ASKARI Magereza aliyekuwa akifanya kazi katika Gereza Kuu la Butimba lililopo katika Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza , amekufa baada ya kujimiminia risasi tatu kichwani.
Akithibitisha tukio hilo kwa waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Simon Sirro alisema tukio hilo lilitokea juzi saa saba mchana katika eneo la Gereza Kuu la Butimba muda ambao askari huyo alikuwa katika eneo lake la kazi gerezani hapo.
Kamanda Sirro alimtaja aliyekufa kuwa ni askari Magereza mwenye namba B5004, Eliasi Bukarima (25) ambaye alikuwa ni mfanyakazi wa gereza hilo.
Hadi sasa hatujapata taarifa sahihi kuhusiana na sababu ambayo imepelekea marehemu kuamua kujitoa uhai, ila kwa taarifa za awali tulizozipata kutoka kwa askari wenzake, zinadai kuwa muda mfupi kabla ya kujiua, marehemu alisikika akiongea na watu kwenye simu yake ya mkononi, alisema Kamanda Sirro.
Alidai maongezi aliyokuwa akizungumza askari huyo kwenye simu, yalikuwa ya kuwalaumu watu aliokuwa akiongea nao kwamba wanamsababishia ugumu wa maisha.
Alisema, baada ya askari huyo kumaliza kuzungumza maneno hayo kwenye simu yake ya mkononi, ndipo alipochukua uamuzi wa kujifyatulia risasi tatu kichwani.
Silaha aliyotumia kujiua ni bunduki aina ya SMG yenye namba 061220 aliyokuwa nayo kazini muda huo, hata hivyo bado tunafanya jitihada za kutafuta namba za huyo mtu wa mwisho aliyeongea naye ili tuweze kubainisha chanzo cha askari huyo kuamua kujiua maana huyo ndio atatwambia hayo maisha magumu ambayo marehemu alisema wanamsababishia ni yapi?" Alieleza Kamanda Sirro.
Alisema, mwili wa askari huyo umehifadhiwa kwenye chumba cha maiti cha Hospitali ya Rufaa Bugando.
Katika tukio jingine, mtu aliyefahamika kwa jina la Mafwele Machumu (27) mkazi wa Mriti Wilaya ya Ukerewe, amekufa baada ya kupigwa mateke tumboni na kichwani.
Kamanda Sirro alimtaja mtuhumiwa katika tukio hilo kuwa ni Pauline Mruti (39) na kwamba chanzo cha kifo hicho ni ugomvi ambao haujafahamika, na mtuhumiwa alikimbia mara baada ya tukio.
Polisi inaendelea na upelelezi huku juhudi za kumtafuta mtuhumiwa zikiendelea, alisema Kamanda Sirro.