diana chumbikino
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 428
- 368
BALOZI wa Palestina nchini Tanzania, Hamdi Mansour AbuAli amempongeza Rais John Magufuli na serikali yake kwa kuimarisha uchumi wa nchi yake. Amesema, Rais Magufuli anasimamia dhamira yake ya kuimarisha uchumi na kutekeleza miradi ya maendeleo hasa katika karne hii ya maendeleo.
Mwakilishi huyo wa Palestina akimtambua Rais Magufuli kwa jina la ‘bulldozer’, amesema kiongozi huyo wa nchini amefanikiwa kuielekeza Tanzania kwenye uchumi wa kipato cha kati kwa kuainisha sera na mazingira ya biashara.
Akitoa pongezi hizo kwa Rais Magufuli, balozi huyo amesisitiza kuwa Palestina itaendelea kuunga mkono mpango wa maendeleo wa taifa 2025, unaolenga kuwezesha uchumi thabiti na wenye ushindani kwa kuhamasisha uwekezaji. “Sote tunaona juhudi za Rais John Pombe Joseph Magufuli katika kukuza maendeleo ya kiuchumi, na kwa kasi hii Tanzania itakuwa moja ya nchi zenye uchumi mkubwa na maendeleo barani Afrika. Serikali yangu inaungana mkono na serikali ya Tanzania ili kuleta maendeleo ya kiuchumi nchini,” amesema.
Balozi Abu Ali amesisitiza, kwamba taifa lake (Palestina) imeendelea katika nyanja ya teknolojia na uvumbuzi, hususani katika sekta za afya, kilimo na ujenzi hivyo kuweza kuwa na ushirikiano kati ya nchi hizi mbili. Ameeleza, tayari kuna kampuni tatu za dawa kutoka Palestina ambazo zimeonesha nia ya kuanzisha ubia na kampuni za ndani na kwamba, Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa wa Palestina (PICA) nchini, linaendelea na utafiti ili kuvumbua maeneo tofauti ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.
“Kwa maagizo kutoka kwa Rais wa Palestina, Mahmoud Abbas na Waziri wa Mambo ya nje na wahamiaji, Dk Riyad Malki, Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Palestina (PICA) linafanya utafiti wa maeneo tofauti ya ushirikiano kati ya nchi zetu mbili. “Lengo ni kuleta maendeleo kwa watu wetu na nchi zetu mbili na hivyo basi, kuboresha uhusiano wetu wa kihistoria ambao ulianza tangu zama za Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na kiongozi wetu Mohammed Yasser Arafat,” amesema.
Pia Balozi AbuAli amepongeza hatua ya Rais Magufuli na serikali yake kwa msimamo wake wa kuendelea kuunga mkono na kushikamana na Palestina. Pia amepongeza hatua ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kupitisha Lugha ya Kiswahili kuwa lugha ya nne rasmi katika jumuiya hiyo.
SOURCE: MWANAHALISI ONLINE