Bado mbumbumbu wengi shule za sekondari za kata

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,082
0001baskeli.jpg

Fredy Azzah
DISEMBA mwaka jana, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, ilitangaza matokeo ya mtihani wa darasa la saba ikieleza kuwa wanafunzi 9,736 wamefutiwa matokeo kutokana na kugundulika kufanya udanganyifu.

Kutokana na hali hiyo, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo akatoa tamko la wanafunzi waliofaulu kupimwa uwezo wao wa kusoma, kuandika na kuhesabu mara baada ya kuripoti katika shule walizopangiwa

Mwananchi imefanya ziara katika baadhi ya shule hasa zile za kata kuangalia namna zoezi hilo lilivyoendeshwa na matokeo yake.

Moja ya shule zilizotembelewa ni Shule ya Sekondari Maneromango ya wilayani Kisarawe, mkoa wa Pwani, ambayo baada ya wanafunzi waliochaguiwa kujiunga shuleni hapo kufanyiwa mtihani huo, wengi wao wamebainika kuwa na uwezo usioridhisha katika kusoma, kuandika na kuhesabu.

Mwalimu wa Taaluma shuleni hapo Jonas Buheruko, anasema hali ni mbaya na siyo kwa mwaka huu bali huo ndio uhalisia kwa miaka mingi.

Akichanganua vigezo walivyotumia kuwapima watoto hao, anasema vilikuwa vimegawanyika katika sehemu kuu tatu ambazo ni kusoma, kuandika na kuhesabu.

A nasema sehemu ya kwanza ilikuwa ni kupima uwezo wa kusoma, ambapo mwanafunzi alitakiwa kusoma kifungu cha maneno pamoja na sentensi fupifupi. Kipengele cha pili kilikuwa ni kuandika kilichojumuisha uandishi wa imla na kuandika hadithi fupifupi.

“Kipimo cha mwisho kilikuwa ni kuhesabu ambacho pia kiligawanyika katika makundi mawili ambayo ni kuhesabu vifungu vya namba pamoja na kuviandika,’’anaongeza
Kuhusu zoezi la hesabu, anasema wanafunzi walipimwa hesabu za kujumlisha, kutoa, kuzidisha na kugawanya, huku kiwango cha ufaulu kikiwa ni kupata alama nane chini ya kumi.

Katika zoezi la kuandika anasema walitakiwa kufaulu maneno 20 kati ya 25 ya imla.
“Katika vipengele vyote, ni wanafunzi watatu tu ndiyo waliweza kufaulu kwa alama sitahili katika darasa lenye zaidi ya watoto 100. Wengine wanasoma na kuhesabu kwa kusitasita kama watoto wa darasa la kwanza,” anasema.

Hata hivyo, matokeo haya hayamshangazi mwalimu Buheruko kwa sababu miongoni mwa wanafunzi waliochaguliwa shuleni hapo, anasema wapo waliopata alama za chini katika mtihani wa taifa wa darasa la saba.Anaeleza kuwa mtihani ulikuwa na alama 250, lakini wao walipata chini ya 100.

Shule nyingine ni Kibuta pia ya Kisarawe ambayo Mkuu wa shule hiyo, Musa Juma anayesema hali siyo mbaya shuleni kwake, ingawa wamegundua wanafunzi wengi wanasoma maandishi kwa kusitasita.

Hata hivyo, anasema inawezekana tamko la Serikali limewatisha wengine wasiojua kusoma na kuandika kuripoti shuleni, kwani kati ya wanafunzi 149 waliopangiwa kwenye shule hiyo, walioripiti ni 96 pekee.

“Inawezekana kabisa kuwa kati ya hawa 53 ambao hawajaripoti wapo ambao hawajui kusoma na kuandika. Kwa hiyo naweza kusema hawa wa mwaka huu wamejichuja wenyewe kabla ya kuja shuleni, kwa sababu miaka mingine huwa tunapata wasiojua kusoma na kuandika,” anaeleza.

Kwa upande wa Shule ya Sekondari Tongoni iliyopo mkoani Tanga, Mkuu wa shule hiyo Ally Bendera, anasema bado wanafunzi wengi wanasoma na kuhesabu mithili ya wanafunzi wa darasa la kwanza.

Anasema kwa jumla wamembaini mwanafunzi mmoja asiyejua kusoma na kuandika kabisa,huku wakifikisha taarifa zake kwa Ofisa Elimu Sekondari kwa hatua zaidi.

“Kati ya wote waliopangiwa kuja hapa, naweza kusema asilimia 20 wapo vizuri, asilimia 50 matokeo yao yalikuwa wastani na asilimia 30 ni tatizo kabisa,” anasema Bendera.

Anasema kuwa, wanafunzi wengi waliopangiwa shule hiyo walifaulu kwa kiwango cha chini ya alama 100 kwenye masomo yao yote na hakuna aliyezidi 125 ya alama 250 zinazotakiwa.

Ofisa Elimu Taaluma wa Wilaya ya Kisarawe, Gidion Shangwe, anasema kwa jumla baada ya jaribio hilo, hali haikuwa mbaya kwa wanafunzi wa wilaya yake.

Kuhusu idadi kubwa ya wanafunzi kufeli katika shule ya Maneromango, anasema: “Pale Maneromango kulikuwa na tatizo kidogo, lengo lilikuwa ni kumpima mtoto, tulichotaka ni kusoma na kuandika. Maneromango waliwapa mitihani kabisa ya hesabu na vitu vingine kwa hiyo tuliwaambiwa warudie.”

Anaongeza kusema: “Kwenye shule nyingine unakuta tatizo ni mwanafunzi mmoja na wengine hata walimu wa shule za msingi wanashangaa walifaulu vipi, ila kwa sababu ule mtihani wa darasa la saba wote ulikuwa wa kuchagua, ni rahisi mtoto kufaulu hata kama hajui kusoma. Akifanikiwa tu kumwigilizia mwenzake atafaulu.’’

Katika matokeo ya mtihani wa darasa la saba yaliyotolewa mwishoni mwa mwaka jana,kiwango cha ufaulu kwa watahiniwa kiliongezeka kwa asilimia 4.76 na kufikia asilimia 58.28 kutoka asilimia 53.52 ya mwaka 2010.
Kwa mujibu wa taarifa ya matokeo hayo, wanafunzi waliofanya mtihani huo walikuwa 983,545, huku waliofaulu wakiwa 567,567.

Bado mbumbumbu wengi shule za sekondari za kata
 
Back
Top Bottom