UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya Uhujumu Uchumi inayomkabili Eric Ayo na wenzake wanaodaiwa kukutwa na vinyonga 164, umebadili hati ya mashtaka na kumuongezea Eric shtaka la utakatishaji fedha.
Hati hiyo mpya ya mashtaka ilisomwa na Wakili wa Serikali, Cathbert Mbilinyi, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shahidi.
Wakili Mbilinyi aliwataja washtakiwa wengine katika kesi hiyo kuwa ni Ally Ringo na Aziz Ndago, ambao wanakabiliwa na mashtaka ya kujihusisha na nyara za serikali ikiwamo vinyonga 164 bila kibali.
Akisoma hati mpya ya mashtaka, Wakili wa Serikali Mbilinyi alidai kati ya Desemba mosi, 2020 hadi Januari 20, 2021, washtakiwa hao waliongoza genge la uhalifu.
Alidai washtakiwa waliongoza genge la uhalifu katika mikoa ya Morogoro, Tanga na Dar es Salaam kwa kukusanya, kusafirisha na kuuza nyara za serikali ambazo ni vinyonga 164, nyoka sita na mijusi 20.
Imedaiwa katika tarehe na maeneo hayo, washtakiwa hao walijihusisha na nyara hizo za serikali bila kibali zenye thamani ya Sh. 20,789,730.