Kanungila Karim
JF-Expert Member
- Apr 29, 2016
- 20,746
- 25,639
Mkazi wa Mtaa wa Nyanza Kata ya Kalangalala, Butogwa Daudi (22), ambaye alinusurika kifo baada ya kutumbukia kwenye shimo la choo na kuokolewa na askari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Geita jana.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Zabrone Muhumha, alisema tukio hilo lilitokea jana majira ya saa 3:49 asubuhi.
Muhumha alisema chanzo cha kutumbukia kwenye shimo hilo kwa mujibu wa mama mzazi, Reema Jumanne (45), alimwagiza binti yake Butogwa kutoa godoro nje na yeye akawa anaendelea kufua nguo.
Alisema alipotoka nje akakuta godoro na kuona kandambili alizokuwa amezivaa binti yake huyo na aliposogea karibu na shimo hilo na kuchungulia ndani alimuona binti yake amesimama ndani.
“Sisi askari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji tulipewa taarifa kutoka kwa Mkuu wa Kituo cha Polisi Geita na baada ya kupata hizo taarifa askari wa Jeshi la la Zimamoto na Uokoaji tulienda eneo la tukio na tulipofika, tukakuta binti huyo yumo ndani ya shimo la choo tulipanua tundu tukaingiza ngazi ndani na tukafanikiwa kumwokoa binti huyo akiwa mzima,” alisema.
Alisema baada ya kutolewa ndani ya shimo aliogeshwa na kupelekwa Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa Geita kwa uchunguzi zaidi.
Baba mzazi wa binti huyo, Jumanne Sizya, alisema binti yake alifikishwa hospitali na kufanyiwa uchunguzi na kukutwa hali yake ni nzuri na kuruhusiwa kurudi nyumbani.
Sizya alisema anamshukuru Mungu kwa sababu maji machafu kwenye shimo hilo yalikuwa machache, yangekuwa mengi mtoto wake angefariki dunia.
Pia, aliwashukuru askari wa Zimamoto na Uokoaji kuwahi kufika kwenye eneo la tukio na kumwokoa binti yake.
©IPPmedia