Barua kwa baba wa taifa mwl jk nyerere

Mtimti

JF-Expert Member
Feb 23, 2008
942
644
Kwako Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, Salaaam!
Ni imani yetu kuwa kwa mapenzi ya Mungu, huko uliko utakuwa umetumisi wanao
tunaoishi tukijivunia Utanzania wetu kwa misingi uliyotujengea na waasisi
wenzako tangu enzi hizo za kuusaka uhuru na hatimaye kuupata toka kwa
wakoloni ambapo amani na utulivu vimeendelea kutawala.

Baba! Katika miaka hii tisa tangu Mola akutangulize huko kunako makazi ya
kudumu, Tanzania yetu hii inashuhudia mambo mengi ambayo leo hii, kama
ungetokea muujiza, ukashuhudia kila kinachojiri, naamini ungeshangaa. Ndiyo.

Kuna madhila tele na maraha kidogo katika nchi yetu hii iliyojengwa nawe kwa
misingi ya ujamaa na kuimarishwa na mizizi ya haki na usawa kwa wote.
Nitakueleza machache tu.

Baba! Enzi zako, kila mtoto wa taifa hili alikuwa na haki ya kuipata elimu
kadri ya uwezo wake kitaaluma.

Watoto wengi wa masikini toka kiijiji cha Liparamba kule Ruvuma, wale wa
Matombo Morogoro, Kashozi Bukoba, Mchambawima Zanzibar, Kasulu Kigoma, Samvu
la Chole mkoani Pwani, Chiwata wilayani Masasi Mtwara na kwingineko kwingi
nchini walipata fursa ya kujiendeleza kadri ya uwezo wao darasani.

Leo hii Baba, licha ya serikali kufanya jitihada kadhaa za kuimarisha elimu
ya msingi na sasa sekondari, bado kuna mambo mengi yanayomuweka kando mtoto
wa \’asiye nacho\’. Shule za Serikali hazina miundombinu ya kutosha. Walimu
ambao wamezingirwa na umasikini wa kutupwa wanazikimbia shule hizi.

Baba, mwisho wa yote, ni watoto wengi wa matajiri ndio ambao wataipata
mikopo hii toka Bodi ya Mikopo maana ni wao ambao husoma shule zenye
mazingira mazuri kutokana na ada ya zaidi ya milioni ambayo wazazi wao
huanza kuwalipia tangu wakiwa shule ya msingi.

Wale wa shule za serikali ambao hutumia vipaji vyao kujisomea katika baadhi
ya masomo ambayo hayana walimu kabisa katika shule nyingi huishia kushinda
madaraja ya chini na kutupwa kando huku wale wasiohitaji kukopeshwa ndio
hukopeshwa!

Baba! Hivi sasa kuna bomoa bomoa ambayo imewaumiza watu wengi hasa wanyonge
waliojenga maeneo yasiyoruhusiwa kutokana na umaskini.

Halafu kabla hatujasahau baba?wale majirani zako wa kijiji cha Butiama
Msasani, hivi sasa wako mguu nje, mguu ndani?yasemekana vijumba vyao mbavu
za mbwa vinachafua mandhari?na bomoa bomoa imepamba moto mji mzima?kwani
walalahoi wana la kusema baba?

Baba! Viwanda vingi ulivyovianzisha havipo tena. Sunguratex ni hadithi, Bora
Shoes ilishabinafsishwa, Mwatex na Kiltex zimefuata nyayo za Sungura,
Kiwanda cha Kusindika Nyama Kawe kimeuzwa na nasikia aliyekinunua anataka
kujenga hoteli (sina uhakika), Kiwanda cha Kusindika Mvinyo Dodoma hakipo
tena, mashamba mengi makubwa ya serikali yamebinafsishwa kwa bei zilizozua
mijadala, Shirika la Reli (TRC) linayumba na mambo mengine kadha wa kadha.

Baba! Kilimo na wakulima ni kama wamesahaulika sasa. Japo kuna mipango mingi
mizuri ya kimaandishi.

Baba! Aibu ya mwaka kuhusiana na biashara zinazowagusa wakulima ni kuwa hivi
sasa, wakati machungwa na matunda mengine yakioza kwa wakulima wa Lushoto,
Morogoro, Geita na Kimanzichana mkoani Pwani, nchi yetu sasa inaruhusu
kuingizwa nchini kwa matunda hayo yanayouzwa kwa bei ya juu mno kwenye
\’Super Markets\’ kadhaa. Baba! Cha kusikitisha zaidi ni kwamba hata juisi
nyingi za maembe na matunda mengine zilizo kwenye maduka yetu hutoka nje
kwenye mataifa ambayo kijiografia, hayana hali bora kulinganisha na sisi.

Baba! Madini uliyotuachia bado hayajawa na msaada mkubwa sana kwetu. Kuna
malalamiko kibao juu ya baadhi ya mikataba yenye utata.

Baba! Rushwa bado ni tatizo. Ukija leo utashangaa kuona baadhi ya watu
wakimiliki mali zisizoendana na vipato vyao. Semina, warsha, mikutano, vikao
na makongamano kadhaa ya kupambana na mdudu huyo uliyemuita \’adui wa haki\’
zimekuwa zikifanyika mara kwa mara.

Baba! Zile nyumba za serikali ambazo nyingi zilijengwa wakati ule wa utawala
wako, hivi sasa zimeuzwa.

Lakini namna ya uuzwaji wake, na bei zake, na wanaouziwa bado ni utata
mkubwa machoni mwa walipa kodi wengi.

Baba! Ujambazi nao umekithiri. Enzi zako ulikuwepo, lakini si kwa kiwango
cha sasa ambapo hata mchana kweupe, mijamaa hiyo huweza kuvamia kokote kule,
kuua na kupora mali na roho za watu.

Baba! Umeme bado ni tatizo. Unauzwa bei mbaya, unatolewa kwa mgao na cha
kushangaza, hadi hii leo ambapo tuko katika karne ya 21, bado kuna urasimu
mkubwa wa kuupata kwa anayehitaji kuunganishiwa.

baba,suala hili la umeme limechangiwa kwa kiasi kikubwa na viongozi wetu ambao waliingia mikataba mibovu yenye harufu ya RUSHWA wakiongozwa na yule yule kijana uliyemkataa mwaka 1995 kwa kigezo kuwa ni mla rushwa (Edward Lowasa) pamoja na rafiki yake aitwaye Rostam aziz.

baba,kabla sijasahau kuhusu chama chako ulichokiunda na kukinadi kuwa ni cha WAKULIMA na WAFANYAKAZI sasa hivi kimekuwa cha MATAJIRI na MAFISADI,kwani kinaipeleka nchi pabaya,hakuna wa kumkemea mwenzie,kijana wako jakaya anaonesha ameshindwa kuongoza,kwani sasa kuna kundi lililoibuka kwenye chama linaitwa MTANDAO,ni kundi la hatari na linaloendesha siasa za kibabe ndani ya chama na lipo tayarui hata kuyagharimu maisha ya mtu ambaye watamuona anatoa upinzani kwao.

Baba! Tatizo la maji bado ni kitendawili kisichokuwa na majibu, kwani hata
yale mabomba uliyohangaika kuyainganisha katika maeneo mbalimbali nchini
sasa yameota kutu na imekuwa ndoto kwa watu hao kupata maji safi na salama.

Baba! Siwezi kukusimulia yote yaliyotokea katika kaipindi cha miaka tisa
uliyotuacha,lakini kwa kweli matumaini ya mtanzania yameshuka sana,gharama za maisha zimepanda sana na kwa kifupi hatuna mtetezi tena kwani hata kingunge na rashidi wamekuwa mafisadi.

Baba! Nakutakia mapumziko mema. Nasi tutafuata huko katika siku, saa na
nukta tusiyoifahamu.
Wasalaaam!
Ni sisi wanao uliotuacha Tanzania.
 
Back
Top Bottom