Bujibuji Simba Nyamaume
JF-Expert Member
- Feb 4, 2009
- 76,579
- 161,430
ALADDIN NA TAA YA AJABU --- SEHEMU YA KWANZA (1)
ALADDIN NA TAA YA AJABU
Hapo zamani kabisa, aliishi mshonaji masikini, ambaye alikuwa na mtoto wa kiume aliyeitwa Aladdin, ambaye alikuwa ni mzembe na mvivu kabisa, asiyependa kufanya kazi yoyote isipokuwa kucheza mitaani na watoto wenzake wavivu kama yeye.
Tabia hii ya mwanawe, ilimhuzunisha sana mshonaji, mpaka ikapelekea apate ugonjwa ambao ulisababisha kifo chake. Ingawa mama yake Aladdin alifanya kila aliloweza, alilia na kufanya kila aina ya maombi, lakini mwanawe hakubadilika, aliendelea na tabia yake ileile.
Siku moja akiwa anacheza mitaani kama kawaida yake, alikuja mgeni mmoja na kumuuliza umri wake, na kama yeye hakuwa mtoto wa Mustafa mshonaji. Alijibu Aladdin; “Ndiye mimi, lakini baba yangu alishakufa muda mrefu uliopita”. Baada ya kusikia hili, yule mgeni ambaye alikuwa ni mchawi maarufu wa kiafrika, alimkumbatia Aladdin na kumbusu, huku alikwambia; “Mmi ni baba mdogo wako, nilikujua kutokana na kufanana kwako na kaka yangu. Nenda kwa mama yako na umwambie kwamba nakuja”.
Aladdin alikimbia kwenda nyumbani, ambako alimwambia mama yake habari za baba yake mdogo. “Kweli, mwanangu. Baba yako alikuwa na ndugu yake, lakini siku zote nilidhani kuwa alishafariki” alisema Mama yake Aladdin. Hata hivyo aliandaa chakula cha usiku, na kumtaka Aladdin akamtafute baba yake mdogo, ambaye alikuja akiwa na mvinyo na matunda.
Alipofika pale, alianguka chini na kubusu sehemu ambayo Mustafa alikuwa akipenda kukaa, huku akimtaka Mama yake Aladdin asishtuke kwa kutomuona hapo kabla, kwa kuwa alikuwa nje ya nchi kwa muda wa miaka arobaini. Kisha alimgeukia Aladdin, na kumuuliza alikuwa akifanya biashara gani, ambapo Aladdin aliinamisha kichwa chini, na Mama yake alianza kulia.
Baada ya kujua kwamba Aladdin alikuwa ni mvivu na hajui kufanya biashara yoyote, alitaka kumchukua na kumfungulia duka ili auze bidhaa. Siku iliyofuata, yule baba mdogo alimnunulia Aladdin, nguo mpya nzuri, na alimchukua na kwenda kutembea nae mjini, aklimuonyesha maeneo mbalimbali, ilipofika usiku alimrudisha kwako, ambapo Mama yake alifurahi sana kumuona mwanawe akiwa yupo vizuri.
Siku iliyofuata, yule mchawi alimchukua Aladdin na kumpeleka kwenye bustani nzuri sana iliyokuwa mbali kidogo na mji. Walikaa chini kwenye chemchem, na yule mchawi alitoa keki kutoka kwenye mfuko wake, aliikata kati na kipande kumpatia Aladdin. Waliendelea kusafiri mpaka wakafika milimani. Aladdin alichoka sana na aliomba warudi.
Mchawi hakutaka warudi, hivyo aliendelea kumlaghai Aladdin kwa hadithi tamu tamu ili safari yao iendelee. Mwisho walifika kwenye milima miwili iliyotenganishwa na bonde jembamba.
Mchawi alimwambia Aladdin; “Tutaishia hapa, hatutaendelea na safari, nitakuonyesha kitu kizuri. Kusanya kuni niwashe moto”. Aladdin alikusanya kuni na mchawi aliwasha moto. Baada ya moto kuwaka, yule mchawi alitoa unga mweupe na kuutupia kwenye ule moto huku akitamka maneno ya kichawi. Ardhi ikatikisika kidogo na ikafunguka, lilionekana jiwe kubwa lenye umbo la mraba likiwa na mshikio katikati.
Aladdin alijaribu kukimbia lakini mchawi alimkamata na kumzaba kibao kilichofanya aanguke chini. Aladdin aliongea kwa upole uliojaa woga; “Nimefanya nini Baba mdogo. Mchawi alijibu kwa upole nae; “Usiogope kitu, nitii mimi. Chini ya jiwe hili kuna hazina ambayo ni ya kwako, na hakuna yeyote awezaye kuigusa, hivyo lazima ufaye kama ninavyokuambia”.
Baada ya kusikia neno ‘hazina’, woga ulimuondoka Aladdin, aliishika kwa nguvu pete kama alivyoambiwa, huku akitaja majina ya Baba na Babu yake. Jiwe lilikuja juu na kufunguka, ngazi zilionekana. Mchawi alimwambia Aladdin; “Nenda, chini kabisa ya hizo ngazi utaona mlango upo wazi ambazo utakupeleka kwenye kumbi kubwa tatu. Kunja kanzu yako na upite bila kugusa kitu chochote au utakufa. Hizo kumbi zinaongoza kwenye bustani ya miti ya matunda matamu. Endelea kwenda mpaka ufike kwenye pembe ya varanda ambapo kuna taa ya chemli inayowaka. Mwaga mafura yake na uniletee”.
Mchawi alivua pete yake na kumpa Aladdin, na kumtakia kila la kheri. Aladdin alikutakila kitu kipo kama mchawi alivyosema, alichuma baadhi ya matunda na kuchuka ile taa, alirudi na kufika kwenye mlango wa pango. Mchawi alimpigia kelele kuwa aharakishe; “Fanya haraka unipe taa hiyo”. Aladdin alikataa kumpa ile taa, akitaka mpaka atoke nje ya pango lile.
Mchawi alishikwa zaidi na hasira, akamwaga unga mwingine kwenye moto na kutamka maneno yake ya kichawi, lile jiwe lilirudi na kujifunga kama mwanzo. Mchawi aliondoka kutoka Fursi daima, jambo lile lilimuonyesha Aladdin kuwa yule hakuwa Baba yake mdogo, ila ni mchawi tu ambaye alisoma kwenye vitabu kuhusu taa ya ajabu, ambayo ingemfanya yeye kuwa mtu mwenye nguvu zaidi duniani.
Ingawa ni yeye (mchawi) tu ndiye aliyejua taa ilipo, lakini ilikuwa ni lazima aipokee kutoka kwenye mikono ya mtu mwingine. Alimchagua mpumbavu Aladdin kwa jambo hili, akiazimia kupata taa na kumuua Aladdin baada ya hapo.
Kwa muda wa siku mbili, Aladdin aliendelea kubaki gizani, akilia na kujuta. Mwisho alikuwa akisugua mikono kwa maombi, katika kufanya aliisugua ile pete, ambayo mchawi aliisahau kuichukua kutoka kwake. Kwa haraka alitokea Jini mkubwa anayetisha sana, akasema; “Unataka nini kwangu? Mimi ni mtumwa wa pete na nitakutii na kufanya chochote utakacho”.
Bila woga Aladdin alijibu; “Nitoe kwenye hii sehemu!”. Ardhi ikajifungua, na Aladdin alijikuta yupo nje. Baada ya kukaa sawa, alianza kurudi nyumbani kwao. Alipofika, alimwambia Mama yake kilichotokea, alimuonyesha taa na matunda, ambayo kumbe yalikuwa ni madini kuhalisia (sio matunda).
Aladdin aliomba chakula kwa Mama yake. Mama alijibu; “Aah!! Mwanangu, hamna kitu leo. Lakini nimechuma pamba kidogo, nitakwenda kuuza na kununua chakula”. Aladdin alimwambia Mama yake ahifadhi pamba yake, badala yake atakwenda yeye (Aladdin) kuuza ile taa. Kwa kuwa ilikuwa chafu sana,Mama yake alianza kuisugua ili iwe safi na aiuze walau kwa bei ya kuridhisha kidogo.
Wakati akiendelea kuisugua ile taa, ghafla alitokea Jini na kuuliza kitu gani anataka. Mama alizimia, lakini Aladdin aliwahi na kusema; “Niletee chakula”, Jini alileta bakuli, sahani kumi na mbili zilizojaa nyama nzuri, vikombe viwili na chupa mbili za mvinyo, vyombo vyote vilikuwa vya fedha.
Mama alipozinduka alisema; “Vyakula hivi vizuri vimeletwa na nani?”. Aladdin alijibu; “Mama usiulize, wewe kula tu”. Walikula, mpaka ilipofika mchana, Aladdin alimwambia Mama yake kuhusiana na taa. Mama alimuomba Aladdin auze ile taa na asijishughulishe na Majini. Aladdin alisema; “Hapana, lazima tuitumie hii taa na hii pete vilevile, ambayo itakuwa kidoleni kwangu kila siku”.
Walipomaliza kula vyakula vyote vilivyoletwa na Jini, Aladdin aliuza moja ya sahani zake za fedha na nyingine mpaka zikaisha zote. Kisha aliendelea kumuita Jini, ambaye alimpatia sahani nyingine, walikula chakula na sahani kuuza. Waliendelea kuishi vile kwa miaka mingi.
Siku moja Aladdin alisikia amri kutoka kwa Sultani, ikisema kwamba kila mmoja anatakiwa asitoke nyumbani kwake na afunge milango na madirisha wakati Bintisultani akienda na kurudi kutoka kuoga. Aladdin alishikwa na tamaa haswa ya kuuona uso wa Bintisultani, kitu ambacho kilikuwa ni kigumu, kwasababu muda wote aliufunika uso wake kwa nikabu.
Aladdin alikwenda kujificha nyuma ya mlango wa bafu, na alikuwa akichungulia kupitia kitobo kidogo. Bintisaltani alipandisha nikabu yake alipokuwa akiingia, alikuwa ni mrembo sana kiasi kwamba Aladdin alijikuta akimpenda na kuzama palepale. Aladdin alirudi nyumbani kwao akiwa amebadilika sana mpaka Mama yake akaogopa labda huenda mwanae kapata tatizo.
Aladdin alimwambia Mama yake kwamba amempenda Bintisultani sana kiasi kwamba hatoweza kuishi bila yeye na anahitaji kumuowa. Mama yake aliposikia hili, aliangua kicheko kikubwa, lakini Aladdin alimuomba Mama yake aende kwa Sultani akafikishe ombi lake. Mama alichukua kitambaa na kuweka ndani yake yale matunda ya kichawi kutoka bustani ya kichawi, ambayo yaling’aa kama vito vizuri vya rhamani. Mama alibeba vitu vile ili walau amfurahishe Sultani.
Mama alitoka na kuelekea Ikulu, Mshauri mkuu na Wakuu wengine wa serikali waliingia kwenye ukumbi wa mkutano. Wakati huo Mama yake Aladdin naye aliingia ukimbini pale na kusimama sehemu ya mbele akiangalia kiti cha enzi cha Sultani. Hatahivyo, Sultani hakumzingatia (hakumtilia maanani).
Mama aliendelea kwenda pale kila siku kwa muda wa wiki nzima. Pindi mkutano ulipoisha kwenye siku ya sita, Sultani alimuuliza Mshauri wake; “Huwa ninamuona mwanamke fulani kwenye chumba cha mikutano kila siku akiwa amebeba kitu kwenye kitambaa. Nataka umuite, ili nijue anahitaji kitu gani”.
Siku iliyofuata, kwa ishara ya Mshauri mkuu, Mama yake Aladdin alikwenda kwenye kiti cha enzi na kubaki akiwa amepiga magoti huku macho ameinamisha chini mpaka Sultani alipomwambia; “Inuka ewe mwanamke mwema na uniambie unataka nini”. Mama alisita kidogo, hivyo Sultani aliondoa watu wote isipokuwa Mshauri wake, na kumuomba azungumze kwa uhuru, huku akimuahidi kutochukizwa na kusamehe kwa chochote atakachozungumza.
Mama alimueleza Sultani kuhusu suala la mwanawe (Aladdin) kumpenda sana Bintisultani. “Nilimuomba sana amsahau” alisema Mama, “Lakini ilishindikana, alitishia kufanya kitu kibaya kama ningekataa kuja kukuambia kuhusu yeye kutaka kumposa Binti yako. Sultani naomba unisamehe mimi na mwanangu”.
Sultani kwa upole alimuuliza yule Mama kitu gani amebeba kwenye kitambaa, Mama alifungua kitambaa chake na kumuonyesha Sultani vile vito vya thamani kubwa alivyobeba. Sultani alipigwa na butwaa, akamgeukia Mshauri wake na kumwambia; “Ulisema nini? Hivi sihitajiki kumuoza Binti yangu kwa mtu ambaye anamthamini kwa gharama kama hii?”.
Mshauri, ambaye alikuwa akitaka Bintisultani aolewe na mwanaye, alimuomba Sultani aendelee kusubiri kwa miezi mitatu, huku akiwa na tumaini kwamba mwanaye atamletea Sultani zawadi za gharama kubwa kuliko zile. Sultani alikubaliana na jambo lile, na kumwambia Mama Aladdin kwamba ingawa yeye amekubali na jambo la ndoa, lakini Mama Aladdin hatakiwi kuja tena kwa Sultani mpaka ipite miezi mitatu.
Aladdin aliendelea kusubiri kwa karibu miezi mitatu, lakini baada ya miezi miwili kupita, Mama Aladdin alikwenda mjini kununua mafuta, alimkuta kila mtu akifurahi, aliuliza ni kitu gani kinaendelea. “Hujui!! Mtoto wa Mshauri mkuu anamuoa Bintisultani usiku wa leo?” hilo ndio lilikuwa jibu.
Mama Aladdin akiwa kaishiwa pumzi, alirudi nyumbani haraka na kumwambia Aladdin habari zile, alipatwa na mshtuko mkubwa, lakini alitulia na baadae kidogo aliikumbuka taa yake. Aliisugua na Jini alitokea na kusema; “Unataka nini?”. Aladdin alijibu; “Sultani kama unavyomjua, amevunja ahadi yake kwangu, na amamuoza Binti yake kwa mtoto wa Mshauri. Amri yangu ni kwamba, usiku wa leo uwalete hapa bwana na bibiharusi”. “Ninatii, Bwana wangu” alisema Jini.
Aladdin alikwenda chumbani kwake,ambapo usiku ule, Jini alileta kitanda kilichowabeba Bintimfalme na mumewe. Aladdin alimwambia Jini; “Mchukue huyu bwanaharusi mpya umpeleke nje kwenye baridi, kisha urudi asubuhi”. Jini alimchukua mtoto wa Mshauri mkuu na kumpeleka nje huku kitandani akibaki Aladdin na Bintisultani. Aladdin alimwambia Bintisultani; “Usiogope kitu, wewe ni mke wangu, niliyeahidiwa na Baba yako asiyetenda haki, na hautadhurika na chochote”. Bintisultani aliogopa sana na usiku ule ulikuwa ndio usiku mgumu kwenye maisha yake, wakati akiwa amelala pembeni yake tena akikoroma sana.
Muda ulipofika, Jini alirudi akamchukua bwanaharusi kutoka kwenye baridi na kumlaza kitandani, kisha alikirudisha kile kitanda ikulu. Sultani alikwenda kumsalimia Binti yake, mtoto wa Mshauri alijificha, wakati Bintisultani hakuweza kusema neno lolote na alikuwa ni mwenye huzuni sana.
Sultani alipoona hali ile, alimtuma mkewe akazungumze na mwanawe; “Vipi mwanangu hauzungumzi na Baba yako? Nini kimetokea?”. Bintisultani alishusha pumzi nzito na kumwambia Mama yake, wakati wa usiku, kitanda chao kilipelekwa kwenye nyumba ngeni, na kilichotokea huko. Mama yake hakumuamini, lakini alimuomba aichukulie ile kama ni ndoto mbaya tu.
Usiku uliofuata, kitu kile kile kilitokea tena, na asubuhi iliyofuata kwa kitendo cha Bintisultani kukataa kuongea na Sultani, Sutani alitishia kumkata kichwa. Bintisultani kwa kuogopea maisha yake, alisema yaliyotokea yote kwa Sultani, na kumwambia kama ataona ni uongo basi amuulize mtoto wa Mshauri mkuu (ambaye ndiye mume wa Bintisultani).
Sultani alimwambia Mshauri wake amuulize mtoto wake, ambaye alisema ukweli wote, na kuongeza kwamba, ingawa alimpenda sana Bintimfalme, lakini yupo ni bora kwake kufa kuliko kupitisha usiku mwingine wa kutisha na kuomba aachanishwe na Bintimsultani. Ombi la mtoto wa Mshauri mkuu lilikubali na hivyo kuachana na Bintisultani.
Pindi miezi mitatu ilipoisha, Aladdin alimtuma Mama yake kwenda kumkumbusha Sultani kuhusu ahadi yake. Sultani alipoona Mama yake ni masikini sana, alijihisi uzito kutekeleza ahadi yake, alitaka ushauri kutoka kwa Mshauri wake, alimshauri Sultani kuweka mahari kubwa sana ambayo hakuna mtu yeyote atakayeweza kuimudu.
Sultani alimgeukia Mama Aladdin na kumwambia; “Mwanamke mwema, Sultani lazima akumbuke ahadi yake, na mimi nitaikumbuka ya kwangu, lakini mtoto lazima aniletee mabakuli arobaini ya dhahabu yaliyojaa vito vya thamani, yakiwa yamebebwa na watumwa arobaini weusi, wakiwa wamevaa mavazi ya thamani. Mwambie mwanao nasubiri jibu lake”.
Mama Aladdin alirudi nyumbani akihisi tayari wameshindwa. Alifikisha ujumbe kwa Aladdin na kumwambia; “Ametoa muda mrefu wa kusubiri jibu kutoka kwako”. “Sio muda mrefu Mama, kama unavyofikiria” alijibu Aladdin, “Nitafanya jambo kubwa zaidi ya hilo kwa ajili ya Bintimfalme”.
Aladdin alimuita Jini, na ndani ya muda mfupi walifika watumwa themanini na kujaa nyumba nzima mpaka kwenye bustani. Aladdin aliwataka waelekee ikulu, wawili kwa wawili, wakiongozwa na Mama yake. Walikuwa na wamevaa ya gharama sana, wakiwa na vito vya thamani kwenye mikanda yao, huku wakiwa mabakuli ya dhahabu vichwani mwao, watu walikusanyika kwa wingi kuwaangalia.
Waliingia ikulu, na baada ya kupiga magoti mbele ya Sultani, walisimama nusu mduara kuzunguka kiti cha enzi, wakati huo Mama yake Aladdin aliwatambulisha kwa Sultani. Sultani hakusita tena, ila alisema; “Mwanamke mwema, rudi na umwambie mwanao kwamba ninamsubiri kwa mikono mikunjufu kabisa”.
Mama hakupoteza muda kwenda kumwambia Aladdin na kumtaka afanye haraka. Lakini Aladdin kwanza alimuita Jini na kumwambia; “Nahitaji kuoga maji yanayonukia, farasi mzuri kuliko wa Sultani, watumwa ishirini. Pia nahitaji watumwa sita wakiwa na mavazi ya gharama wakumsindikiza Mama yangu, na mwisho nahitaji vipande elfu kumi vya dhahabu vikiwa ndani mikoba kumi”. Vitu vyote hivyo vikatokea palepale.
Aladdin alipanda farasi wake na kupita mitaani, watumwa wake walikuwa wakirusha dhahabu huhu na huko wakati wanakwenda. Wale waliocheza naye utotoni, hawakumjua kabisa, alikuwa amependezac sana. Sultani alipomuona Aladdin akija, alishuka kwenye kiti chake cha enzi ili kumlaki, na kumuongoza mpaka kwenye ukumbi ambako kuliandaliwa sherehe kubwa, huku Sultani akiwa ameazimia kumuoza Binti yake kwa Aladdin siku ileile.
Lakini Aladdin alikataa kuoa siku ile na kusema; “Lazima nijenge Kasri linaloendana na Bintisultani”. Baada ya kusema vile Aladdin aliondoka. Alipofika nyumbani alimwambia Jini; “Nijengee Kasri kubwa lenye kunakshiwa kwa marumaru na mawe mengine ya thamani. Katikati ya Kasri kujengwe kuba, kuta nne za dhahabu na fedha, kila upande liwe na madirisha sita, isipokuwa moja, liachwe likiwa halijamaliziwa matengenezo yake, hayo madirisha yapambwe kwa almasi na yakuti. Lazima kuwe na farasi, wachungaji wake na watumwa”.
Siku iliyofuata, kazi ya kujenga Kasri ilikuwa imeisha na Jini alimchukua Aladdin na kumpeleka kumuonyesha, na kulitandikwa kapeti kutoka kwenye Kasri ya Aladdin mpaka kwa Sultani. Mama Aladdin alivaa vizuri, na kuanza safari ya kuelekea ikulu akiwa na watumwa wake, huku Aladdin akimfuata Mama yake kwa nyuma akiwa juu ya farasi.
Sultani alipeleka wanamuziki wakiwa na matarumbeta na ngoma kwenda kuwapokea. Mama Aladdin alipelekwa kwa Bintisultani, ambaye alimsalimia kwa heshima kubwa sana. Usiku Bintisultani alimuaga baba yake, na kuanza safari kuelekea kwenye Kasri ya Aladdin akiwa na Mama yake huku akifuatwa na watumwa mia. Bintisultani alifarishwa alifurahishwa na muonekano wa Aladdin, ambaye aliwahi kumpokea.
“Bintisultani, ulaumu uzuri wako kwa vitendo vyangu kama nitakuwa nimekuudhi” alisema Aladdin. Bintisultani alimwambia kwamba, kwa kule kumuona tu, basi amekubaliana na baba yake kwa moyo wote juu ya jambo lile la ndoa.
badala ya kucheza cheza Mwl anakuja kutusomea hadithi, R.I.P Mwl Nswima.