigogo wengine wa serikali walioko kwenye pay roll yako au ni wafanyakazi wa Vodacom. Nataka nijue mpenzi maana nasikia siku hizi mpaka baadhi ya viongozi wa upinzani umewapa ajira. Mi nakusifu tu mpenzi unavyojua kutengeneza mitandao!


Mmmhh Sweeet. Ndio nini hivyo kumshushua mwenzio kuhusu akaunti za nje. Umemwabia kabisa kuwa na yeye anayo yake. L:akini mpenzi, mbona mwenzio alikuwa anazungumzia kutoroshea fedha nje? Na si akaunti za kawaida. Halafu naona mpenzi hapo umekiri kiaina kuwa unazo akaunti nje. Sasa mbona siku zote hujaniambia mpenzi. Halafu hapo naona umefanya two wrong makes it right!

Mpenzi umetaja magazeti. Naona hayo mengine uliyoyataja yako siko zote. Naona mapya hapo ni Sema Usike, Taifa Tanzania na Acha Umbeya. Lakini Mpenzi haya si yalianzishwa baada ya wewe, karamagi na subash kufungua rundo la magazeti? Sijua taifa Tanzania, sauti huru halafu mkayaibua yale ya zamani ya Nyundo, Tazama na msururu mrefu kweli mkaanza kumsulubu Mangi wa watu. Mangi akalalamika weeeeeeeeeeee lakini si MCT, Maelezo wala Wizara ya habari waliosikia kilio chake. Na yaye ndio akajibu mapigo. Sikujua kama hayo magazeti yana kukura hivyo. Si uyapuuze tu.

Umemuita mzee wa watu kuwa anachanganyikiwa. Kwamba ni paranoid old man. Lakini mpenzi mi naona ungeweza kusema vizuri zaidi maana hapa nahofia watu watukuona zaidi kuwa wewe ndio paranoid young man. Hukupaswa kabisa mpenzi kuonyesha kwamba kuitwa papa kumekuuma. Kwani hata kule Roma si kuna papa wa kanisa lao hao wakristu jamani? Mi naona haya matuhuma kila siku yatakuchanganya akili mpenzi, mi nakushauri uyapuuze tu kama rafiki yako Mkapa.

Heee, mpenzi naona unamtisha JK kuwa Mengi anavuruga serikali yake. Unataka sasa wambane eeeh. Lakini Mpenzi, mama alisema kwamba haya matuhuma ya EPA, TANGOLD, Deep Green nk haya ndio yanamvuruga Kikwete. Na kadiri yanavyoendelea haya, yanazidi kuivuruga serikali. Dawa ni huyo Rais achukue hatua. Lakini sasa Mengi naona amekosea kukutaja wewe wakati wewe toka mwaka 1995 ndio ulikuwa unashirikiana na Lowassa kupanga safu za mtandao kuanzia polisi, usalama, jeshi, mahakama. Na naona mwaka 2005 umefanikiwa kuweka na wabunge na swahiba wako Kikwete kuwa Rais; sasa huyo Mengi anadhani wewe utaguswa? Ndio maana naona umepeleka hayo makabrasha ya tuhuma zake kwa vyombo vya dola. Kama uliweza kuifanya TAKUKURU ikaisafisha RICHMOND naona sasa utafanya hayo mavyombo yatoke na ushahidi kuwa Mengi ni fisadi nyangumi.

Ndio maana mi nakupenda mpenzi, una nguvu kama za Simba. Huyo hana Moral authority ya kukupasha, lakini mpenzi wewe ulikuwa na moral authority ya kumpasha? Halafu mbona hukuyasema haya Dr Slaa alipokutaja kwenye Orodha ya Mafisadi? Ulimuogopa kutokana na Moral Authority yake au Mengi amekutisha? Hebu niambie ukweli basi mpenzi maana mi siku zote huwa nakutunzia siri zako.


Nakupenda, lakini jua nampenda Mungu zaidi yako.

Asha

PS. Mwambie Al Adawi kuwa yule dada Mkwe wa Oman ameshampa ule mzigo yule jamaa yetu. Tumeifungulia TANESCO kesi lakini baada ya hapo mambo ya Dowans yapo pale pale. Nitampa taarifa pia kuwa umeshaanza kumshughulikia Mengi tena.

 
Asha nakupa big up X1000. Ehee hebu niambia mwenzetu ulisomea wapi uanshishi mahiri namna hiyo tuwapeleke na wenzio wakajifunze kuchambua mambo. Laiti upeo wa watanzania kuchambua mambo ungekuwa hivi mbona raha
 
Nasifu uchambuzi mzuri dhidi ya hoja zilizotolewa na RA. Ingekuwa vizuri kama angepata forum ya kuzipata na kuweza kujibu.
 
kweli asha unajua kuandika, una upeo mkubwa wa kuchanganua mambo.

wote hawa ni wezi (rotam na mengi)
 
Back
Top Bottom